Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI YA KUJIFUNZA YA 25

Musikwaze “Hawa Wadogo”

Musikwaze “Hawa Wadogo”

“Musizarau mumoja wa hawa wadogo.”​—MT. 18:10.

Wimbo 113 Tuko Wenye Amani

KIFUPI CHA HABARI *

1. Ni kitu gani Yehova amefanyia kila mumoja wetu?

YEHOVA amemuvuta kila mumoja wetu kwake. (Yoh. 6:44) Waza kidogo juu ya ile. Yehova alichunguza kwa uangalifu kati ya mamiliare ya watu wenye kuishi mu dunia, na akakuona na akatambua kama uko na kitu fulani ya muzuri ndani yako​—aliona kama unamupenda. (1 Ny. 28:9) Yehova anakujua, anakuelewa na anakupenda. Ile inatia moyo sana, hauone vile?

2. Namna gani mufano wenye Yesu alileta unatusaidia kuona kama Yehova anahangaikia kila mumoja wetu?

2 Yehova anakuhangaikia sana na anahangaikia pia ndugu na dada zako. Juu ya kukusaidia uelewe ile jambo, kumbuka kama Yesu alilinganisha Yehova na muchungaji. Kama muchungaji iko na kondoo  100 na 1 anapotea, muchungaji atafanya nini? Ataacha ‘wale 99 kwenye milima na kuenda kutafuta ule mwenye alipotea.’ Na wakati muchungaji anapata ule kondoo, hatamukasirikia lakini atafurahi. Wazo ni nini hapa? Kila kondoo iko wa maana sana ku macho ya Yehova. Yesu alisema hivi: “Baba yangu mwenye kuwa mbinguni hapendi hata mumoja wa hawa wadogo aangamie.”​—Mt. 18:12-14.

3. Ni mambo gani tutazungumuzia mu hii habari?

3 Kusema kweli, hakuna mumoja kati yetu mwenye atapenda kuvunja moyo ndugu ao dada yake. Lakini, namna gani tunaweza kuepuka kukwaza wengine? Na tunaweza kufanya nini kama mutu fulani anatuumiza? Tutajibia ile maulizo mu hii Habari. Lakini, mbele ya yote tuzungumuzie kwanza “hawa wadogo” wenye wanazungumuziwa mu kitabu ya Matayo sura ya 18.

“HAWA WADOGO” NJO WA NANI?

4. “Hawa wadogo” njo wa nani?

4 “Hawa Wadogo” ni wanafunzi wa Yesu wenye kuwa na miaka mbalimbali. Ijapokuwa miaka yao, wote “wako kama watoto wadogo” juu wako tayari kufundishwa na Yesu. (Mt. 18:3) Hata kama wanatoka fasi mbalimbali, wako na desturi mbalimbali na wako na mawazo na utu mbalimbali, wote wanaonyesha imani katika Kristo. Na yeye, ni kusema Yesu, anawapenda sana, sana kabisa.​—Mt. 18:6; Yoh. 1:12.

5. Yehova anajisikiaka namna gani wakati mutu fulani anakwaza ao anaumiza mumoja kati ya watumishi wake?

5 “Hawa wadogo” wote wako wa maana sana ku macho ya Yehova. Juu tuelewe namna Yehova anajisikiaka, fikiria vile tunaonaka watoto. Tunawaonaka kuwa wa maana sana. Tunapendaka kulinda watoto juu hawana nguvu, uzoefu na hekima sawa ya watu wazima. Hatufurahiake kuona wakati mutu fulani anatendea mwingine mubaya na tunakasirikaka sana wakati ule mutu mwenye anatendewa mubaya ni mutoto. Vilevile, Yehova anapenda kutulinda. Hafurahi ao hata anakasirika, wakati mutu fulani anakwaza ao anaumiza mumoja kati ya watumishi Wake!​—Isa. 63:9; Mk. 9:42.

6. Kulingana na 1 Wakorinto 1:26-29, leo mu dunia, wanaona wanafunzi wa Yesu namna gani?

6 Ni mu njia gani ingine wanafunzi wa Yesu wako sawa “wadogo”? Mu dunia leo, nani njo watu wanaonaka kuwa mutu wa maana? Tajiri, mutu mwenye kujulikana sana, na mwenye iko na mamlaka. Lakini, leo watu wanaona wanafunzi wa Yesu kuwa watu wenye hawako wa maana, “wadogo” kabisa, watu wa bure-bure. (Soma 1 Wakorinto 1:26-29.) Lakini Yehova hawaone vile.

