Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI YA KUJIFUNZA YA 15

Umuige Yesu ili Uendelee Kuwa na Amani

Umuige Yesu ili Uendelee Kuwa na Amani

“Amani ya Mungu yenye kupita uelewaji wote italinda mioyo yenu.”​—FLP. 4:7.

WIMBO 113 Amani Tuliyo Nayo

KIFUPI CHA HABARI *

1-2. Juu ya nini Yesu alivurugika?

KATIKA siku ya mwisho ya maisha yake hapa ku dunia, Yesu alivurugika. Watu wabaya walikuwa karibu kumutesa na kumuua. Lakini, Yesu hakuhangaika tu kwa sababu ya kujua kama alikuwa karibu kufa. Alipenda sana Baba yake na alitaka kumufurahisha. Yesu alijua kama ikiwa angebakia muaminifu katika mateso yenye alikuwa karibu kupata, angesaidia kutetewa kwa jina la Yehova. Tena Yesu alipenda watu, na alijua kama tungekuwa na tumaini la kuishi milele wakati wenye kuja, ikiwa tu angebakia muaminifu kwa Yehova mupaka kifo.

2 Hata kama Yesu alikuwa mwenye kuvurugika sana, alikuwa na amani. Alikuwa ameambia mitume wake hivi: “Ninawapatia amani yangu.” (Yoh. 14:27) Alikuwa na “amani ya Mungu,” ni kusema, utulivu wenye mutu anapata wakati iko na urafiki muzuri pamoja na Yehova. Amani hiyo ilisaidia Yesu akuwe mwenye kutulia katika akili na mu moyo wake.​—Flp. 4:6, 7.

3. Tutazungumuzia nini mu habari hii?

3 Hakuna mumoja wetu mwenye atapatwa hata siku moja na mukazo wenye Yesu alivumilia, lakini watu wote wenye kumufuata Yesu watapata mateso. (Mt. 16:24, 25; Yoh. 15:20) Na kama Yesu, tutajisikia kuwa wenye kuvurugika wakati fulani. Tunaweza kufanya nini ili tusihangaike sana na kupoteza furaha yetu? Tuchunguze basi mambo tatu yenye Yesu alifanya wakati wa utumishi wake hapa ku dunia, na tuone namna tunaweza kumuiga wakati tunapatwa na magumu.

YESU ALIENDELEA KUSALI

Kusali kunaweza kutusaidia tuendelee kuwa na amani (Picha hizi zinapatana na fungu la 4-7)

4. Kwa kufikiria andiko la 1 Watesalonike 5:17, ni mifano gani fulani yenye kuonyesha kama Yesu alisali mara mingi katika siku ya mwisho ya maisha yake hapa ku dunia?

4 Soma 1 Watesalonike 5:17. Katika siku ya mwisho ya maisha yake ku dunia, Yesu alisali mara mingi. Wakati alianzisha Ukumbusho wa kifo chake, alisali kwa ajili ya mukate na divai. (1 Ko. 11:23-25) Mbele ya kutoka mahali kwenye walikuwa wamefanyia Pasaka, alisali pamoja na wanafunzi wake. (Yoh. 17:1-26) Wakati yeye na mitume wake walifika ku Mulima wa Mizeituni usiku huo, alisali tena na tena. (Mt. 26:36-39, 42, 44) Na maneno ya mwisho kabisa yenye Yesu alisema mbele akufe ilikuwa sala. (Lu. 23:46) Yesu alisali kwa Yehova juu ya kila tukio kubwa lenye lilitokea katika siku hiyo ya mwisho ya maisha yake hapa ku dunia.

5. Juu ya nini mitume walipoteza uhodari wao?

5 Sababu moja yenye ilisaidia Yesu avumilie majaribu yenye alipata ni hii: alisali mara mingi kwa Baba yake na kumuomba amusaidie kuvumilia. Kwa upande mwingine, usiku huo mitume walishindwa kuendelea kusali. Kwa hiyo, walishindwa kuwa hodari wakati walipata majaribu. (Mt. 26:40, 41, 43, 45, 56) Wakati tunapatwa na majaribu, tutaendelea kuwa waaminifu ikiwa tu tunafuata mufano wa Yesu na “kusali bila kuacha.” Tunaweza kusali juu ya mambo gani?

