Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI JUU YA MAISHA YA WATU

Nimefarijiwa Katika Mahangaiko Yangu Yote

Nimefarijiwa Katika Mahangaiko Yangu Yote

Nilizaliwa tarehe 9 Mwezi wa 11, 1929 katika sehemu ya mangaribi ya pembeni ya Muto Indus, katika inchi yenye kuitwa leo Pakistan, zamani eneo hilo liliitwa muji wa Sukkur. Karibu na wakati huo misionere mumoja Mwingereza alipatia wazazi wangu vitabu vyenye rangi mbalimbali zenye kuangara. Wakati niliendelea kukomaa, vichapo hivyo vyenye kutegemea Biblia vilinisaidia kukubali kweli.

VITABU hivyo viliitwa upinde wa mvua. Kadiri niliendelea kuvichunguza niliona picha mbalimbali zenye zilinipendeza sana. Kwa hiyo, kuanzia wakati nilikuwa mutoto nilipenda kujifunza mambo yenye kuwa katika Biblia, kama yale yenye yalikuwa yameonyeshwa katika vitabu hivyo.

Wakati Vita ya Pili ya Ulimwengu ilikaribia kuingia katika India, maisha yangu yalianza kugeuka na kuwa mubaya zaidi. Wazazi wangu walitengana na kisha wakavunja ndoa yao. Sikuweza kuelewa sababu gani watu wawili wenye nilipenda wangeachana. Nilisikia sana huzuni katika moyo wangu na kuona kama nimeachwa. Hata kama nilikuwa mutoto mumoja tu, ilionekana kama sikupata mambo yenye nilikuwa nayo lazima sana, ni kusema, faraja na utegemezo.

Mimi na mama yangu tulikuwa tunaishi Karachi, muji mukubwa wa jimbo la Sindh. Siku moja, Fred Hardaker, munganga mwenye kuzeeka, mwenye alikuwa Shahidi wa Yehova aligonga kwenye mulango wetu. Alikuwa katika dini moja na ule misionere mwenye alikuwa amepatia familia yetu vitabu hivyo. Aliomba mama yangu aanze kujifunza Biblia. Mama alikataa lakini alisema kama mimi ninaweza kupendezwa na funzo hilo. Nilianza kujifunza Biblia pamoja na Ndugu Hardaker juma lenye lilifuata.

Kisha majuma fulani, nilianza kuhuzuria mikutano ya Kikristo kwenye hospitali ya Ndugu Hardaker. Mashahidi 12 hivi wenye kuzeeka walikusanyika pale ili kuabudu. Walinifariji na kunihangaikia kama vile mutoto wao. Ninakumbuka kwa furaha namna walikuwa wanakaa pamoja na mimi na kuinama ili wakuwe na urefu mumoja na mimi, na walizungumuza na mimi kama marafiki wa kweli, wenye nilikuwa nao lazima sana wakati huo.

Kisha muda mufupi, ndugu Hardaker aliniomba nimusindikize katika mahubiri. Alinifundisha namna ya kutumia fonografe ya kubeba kwa mukono ili tuweze kusikilizisha watu hotuba fupi za Biblia zenye kurekoridiwa. Hotuba fulani zilikuwa zinasema mambo waziwazi, na wasikilizaji fulani hawakufurahia ujumbe huo. Lakini, nilifurahia kuhubiria wengine. Nilikuwa na bidii nyingi kwa ajili ya kweli ya Biblia na nilifurahia kuelezea watu wengine juu ya kweli hiyo.

Wakati jeshi la Japani lilikaribia kuingia India, viongozi wa serikali ya Uingereza waliwekea Mashahidi wa Yehova mikazo mingi. Mwishowe katika Mwezi wa 7, 1943, mikazo hiyo ilinigusa kipekee. Musimamizi wa masomo, mwenye alikuwa kiongozi katika dini ya Waanglikani, alinifukuza kwenye masomo, alisema kama nilikuwa “mutu mwenye hastahili.” Aliambia mama yangu kama niliwekea wanafunzi wengine mufano mubaya kwa sababu nilijiunga na Mashahidi wa Yehova. Mama yangu aliogopa sana na akanikataza kujiunga na Mashahidi. Kisha alinituma kwa baba yangu katika Peshawar, muji wenye kuwa kwenye kilometre 1370 katika eneo la kaskazini. Kwa sababu sikukuwa na chakula cha kiroho na sikujiunga na Wakristo wengine, urafiki wangu pamoja na Yehova ukakuwa zaifu.

