Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI JUU YA MAISHA YA WATU

Nimefanya Yale Nilipaswa Kufanya

Nimefanya Yale Nilipaswa Kufanya

KWA zaidi ya miaka 30, Donald Ridley alitetea Mashahidi wa Yehova mbele ya tribinali mbalimbali. Alisaidia sana katika kutetea haki ya mugonjwa ya kukataa matunzo yenye kuomba damu. Alisaidia sana Mashahidi wapate ushindi mingi mbele ya Tribinali Kubwa mbalimbali mu Inchi ya Amerika. Marafiki wake walikuwa wanamuita Don. Alikuwa mwenye bidii ya kazi, munyenyekevu, na tayari kutumikia wengine.

Mu mwaka wa 2019, wanganga walivumbua kama Don alikuwa na ugonjwa fulani wa ubongo, wenye hauzoee kupata watu. Hali iliharibika haraka, na akakufa tarehe 16 Mwezi wa 8, 2019. Hii njo habari ya maisha yake.

Nilizaliwa mu mwaka wa 1954 katika Inchi ya Amerika, mu muji wa Saint Paul, wenye kuwa katika jimbo la Minnesota. Familia yetu ilikuwa ya Kikatoliki na tuliishi maisha ya kawaida. Niko wa pili katika familia ya watoto tano. Nilisomea ku masomo ya musingi ya Wakatoliki, na nilikuwa ninasaidia padri wakati wa ibada. Lakini, sikujua mambo mingi kuhusu Biblia. Hata kama niliamini kwamba kunapaswa kuwa Mungu mwenye aliumba vitu vyote, sikuwazia kama kanisa linaweza kunisaidia kabisa.

NINAVUMBUA KWELI

Nilianza kujifunza mambo ya sheria ku masomo yenye kuitwa William Mitchell College of Law. Mu mwaka wangu wa kwanza kule, Mashahidi wa Yehova walinitembelea. Sikukuwa na wakati wa kuzungumuza nao juu nilikuwa ninafua manguo, lakini kwa heshima wale bibi na bwana waliitika kuja kunitembelea wakati ingine. Wakati walirudia, niliwauliza maulizo mbili: “Juu ya nini watu wazuri hawana maisha ya muzuri kama vile watu wabaya?” na “Mutu anaweza kufanya nini juu akuwe na furaha?” Nilikubali kitabu Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele na Biblia Takatifu​—Tafsiri ya Ulimwengu Mupya, yenye ilikuwa na jalada la rangi ya majani. Nilikubali pia funzo la Biblia. Kusema kweli, ile ilinifungua macho. Nilifurahi sana kujua kama Ufalme wa Mungu ni serikali yenye itatawala dunia. Niliona wazi kama utawala wa kichoyo wa mwanadamu umeshindwa kabisa na umefanya dunia ijae mateso, maumivu, ukosefu wa haki, na misiba.

Niliamua kutoa maisha yangu kwa Yehova ku mwanzo wa mwaka wa 1982 na kisha nikabatizwa mu ile mwaka ku mukusanyiko wa wilaya wenye kichwa “Ukweli wa Ufalme,” wenye ulifanywa katika jumba fulani kubwa, lenye kuwa katika muji wa Saint Paul, katika jimbo la Minnesota. Juma lenye lilifuata, nilirudia katika jumba hilo ili kufanya mashindano kuhusu mambo ya sheria. Ku mwanzo wa Mwezi wa 10, nilipata habari kama niliweza ile mashindano, na ile ilifanya nikuwe sasa mwanasheria (avocat).

Ku mukusanyiko wenye kichwa “Ukweli wa Ufalme,” nilikutana na Mike Richardson, mwenye alikuwa Mwanabeteli kule Brooklyn. Aliniambia kama biro ya mambo ya sheria ilikuwa imeanzishwa ku makao makubwa. Nilikumbuka maneno ya ule towashi Mwetiopia, yenye kuwa katika Matendo 8:36 na nilijiuliza hivi, ‘Ni nini inanizuia nisiombe kutumika katika Biro ya Mambo ya Sheria?’ Kwa hiyo, nikajaza ombi la utumishi wa Beteli.

Wazazi wangu hawakufurahi vile nilifikia kuwa Shahidi wa Yehova. Baba alipenda kujua kama utumishi wa Beteli ungeniletea faida gani mu kazi yangu ya mwanasheria. Nilimuambia kama ningeanza kufanya kazi ya kujitolea. Na nilimuambia kama wangekuwa wananipatia dolare 75, yenye Wanabeteli walikuwa wanapewa kila mwezi ili kutimiza mahitaji yao.

