Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Umuige Yehova kwa Kufikiria Wengine na Kuwatendea kwa Wema

Umuige Yehova kwa Kufikiria Wengine na Kuwatendea kwa Wema

“Mwenye furaha ni mutu yeyote mwenye anamuhangaikia [ao, anamufikiria] mutu wa hali ya chini.”​—ZB. 41:1.

NYIMBO: 130, 107

1. Namna gani waabudu wa Yehova wanaonyesha kama wanapendana?

WAABUDU wa Yehova katika dunia yote ni watu wa familia moja. Wote ni ndugu na dada wenye kupendana. (1 Yo. 4:16, 21) Wakati fulani, wanajitoa sana kwa ajili ya ndugu zao, lakini mara nyingi wanaonyesha upendo wao kupitia mambo ya kidogo-kidogo yenye wanawafanyia. Kwa mufano, wanaweza kuambia ndugu na dada wenzao jambo fulani la muzuri ao kuwatendea kwa wema. Wakati tunafikiria wengine, tunamuiga Baba yetu wa mbinguni.​—Efe. 5:1.

2. Namna gani Yesu aliiga upendo wa Baba yake?

2 Yesu alimuiga Baba yake kwa ukamilifu. Sikuzote, alitendea wengine kwa wema. Alisema hivi: “Mukuje kwangu, ninyi wote wenye kuteseka na wenye kulemewa na mizigo, na mimi nitawapumuzisha.” (Mt. 11:28, 29) Wakati tunamuiga Yesu na kuonyesha kama ‘tunamuhangaikia mutu wa hali ya chini,’ tunamufurahisha Yehova, na sisi tutakuwa na furaha pia. (Zb. 41:1) Katika habari hii, tutaona namna tunaweza kuonyesha kama tunafikiria watu wa familia yetu, ndugu na dada zetu, na watu wenye tunakutana nao mu mahubiri.

UFIKIRIE WENGINE MU FAMILIA

3. Namna gani bwana anaweza kuonyesha kama anamufikiria bibi yake? (Ona picha kwenye mwanzo wa habari hii.)

3 Bwana wanapaswa kuwa mufano na kuonyesha kama wanahangaikia sana watu wa familia yao. (Efe. 5:25; 6:4) Biblia inasema kama bwana wanapaswa kufikiria bibi zao na kuwaelewa. (1 Pe. 3:7; maelezo ya chini) Bwana mwenye kumuelewa bibi yake anajua kwamba, hata kama iko tofauti na bibi yake katika njia nyingi, haiko wa maana sana kumupita. (Mwa. 2:18) Anahangaikia namna bibi yake anajisikia na anamutendea kwa adabu na heshima. Bibi mumoja wa Kanada anasema hivi juu ya bwana yake: “Hazarau hata kidogo namna ninajisikia ao kusema, ‘Haupaswe kujisikia vile.’ Tena, ni musikilizaji muzuri. Wakati ananisaidia kubadilisha mawazo yangu juu ya jambo fulani, anafanya vile kwa upole.”

4. Kupitia namna bwana anatendea wanamuke wengine, namna gani anaweza kuonyesha kama anafikiria namna bibi yake anajisikia?

4 Bwana mwenye anafikiria namna bibi yake anajisikia hachezee hata kidogo wanamuke wengine kimapenzi ao kupendezwa nao kwa njia yenye haifae, ikuwe moja kwa moja, kwenye adresi za Enternete za kuzungumuza na watu wengi, ao kwenye Enternete. (Yob. 31:1) Hatumikishe site za Enternete za kupashana habari na watu wengi ili kuchezea wengine kimapenzi, na haangalie site za Enternete zenye hazifae. Kwa kweli, anaendelea kuwa muaminifu kwa bibi yake kwa sababu anamupenda na kwa sababu anamupenda Yehova na anachukia mambo ya mubaya.​—Soma Zaburi 19:14; 97:10.

5. Namna gani bibi anaweza kuonyesha kama anamufikiria bwana yake?

5 Wakati bwana anaiga mufano wenye upendo wa Yesu Kristo, mwenye kuwa kichwa chake, bibi yake atakuwa tayari “kumuheshimia sana.” (Efe. 5:22-25, 33) Na wakati bibi anamuheshimia bwana yake, atajikaza kuelewa namna anajisikia na kumutendea kwa wema wakati iko na kazi nyingi za kutaniko za kufanya ao wakati anapaswa kushugulikia magumu fulani. Bwana mumoja katika Uingereza anasema hivi: “Wakati fulani, bibi yangu anatambua kama jambo fulani linanisumbua wakati anaona kama siko vile ninakuwaka. Kisha anatumia kanuni yenye kupatikana katika Mezali 20:5, hata kama anapaswa kungojea wakati wenye kufaa kusudi ‘ashote’ mawazo yangu kama ni jambo fulani lenye ninaweza kuzungumuzia pamoja naye.”