NINAKUWA TENA NA URAFIKI PAMOJA NA YEHOVA

Katika mwaka wa 1947, nilirudia Karachi ili kutafuta kazi. Wakati nilikuwa huko nilitembelea hospitali ya munganga Hardaker. Alinikaribisha kwa uchangamufu na kwa moyo wote.

Aliniuliza hivi: “Ni nini inakusumbua?” Aliuliza hivyo kwa sababu alifikiri kama nilikuja kwa ajili ya matunzo.

Nilijibia hivi: “Munganga, siko mugonjwa kimwili. Niko mugonjwa kiroho. Niko na lazima ya kujifunza Biblia.”

Aliniuliza hivi: “Unapenda kuanza wakati gani?”

Nilijibia hivi: “Sasa hivi ikiwa inawezakana.”

Tulifurahia kujifunza Biblia mangaribi hiyo. Nilijisikia kuwa mwenye kutulia na mwenye kutiwa moyo kwa sababu nilikuwa tena pamoja na watu wa Yehova. Mama yangu alijikaza sana ili kunizuia, lakini wakati huo nilikuwa nimekamata uamuzi wa pekee wa kumutumikia Yehova. Tarehe 31 Mwezi wa 8, 1947, nilijitoa kwa Yehova na kubatizwa katika maji. Kisha muda mufupi, wakati nilikuwa na miaka 17, nilianza kufanya kazi ya upainia wa kawaida.

KAZI YA UPAINIA YENYE FURAHA

Mugawo wangu wa kwanza katika kazi ya upainia ulikuwa muji wenye ulikuwa zamani makao ya maaskari wa Uingereza. Katika mwaka wa 1947, inchi iligawanywa na kuwa India na Pakistan. * Tukio hilo lilifanya kukuwe matendo mengi ya jeuri kati ya watu wa dini tofauti, na kufanya watu wengi sana wahame kuliko wakati mwingine wowote katika historia. Wakimbizi milioni 14 hivi walihamishwa. Waislamu wenye walikuwa katika India walienda Pakistan, na Wahindu na Wasikh walihamia katika India. Wakati wa muvurugo huo wote, niliingia katika treni moja katika Karachi yenye ilijaa sana watu na karibu safari yote ya kuenda Quetta, nilikamata kwa uangalifu kwenye vyuma vyenye kuzuia watu kuanguka.

Nilihuzuria mukusanyiko wa muzunguko katika India katika mwaka wa 1948

Katika Quetta, nilikutana na George, painia wa pekee mwenye alikuwa na miaka 25 hivi. George alinipatia kinga yenye ilikuwa imekwisha kutumiwa yenye ningeweza kutembeza (ao kusukuma) katika eneo hilo lenye kuwa na milima. Mara nyingi, nilihubiri mimi peke yangu. Kisha miezi sita, nilikuwa na mafunzo 17, na wamoja kati ya wanafunzi hao walifikia kuingia katika kweli. Mumoja kati yao alikuwa mukubwa mumoja wa jeshi mwenye kuitwa Sadiq Masih, alinisaidia mimi na George kutafsiri vichapo fulani vyenye kutegemea Biblia katika luga ya Urdu, luga ya taifa ya Pakistan. Kisha, Sadiq alifikia kuwa muhubiri wa habari njema mwenye bidii.

Niko katika mashua Queen Elizabeth, niko ninaenda kwenye Masomo ya Gileadi

Kisha nilirudia Karachi na nikatumika pamoja na Henry Finch na Harry Forrest, wamisionere wapya wenye walikuwa wametoka kwenye masomo ya Gileadi. Kwa kweli, walinitolea mazoezi ya muzuri kabisa ya kiteokrasi! Wakati fulani nilisindikiza Ndugu Finch katika safari ya kuenda kuhubiri kaskazini mwa Pakistan. Kwenye mwanzo wa milima mirefu yenye kufuatana, tulikutana na watu wengi wanyenyekevu wenye kuzungumuza luga ya Urdu wenye kuwa na kiu ya kweli ya Biblia. Kisha kupita miaka mbili, mimi pia nilialikwa kwenye Masomo ya Gileadi; nilirudia Pakistan kwenye nilifanya kazi ya muzunguko kwa wakati mbalimbali. Niliishi katika nyumba ya wamisionere katika Lahore pamoja na ndugu wengine watatu wenye walikuwa wamisionere.

