Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Maulizo ya Wasomaji Wetu

Maulizo ya Wasomaji Wetu

Mashahidi wa Yehova wako na mawazo gani juu ya site za Enternete za kutafuta mutu wa kuoana naye?

Kusema kweli, Yehova anapenda watu wawili wenye wanaoana wakuwe na furaha na waendelee kuwa na urafiki wa karibu sana. (Mt. 19:4-6) Kama unapenda kuoa ao kuolewa, namna gani unaweza kupata bibi ao bwana mwenye atakufaa? Juu iko Muumbaji wetu, Yehova anajua nini njo tunapaswa kufanya ili tukuwe na ndoa yenye furaha. Njo maana kama unatumikisha kanuni za Biblia zenye ametupatia, utakuwa na furaha kabisa. Tuzungumuzie basi kanuni fulani.

Kwanza, tunapaswa kuelewa hii jambo: “Moyo [wetu] ni mudanganyifu kuliko kitu kingine chochote na uko hatari.” (Yer. 17:9) Kadiri mutu anajaribu kupata wa kuoana naye, ni vile pia hisia zake kuelekea ule mutu zinaweza kukomala mbio sana na kumufanya hata asitilie uangalifu mambo fulani ya maana. Mara mingi wakati mutu anaamua kuoa ao kuolewa juu tu ya hisia, ile inaletaka magumu. (Mez. 28:26) Njo maana, haiko muzuri kuambiana mambo ya ndani sana na mungali tu ku mwanzo-mwanzo ya urafiki ao kumuahidi mwengine kitu fulani na hamuyajuana hata muzuri.

Mezali 22:3 inasema: “Mutu mwerevu anaona hatari na kujificha, lakini wenye hawana uzoefu wanaendelea mbele na kupata matokeo ya mubaya.” Hatari inaweza kuwa nini wakati tunatumia site za Enternete za kutafuta mutu wa kuoana naye? Jambo ya kuhuzunisha, wamoja wamezungumuza ku Enternete na watu fulani wenye hawajuane nao muzuri, wameanzisha hata urafiki wa kimapenzi nao, na ku mwisho wamefikia kuvunjika moyo bure. Pia, watu wadanganyifu wamefungulisha konte za bongo ili kuiba wengine makuta yao. Na wakati fulani, wale wenye walikuwa wanafanya ile mambo ya mubaya walisema kama walikuwa Mashahidi.

Fikiria hatari ingine. Site fulani za Enternete za kutafuta mutu wa kuoana naye zinatumia hesabu fulani yenye kuonyesha kama nani anapaswa kuoana na nani. Kusema kweli, hakuna ushuhuda wenye unaonyesha kama zile njia zinasaidia. Unawaza ni jambo ya hekima kutumia njia zenye mwanadamu amefanya ili kukamata uamuzi wa maana sana sawa vile wa kutafuta mutu wa kuoana naye? Hesabu zenye mwanadamu amefanya haziwezi hata kidogo kulinganishwa na kanuni za Biblia, hauone vile?​—Mez. 1:7; 3:5-7.

Kanuni ya Biblia yenye kuwa mu Mezali 14:15 inasema hivi: “Mujinga anaamini kila neno, lakini mwerevu anafikiria sana kila hatua.” Mbele ya kusema kama huyu njo mwenye anaweza kuwa bibi ao bwana mwenye kufaa kwangu, ni muzuri kwanza umujue kabisa. Njo maana kuzungumuza ku Enternete kunaweza kufanya ikuwe nguvu kujua ule mutu muzuri. Hata kama unaambia mwengine mambo yenye kukuhusu na munapitisha wakati mingi kwa kutumiana ujumbe, unaweza kabisa kusema kama unajua muzuri ule mutu? Watu fulani wenye waliwaza kama wamepata mutu mwenye wataishi naye maisha yote, walivunjika moyo sana wakati walionana na ule mutu uso kwa uso.

Mutunga zaburi alisema hivi: “Sishirikiane na watu wadanganyifu, na ninaepuka wale wenye kuficha namna wako.” (Zb. 26:4) Watu wengi wanaona kama ni kawaida kutia habari za uongo kuhusu maisha yao juu tu waonekane kuwa watu wazuri sana wakati wanatafuta mutu wa kuoa ao kuolewa naye. Wanaweza hata kuficha tabia zao za mubaya ao zile tabia haziwezi kuonekana waziwazi wakati wanatumia wengine ujumbe. Na wengine wanaweza kusema kama wako Mashahidi wa Yehova. Je, ni Wakristo wenye kubatizwa kweli? Ni wakomavu kiroho? Wako na uhusiano wa muzuri pamoja na Yehova? Wanaheshimiwa mu kutaniko? Ao pengine wako mifano ya mubaya ao hata “mashirika ya mubaya”? (1 Ko. 15:33; 2 Ti. 2:20, 21) Wako kabisa huru kuoa ao kuolewa kulingana na Maandiko? Unapaswa kujua ile mambo yote, lakini ni nguvu kujua ile yote bila kuuliza Mashahidi wengine wenye wanamujua muzuri ule mutu. (Mez. 15:22) Bila shaka mutumishi wa Yehova hawezi kufikiria hata kufunga “nira yenye haiko sawa” pamoja na mutu mwenye haiko mwamini.​—2 Ko. 6:14; 1 Ko. 7:39.

Juu kuko hatari za kutumia site za Enternete za kutafuta mutu wa kuoana naye, ni jambo ya maana kutumia njia za muzuri zaidi ili kutafuta na kujua muzuri mutu mwenye anaweza kuwa bibi ao bwana yetu. Ni wapi unaweza kupata mutu mwenye anaweza kuwa bwana ao bibi mwenye kufaa? Wakati inawezekana watu wengi wakusanyike fasi moja, Mashahidi wako na nafasi ya kujuana na wengine ku mikutano yao na mikusanyiko yao mbalimbali.

Kuendelea kupitisha wakati pamoja, kutakusaidia uone waziwazi ikiwa miradi yenu inapatana ao hapana

Lakini, wakati haiwezekane watu wengi wakusanyike fasi moja, sawa vile mu kipindi ya Corona, tunatumia vyombo vya kielektroniki juu ya kukusanyika na ile inapatia nafasi Mashahidi wenye hawajaoa ao kuolewa wajuane. Unaweza kuona namna wanatoa vipindi vyao na unaweza kusikia maelezo yao. (1 Ti. 6:11, 12) Unaweza pia kuzungumuza na wengine kisha mikutano. Wakati munakusanyika na Mashahidi wengine mu njia ya kielektroniki ile inaweza kupatia nafasi ya kuona namna ule mutu mwenye unafurahia iko anazungumuza na wengine, na ile inaweza kukusaidia ujue kama ule ni mutu wa namna gani. (1 Pe. 3:4) Vile wakati iko napita na kadiri muko munaendelea kujuana zaidi, mutaona kama miradi yenu inapatana na kama munaweza kuoana ao hapana.

Wakati mutu mwenye hajaoa ao kuolewa anatafuta mutu wa kuoana naye mu njia yenye inapatana na kanuni za Biblia anaweza kabisa kujionea ukweli wa hii mezali yenye inasema: “Mwenye anapata bibi muzuri [ao bwana] anapata kitu kizuri, na anapata wema wa Yehova.”​—Mez. 18:22.