Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI YA KUJIFUNZA YA 35

Yehova Anaona Watumishi Wake Wanyenyekevu Kuwa wa Maana

Yehova Anaona Watumishi Wake Wanyenyekevu Kuwa wa Maana

“Yehova . . . anaona wanyenyekevu.”​—ZB. 138:6.

WIMBO 48 Kutembea na Yehova Kila Siku

KIFUPI CHA HABARI *

1. Namna gani Yehova anaona watu wanyenyekevu? Fasiria.

YEHOVA anapenda watu wanyenyekevu. Ni wale tu wenye kuwa wanyenyekevu njo wanaweza kuwa na urafiki wa sana na wa pekee pamoja na yeye. Lakini, watu “wenye majivuno anawajua tu kwa mbali.” (Zb. 138:6) Sisi wote tunapenda kumufurahisha Yehova na tunataka atukaribie. Kwa hiyo, tuko na sababu za muzuri za kuwa wanyenyekevu.

2. Tutazungumuzia nini katika habari hii?

2 Katika habari hii, tutazungumuzia majibu ya maulizo tatu yenye kufuata: (1) Unyenyekevu maana yake nini? (2) Juu ya nini tunapaswa kuwa wanyenyekevu? (3) Ni hali gani zenye zinaweza kufanya ikuwe nguvu kwetu kuonyesha unyenyekevu? Kama vile tutaona, wakati tunajikaza kuonyesha unyenyekevu, tunamufurahisha Yehova na tunajiletea faida sisi wenyewe.​—Mez. 27:11; Isa. 48:17.

UNYENYEKEVU MAANA YAKE NINI?

3. Unyenyekevu maana yake nini?

3 Unyenyekevu ni kuepuka kujiona kuwa wa maana sana, kuepuka kuwa na kiburi ao majivuno. Biblia inaonyesha kama mutu munyenyekevu anaelewa kama Yehova iko mukubwa zaidi kuliko yeye. Pia, anaelewa kama kila mutu iko wa muzuri zaidi kuliko yeye katika njia fulani.​—Flp. 2:3, 4.

4-5. Kama mutu anaonekana kwa inje kuwa munyenyekevu, ni kusema kama iko munyenyekevu kabisa?

4 Watu fulani wanaonekana tu kwa inje kuwa wanyenyekevu. Wanaweza kuwa watu wa kimya-kimya. Ao wanaweza kuonyesha heshima ao adabu kwa sababu ya desturi yao ao kwa sababu ya namna walikomaa. Lakini, ndani yao kabisa, wanaweza kuwa wenye kiburi sana. Siku moja, wataonyesha namna wako kabisa mu moyo wao.​—Lu. 6:45.

5 Watu wengine wanaonekana kuwa wenye kujitumainia na wanasema waziwazi mambo yenye wanawaza, lakini hilo halimaanishe kama wako na majivuno. (Yoh. 1:46, 47) Hata hivyo, watu wenye kujua kusema muzuri na wenye kuwa na uwezo mbalimbali wanapaswa kuwa waangalifu ili wasitumainie uwezo wao. Ikuwe tunajua kusema muzuri na tuko na uwezo mbalimbali ao hapana, sisi wote tunapaswa kujikaza sana ili tukuwe wanyenyekevu.

Mutume Paulo alikuwa munyenyekevu na hakuwaza kama alikuwa wa maana zaidi kupita wengine (Picha hii inapatana na fungu la 6) *

6. Kama vile andiko la 1 Wakorinto 15:10 linaonyesha, mufano wa Paulo unaweza kutufundisha nini?

6 Fikiria mufano wa mutume Paulo. Yehova alimutumia sana ili kuanzisha makutaniko ya mupya mu miji mbalimbali. Pengine yeye njo alifanya mambo mingi mu kazi ya Mungu kupita mitume wengine wote wa Yesu Kristo. Lakini, Paulo hakujiona kuwa wa maana kupita ndugu zake. Alisema hivi kwa unyenyekevu: “Mimi ni mudogo zaidi kati ya mitume, na sistahili kuitwa mutume, kwa sababu nilitesa kutaniko la Mungu.” (1 Ko. 15:9) Njo maana, Paulo hakukosea wakati alisema kama alikuwa na urafiki wa muzuri pamoja na Yehova kwa sababu tu Yehova alimuonyesha fazili zenye hazistahiliwe, haiko juu alikuwa mutu wa pekee ao juu alifanya mambo mingi. (Soma 1 Wakorinto 15:10.) Paulo alionyesha mufano muzuri sana wa unyenyekevu. Wakati aliandikia Wakristo wa Korinto barua, hakujivuna, hata kama ndugu na dada fulani mu kutaniko walikuwa wanamuzarau!​—2 Ko. 10:10.