Niliingia ku Beteli, kule Brooklyn, katika New York, mu mwaka wa 1984, kisha kumalizia kazi zenye nilikuwa ninafanya ku tribinali fulani. Nilipewa mugao wa kutumika katika Biro ya Mambo ya Sheria. Uzoefu wenye nilipata mu kazi yangu ya mwanasheria ulinitayarisha kwa ajili ya mugao wangu mupya wa utumishi.

KAZI YA KUTENGENEZA JUMBA LA STANLEY

Namna jumba la Stanley lilikuwa wakati liliuzwa

Jumba la Stanley lenye kuwa Jersey City, mu jimbo la New Jersey, liliuzwa mu Mwezi wa 11, 1983. Ndugu walipenda kutengeneza upya mambo ya umeme na mabomba (tuyaux). Wakati ndugu zetu walikutana na wakubwa wa eneo, waliwaambia kama walikuwa wanafikiria jumba la Stanley likuwe nafasi ya kufanyia mikusanyiko ya Mashahidi wa Yehova. Ile ilitokeza tatizo. Sheria kuhusu namna ya kujenga ilisema kama nafasi za ibada zilipaswa kujengwa tu katika eneo lenye watu wanakaa. Lakini jumba la Stanley lilikuwa katikati ya muji, mu eneo la kufanyia biashara. Kwa hiyo, wale wakubwa hawakutupatia ruhusa. Ndugu wakaomba ile mambo isikilizwe ku tribinali, lakini ombi lao lilikataliwa.

Katika juma langu la kwanza ku Beteli, tengenezo lilipeleka kesi yetu ku tribinali ya wilaya. Juu nilikuwa nimemaliza miaka mbili ya mazoezi ku tribinali ya wilaya ya Saint Paul, kule Minnesota, tayari nilikuwa mwenye kuzoea namna ya kushugulikia kesi za vile. Mumoja kati ya wale wenye walikuwa wanatutetea alionyesha kama jumba la Stanley lilikuwa limetumiwa kwa ajili ya matukio fulani, kama vile kuonyesha filme na pia miziki. Sasa, juu ya nini kufanyia mambo ya dini pale ilikuwa kuvunja sheria? Tribinali ilichunguza kesi yetu na ilifikia kusema kama wakubwa wa muji wa Jersey City hawakuheshimia haki yetu ya uhuru wa dini. Kwa hiyo, tribinali ililazimisha watupatie ruhusa zote zenye tuliomba, na pale nikaanza kuona namna Yehova alikuwa anabariki tengenezo lake kupitia mambo ya sheria ili kuendeleza kazi yake. Nilifurahi sana kuwa kati ya wale wenye walisaidia mu ile njia.

Ndugu walianza kazi kubwa ya kutengeneza, na tarehe 8 Mwezi wa 9, 1985, ni kusema, chini ya mwaka moja tu kisha ile kazi kuanza, wanafunzi wa masomo ya 79 ya Gileadi walipewa diplome zao mu Jumba la Mikusanyiko la Jersey City. Niliona kuwa ni pendeleo kubwa kutumika pamoja na biro yetu ya mambo ya sheria ili kusaidia kazi ya Ufalme isonge mbele. Na furaha yenye nilipata ilikuwa kubwa sana kupita yenye nilipata wakati nilikuwa ninafanya kazi ya mwanasheria mbele nikuje ku Beteli. Lakini, sikujua kama Yehova alikuwa ananitayarishia mambo ingine mingi ya muzuri.

KUTETEA HAKI YA MUGONJWA YA KUTUNZWA BILA KUTUMIA DAMU

Mu miaka ya 1980, wanganga na hospitali mingi hawakukuwa wanaheshimia haki ya Shahidi mwenye kukomaa ya kutunzwa bila kutumia dawa zenye zilitengenezwa na damu. Wanamuke wenye mimba walipata magumu, sababu mara mingi waamuzi walisema kama wale wanamuke hawakukuwa na haki ya kukataa kutiwa damu. Waamuzi walifikiri kama ikiwa mama angekataa kutiwa damu, yeye angekufa na mutoto angebakia bila mama.