KUPONA KISHA MAGUMU

Jambo la kuhuzunisha ni kwamba katika mwaka wa 1954, wamisionere wenye walikuwa katika Lahore walikuwa na magumu ya kuelewana, na hilo lilifanya biro ya tawi ibadilishe migawo. Kwa sababu nilikosa hekima kwa kuunga mukono upande mumoja katika mabishano hayo, nilipewa mashauri makali. Nilihuzunika sana na kujisikia kama nilikuwa nimeshindwa kabisa katika mambo ya kiroho. Nilihamia tena katika Karachi, na kisha nikahamia Londres, Uingereza, kwa sababu nilipenda kuanza upya utumishi wangu wa kiroho.

Katika Londres, kutaniko letu lilikuwa na watu wengi wa familia ya Beteli ya Londres. Pryce Hughes, mutumishi wa tawi mwenye kuhangaikia wengine, alinizoeza kwa upendo. Siku moja, aliniambia namna wakati fulani alipewa mashauri makali na ndugu Joseph Rutherford mwenye alikuwa anasimamia kazi ya kuhubiri katika dunia yote. Wakati Ndugu Hughes alijaribu kujitetea, Ndugu Rutherford alimukaripia kabisa. Nilishangaa kuona Ndugu Hughes anaonyesha sura ya kicheko wakati anakumbuka habari hiyo. Alisema kama jambo hilo lilimukasirisha kwanza. Lakini kisha alitambua kama alikuwa na lazima ya mashauri hayo makali na kwamba yalionyesha kama Yehova anamupenda. (Ebr. 12:6) Maneno yake yaligusa moyo wangu na kunisaidia nimutumikie tena Yehova kwa furaha.

Karibu na wakati huo, mama yangu alihamia Londres na alikubali kujifunza Biblia pamoja na John Barr, mwenye alifikia kutumikia katika Baraza Lenye Kuongoza. Alifanya maendeleo ya muzuri ya kiroho na akabatizwa katika mwaka wa 1957. Kisha nilifikia kujua kama mbele baba yangu akufe, yeye pia alijifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova.

Katika mwaka wa 1958, nilioa Lene, dada mwenye alitoka katika inchi ya Denmaki mwenye alikuwa anaishi Londres. Mwaka wenye ulifuata, tulipata baraka ya kumuzaa mutoto wetu mwanamuke, Jane, mutoto wa kwanza kati ya watoto wetu tano. Nilipewa pia mapendeleo ya utumishi katika Kutaniko Fulham. Lakini, kisha wakati fulani, kwa sababu ya matatizo ya afya ya Lene tulipaswa kuhamia mahali penye kuwa na joto zaidi. Kwa hiyo, katika mwaka wa 1967, tulihamia Adelaide, Australia.

MUSIBA WENYE KUVUNJA SANA MOYO

Katika kutaniko letu la Adelaide kulikuwa Wakristo watiwa mafuta 12 wenye kuzeeka. Walikuwa na bidii sana katika kazi ya kuhubiri. Bila kukawia, tulikuwa tena na programu ya muzuri ya kufanya mambo ya kiroho.

