Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI YA KUJIFUNZA YA 26

Saidia Wengine Wapiganishe Mahangaiko

Saidia Wengine Wapiganishe Mahangaiko

“Ninyi wote mukuwe na umoja wa akili, mujitie pa nafasi ya wengine, mukuwe na upendo wa kindugu, huruma yenye upole, na unyenyekevu.”​—1 PE. 3:8.

WIMBO 107 Mungu​—Kielelezo cha Upendo

KIFUPI CHA HABARI *

1. Namna gani tunaweza kumuiga Yehova, Baba yetu mwenye upendo?

YEHOVA anatupenda sana. (Yoh. 3:16) Tunapenda kumuiga Baba yetu mwenye upendo. Kwa hiyo, tunajikaza ‘kujitia pa nafasi ya wengine, kuwa na upendo wa kindugu, [na] huruma yenye upole’ kwa watu wote lakini zaidi sana kwa wale wenye kuwa “wa jamaa yetu katika imani.” (1 Pe. 3:8; Gal. 6:10) Wakati watu wa familia yetu ya kiroho wanapiganisha magumu yenye kuleta mahangaiko, tunapenda kuwasaidia.

2. Tutazungumuzia nini katika habari hii?

2 Watu wote wenye wanapenda kuwa mu familia ya Yehova watapatwa na hali zenye kuleta mahangaiko. (Mk. 10:29, 30) Inawezekana kabisa kuwa tutapata magumu mingi zaidi kadiri tunaendelea kukaribia mwisho wa ulimwengu huu. Namna gani tunaweza kusaidiana? Tuzungumuzie basi mambo yenye tunaweza kujifunza kupitia habari zenye Biblia inazungumuzia juu ya Loti, Yobu, na Naomi. Tutazungumuzia pia magumu yenye ndugu na dada zetu wako wanapata leo na tutaona namna tunaweza kuwasaidia wapiganishe ile magumu.

TUONYESHE UVUMILIVU

3. Kulingana na 2 Petro 2:7, 8, Loti alikamata uamuzi gani mubaya, na uamuzi huo ulimuletea matokeo gani?

3 Loti alikamata uamuzi mubaya wakati aliamua kuishi kati ya watu wa muji wa Sodoma wenye walikuwa na mwenendo muchafu sana. (Soma 2 Petro 2:7, 8.) Eneo hilo lilikuwa na utajiri, lakini Loti alipata magumu mingi kwa sababu alihamia Sodoma. (Mwa. 13:8-13; 14:12) Inawezekana bibi yake alipenda sana muji huo ao watu fulani wa muji huo na hilo lilifanya akose kumutii Yehova. Alipoteza uzima wake wakati Mungu alifanya mvua ya moto na kiberiti inyeshe juu ya muji huo. Fikiria pia watoto wanamuke wawili wa Loti. Walikuwa wanachumbiwa na wanaume wenye walikufa katika Sodoma. Loti alipoteza nyumba yake, mali yake, na jambo la kuhuzunisha zaidi, alipoteza bibi yake. (Mwa. 19:12-14, 17, 26) Wakati huo wa mahangaiko, je, Yehova aliacha kumuonyesha Loti uvumilivu? Hapana.

Kwa huruma, Yehova alituma malaika ili wamuokoe Loti na familia yake (Picha hii inapatana na fungu la 4)

4. Namna gani Yehova alimuonyesha Loti uvumilivu? (Ona picha ku jalada ya gazeti hili.)

4 Hata kama Loti aliamua kuishi mu muji wa Sodoma, kwa huruma Yehova alituma malaika ili wamuokoe yeye na familia yake. Lakini, Loti “aliendelea kukawia” kuliko kutii palepale amri yenye malaika walimutolea ya kutoka haraka mu muji wa Sodoma. Malaika walilazimika kumukamata mukono na kumusaidia yeye na familia yake wakimbie kutoka mu muji huo. (Mwa. 19:15, 16) Kisha malaika wakamuambia akimbilie katika eneo la milima. Lakini, kuliko kumutii Yehova, Loti aliomba ikiwa angeweza kuenda mu muji wenye ulikuwa karibu. (Mwa. 19:17-20) Yehova alimusikiliza Loti kwa uvumilivu na alimuruhusu aende mu muji huo. Kisha wakati fulani, Loti aliogopa kuishi kule na akahamia katika eneo la milima, kule kwenye Yehova alimuambiaka kwanza aende. (Mwa. 19:30) Yehova alimuonyesha Loti uvumilivu kabisa! Namna gani tunaweza kumuiga?