7. Yehova anapenda tukuwe na mawazo gani juu ya ndugu na dada zetu?

7 Yehova anapenda watumishi wake wote, ikuwe wamemutumikia kwa miaka mingi ao hapana. Ndugu na dada zetu wako wa maana sana ku macho ya Yehova; ni vile pia tunapaswa kuwaona. Kusudi yetu haiko tu kupenda ndugu fulani, lakini ni ‘kupenda ushirika muzima wa ndugu.’ (1 Pe. 2:17) Tunapaswa kuwa tayari kufanya yetu yote juu ya kuwalinda na kuwahangaikia. Wakituambia kama tulikwaza ao kuumiza mutu fulani, hatupaswe kufanya tu sawa vile hakuna kitu na kuwaza kama, naye anakwazikaka tu mbio-mbio bure. Asamehe tu na biishie pale. Pengine ni juu ya nini watu fulani wanakwazikaka? Pengine ni juu ya namna walikomala. Ndugu na dada fulani wanajilinganisha na wengine na wanajiona kuwa watu wa hali ya chini. Na wengine ni wapya mu tengenezo; hawajue muzuri namna ya kusamehe watu wengine wakati wanawakosea. Hata kama hali ni gani, tunapaswa tu kujikaza kurudisha amani. Zaidi ya ile, kama mara mingi mutu anakuwaka iko anakwazika-kwazika na wengine, anapaswa kutambua kama ile njo uzaifu wake na ni muzuri aifanyie mabadiliko. Anapaswa kufanya vile ili kuwa na amani ya akili na ili kuwa na uhusiano wa muzuri pamoja na ndugu na dada.

UONE WENGINE KUWA WAZURI ZAIDI

8. Mu wakati wa Yesu, watu walikuwa na mawazo gani na ile ilikuwa na matokeo gani juu ya wanafunzi wake?

8 Ni nini ilimuchochea Yesu azungumuze juu ya “hawa wadogo”? Ni juu wanafunzi wake walikuwa walishamuuliza hivi: “Kwa kweli, ni nani ndiye mukubwa zaidi katika Ufalme wa mbinguni?” (Mt. 18:1) Mu ile wakati, Wayahudi wengi waliona cheo kuwa ya maana sana. Mwanaume mumoja mwenye elimu anasema hivi: “Wanadamu waliishi na kufa juu tu ya kutafuta kupata utukufu, kujulikana, kukubaliwa na kuheshimiwa.”

9. Wanafunzi wa Yesu walipaswa kufanya nini?

9 Yesu alijua kama wanafunzi wake walipaswa kujikaza ili kupiganisha roho ya mashindano yenye ilikuwa ilishatia mizizi mu desturi ya Wayahudi. Aliwaambia hivi: “Lakini ule mwenye iko mukubwa zaidi kati yenu akuwe kama mudogo zaidi, na ule mwenye anaongoza akuwe kama mutu wa kuwatumikia.” (Lu. 22:26) Tunajiendesha kama “mudogo zaidi” wakati “tunaona wengine kuwa wazuri zaidi kuliko” siye. (Flp. 2:3) Kama tunaendelea kufanya vile, tutaepuka kukwaza wengine sana.

10. Ni shauri gani ya Paulo tunapaswa kutia mu akili?

10 Ndugu na dada zetu wote wako wazuri zaidi kuliko siye mu njia moja ao ingine. Haiko nguvu kuona ile wakati tunakazia sana sifa zao za muzuri. Tunapaswa kutia mu akili hii shauri yenye mutume mutume Paulo alipatia Wakorinto: “Ni nani mwenye anakufanya wewe kuwa tofauti na mwingine? Kwa kweli, uko na nini chenye haukupokea? Basi, kama kwa kweli ulikipokea, sababu gani unajisifu kama vile haukukipokea?” (1 Ko. 4:7) Tunapaswa kuwa waangalifu sana juu tusiangukie mu mutego wa kutaka wengine watusifu-sifu ao kuanza kuwaza kama siye tuko wazuri zaidi kuliko wengine. Kama ndugu anatoa hotuba ya muzuri sana ao dada ni fundi sana mu kuanzisha mafunzo ya Biblia anapaswa njo kuacha sifa imuendee Yehova, hapana yeye.