6. Namna gani sisi wote tunaweza kutia watoto moyo wafikirie watu wengine na kuonyesha adabu, na watoto watapata faida gani kwa kufanya vile?

6 Wakati kila muzazi anafikiria mwenzake, wanaonyesha watoto wao mufano muzuri. Tena, wanapaswa kufundisha watoto wao kufikiria watu wengine na kuonyesha adabu. Kwa mufano, wazazi wanaweza kufundisha watoto wao wasikimbie-kimbie mu Jumba la Ufalme. Ao wakati wanakutana na watu wengine ili kujifurahisha, wanaweza kuambia watoto wao wangojee kwanza watu wazima wakamate chakula. Kwa kweli, kila mutu katika kutaniko anaweza kusaidia wazazi. Kwa hiyo, tunaweza kupongeza mutoto wakati anafanya jambo fulani la muzuri, kwa mufano, wakati anatufungulia mulango. Hilo litafanya mutoto ajisikie muzuri na kumusaidia ajue kama “kuko furaha zaidi katika kutoa kuliko katika kupokea.”​—Mdo. 20:35.

UFIKIRIE WENGINE MU KUTANIKO

7. Namna gani Yesu alifikiria mwanaume mumoja kiziwi, na mufano wake unaweza kutufundisha nini?

7 Siku moja, Yesu alikuwa katika eneo la Dekapoli, wakati huo watu “wakamuletea mutu mwenye alikuwa kiziwi na alikuwa na ugumu wa kusema.” (Mk. 7:31-35) Yesu alimuponyesha, lakini hakufanya vile mbele ya watu wengine. Juu ya nini? Juu mutu huyo alikuwa kiziwi, pengine hakujisikia muzuri mbele ya watu wengi. Yesu alielewa namna mutu huyo alijisikia, na “akamuchukua na kuenda naye pembeni” mahali kwenye watu hawakukuwa na akamuponyeshea kule. Kwa kweli, hatuwezi kufanya miujiza, lakini tunapaswa kufikiria mahitaji ya ndugu na dada zetu na namna wanajisikia na kuwaonyesha wema. Mutume Paulo aliandika hivi: “Tufikiriane ili kuchocheana katika upendo na matendo ya muzuri.” (Ebr. 10:24) Yesu alielewa namna mutu huyo mwenye alikuwa kiziwi alijisikia na alimutendea kwa wema. Huo ni mufano muzuri kabisa wenye alituonyesha!

8, 9. Namna gani tunaweza kuonyesha kama tunafikiria watu wenye kuzeeka na wale wenye kuwa na uzaifu mbalimbali? Leta mifano.

8 Fikiria watu wenye kuzeeka na wale wenye kuwa na uzaifu mbalimbali. Jambo la maana zaidi lenye kutambulisha kutaniko la Kikristo ni upendo, haiko uwezo wa kutimiza mambo mengi kwa wakati kidogo. (Yoh. 13:34, 35) Upendo unatuchochea kufanya yote yenye tunaweza ili kusaidia ndugu na dada wenye kuzeeka ao wenye kuwa na uzaifu mbalimbali kusudi wafike ku mikutano ao ku mahubiri. Tunawasaidia hata kama haiko mwepesi kufanya vile ao hata kama hawawezi kufanya mambo mengi. (Mt. 13:23) Michael, mwenye kutembea kwa kutumia kinga ya vilema, iko mwenye shukrani sana juu ya musaada wenye familia yake na ndugu na dada wa kutaniko lake wanamutolea. Anasema hivi: “Juu ya musaada wenye wote wananitolea, ninaweza kufika ku mikutano karibu yote na kuenda kwa ukawaida mu kazi ya kuhubiri. Ninafurahia zaidi kuhubiri mahali pa watu wengi.”

