Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Salamu Iko na Nguvu Nyingi

Salamu Iko na Nguvu Nyingi

“JAMBO! Habari gani?”

Kwa kweli, umetumia salamu kama hiyo mara nyingi. Pengine hata ulipatia mutu mukono wakati ulimusalimia. Desturi na maneno vinaweza kuwa tofauti kulingana na mahali, lakini salamu inatimiza jambo lilelile la musingi. Kwa kweli, ikiwa tunakosa kusalimia wengine ao kujibia wakati wengine wanatusalimia, wanaweza kuona kama hatuna upendo ao hatuna adabu.

Lakini, haiko watu wote ndio wanajisikia huru kusalimia wengine. Watu fulani wanasita kusalimia wengine kwa sababu ya haya ao kwa sababu wanajiona kuwa hawana maana. Wengine wanaona kuwa ni vigumu kusalimia watu wenye kutoka mahali pengine, wa desturi ingine, ao wenye kuwa tofauti nao katika mambo mbalimbali. Lakini, hata salamu ya mufupi inaweza kuwa na matokeo ya muzuri sana.

Ujiulize hivi: ‘Kusalimia wengine kunaweza kuwa na matokeo gani? Na neno la Mungu linaweza kunifundisha nini juu ya salamu?’

SALIMIA “WATU WA NAMNA ZOTE”

Petro alisema hivi wakati alikaribisha katika kutaniko la Kikristo, Kornelio, mutu wa kwanza wa Mataifa: “Mungu hana ubaguzi.” (Mdo. 10:34) Kisha, Petro aliandika kama Mungu ‘anataka wote wafikie toba.’ (2 Pet. 3:9) Tunaweza kwanza kutumia maandiko hayo juu ya watu wenye wanajifunza Biblia. Lakini Petro alishauria pia Wakristo hivi: ‘Muheshimu watu wa namna zote, mupende ushirika muzima wa akina ndugu.’ (1 Pet. 2:17) Kwa hiyo, ni muzuri tusalimie wengine hata kama wanatoka wapi, ni wa desturi gani ao wako na maisha ya namna gani. Hiyo inaweza kuwa njia moja ya kuwaonyesha heshima na upendo.

Mutume Paulo alishauri hivi wale wenye kuwa katika kutaniko: ‘Mukaribishane, kama vile Kristo pia alivyowakaribisha ninyi.’ (Rom. 15:7) Paulo alitaja moja kwa moja ndugu wenye walikuwa ‘musaada wenye kutia nguvu’ kwake. Tunapaswa kufanya hivyo zaidi sana juu ya ndugu na dada zetu leo wenye wako na lazima ya kutiwa moyo wakati huu wenye Shetani anaendelea kushambulia zaidi watu wa Mungu.​—Kol. 4:11; Ufu. 12:12, 17.

Mifano yenye kuwa katika Maandiko inaonyesha kama zaidi ya kufanya mutu ajisikie kuwa amekaribishwa, salamu inaweza kutimiza mambo mengi zaidi.

FAIDA YA SALAMU

Wakati Yehova alitaka kuhamishia uzima wa Mwana wake katika tumbo la uzazi la Maria, alituma malaika azungumuze na Maria. Malaika alianza kwa kusema hivi: “Siku njema [ao, salamu], uliyependelewa sana, Yehova yuko pamoja nawe.” Maria ‘alishitushwa sana,’ kwa sababu hakujua sababu gani malaika alikuwa anazungumuza naye. Malaika aliona jambo hilo, na akamuambia hivi: “Usiogope, Maria, kwa maana umepata kibali cha Mungu.” Alimufasiria kama kusudi la Mungu lilikuwa azae Masiya. Kuliko kuendelea kuwa na wasiwasi, Maria alijibia hivi kwa utiifu: “Tazama! Kijakazi wa Yehova! Na itendeke kwangu kulingana na tangazo lako.”​—Lu. 1:26-38.

Ilikuwa pendeleo kubwa kwa malaika huyo kupeleka ujumbe wa Yehova; lakini hakuona kama ilikuwa kujishusha ao kujishushia heshima kuzungumuza na mwanadamu mwenye hakamilike. Alimusalimia kwanza. Mufano wake unaweza kutufundisha nini? Tunapaswa kuwa tayari kusalimia wengine na kuwatia moyo. Kwa kutumia maneno madogo tu, tunaweza kusaidia wengine na kuwafanya wakuwe hakika kama wako kabisa sehemu ya watu wa Yehova.