5-6. Namna gani tunaweza kutumia shauri lenye kuwa katika 1 Watesalonike 5:14 ili kumuiga Mungu?

5 Kama Loti, mutu fulani wa familia yetu ya kiroho anaweza kukamata maamuzi ya mubaya na kujiletea matatizo makubwa. Kama jambo hilo linatokea, tutafanya nini? Tunaweza kushawishiwa kumuambia kama anavuna kile chenye alipanda, na ile inaweza kuwa kweli. (Gal. 6:7) Lakini, tunaweza kufanya jambo la muzuri zaidi. Tunaweza kuiga namna Yehova alimusaidia Loti. Namna gani?

6 Yehova alituma malaika ili wamuonye Loti lakini pia ili wamusaidie aokoke uharibifu juu ya muji wa Sodoma. Na sisi, tunaweza kulazimika kumuonya ndugu ao dada yetu wakati tunaona kama iko anafanya jambo fulani lenye linaweza kumuletea magumu. Lakini tunaweza pia kumusaidia. Hata kama hatumie haraka mashauri yenye kutegemea Biblia yenye tunamutolea, tunapaswa kumuonyesha uvumilivu. Tufanye kama wale malaika wawili. Kuliko kuchoka na kumuacha ndugu ao dada yetu, tunapaswa kutafuta njia za kumusaidia. (1 Yo. 3:18) Tunaweza kumukamata mukono kwa njia ya mufano, na kumusaidia atumie mashauri ya muzuri yenye tulimutolea.​—Soma 1 Watesalonike 5:14.

7. Namna gani tunaweza kuiga namna Yehova alimuona Loti?

7 Yehova angekazia akili uzaifu wa Loti. Lakini hakufanya vile. Kisha wakati fulani, alimuongoza Petro kupitia roho yake azungumuzie Loti kuwa mutu mwenye haki. Tuko wenye furaha sana kwa sababu Yehova hakazie akili makosa yetu! (Zb. 130:3) Tunaweza kuiga namna Yehova alimuona Loti? Kama tunakazia akili sifa za muzuri za ndugu na dada zetu, tutawaonyesha uvumilivu zaidi. Kama tunafanya vile, watakuwa tayari zaidi kukubali musaada wenye tunawatolea.

TUONYESHE HURUMA

8. Sifa ya huruma itatuchochea kufanya nini?

8 Loti aliteseka kwa sababu ya uamuzi mubaya wenye alikamata, lakini Yobu hakuteseka kwa sababu alikamata uamuzi fulani mubaya. Hata hivyo, alipata matatizo makubwa: alipoteza vitu vyake vyote, cheo chake katika eneo, na afya yake iliharibika sana. Jambo la mubaya zaidi, yeye na bibi yake walifiwa na watoto wao wote. Pia, marafiki wake tatu wa uongo walimushitaki. Wale wafariji tatu wa uongo wa Yobu hawakumuonyesha huruma, sababu moja ni gani? Hawakujaribu kuelewa muzuri hali yake. Kwa hiyo, walimuwazia mubaya na wakamuhukumu kwa ukali. Tunaweza kufanya nini ili tusifanye kosa kama hilo? Ukumbuke kama Yehova tu njo mwenye anajua mambo yote juu ya hali ya mutu. Usikilize kwa uangalifu mambo yenye mutu mwenye kuteseka anasema. Usisikilize maneno tu; ujaribu pia kusikia maumivu yake. Kama unafanya vile, utaweza kuonyesha sifa ya kweli ya kujitia pa nafasi ya ndugu ao dada yako.