Tarehe 29 Mwezi wa 12, 1988, Dada Denise Nicoleau alipoteza damu mingi kisha kuzaa mutoto wake mwanaume. Juu uzima wake ulikuwa mu hatari sana, munganga alipenda dada akubali kutiwa damu. Dada Nicoleau alikataa. Kesho yake asubui, wanganga walifanya yao yote ili waruhusiwe na tribinali kutia wagonjwa damu kama ni lazima. Bila hata kusikiliza ao kujulisha Dada Nicoleau ao bwana yake kuhusu ile jambo, muamuzi akaruhusu wanganga wakuwe wanatia wagonjwa damu.

Siku ya Tano, tarehe 30 Mwezi wa 12, wanganga wakamutia Dada Nicoleau damu hata kama bwana yake na watu wa familia wenye walikuwa pale walikataa. Mangaribi ya ile siku, watu wengi wa familia yake na muzee mumoja ao wawili walifungwa, sababu wanganga waliwashitaki kama walipenda kuwazuia wasimutie dada yetu damu. Siku ya Posho asubui, tarehe 31 Mwezi wa 12, vyombo vya habari vya New York na Long Island vilizungumuzia namna wale watu walifungwa.

Pamoja na Philip Brumley wakati tulikuwa vijana

Siku ya Kwanza asubui, nilizungumuza na Milton Mollen, muamuzi mukubwa wa tribinali. Nilimufasiria vile mambo ilikuwa, na nilimuonyesha kama muamuzi alitoa ruhusa ya kutia wagonjwa damu bila kuwasikiliza. Mollen aliomba niende kumuona ku biro yake kisha midi ili kuzungumuzia ile mambo na pia kuchunguza sheria zenye zinahusu ile hali. Ndugu Philip Brumley, mwangalizi wangu, alinipeleka kwa Mollen. Mollen alialika pia mwenye alikuwa anatetea ile hospitali. Mazungumuzo yetu ilikuwa moto kabisa. Wakati fulani, Ndugu Brumley aliniandikia maneno kwenye karatasi; aliniambia ‘nitulie kidogo.’ Nilifikia kuelewa kama ile shauri ilikuwa ya muzuri sana, sababu nilianza kukasirika sana juu tu ya kujaribu kuonyesha kama ule mwanasheria mwingine alikuwa na kosa.

Kuanzia kushoto kuenda kuume: Richard Moake, Gregory Olds, Paul Polidoro, Philip Brumley, mimi, na Mario Moreno​—kikundi cha wanasheria wetu siku tulisikilizwa mbele ya Tribinali Kubwa ya Amerika kuhusu kesi kati ya Watchtower na Commune de Stratton.​—Ona Amuka! ya tarehe 8 Mwezi wa 1, 2003 ukurasa wa 4-5; na ukurasa wa 9-11

Kisha saa moja, Muamuzi Mukubwa Mollen alisema kama kesi yetu njo ingechunguzwa ya kwanza kesho asubui. Wakati tulikuwa tunatoka mu biro yake, alituambia kama, ule mwanasheria wa hospitali angekuwa na “kazi ya nguvu kesho.” Alipenda tu kusema kama ule mwanasheria hangeweza kufasiria sababu gani wanganga walilazimisha Dada Nicoleau atiwe damu. Ilikuwa sawa vile Yehova alikuwa ananihakikishia kama tayari tulikuwa tumepata ushindi. Kujua kama Yehova alikuwa anatutumia ili kutimiza mapenzi yake, kulinigusa kabisa.

Tulitumika mupaka usiku sana juu ya kutayarisha mawazo fulani yenye tungetumia kesho ili kutetea kesi yetu. Juu tribinali haikukuwa mbali kabisa na Beteli, washiriki wa kikundi chetu cha Biro ya Mambo ya Sheria walienda kule kwa miguu. Kisha kusikiliza mawazo yenye tulitoa, wale waamuzi ine walifikia kusema kama ruhusa ya kutia dada yetu damu haikupaswa kutolewa. Tribinali kubwa ilipatia Dada Nicoleau haki yake, na ilionyesha kama kujaribu kupata ruhusa ya tribinali ili kutia mugonjwa damu bila kusikiliza maoni yake, ni kuvunja haki za musingi za sheria.