USAMEHE “KUTOKA MOYONI”

11. Mufano wa Yesu kuhusu mufalme na mutumwa wake unatufundisha nini?

11 Kisha Yesu kushauria wafuasi wake wasikwaze wengine, alitoa mufano wa mufalme na mutumwa. Mufalme alifuta deni kubwa la mutumwa wake, lenye ule mutumwa hangewezaka kulipa. Lakini kisha, uleule mutumwa alikatala kufuta deni kidogo lenye mutumwa mwenzake alipaswa kumulipa. Ku mwisho, mufalme akamutupa ule mutumwa mwenye hana huruma mu gereza. Tunajifunza nini hapa? Yesu alisema hivi: “Ni vile pia Baba yangu wa mbinguni atawatendea ninyi kama kila mumoja wenu hamusamehe ndugu yake kutoka moyoni.”​—Mt. 18:21-35.

12. Kama tunakatala kusamehe, namna gani tunaweza kuumiza wengine?

12 Matendo ya ule mutumwa haikumuumiza yeye peke tu, lakini pia wengine. Kwanza, aliumiza mutumwa mwenzake kwa kuagiza “atupwe katika gereza mupaka alipe deni lake.” Pili, aliumiza watumwa wengine wenye walikuwa wanaona mambo alifanya. Wakati “watumwa wenzake waliona jambo lenye lilitendeka, wakahuzunika sana.” Ni vile pia na siye leo. Matendo yetu inaweza kuumiza watu wengine. Kama mutu fulani anatukosea na siye tunakatala kumusamehe, ni nini itatokea? Kwanza, tutamuumiza sababu tutakuwa tumekatala kumusamehe, kuonyesha kama tunamupenda na kuonyesha kama tunamuona kuwa wa maana. Pili, tutafanya watu wengine mu kutaniko wakose furaha, juu wataona kama hatuishi kwa amani pamoja na ule mutu.

Utaweka kinyongo ao utasamehe kutoka ku moyo? (Ona fungu la 13-14) *

13. Mufano moja wa dada painia unakufundisha nini?

13 Siye na wengine tunapata faida wakati tuko tayari kusamehe ndugu na dada zetu. Dada mumoja painia mwenye tutaita Crystal alijionea ile. Kuko dada moja mu kutaniko mwenye alimukwazaka sana. Crystal anasema hivi: “ Wakati fulani maneno ya ule dada ilikuwa inanichoma sawa vile kisu. Sikupenda kuhubiri hata naye. Nilianza kupoteza bidii na furaha yangu.” Crystal aliwaza kama alikuwa na haki ya kukasirika. Hakumuwekea kinyongo dada yake ao kuanza kufikiria zaidi sana namna alikuwa anajisikia. Kuliko kufanya vile, kwa unyekevu wote, alitumikisha mashauri ya Biblia yenye kuwa mu habari yenye kichwa “Samehe Kutoka Moyoni” yenye kuwa mu Munara wa Mulinzi wa tarehe 15 Mwezi wa 10, 1999. Alimusamehe ule dada. Crystal anasema hivi: “Sasa naelewa kama siye wote tuko tunajikaza kuvala utu mupya na kama Yehova iko tayari kutusamehe kwa kupenda na anafanya vile kila siku. Nimejisikia sawa vile wamenitosha muzigo wenye nilikuwa nao ku mabega. Nimepata tena furaha yangu.”

14. Kulingana na Matayo 18:21, 22, inaonekana ni tatizo gani mutume Petro alikuwa nayo na jibu yenye Yesu alimupatia inakufundisha nini?

14 Tunapaswa kusamehe; ni muzuri kufanya vile. Lakini haiko mwepesi. Inawezekana wakati fulani mutume Petro alijisikia vile. (Soma Matayo 18:21, 22.) Sasa nini njo inaweza kukusaidia? Kwanza, ufikiri sana juu ya namna Yehova amekusamehe. (Mt. 18:32, 33) Hatustahili musamaha wake, lakini iko tayari kutusamehe. (Zb. 103:8-10) Tena tusisahau kama, “sisi pia tunalazimika kupendana.” Njo maana hatupaswe kusema kama tutasemehe kama tunapenda. Tunapaswa kusamehe ndugu na dada zetu. (1 Yo. 4:11) Pili, fikiria matokeo ya muzuri wakati unasamehe. Tunaweza kusaidia mutu mwenye alitukosea, tunaweza kutia nguvu umoja wa kutaniko, tunaweza kulinda urafiki wetu pamoja na Yehova, na tutatosha muzigo wenye tuko nao ku mabega yetu. (2 Ko. 2:7; Kol. 3:14) Tatu, sali kwa mwenye anatuomba tusamehe wengine. Usiruhusu Shetani aharibishe amani yenye tuko nayo pamoja na ndugu na dada zetu. (Efe. 4:26, 27) Juu tusiangukie mu mitego ya Shetani tuko na lazima ya Yehova.