Katika mwaka wa 1979, Daniel, mutoto wetu wa tano alizaliwa. Alisumbuliwa sana na ugonjwa wenye kuitwa trisomie 21 * (ao Down Syndrome, ugonjwa wenye kufanya uwezo wa mutu wa kukomaa kimwili na kiakili ukuwe wa hali ya chini) na hatukutazamia kama ataishi muda murefu. Hata leo ni vigumu kwangu kueleza huzuni yenye tulisikia. Tulijikaza sana kuhangaikia mahitaji yake, bila kuzarau mahitaji ya watoto wetu wengine ine. Wakati fulani, kwa sababu ya shimo mbili zenye zilikuwa katika moyo wake, Daniel alikosa hewa ya kupumua, na rangi ya mwili wake ilikuwa inageuka na kuwa bleu; kwa hiyo, tulipaswa kumukimbizia kwenye hospitali. Lakini, hata kama alikuwa na afya ya mubaya, alikuwa na akili sana na alikuwa mwenye upendo. Alipenda pia Yehova sana. Wakati familia yetu ilikuwa inasali mbele ya kula chakula, alikuwa anaweka pamoja mikono yake ya kidogo, kuinamisha kichwa chake, na kusema kwa moyo wake wote “Amina!” Angekula chakula chake kisha tu kufanya hivyo.

Wakati Daniel alikuwa na miaka ine, alipatwa na ugonjwa mubaya sana wenye kuitwa lukemia (ugonjwa hatari wa kansere ya damu wenye kuharibu chembe za nyeupe za damu). Mimi na Lene tulikuwa tumechoka sana kimwili na moyoni. Nilijisikia kama kichwa changu kitapasuka. Lakini siku moja wakati tulikuwa tumevunjika moyo sana, mwangalizi wetu wa muzunguko Neville Bromwich, aligonga kwenye mulango wetu. Usiku huo, alitukumbatia kwa machozi. Sisi wote tulilia. Maneno yake yenye upendo na huruma yalitufariji sana. Aliondoka karibu saa saba ya usiku. Muda mufupi kisha hapo Daniel alikufa. Kifo chake lilikuwa jambo lenye kuhuzunisha zaidi katika maisha yetu. Hata hivyo, tulivumilia huzuni yetu, na tuko hakika kama hakuna kitu chenye kinaweza kumutenganisha Daniel na upendo wa Yehova, hata kifo hakiwezi. (Rom. 8:38, 39) Tunangojea kwa hamu kuwa pamoja naye wakati atafufuliwa katika ulimwengu mupya wa Mungu!​—Yoh. 5:28, 29.

KUSAIDIA WENGINE KUNANILETEA FURAHA

Leo, kisha kupona mara mbili ugonjwa mubaya wa kupooza, ninaendelea kuwa muzee wa kutaniko. Mambo yenye yamenifikia katika maisha, yamenichochea nikuwe mwenye kujitia pa nafasi ya wengine na kuwaonyesha huruma, zaidi sana wale wenye kupambana na magumu. Ninajikaza kuepuka kuwahukumu. Lakini, ninajiuliza hivi: ‘Namna gani mambo yenye wamejionea katika maisha yamechochea namna yao ya kujisikia katika moyo ao namna ya kufikiri? Namna gani ninaweza kuwaonyesha kama ninawahangaikia? Namna gani ninaweza kuwatia moyo wafanye mapenzi ya Yehova?’ Kwa kweli, ninapenda kutembelea ndugu na dada katika kutaniko ili kuwatia moyo kiroho! Wakati ninatia moyo wengine na kuwasaidia kiroho, ninajisikia kama ninajifariji na kujisaidia mimi mwenyewe.

Ninaendelea kupata furaha wakati ninatembelea ndugu na dada ili kuwatia moyo kiroho

Ninajisikia kama muandikaji mumoja wa zaburi mwenye alisema hivi: ‘Fikira zangu zinazofazaisha zilipokuwa nyingi ndani yangu, faraja zako [Yehova] mwenyewe zilianza kuikumbatia nafsi yangu.’ (Zab. 94:19) Amenitegemeza wakati wa matatizo ya familia, upinzani wa dini, na wakati wa kuvunjika moyo, na kushuka moyo. Kwa kweli, Yehova amekuwa Baba wa kweli kwangu!

^ fu. 19 Mwanzoni, Pakistan ilifanyizwa na Pakistan ya Mangaribi (yenye kuitwa leo Pakistan) na Pakistan ya Mashariki (yenye kuitwa leo Bangladesh).

^ fu. 29 Ona habari yenye kichwa “Kulea Mtoto Aliye na Down Syndrome​—Kazi Ngumu Inayothawabisha,” katika Amuka! ya Mwezi wa 6, 2011.