Karl Frederick Klein, ndugu munyenyekevu mwenye alitumikia mu Baraza Lenye Kuongoza (Picha hii inapatana na fungu la 7)

7. Katika siku zetu, namna gani ndugu mumoja mwenye kujulikana sana alionyesha unyenyekevu?

7 Habari yenye kuzungumuzia maisha ya Ndugu Karl Frederick Klein, mwenye alitumikia mu Baraza Lenye Kuongoza, imetia moyo watumishi wengi wa Yehova. Katika habari hiyo, Ndugu Klein alizungumuzia kwa unyenyekevu na waziwazi uzaifu wake mbalimbali na magumu yenye alipata mu maisha yake. Kwa mufano, alipima kuhubiri nyumba kwa nyumba kwa mara ya kwanza mu mwaka wa 1922. Ilikuwa nguvu sana kwake, kwa hiyo, alifanya miaka mbili hivi bila kuhubiri tena nyumba kwa nyumba. Kisha, wakati alikuwa anatumikia ku Beteli, ndugu mumoja alimushauria na aliwekea ndugu huyo kinyongo kwa wakati fulani. Pia, wakati fulani aligonjwa ugonjwa wa kushuka moyo, lakini alifikia kupona ugonjwa huo. Hata hivyo, alipewa pia madaraka mbalimbali. Wazia unyenyekevu mukubwa wenye ndugu huyo mwenye kujulikana sana alionyesha wakati alizungumuzia waziwazi uzaifu wake! Ndugu na dada wengi wanamukumbuka sana Ndugu Klein na habari yenye kupendeza yenye ilizungumuzia maisha yake bila kuficha jambo lolote. *

JUU YA NINI TUNAPASWA KUWA WANYENYEKEVU?

8. Namna gani andiko la 1 Petro 5:6 linatusaidia kuelewa kama unyenyekevu unamufurahisha Yehova?

8 Sababu ya maana sana yenye kufanya tukuwe wanyenyekevu ni hii: unyenyekevu unamufurahisha Yehova. Mutume Petro alionyesha waziwazi sababu hiyo. (Soma 1 Petro 5:6.) Kitabu ‘Njoo Uwe Mfuasi Wangu’ kinatoa maelezo fulani juu ya maneno ya Petro. Kinasema hivi: ‘Majivuno iko kama sumu. Matokeo yake inaweza kuwa ya mubaya sana. Majivuno inaweza kumufanya mutu mwenye vipawa mingi [ao uwezo mingi wa kizalikio] asikuwe wa maana hata kidogo mu macho ya Mungu. Kwa upande mwingine, unyenyekevu unaweza kumufanya hata mutu wa hali ya chini zaidi akuwe wa maana sana mu macho ya Yehova. . . . Atafurahia kukupa zawabu kwa sababu ya unyenyekevu wako.’ * Kwa kweli, kumufurahisha Yehova njo jambo la muzuri zaidi lenye tunaweza kufanya!​—Mez. 23:15.

9. Juu ya nini sifa ya unyenyekevu inafanya watu wengine watukaribie?

9 Zaidi ya kumufurahisha Yehova, tunapata faida mingi wakati tunaonyesha unyenyekevu. Unyenyekevu unafanya watu wengine watukaribie. Juu ya nini? Fikiria watu wenye unapendaka kuwa pamoja nao. (Mt. 7:12) Karibu sisi wote hatupendake kuwa pamoja na watu wenye wanapenda tu tufuate mawazo yao na wenye wanakataa kusikiliza mawazo ya watu wengine. Lakini, tunafurahia kuwa pamoja na ndugu na dada zetu wakati wanaonyesha sifa ya ‘kujitia pa nafasi ya wengine, upendo wa kindugu, huruma yenye upole, na unyenyekevu.’ (1 Pe. 3:8) Kama tunapendaka kukaribia watu wa namna hiyo, nao pia watapenda kutukaribia, kama tu tuko wanyenyekevu.

10. Juu ya nini ni mwepesi kwa watu wanyenyekevu kuvumilia magumu mu maisha?

10 Pia, sifa ya unyenyekevu inafanya ikuwe mwepesi kwetu kuvumilia magumu mu maisha. Kwa kweli, wakati fulani tunaweza kuona mambo fulani yenye inaonekana kuwa haiko ya haki. Sulemani, mufalme mwenye hekima, alisema hivi: “Nimeona watumishi wakiwa kwenye migongo ya farasi lakini wakubwa wakitembea kwa miguu kama vile watumishi.” (Muh. 10:7) Wakati fulani, watu wenye kuwa na uwezo mukubwa hawapate sifa. Na wakati fulani, watu wenye hawana uwezo mingi wanapata sifa. Hata hivyo, Sulemani alitambua kama ni jambo la hekima tukubali maisha namna iko kuliko kukasirika wakati mambo haiendeke muzuri mu maisha. (Muh. 6:9) Kama tuko wanyenyekevu, itakuwa mwepesi zaidi kukubali mambo yenye hatupendi mu maisha yetu.