USIKUWE HARAKA KUKWAZIKA

15. Kulingana na Wakolosai 3:13, unaweza kufanya nini kama matendo ya ndugu ao dada inakukwaza?

15 Tuseme nini kama Mukristo mwenzako anatenda mu njia yenye inakukwaza? Unapaswa kufanya nini? Fanya yako yote juu ulinde amani. Usali kwa Yehova na umuambie namna unajisikia. Umuombe Yehova amusaidia ule mutu mwenye alikukwaza na akusaidie uone sifa za muzuri za ule mutu​—ndiyo, sifa za muzuri zenye iko nazo na zenye Yehova anapenda kwa ule mutu. (Lu. 6:28) Kama hauwezi kusahau mambo yenye ndugu ao dada amekufanyia, fikiria namna unaweza kuongea naye. Haiko muzuri kuwaza kama ndugu yako ao dada yako anaweza kufurahia tu kukukwaza kwa kupenda, hapana! (Mt. 5:23, 24; 1 Ko. 13:7) Wakati unaenda kuongea naye uonyeshe kama unamutumainia na kama iko na nia ya muzuri. Sasa tuseme nini kama hapendi kufanya amani? ‘Uendelee kumuvumilia.’ (Soma Wakolosai 3:13.) Ya maana zaidi, epuka kumuwekea kinyongo ndugu yako, juu usiharibishe urafiki wako pamoja na Yehova. Usiache jambo yoyote ifanye ukwazike. Wakati unafanya vile, unaonyesha kama unamupenda Yehova zaidi kuliko kitu yoyote.​—Zb. 119:165.

16. Kila mumoja wetu iko na daraka gani?

16 Tunafurahi sana kuwa na pendeleo la kumutumikia Yehova kwa umoja kama “kundi moja” chini ya “muchungaji mumoja”! (Yoh. 10:16) Tunasoma hivi mu fungu la 8 sura ya 16 ya kitabu Tengenezo Yenye Kufanya Mapenzi ya Yehova: “Juu ile umoja iko nakuletea pia faida, uko na daraka ya kusaidia kulinda umoja yenyewe.” Njo maana, tunapaswa ‘kujikaza ili kuona ndugu na dada zetu vile Yehova anawaona.’ Ku macho ya Yehova siye wote tuko “wadogo” na wa maana sana. Njo vile na weye unaonaka ndugu na dada zako? Mambo yenye unafanya ili kuwasaidia na kuwahangaikia, Yehova anaiona kuwa ya maana sana.​—Mt. 10:42.

17. Tumeazimia kufanya nini?

17 Tunapenda ndugu na dada zetu. Njo maana ‘tunafanya nguvu yetu yote ili tusiweke kikwazo ao kizuizi mbele ya ndugu.’ (Ro. 14:13) Tunaona ndugu na dada zetu kuwa wazuri zaidi kuliko siye na tunapenda kuwasamehe kutoka ku moyo. Tusiache hata kidogo mambo yenye wengine wanafanya ifanye tujikwae. Kuliko kufanya vile, tufuatilie “mambo yenye yanafanya kukuwe amani na mambo ya kujengana mumoja na mwingine.”​—Ro. 14:19.

WIMBO 130 Tusameheane

^ fu. 5 Juu hatukamilike tunaweza kufanya ao kusema mambo yenye inaweza kukwaza ndugu na dada zetu. Tunaweza kufanya nini kama hali ya vile inatokea? Unajikazaka kurudisha amani? Unakuwaka tayari kusamehe? Ao unasemaka, kama anakwazika ile inamuangalia ye peke, hapana miye? Unakwazikaka mbio-mbio kama wengine wanafanya ao wanasema mambo yenye haikufurahishe? Ao unasemaka, vile tu njo miye nakuwaka? Ao unaelewaka kama ile njo uzaifu wako na kama unapaswa kubadilika?

^ fu. 53 MAFASIRIO YA PICHA: Dada mumoja anakasirikia dada mwingine wa mu kutaniko yao. Wale dada wawili wako wanaongea pamoja juu ya matatizo yao, kisha mambo inapita na wanaendelea kumutumikia Yehova kwa furaha.