6. Namna gani imani itatusaidia tuendelee kuwa na amani?

6 Tunaweza kusali ili kumuomba Yehova ‘atupatie imani zaidi.’ (Lu. 17:5; Yoh. 14:1) Tuko na lazima ya imani juu Shetani atajaribu wale wote wenye kumufuata Yesu. (Lu. 22:31) Namna gani imani itatusaidia tuendelee kuwa na amani hata wakati tunapatwa na magumu yenye kufuatana? Kisha kufanya nguvu yetu yote ili kupiganisha magumu fulani, imani itatuchochea tuache mambo mu mikono ya Yehova. Kwa sababu tunajua kama anaweza kushugulikia mambo muzuri zaidi kuliko sisi, tunakuwa na amani ya akili na amani ya moyo.​—1 Pe. 5:6, 7.

7. Mambo yenye Robert anasema inakufundisha nini?

7 Sala inatusaidia tuendelee kuwa na amani ya akili hata kama tunapambana na magumu ya namna gani. Fikiria mufano wa Robert, muzee wa kutaniko muaminifu, mwenye kuwa sasa na miaka zaidi ya 80. Anasema hivi: “Mashauri yenye kuwa mu Wafilipi 4:6, 7 imenisaidia kupiganisha magumu mingi mu maisha yangu. Nimepambana na magumu ya kupata feza. Na kwa wakati fulani nilipoteza pendeleo langu la kuwa muzee wa kutaniko.” Ni nini imemusaidia Robert aendelee kuwa na amani ya akili? Anasema hivi: “Ninasali wakati tu ninaanza kuwa na mahangaiko. Ninaamini kama wakati ninasali mara mingi na kwa bidii, ninajisikia kuwa na amani zaidi.”

YESU ALIHUBIRI KWA BIDII

Kazi ya kuhubiri inaweza kutusaidia tuendelee kuwa na amani (Picha hizi zinapatana na fungu la 8-10)

8. Kulingana na Yohana 8:29, ni sababu gani ingine yenye ilifanya Yesu akuwe na amani ya akili?

8 Soma Yohana 8:29. Hata wakati Yesu alikuwa anateswa, alikuwa na amani ya akili kwa sababu alijua kama alikuwa anamufurahisha Baba yake. Aliendelea kumutii Baba yake wakati ilikuwa nguvu kufanya vile. Alipenda Baba yake na alifanya utumishi wake kwa Yehova kuwa jambo la maana zaidi mu maisha yake. Mbele akuje ku dunia, alikuwa “fundi wa kazi.” (Mez. 8:30). Na wakati alikuwa ku dunia, alifundisha wengine kwa bidii juu ya Baba yake. (Mt. 6:9; Yoh. 5:17) Kazi hiyo ilimuletea Yesu furaha kubwa.​—Yoh. 4:34-36.

9. Juu ya nini kuhubiri kwa bidii kunatusaidia ili tuendelee kuwa na amani ya akili?

9 Tunaweza kumuiga Yesu kwa kumutii Yehova na ‘sikuzote kuwa na mambo mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana.’ (1 Ko. 15:58) Wakati ‘tunahangaikia sana’ kazi ya kuhubiri, tunakuwa na mawazo yenye kufaa zaidi juu ya magumu yetu. (Mdo. 18:5) Kwa mufano, mara mingi watu wenye tunakutana nao mu kazi ya kuhubiri, wanapambana na magumu makali zaidi kuliko sisi. Lakini, wakati wanajifunza kumupenda Yehova na kutumia mashauri yake, maisha yao inakuwa muzuri zaidi na wanakuwa na furaha zaidi. Kila wakati tunaona jambo hilo, tunakuwa hakika zaidi kama Yehova atatuhangaikia. Na kuwa na uhakika huo, kunatusaidia tuendelee kuwa na amani ya akili. Dada mumoja mwenye katika maisha yake yote amepiganisha tatizo la kushuka moyo na mawazo ya kujisikia kuwa mutu wa bure, aliona kuwa jambo hilo ni la kweli. Anasema hivi: “Wakati niko na bidii mu kazi ya kuhubiri, ninajisikia kuwa mwenye kutulia zaidi mu moyo na mwenye furaha zaidi. Ninawaza kama ni kwa sababu wakati niko mu mahubiri, ninajisikia kuwa karibu zaidi na Yehova.”