9. Sifa ya huruma itatuzuia kufanya nini, na juu ya nini?

9 Sifa ya huruma itatuzuia kueneza habari zenye kuumiza juu ya magumu yenye wengine wako wanapiganisha. Mutu mwenye kueneza habari zenye kuumiza juu ya wengine hajenge kutaniko, lakini anabomoa kutaniko. (Mez. 20:19; Ro. 14:19) Mutu kama huyo hana upendo lakini anasema-sema bila kufikiri, na maneno yake inaweza kuumiza zaidi mutu mwenye iko anateseka. (Mez. 12:18; Efe. 4:31, 32) Ni muzuri zaidi wakati tunaona sifa za muzuri za mutu na kufikiria namna tunaweza kumusaidia apiganishe magumu yake!

Usikilize kwa uvumilivu wakati Mukristo mwenzako anaanza kuwa na “mazungumuzo ya ovyoovyo,” na useme maneno ya kufariji kwa wakati wenye kufaa (Picha hizi zinapatana na fungu la 10-11) *

10. Maneno ya andiko la Yobu 6:2, 3 inatufundisha nini?

10 Soma Yobu 6:2, 3. Wakati fulani, Yobu alianza kuwa na “mazungumuzo ya ovyoovyo.” Lakini kisha, aliitika kama maneno fulani yenye alikuwa amesema ilikuwa ya mubaya. (Yob. 42:6) Kama vile Yobu, leo mutu mwenye anavumilia magumu yenye kuleta mahangaiko, anaweza kuanza kuwa na mazungumuzo ya ovyoovyo, na kusema mambo yenye atahuzunikia kisha. Tunapaswa kutenda namna gani? Kuliko kumuchambua-chambua, tunapaswa kumuonyesha huruma. Tukumbuke kama Yehova hakukusudia hata mumoja wetu apate magumu na mahangaiko yenye tuko nayo leo. Kwa hiyo, hatuwezi kushangaa wakati mutumishi muaminifu wa Yehova anasema mambo bila kufikiri wakati anavumilia mahangaiko makali. Hata kama anasema mambo yenye haifae juu ya Yehova ao juu yetu, hatupaswe kumukasirikia haraka ao kumuhukumu kwa sababu alisema ile maneno.​—Mez. 19:11.

11. Namna gani wazee wanaweza kumuiga Elihu wakati wanatoa mashauri?

11 Wakati fulani, mutu mwenye iko anapiganisha magumu fulani yenye kuleta mahangaiko anaweza kuwa na lazima ya kupewa mashauri fulani ao nizamu ya kumusaidia. (Gal. 6:1) Wazee wanaweza kufanya vile namna gani? Wanapaswa kumuiga Elihu, mwenye alimusikiliza Yobu kwa huruma sana. (Yob. 33:6, 7) Elihu alimutolea Yobu mashauri kisha tu kuelewa mawazo yake. Wazee wenye wanafuata mufano wa Elihu, wanapaswa kumusikiliza mutu kwa uangalifu na kujaribu kuelewa hali yake. Kisha, wakati wanatoa mashauri, inawezekana kabisa kuwa wanaweza kugusa moyo wa musikilizaji wao.

TUSEME KWA NAMNA YENYE KUFARIJI

12. Kisha kufiwa na bwana yake na watoto wake wawili wanaume, Naomi alijisikia namna gani?

12 Naomi alikuwa mwanamuke mushikamanifu mwenye alimupenda Yehova. Lakini, kisha kufiwa na bwana yake na watoto wake wawili wanaume, alipenda kubadilisha jina lake la Naomi likuwe “Mara,” maana yake “Uchungu.” (Rut. 1:3, 5, 20, maelezo ya chini, 21) Rutu, binti-mukwe wa Naomi alishikamana naye katika magumu yake yote. Rutu hakumutolea tu Naomi musaada, lakini alisema naye kwa namna yenye kufariji. Alimuonyesha Naomi upendo na alimutegemeza kwa kutumia maneno ya mwepesi na yenye kutoka mu moyo.​—Rut. 1:16, 17.