9 Katika Beteli nyingi, kuko ndugu na dada waaminifu wenye kuzeeka ao wenye kuwa na uzaifu mbalimbali. Waangalizi wenye kuwahangaikia wanawaonyesha upendo kwa kufanya mipango ili wahubiri kwa kuandikia watu barua na kutumia telefone. Bill, mwenye kuwa na miaka 86 na mwenye kuandikia barua watu wenye kuishi mu maeneo ya mbali, anasema hivi: “Tunafurahia sana pendeleo lenye tuko nalo la kuandikia watu barua.” Nancy, mwenye kuwa na miaka karibu 90, anasema hivi: “Sione kuandika barua kuwa tu kazi ya kujaza bahasha (enveloppe). Ni kazi ya kuhubiri. Watu wako na lazima ya kujua kweli!” Ethel, mwenye alizaliwa mu mwaka wa 1921, anasema hivi: “Ninasikia maumivu kila siku. Siku fulani, ninashindwa kujivalisha nguo.” Hata hivyo, anafurahia kuhubiri kwa kutumia telefone na iko na watu fulani wenye kupendezwa wenye anarudilia. Barbara, mwenye kuwa na miaka 85, anaeleza hivi: “Juu ya afya yangu ya mubaya, ni vigumu sana kwangu kuhubiri kwa ukawaida. Lakini kuhubiri kwa kutumia telefone kunanisaidia kuzungumuza na watu. Aksanti, Yehova!” Mu kipindi cha karibu mwaka moja, kikundi cha ndugu na dada wapendwa wenye kuzeeka walihubiri saa 1 228, waliandika barua 6 265, walizungumuza na watu zaidi ya 2 000 ku telefone, na walitolea watu vichapo 6 315! Tunaweza kuwa hakika kama Yehova alifurahia kabisa bidii yao!​—Mez. 27:11.

10. Namna gani tunaweza kusaidia ndugu na dada zetu kusudi wafaidike na mikutano kadiri inawezekana?

10 Fikiria wengine ku mikutano ya Kikristo. Wakati tunafikiria wengine, tunasaidia ndugu na dada zetu wafaidike na mikutano kadiri inawezekana. Namna gani? Njia moja ni kufika kwa wakati kusudi tusikengeushe wengine. Wakati fulani, mambo yenye hatukutazamia yanaweza kufanya tuchelewe. Lakini kama tunachelewa mara kwa mara, tunapaswa kufikiria matokeo yenye jambo hilo linaletea ndugu na dada zetu na mabadiliko yenye tunaweza kufanya kusudi tuonyeshe kama tunawahangaikia. Pia, tukumbuke kama ni Yehova na Mwana wake ndio wanatualika ku mikutano. (Mt. 18:20) Kwa kweli, tunapaswa kuwaonyesha heshima kwa kufika kwa wakati!

11. Juu ya nini ndugu wenye kuwa na migao ku mikutano wanapaswa kufuata shauri lenye kutolewa katika 1 Wakorinto 14:40?

11 Kama tunafikiria ndugu na dada zetu, tutafuata agizo hili la Biblia: “Mambo yote yatendeke kwa adabu na kwa utaratibu.” (1 Ko. 14:40) Ndugu wenye kuwa na migao katika mukutano fulani wanafuata agizo hilo wakati wanamaliza mugao wao kwa wakati. Wakati wanafanya vile, hawafikirie tu musemaji mwenye kufuata lakini wanafikiria pia kutaniko lote. Fikiria matokeo yenye hilo linaweza kuletea wengine ikiwa hatumalize mikutano kwa wakati. Ndugu na dada fulani wanapaswa kutembeza gari njia murefu sana ili kurudia ku nyumba. Wengine wanapaswa kukamata bisi ao kutembea kwa miguu njia murefu kusudi warudie ku nyumba. Na wengine wako na bibi ao bwana wenye hawako Mashahidi wenye wanawaomba wafike ku nyumba kwa wakati fulani.

12. Juu ya nini tunapaswa kuonyesha wazee heshima na upendo? (Ona kisanduku “ Fikiria Wale Wenye Wanaongoza.”)

12 Wazee wanafanya kazi kwa bidii mu kutaniko na mu kazi ya kuhubiri. Kwa hiyo, tunapaswa kuwaonyesha heshima na upendo. (Soma 1 Watesalonike 5:12, 13.) Kwa kweli, uko mwenye shukrani sana juu ya mambo yote yenye wanakufanyia. Unaweza kuonyesha shukrani hiyo kwa kuwa tayari kuwatii na kuwaunga mukono, kwa sababu “wanaendelea kuwalinda ninyi kama wale wenye watatoa hesabu.”​—Ebr. 13:7, 17.

FIKIRIA WENGINE MU KAZI YA KUHUBIRI

13. Namna Yesu alitendea watu inaweza kutufundisha nini?

13 Katika unabii moja juu ya Yesu, Isaya alisema hivi: “Hatavunja utete wenye kupondekana, na hatazima utambi wenye kutoa moshi.” (Isa. 42:3) Upendo wenye Yesu alikuwa nao kwa ajili ya watu ulimuchochea Yesu ajitie pa nafasi yao. Alielewa namna wale wenye walikuwa wamevunjika moyo na wazaifu walijisikia, walikuwa kama “utete wenye kupondekana” ao “utambi wenye kutoa moshi.” Kwa hiyo, aliwatendea kwa wema na kwa uvumilivu. Hata watoto walipenda kuwa pamoja na Yesu. (Mk. 10:14) Kwa kweli, hatuwezi kuelewa watu ao kuwafundisha namna Yesu alifanya! Lakini, tunaweza kuonyesha kama tunafikiria watu wa eneo letu kupitia namna tunazungumuza nao, wakati wenye tunawatembelea, na muda wenye tunapitisha pamoja nao.