Paulo alifikia kujua ndugu na dada wengi katika makutaniko ya Asia Ndogo na Ulaya. Barua zake ziko na salamu nyingi zenye alitumia watu kipekee. Tunaona jambo hilo kwenye Waroma sura ya 16. Paulo alituma salamu kwa Wakristo wenzake wengi. Alimutaja Fibi, “dada yetu,” na kuomba ndugu ‘wamukaribishe katika Bwana kwa njia inayowastahili watakatifu, na kwamba wamusaidie katika jambo lolote ambalo huenda [pengine] akahitaji.’ Paulo alisalimia Priska na Akila, “ambao si mimi tu bali pia makutaniko yote ya mataifa yanawashukuru.” Alisalimia ndugu na dada fulani wenye hawajulikane sana leo kama vile ‘Epaineto mupendwa wangu’ na “Trifaina na Trifosa, wanawake wanaofanya kazi kwa bidii katika Bwana.” Ndiyo, Paulo, alikuwa tayari kusalimia ndugu na dada zake.​—Rom. 16:1-16.

Wazia furaha yenye walikuwa nayo ya kujua kama Paulo aliwakumbuka kwa upendo. Kwa kweli, upendo wao kwa Paulo na kati yao uliongezeka! Na bila shaka kusikia salamu hizo zenye upendo kulitia moyo Wakristo wengine, na kuwasaidia waendelee kuwa na imani yenye nguvu. Kwa kweli, salamu zenye kuonyesha kama tunahangaikia kabisa wengine na kuwapongeza zinatia urafiki nguvu na zinaunganisha watumishi washikamanifu wa Mungu.

Wakati Paulo alifika Puteoli kwenye mashua ilizoea kusimama, na kuanza safari ya kuenda Roma, Wakristo wa eneo hilo walitoka kusini ili kukutana naye. Wakati tu Paulo aliwaona kwa mbali, ‘akamushukuru Mungu na kujipa moyo.’ (Mdo. 28:13-15) Wakati fulani, tunaweza tu kuonyesha mutu sura ya kicheko ao kumupepea ili kumusalimia. Lakini, hata kufanya hivyo kunaweza kutia moyo mutu mwenye pengine amevunjika moyo ao mwenye kuwa na huzuni.

KUELEWANA NA WENGINE

Mwanafunzi Yakobo alipaswa kutolea Wakristo fulani mashauri makali. Wakristo fulani walikuwa wazinifu kiroho kwa kufanya urafiki pamoja na ulimwengu. (Yak. 4:4) Lakini, ona namna Yakobo alianza barua yake:

‘Yakobo, mutumwa wa Mungu na wa Bwana Yesu Kristo, kwa makabila kumi na mawili yaliyotawanyika huku na huku: Salamu!’ (Yak. 1:1) Bila shaka ilikuwa mwepesi kwa wale wenye walisoma barua hiyo kukubali mashauri yake wakati waliona kupitia salamu yake kama wote walikuwa sawa mbele za Mungu. Kwa kweli, salamu yenye unyenyekevu inaweza kufanya ikuwe mwepesi kuzungumuza, hata kuzungumuzia mambo mazito.

Ili salamu ikuwe na matokeo ya muzuri, hata kama ni fupi, inapaswa kutoka katika moyo na kuonyesha upendo wa kweli. Ni hivyo hata kama inaonekana kuwa mutu mwenye tulisalimia hasikie. (Mt. 22:39) Siku fulani dada mumoja katika Irelandi alifika kwenye Jumba la Ufalme wakati tu mikutano ilikaribia kuanza. Wakati alikuwa anaingia haraka, ndugu mumoja aligeuka, akamuonyesha sura ya kicheko, na akamuambia hivi: “Jambo. Nafurahi kukuona.” Dada huyo alikaa tu.

Majuma fulani kisha hapo, alikaribia ndugu huyo na kumuambia kama kwa wakati fulani nyumbani, alikuwa anapambana na hali fulani yenye kuleta mahangaiko. Alisema hivi: “Nilikuwa ninahuzunika sana mangaribi hiyo, na nilikuwa hata karibu kuacha kufika kwenye Jumba la Ufalme. Sikumbuke mambo mengi yenye yalifundishwa kwenye mikutano, ninakumbuka tu salamu yako. Ilifanya nijisikie kuwa ninakaribishwa kabisa. Aksanti.”

Ndugu huyo hakujua namna salamu yake ya mufupi iligusa sana moyo wa dada huyo. Anasema hivi: “Wakati aliniambia namna maneno hayo mafupi yalimutia moyo, nilifurahi sana kwa sababu nilijikaza kumusalimia. Hilo lilifanya nijisikie pia muzuri.”

Sulemani aliandika hivi: ‘Tupa mukate wako juu ya uso wa maji, kwa maana baada ya siku nyingi utaupata tena.’ (Mhu. 11:1) Wakati tunajua faida ya salamu zetu, zaidi sana kwa Wakristo wenzetu tunasaidia wengine wakuwe na furaha, na sisi pia tunakuwa na furaha. Kwa hiyo, tusizarau nguvu ya salamu.