13. Juu ya nini wale wenye wamefiwa na bibi ao bwana yao wako na lazima tuwategemeze?

13 Wakati mutu fulani wa familia yetu ya kiroho anafiwa na bibi ao bwana yake, iko na lazima tumutegemeze. Bibi na bwana wanaweza kufananishwa na miti mbili yenye imekomalia pamoja. Kisha miaka fulani, mizizi ya miti hiyo inaingiana-ingiana. Wakati muti moja unaongolewa na kufa, ule mwingine unaweza kupatwa na matokeo ya mubaya sana. Vilevile, wakati mutu fulani anafiwa na bibi ao bwana yake, anaweza kuwa na huzuni mingi kwa wakati murefu. Paula, * mwenye bwana yake alikufa kwa kushitukia, anasema hivi: “Maisha yangu ilibadilika kabisa, na nilijisikia kuwa ninaishiwa. Nilipoteza rafiki yangu wa muzuri zaidi. Nilikuwa ninazungumuza na bwana yangu juu ya kila kitu. Wakati nilikuwa na furaha, naye alikuwa na furaha na alinitegemeza wakati wa magumu. Alikuwa ananisikiliza wakati nilikuwa ninamuambia mambo yenye ilinihangaisha. Kwa kweli, nilijisikia kama vile dunia inanigeukia.”

Tunaweza kufanya nini ili kutegemeza wale wenye wamefiwa na bibi ao bwana yao? (Picha hii inapatana na fungu la 14-15) *

14-15. Tunaweza kufanya nini ili kufariji mutu fulani mwenye amefiwa na bibi ao bwana yake?

14 Tunaweza kufanya nini ili kufariji mutu fulani mwenye amefiwa na bibi ao bwana yake? Jambo la kwanza lenye tunaweza kufanya ni kuzungumuza naye, hata kama tunaweza kuwa na wasiwasi ao hata kama hatujue tuseme nini. Paula, mwenye tumekwisha kutaja, anasema hivi: “Ninaelewa kama watu hawapendake kuzungumuza juu ya kifo. Wanaogopa kwamba wanaweza kusema jambo fulani lenye litakwaza wengine. Lakini, jambo la mubaya zaidi ni kukosa kusema jambo lolote.” Mutu mwenye alifiwa hatutazamie tuseme jambo fulani la hekima. Paula anasema hivi: “Nilifurahi wakati marafiki walikuwa wanasema tu, ‘Pole sana juu ya jambo lenye lilikufikia.’”

15 William, mwenye bibi yake alikufa miaka fulani yenye imepita, anasema hivi: “Ninafurahi wakati wengine wananielezea mambo ya muzuri yenye wanakumbuka juu ya bibi yangu; hilo linanihakikishia kama walikuwa wanamupenda na kumuheshimia. Kunitegemeza katika njia hiyo kunanisaidia sana. Maneno yao inanifariji sana, kwa sababu bibi yangu alikuwa wa samani sana kwangu na alikuwa mutu wa maana katika maisha yangu.” Mujane mumoja mwenye kuitwa Bianca anasema hivi: “Ninafarijiwa wakati wengine wanasali pamoja na mimi na kunisomea andiko moja ao maandiko mbili. Ninajisikia muzuri wakati wanazungumuza juu ya bwana yangu na wakati wananisikiliza nikizungumuza juu yake.”

16. (a) Juu ya nini tunapaswa kuendelea kutegemeza mutu fulani mwenye amefiwa na mupendwa wake? (b) Kulingana na Yakobo 1:27, tuko na daraka gani?

16 Kama vile Rutu alishikamana na mujane Naomi, tunapaswa kuendelea kufariji watu wenye wamefiwa na wapendwa wao. Paula, mwenye tumekwisha kutaja, anasema hivi: “Kisha tu kifo cha bwana yangu, watu walinitegemeza sana. Lakini, kisha wakati fulani, walirudilia maisha yao ya kawaida. Hata hivyo, maisha yangu ilikuwa imebadilika kabisa. Inasaidia sana wakati wengine wanatambua kama mutu mwenye alifiwa iko na lazima ya kutegemezwa kwa miezi ao hata miaka mingi kisha kufiwa.” Kwa kweli, watu hawajisikie namna moja. Watu fulani wanaonekana kuwa wanajipatanisha haraka na hali zao za mupya. Lakini, wengine wanasikia huzuni kila wakati wanafanya jambo fulani lenye walikuwa wanafanya pamoja na bibi ao bwana yao. Kila mutu iko na namna yake ya kuonyesha huzuni. Tukumbuke basi kama Yehova anatupatia pendeleo na daraka la kuhangaikia wale wenye wamefiwa na bibi ao bwana yao.​—Soma Yakobo 1:27.