14. Juu ya nini tunapaswa kufikiria namna tunazungumuza na watu?

14 Namna gani tunapaswa kuzungumuza na watu? Watu wengi leo “wamechunwa ngozi na kutupwa huku na huku” na viongozi wa biashara, viongozi wa politike, na viongozi wa dini wa ulimwengu huu wenye kuwa wabaya na wenye hawana huruma. (Mt. 9:36) Kwa hiyo, wengi hawatumainie mutu na hawana tumaini. Ndiyo maana maneno yenye tunatumia na sauti yetu vinapaswa kuwaonyesha kama tuko wema na kama tunawahangaikia! Watu wengi wanapenda kusikiliza ujumbe wetu haiko tu kwa sababu tunatumia muzuri Biblia lakini pia kwa sababu tunapendezwa nao kabisa na tunawaonyesha heshima.

15. Tunaweza kufikiria watu wa eneo letu mu njia gani fulani?

15 Kuko njia nyingi za kuonyesha kama tunafikiria watu wa eneo letu. Tunapaswa kuuliza maulizo kwa njia ya adabu na heshima. Painia mumoja alitumikia mu eneo kwenye watu wengi walikuwa wenye haya, kwa hiyo alikuwa anaepuka kuwauliza maulizo yenye yangewafanya wasikie haya kama hawajue jibu la muzuri. Hakukuwa anawauliza hivi: “Unajua jina la Mungu?” ao “Unajua Ufalme wa Mungu ni nini?” Lakini, alikuwa anasema jambo fulani kama vile, “Nimejifunza katika Biblia kama Mungu iko na jina la pekee. Ninaweza kukuonyesha jina hilo?” Hatuwezi kutumia njia hiyo mu kila eneo, kwa sababu watu hawako namna moja na pia kila watu wako na desturi zao. Lakini, sikuzote tunapaswa kutendea watu wa eneo letu kwa wema na kwa heshima. Kusudi tufanye vile, tunapaswa kuwajua muzuri.

16, 17. Namna gani tunaweza kuonyesha wema wakati tunaamua (a) ni wakati gani tutatembelea watu? (b) tutapitisha nao muda gani?

16 Tunapaswa kutembelea watu wakati gani? Wakati tunahubiri nyumba kwa nyumba, watu hawajue kama tutakuja juu hawakutualika. Kwa hiyo, ni jambo la maana sana kuwatembelea wakati wenye wanaweza kuwa tayari zaidi kuzungumuza. (Mt. 7:12) Kwa mufano, je, watu wa eneo lenu wanapenda kulala sana Siku ya Posho na Siku ya Yenga? Kama ni vile, unaweza kwanza kuhubiri ku barabara, mahali pa watu wengi, ao kurudilia watu wenye unajua kama watakuwa tayari kuzungumuza.

17 Tunapaswa kupitisha muda gani pamoja nao? Watu wengi wako na kazi nyingi sana, kwa hiyo, inaweza kuwa muzuri tusizungumuze na watu muda murefu, zaidi sana ku mwanzo. Ni muzuri zaidi kumaliza mazungumuzo yetu haraka kuliko kubakia muda murefu sana. (1 Ko. 9:20-23) Watu wakiona kama tunaelewa kuwa wako na kazi nyingi, wanaweza kuwa tayari zaidi kuzungumuza na sisi wakati ingine. Kama tunaonyesha sifa zenye kutokana na roho ya Mungu, tutakuwa kabisa “wafanyakazi pamoja na Mungu.” Yehova anaweza hata kututumia ili kusaidia mutu fulani ajifunze kweli!​—1 Ko. 3:6, 7, 9.

18. Wakati tunafikiria wengine, tunaweza kuwa na tumaini kama tutapata baraka gani?

18 Basi, tufanye yote tunaweza kusudi tuonyeshe kama tunafikiria watu wa familia yetu, ndugu na dada zetu, na watu wenye tunakutana nao mu mahubiri. Tukifanya vile, tutapata baraka nyingi, leo na wakati wenye kuja. Kama vile Zaburi 41:1, 2 inasema: “Mwenye furaha ni mutu yeyote mwenye anamuhangaikia mutu wa hali ya chini; Yehova atamuokoa katika siku ya musiba. Yehova atamuchunga na kulinda uzima wake. Atatangazwa kuwa mwenye furaha katika dunia.”