10. Mambo yenye Brenda anasema inakufundisha nini?

10 Fikiria pia mufano wa dada mumoja mwenye kuitwa Brenda. Yeye na mutoto wake mwanamuke wako na ugonjwa fulani wa mishipa ya ufahamu. Brenda anatumia kinga ya vilema kwa sababu hawezi kutembea na iko na nguvu kidogo. Anahubiri nyumba kwa nyumba wakati iko na uwezo wa kufanya vile, lakini anahubiri zaidi sana kwa kuandikia watu barua. Anasema hivi: “Wakati nilielewa kama ugonjwa wangu hauwezi kupona mu ulimwengu wa leo, niliweza kukaza akili yangu juu ya kazi yangu ya kuhubiri. Kwa kweli, kazi ya kuhubiri inanisaidia nisifikiri sana juu ya mahangaiko yangu. Inanifanya nikaze akili yangu juu ya watu wa eneo la kutaniko letu wenye ninahubiria. Na inanikumbusha sikuzote juu ya tumaini lenye niko nalo juu ya wakati wenye kuja.”

YESU ALIKUBALI MUSAADA WENYE MARAFIKI WAKE WALIMUTOLEA

Kupitisha wakati pamoja na marafiki wazuri kunaweza kutusaidia tuendelee kuwa na amani (Picha hizi zinapatana na fungu la 11-15)

11-13. (a) Namna gani mitume na watu wengine walijionyesha kuwa marafiki wa kweli wa Yesu? (b) Marafiki wa Yesu walimufanya ajisikie namna gani?

11 Wakati wote wa utumishi wa Yesu wenye ulikuwa na magumu, mitume waaminifu walijionyesha kuwa marafiki wake wa kweli. Walikuwa marafiki wenye Biblia inasema hivi juu yao: “Kuko rafiki mwenye anashikamana sana na mutu kuliko ndugu.” (Mez. 18:24) Yesu aliona marafiki kama hao kuwa wa maana. Wakati wa utumishi wake hapa ku dunia, hakuna mumoja kati ya ndugu zake mwenye alimuamini. (Yoh. 7:3-5) Wakati fulani, watu wa jamaa yake walifikiri kama alikuwa amepoteza akili. (Mk. 3:21) Lakini, usiku mbele ya kifo chake, Yesu alisema hivi juu ya mitume wake waaminifu: “Ninyi ndio mumeshikamana na mimi katika majaribu yangu.”​—Lu. 22:28.

12 Wakati fulani mitume walimuhuzunisha Yesu, lakini Yesu hakukazia akili makosa yao, aliona kama walikuwa na imani kwake. (Mt. 26:40; Mk. 10:13, 14; Yoh. 6:66-69) Katika usiku wa mwisho wenye Yesu alipitisha pamoja na wanaume hao washikamanifu mbele auawe, aliwaambia hivi: “Nimewaita ninyi marafiki, kwa sababu nimewajulisha mambo yote yenye nilisikia kutoka kwa Baba yangu.” (Yoh. 15:15) Kwa kweli, marafiki wa Yesu walimutia moyo sana. Musaada wenye walimutolea Yesu mu utumishi wake, ulifanya afurahi sana.​—Lu. 10:17, 21.

13 Zaidi ya mitume, Yesu alikuwa na marafiki wengine, wanaume na wanamuke, wenye walimusaidia kufanya kazi ya kuhubiri na kumusaidia mu njia zingine mbalimbali. Wamoja walimualika mu nyumba zao ili akule chakula. (Lu. 10:38-42; Yoh. 12:1, 2) Wengine walisafiri pamoja naye na kuchangia mali zao pamoja naye. (Lu. 8:3) Yesu alikuwa na marafiki wazuri juu alikuwa rafiki muzuri kwao. Aliwafanyia mambo ya muzuri na hakuwaomba wafanye mambo yenye ilipita uwezo wao. Yesu alikuwa mukamilifu, lakini marafiki wake hawakukuwa wakamilifu, hata hivyo, alikuwa mwenye shukrani kwao kwa sababu walimutegemeza. Na tunaweza kuwa hakika kama, walimusaidia aendelee kuwa na amani ya akili.

14-15. Tunaweza kufanya nini ili tupate marafiki wazuri, na namna gani wanaweza kutusaidia?