17. Juu ya nini wale wenye wameachwa na bibi ao bwana zao wako na lazima tuwategemeze?

17 Bibi ao bwana fulani wanapaswa kupiganisha huzuni mingi na mahangaiko ya mingi yenye wanapata wakati bibi ao bwana zao wanawaacha. Joyce, mwenye bwana yake aliacha na kuoa bibi mwingine, anasema hivi: “Maumivu yenye nilisikia kwa sababu ndoa yangu ilivunjika ilikuwa ya mubaya zaidi kupita maumivu yenye ningesikia ikiwa bwana yangu angekufa. Kama angekufa katika aksidenti ao kwa sababu ya ugonjwa fulani, hilo lingekuwa jambo fulani lenye hakuchagua yeye mwenyewe. Lakini katika hali hii, bwana yangu aliamua kuniacha. Nilijisikia kuwa nilishushiwa heshima na kuzarauliwa.”

18. Tunaweza kufanya nini ili kusaidia wale wenye hawana tena bibi ao bwana?

18 Wakati tunafanyia wale wenye hawana tena bibi ao bwana mambo fulani ya kidogo-kidogo ya wema, tunawaonyesha kama tunawapenda kabisa. Kwa sababu sasa wamebakia peke yao, wako na lazima ya marafiki wazuri. (Mez. 17:17) Unaweza kufanya nini ili ujionyeshe kuwa rafiki yao? Unaweza kuwaalika ili mukule chakula pamoja. Na unaweza kuwaomba mupitishe wakati pamoja katika jambo fulani la kujifurahisha ao katika mahubiri. Unaweza pia kuwaomba wakuje ku ibada yenu ya familia wakati fulani. Kama unafanya vile, utamufurahisha Yehova, kwa sababu iko “karibu na wale wenye kuvunjika moyo” na iko “mulinzi wa wajane.”​—Zb. 34:18; 68:5.

19. Andiko la 1 Petro 3:8 linatuomba tufanye nini?

19 Hivi karibuni, wakati Ufalme wa Mungu utatawala dunia, tutasahau mateso yote. Tunangojea kwa hamu sana wakati wenye “mambo ya zamani hayatakumbukwa, wala hayataingia katika moyo.” (Isa. 65:16, 17) Mbele wakati huo ufike, tutegemezane basi na tuonyeshe kupitia maneno na matendo yetu kama tunapenda watu wote katika familia yetu ya kiroho.​—Soma 1 Petro 3:8.

WIMBO 111 Sababu za Kuwa na Shangwe

^ fu. 5 Loti, Yobu, na Naomi walimutumikia Yehova kwa ushikamanifu, lakini walipaswa kuvumilia hali zenye kuleta mahangaiko katika maisha yao. Habari hii itazungumuzia mambo yenye mufano wao unaweza kutufundisha. Itazungumuzia pia juu ya nini ni jambo la maana tuonyeshe uvumilivu na huruma na kusema kwa namna yenye kufariji ndugu na dada zetu wakati wanapata magumu.

^ fu. 13 Majina imebadilishwa katika habari hii.

^ fu. 57 MAFASIRIO YA PICHA: Ndugu anakasirika sana na anaanza kuwa na “mazungumuzo ya ovyoovyo” wakati muzee mumoja anamusikiliza kwa uvumilivu. Kisha ndugu huyo kutulia, muzee anamutolea mashauri kwa upendo.

^ fu. 59 MAFASIRIO YA PICHA: Bibi na bwana wenye wangali vijana wanapitisha wakati pamoja na ndugu mwenye bibi yake amekufa hivi karibuni. Wanazungumuzia mambo yenye kufurahisha yenye wanakumbuka juu ya bibi huyo.