Kisha wakati fulani, tribinali kubwa ya New York ilihakikisha kama Dada Nicoleau alikuwa na haki ya kupata matunzo yenye haiombe kutumia damu. Nilipata pendeleo la kutetea Mashahidi kuhusu mambo ya damu katika kesi ine kwenye tribinali mbalimbali za Inchi ya Amerika. (Ona kisanduku “ Ushindi Mbalimbali Wenye Tulipata Kwenye Tribinali Kubwa.”) Kesi ya Dada Nicoleau njo ilikuwa ya kwanza. Ku Beteli, nilipata pia nafasi ya kutumika pamoja na wanasheria wengine katika kesi zenye kuhusu haki ya kuchunga watoto kisha ndoa kuvunjika, haki ya kuvunja ndoa, na hata pia kuhusu sheria juu ya mambo ya udongo na majengo.

NDOA NA MAISHA YA FAMILIA

Pamoja na Dawn, bibi yangu

Wakati nilikutana kwa mara ya kwanza na Dawn, alikuwa amekwisha kuvunja ndoa, na alikuwa anakomalisha yeye peke watoto tatu. Alikuwa anatumika juu ya kutimiza mahitaji ya familia yake na pia alikuwa painia. Hata kama alikuwa na maisha ya nguvu, nilipendezwa na bidii yake katika kazi ya Yehova. Mu 1992, tulihuzuria mukusanyiko wa wilaya wenye kichwa “Wachukuaji Nuru,” katika muji wa New York. Na ni ku ile mukusanyiko njo nilimuomba tuanzishe urafiki wa kimapenzi. Tulioana kisha mwaka moja. Kuwa na bibi wa kiroho na mwenye kupenda kucheka ilikuwa zawadi kutoka kwa Yehova. Kusema kweli, Dawn amenipatia zawabu ya mema siku zote za maisha yetu.​—Mez. 31:12.

Wakati tulioana, watoto walikuwa na miaka 11, 13, na 16. Nilipenda kuwa baba muzuri kwao, kwa hiyo, nilisoma kwa uangalifu na kutumia habari zenye nilipata katika vichapo vyetu kuhusu namna ya kuishi na watoto wa bibi ao bwana yako. Kulikuwa magumu mingi kwa miaka fulani, lakini nafurahi kuona kama watoto walifikia kunikubali kuwa rafiki yao mwenye wanatumainia na pia baba mwenye upendo. Mulango ulikuwa wazi kwa marafiki wa watoto wetu na tulipenda nyumba yetu ijae vijana wenye nguvu.

Mu 2013, Dawn na mimi tulihamia Wisconsin ili kuchunga wazazi wetu wenye kuzeeka. Nilishangaa kuona kama utumishi wangu wa Beteli haukusimamishwa. Niliendelea kusaidia tengenezo letu kuhusu mambo ya sheria nikiwa mujitoleaji wa muda.

BADILIKO LA KUSHITUKIA

Mu mwezi wa 9, 2018, niliona kama nilianza kukohoa sana. Munganga wetu alinichunguza, lakini hakupata sababu yenye ilifanya nikuwe ninakohoa sana. Kisha, munganga mwingine alinishauria nione munganga wa mambo ya ubongo. Mu mwezi wa 1, 2019, ule munganga alijaribu kuchunguza hali yangu, na akasema kama inawezekana ubongo wangu uko na tatizo lenye halizoee kutokea sana na lenye linaitwa paralysie supranucléaire progressive (PSP).

Siku tatu kisha pale, wakati nilikuwa ninacheza juu ya glase, nilianguka, na kiganja (poignet) cha mukono wangu wa kuume kikavunjika. Nilicheza ule muchezo miaka mingi; ilikuwa sehemu ya maisha yangu. Lakini kwa sababu ya ile aksidenti nilianza kupoteza uwezo wa kuongoza misuli yangu. Hali yangu iliharibika haraka sana. Nilikuwa na magumu ya kusema, kutikisika, na kumeza kitu fulani.

Nafurahi sana kwamba, nimeweza kutumia uwezo wangu mudogo nikiwa mwanasheria ili kusaidia tengenezo la Yehova. Nafurahi pia, sababu nimeandika habari mingi sana kwa ajili ya magazeti fulani yenye inasomwa na wanganga, wanasheria, na waamuzi, na pia nimesimamia mikutano mingi mu dunia kuhusu mambo ya sheria na matunzo. Nimepata pendeleo la kutetea watumishi wa Yehova kuhusu haki yao ya kuchagua matunzo na upasuaji wenye hauombe kutumia damu. Lakini kama vile Luka 17:10 inasema, ‘mimi ni mutumwa mwenye hana mafaa yoyote. Nimefanya yale nilipaswa kufanya.’