14 Marafiki wazuri watatusaidia tuendelee kuwa washikamanifu kwa Yehova. Na njia ya muzuri zaidi ya kupata marafiki wazuri ni kuwa rafiki muzuri. (Mt. 7:12) Kwa mufano, Biblia inatutia moyo tujitoe kwa ajili ya wengine, zaidi sana wale wenye kuwa “katika uhitaji.” (Efe. 4:28) Fikiria mutu fulani mu kutaniko lenu mwenye unaweza kusaidia. Unaweza kuenda kuuza vitu fulani kwa ajili ya muhubiri mwenye hawezi kutoka ku nyumba kwa sababu ya uzee ao ugonjwa. Unaweza kutolea chakula familia yenye kuwa na magumu ya kupata feza. Na kama unajua namna ya kutumia site yetu ya Enternete jw.org® na programu JW Library®, unaweza kusaidia wengine mu kutaniko lenu ili wajue namna ya kutumia vyombo hivyo. Wakati tunakaza akili yetu juu ya kusaidia wengine, inawezekana kabisa kama tutakuwa na furaha.​—Mdo. 20:35.

15 Marafiki wenye tunapata watatutegemeza wakati tunapambana na magumu, na watatusaidia tuendelee kuwa na amani ya akili. Kama tu vile Elihu alisikiliza wakati Yobu alikuwa anazungumuza juu ya magumu yake, marafiki wetu wanatusaidia kwa kutusikiliza kwa uvumilivu wakati tunawaelezea mahangaiko yetu. (Yob. 32:4) Hatupaswe kutazamia kama marafiki wetu watakamata maamuzi pa nafasi yetu, lakini tunatenda kwa hekima wakati tunasikiliza mashauri yao yenye kutegemea Biblia. (Mez. 15:22) Na kama vile tu Mufalme Daudi alikubali kwa unyenyekevu musaada wa marafiki wake, majivuno haipaswe kutuzuia kukubali musaada wenye marafiki wetu wanatutolea wakati tuko na uhitaji. (2 Sa. 17:27-29) Kwa kweli, marafiki wazuri kama hao ni zawadi kutoka kwa Yehova.​—Yak. 1:17.

MAMBO YA KUFANYA ILI TUENDELEE KUWA NA AMANI

16. Kulingana na Wafilipi 4:6, 7, njia moja tu ya kupata amani ni gani? Fasiria.

16 Soma Wafilipi 4:6, 7. Juu ya nini Yehova anatuambia kama ni “kupitia Kristo Yesu” njo tunaweza kupata amani yenye anatoa? Juu tunaweza kuendelea kuwa na amani ya akili na ya moyo kama tu tunaelewa daraka lenye Yesu iko nalo katika kusudi la Mungu na kama tuko na imani katika daraka hilo. Kwa mufano, kupitia zabihu ya bei ya ukombozi ya Yesu, zambi zetu zote zinaweza kusamehewa. (1 Yo. 2:12) Wakati tunafikiri juu ya jambo hilo, tunapata kitulizo kabisa! Kwa sababu Yesu ni Mufalme wa Ufalme wa Mungu, atamaliza mateso yote yenye Shetani na ulimwengu wanatuletea. (Isa. 65:17; 1 Yo. 3:8; Ufu. 21:3, 4) Hilo linatupatia tumaini la muzuri sana! Na hata kama Yesu ametupatia kazi ya nguvu, iko pamoja na sisi, na anatutegemeza mu siku za mwisho za ulimwengu huu. (Mt. 28:19, 20) Hilo linatupatia uhodari kabisa! Ili tukuwe na amani, tuko na lazima ya mambo tatu ya maana sana, ni kusema, utulivu, tumaini, na uhodari.

17. (a) Mukristo anaweza kufanya nini ili aendelee kuwa na amani ya akili? (b) Kama vile Yohana 16:33 inaahidi, tutaweza kufanya nini?

17 Kwa hiyo, namna gani unaweza kuendelea kuwa na amani ya akili wakati unapambana na magumu makali? Unaweza kuwa na amani hiyo kama unafanya mambo yenye Yesu alifanya. Kwanza, usali na udumu katika sala. Pili, umutii Yehova na uhubiri kwa bidii hata wakati ni nguvu kufanya vile. Na tatu, utegemee marafiki wako ili wakusaidie wakati wa magumu. Kisha, amani ya Mungu italinda akili yako na moyo wako. Na kama Yesu, utashinda majaribu yoyote.​—Soma Yohana 16:33.

WIMBO 41 Tafadhali Sikiliza Sala Yangu

^ fu. 5 Sisi wote tunapambana na magumu yenye inaweza kufanya tupoteze amani yetu. Habari hii itazungumuzia mambo tatu yenye Yesu alifanya, na yenye sisi pia tunaweza kufanya ili tuendelee kuwa na amani, hata wakati tuko na magumu makali.