NI HALI GANI ZENYE ZINAWEZA KUFANYA IKUWE NGUVU KWETU KUONYESHA UNYENYEKEVU?

Juu ya nini inaweza kuwa nguvu kwetu kuwa wanyenyekevu mu hali kama hii? (Picha hii inapatana na fungu la 11-12) *

11. Tunapaswa kutenda namna gani wakati mutu fulani anatupatia shauri?

11 Kila siku, tuko na nafasi za mingi sana za kuonyesha unyenyekevu. Fikiria hali fulani. Wakati tunapewa shauri. Tunapaswa kukumbuka kama, ikiwa mutu fulani anajikaza kutupatia shauri, pengine tumekosea sana bila sisi kujua. Wakati mutu anatupatia shauri, tunaweza mara moja kukataa shauri hilo. Tunaweza kuchambua-chambua mutu mwenye alitushauria ao namna alitupatia shauri. Lakini kama tuko wanyenyekevu, tutajikaza kukubali shauri hilo.

12. Kulingana na Mezali 27:5, 6, juu ya nini tunapaswa kuwa wenye shukrani wakati mutu anatupatia shauri? Leta mufano.

12 Mutu munyenyekevu anaonyesha shukrani wakati anapewa shauri. Kwa mufano: Wazia uko ku mukutano wa kutaniko. Kisha kuzungumuza na ndugu na dada fulani, mumoja kati yao anakubeba pembeni na anakuambia kama uko na chakula fulani ku meno yako. Kwa kweli, hautajisikia muzuri. Lakini, utakuwa pia mwenye shukrani kuona ndugu ao dada huyo alikuambia jambo hilo. Kwa kweli, ungefurahi ikiwa mutu angekuambia vile mbele ya wakati! Vilevile, tunapaswa kuwa wanyenyekevu na wenye shukrani wakati ndugu ao dada anajikaza kutupatia shauri wakati tuko na lazima ya shauri hilo. Tunapaswa kumuona ndugu ao dada huyo kuwa rafiki yetu, hapana adui yetu.​—Soma Mezali 27:5, 6; Gal. 4:16.

Juu ya nini ni lazima tukuwe wanyenyekevu wakati wengine wanapata mapendeleo ya utumishi? (Picha hii inapatana na fungu la 13-14) *

13. Namna gani tunaweza kuonyesha unyenyekevu wakati wengine wanapata mapendeleo ya utumishi?

13 Wakati wengine wanapata mapendeleo ya utumishi. Muzee mumoja wa kutaniko mwenye kuitwa Jason anasema hivi: “Wakati ninaona wengine wanapata mapendeleo, wakati fulani ninajiuliza juu ya nini mimi sikupata ile mapendeleo.” Na wewe umekwisha kujisikia vile? Haiko mubaya wakati mutu “anajikaza” ili kupata mapendeleo zaidi ya utumishi. (1 Ti. 3:1) Lakini, tunapaswa kuwa waangalifu juu ya mawazo yetu. Kama hatuko waangalifu, tunaweza kuacha kiburi kikomae mu moyo wetu. Kwa mufano, mwanaume Mukristo anaweza kuanza kuwaza kama yeye njo anastahili sana kufanya muzuri mugao fulani. Ao dada Mukristo anaweza kuwaza hivi: ‘Bwana yangu njo anastahili zaidi kufanya mugao fulani kuliko ndugu fulani!’ Lakini, kama tuko wanyenyekevu kabisa, tutaepuka kabisa roho hiyo ya kiburi.

14. Namna Musa alitenda wakati wengine walipata mapendeleo, inaweza kutufundisha nini?

14 Namna Musa alitenda wakati wengine walipata mapendeleo inaweza kutufundisha jambo fulani. Musa alifurahia sana daraka lake la kuongoza taifa la Israeli. Musa alitenda namna gani wakati Yehova aliruhusu wengine watumike pamoja na yeye? Hakukuwa na wivu. (Hes. 11:24-29) Alionyesha unyenyekevu na aliruhusu wengine wamusaidie kufanya kazi ya kuhukumu watu. (Kut. 18:13-24) Kufanya vile kulisaidia Waisraeli wakuwe na wanaume wengi wa kuwahukumu na hawakukuwa tena wanangojea wakati murefu ili mambo yao iamuliwe. Hilo linaonyesha kama Musa hakuona madaraka yake kuwa ya maana kuliko faida ya watu wengine. Huo ni mufano muzuri kwetu! Tunapaswa kukumbuka kama, ikiwa tunapenda Yehova atutumie kabisa, ni jambo la maana zaidi tukuwe wanyenyekevu kuliko kuwa na uwezo mukubwa. Hata kama “Yehova iko juu, yeye anaona wanyenyekevu.”​—Zb. 138:6.

15. Ni mabadiliko gani yenye ilitokea mu maisha ya ndugu na dada wengi?

15 Wakati hali zetu zinabadilika. Mu miaka ya hivi majuzi, ndugu na dada wengi wenye wamemutumikia Yehova kwa miaka mingi wamepewa migao ingine. Kwa mufano, kuanzia mwaka wa 2014, waangalizi wa wilaya na bibi zao walipewa mugao mwingine katika utumishi wa wakati wote. Kuanzia mwaka huo, tengenezo liliamua kama wakati mwangalizi wa muzunguko anakuwa na miaka 70, hawezi kuendelea tena kufanya mugao wake. Na ndugu wenye kuwa na miaka 80 hawawezi kuendelea tena kuwa waratibu wa baraza la wazee wa kutaniko. Tena, mu miaka fulani yenye imepita, Wanabeteli wengi wametumwa kufanya kazi ya upainia mu makutaniko. Wengine walipaswa kuacha utumishi wa wakati wote kwa sababu ya afya, kwa sababu familia yao ilikuwa na lazima ya musaada, ao kwa sababu ya hali zingine za kipekee.

16. Namna gani ndugu na dada zetu wameonyesha unyenyekevu wakati hali zao zilibadilika?

16 Haikukuwa mwepesi kwa ndugu na dada hao kuzoea ile mabadiliko. Kwa kweli, walikuwa wanapenda sana migao yao, zaidi sana migao yenye walikuwa nayo kwa miaka mingi. Wakati wamoja walipewa migao ya mupya, wakati fulani walisikia huzuni sana juu ya kupoteza migao yenye walikuwa wanapenda sana. Lakini, kisha wakati fulani, walizoea. Ni nini iliwasaidia? Zaidi sana ni upendo wao kwa Yehova. Walijua kama walijitoa kwa Mungu, hawakujitoa kwa kazi fulani, cheo fulani, ao mugao fulani. (Kol. 3:23) Wanafurahia kuendelea kumutumikia Yehova kwa unyenyekevu katika mugao wowote. ‘Wanamutupia mahangaiko yao yote,’ kwa sababu wanajua kama anawahangaikia.​—1 Pe. 5:6, 7.

17. Juu ya nini tuko wenye shukrani kuona Neno la Mungu linatutia moyo tukuwe wanyenyekevu?

17 Tuko wenye shukrani sana kuona Neno la Mungu linatutia moyo tukuwe wanyenyekevu. Juu ya nini? Juu wakati tunajikaza kuwa na ile sifa ya muzuri sana, tunapata faida sisi wenyewe na wengine pia. Inakuwa mwepesi kwetu kuvumilia magumu mu maisha. Na zaidi ya yote, tunamukaribia sana Baba yetu wa mbinguni. Tuko wenye furaha sana kujua kwamba, hata kama Yehova ni mwenye “Kuwa Juu na Mwenye Kuinuka Sana,” anapenda watumishi wake wanyenyekevu na anawaona kuwa wa maana!​—Isa. 57:15.

WIMBO 45 Kutafakari kwa Moyo Wangu

^ fu. 5 Unyenyekevu ni moja kati ya sifa za maana sana zenye tunapaswa kuwa nazo. Unyenyekevu maana yake nini? Juu ya nini tunapaswa kuwa wanyenyekevu? Na juu ya nini inaweza kuwa nguvu kuendelea kuwa wanyenyekevu wakati hali zetu zinabadilika? Habari hii itazungumuzia ile maulizo ya maana.

^ fu. 7 Ona habari Jéhovah m’a traité d’une manière salutairekatika Munara wa Mulinzi wa tarehe 1 Mwezi wa 5, 1985 (katika Kifaransa).

^ fu. 53 MAFASIRIO YA PICHA: Wakati mutume Paulo iko mu nyumba ya ndugu fulani, anazungumuza kwa unyenyekevu na ndugu na dada, na hata watoto.

^ fu. 57 MAFASIRIO YA PICHA: Ndugu mumoja anakubali mashauri yenye kutegemea Biblia yenye ndugu kijana anamupatia.

^ fu. 59 MAFASIRIO YA PICHA: Ndugu mwenye kuzeeka hasikilie wivu ndugu kijana mwenye anatimiza mugao fulani mu kutaniko.