Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI YA KUJIFUNZA YA 39

Wakati Mupendwa Wako Anamuacha Yehova

Wakati Mupendwa Wako Anamuacha Yehova

“Mara nyingi . . . walimuhuzunisha.”​—ZB. 78:40.

WIMBO 102 ‘Musaidie Wale Wenye Kuwa Wazaifu’

KIFUPI YA HABARI *

1. Watu fulani wanaweza kujisikia namna gani wakati mutu wa familia yao anatengwa?

 UKO na mutu fulani mu familia yako mwenye ametengwa na kutaniko? Ile ni jambo ya kuhuzunisha sana! Dada Hilda anasema hivi *: “Wakati bwana yangu mupendwa alikufa kisha kupitisha naye miaka 41 mu ndoa, niliwaza kama ile njo jaribu ya nguvu sana kupita yote. Lakini wakati mutoto yangu alitengwa na kisha akaacha bibi yake na watoto wake, niliona kama ile njo jaribu ya nguvu, ya nguvu sana kupita yote.”

Yehova anaelewa huzuni yenye uko nayo juu mupendwa wako aliacha kumutumikia (Ona fungu ya 2-3) *

2-3. Kulingana na Zaburi 78:40, 41, Yehova anajisikiaka namna gani wakati watumishi wake wanamuacha?

2 Waza sasa namna Yehova alihuzunika sana wakati aliona na macho yake malaika fulani wanamutupia mugongo! (Yud. 6) Waza pia namna alihuzunika sana wakati aliona wapendwa wake, ni kusema Waisraeli, wanamuasi mara mingi. (Soma Zaburi 78:40, 41.) Ukuwe hakika kama Baba yetu mwenye upendo pia anahuzunika sana wakati mutu fulani mwenye unapenda anamuacha. Anaelewa kabisa huzuni yako na ukuwe hakika kama atakutia moyo na atakutegemeza.

3 Mu hii habari, tutaona ni nini tunaweza kufanya ili tupate musaada wa Yehova wakati mupendwa wetu anatengwa. Tena, tutaona namna tunaweza kusaidia wengine mu kutaniko wenye wako wanapambana na ile hali. Lakini mbele ya yote, tuone kwanza mawazo ya mubaya yenye tunapaswa kuepuka.

EPUKA KUJIHUKUMU

4. Wazazi wengi wanajisikiaka namna gani wakati mutoto yao anamuacha Yehova?

4 Wakati mutoto yao anamuacha Yehova, ni kawaida kwa wazazi kujiuliza kama wangefanya nini tena ingine ili kusaidia mutoto yao abakie katika kweli. Kisha mutoto yake mwanaume kutengwa, ndugu Luke alisema hivi: “Nilijihukumu. Nilikosa usingizi. Wakati fulani nilikuwa nalia na roho iliniluma.” Elizabeth, dada mwenye alipata hali yenye kufanana na ile, alisema hivi: “Nilikuwa mama muzuri kabisa? Nilianza kuwaza kama ni juu nilishindwa kumufundisha muzuri mutoto yangu mwanaume kweli.”

5. Kosa ni ya nani wakati mutu fulani anaacha kumutumikia Yehova?

5 Tusisahau kama Yehova alipatia kila mumoja wetu uhuru wa kuchagua. Ile inamaanisha kama tunaweza kuchagua ikiwa tutamutii ao hapana. Vijana fulani hawakukuwa na wazazi wenye walikuwa mufano muzuri, lakini waliamua kumutumikia Yehova na kubakia waaminifu kwake. Wazazi wengine walifanya yao yote ili kufundisha watoto wao wamupende Yehova, lakini wakati watoto walikomala walimuacha Yehova. Njo maana kila mumoja wetu anapaswa kuchagua ikiwa atamutumikia Yehova. (Yos. 24:15) Kwa hiyo, nyie wazazi wenye muko na huzuni kwa sababu mutoto yenu aliacha kumutumikia Yehova, tafazali muache kuwaza kama ile ni kosa yenu!

6. Kijana anaweza kujisikia namna gani wakati muzazi wake anaacha kumutumikia Yehova?

6 Wakati fulani, ni muzazi njo anaacha kweli na hata familia. (Zb. 27:10) Ile hali ni ya mubaya sana kwa watoto wenye walikuwa wanaona wazazi wao kuwa mufano muzuri. Esther, mwenye baba yake alitengwa, anasema hivi: “Mara mingi nilikuwa nalia juu nilitambua kama hakuacha tu kweli, yeye peke alichagua pia kumuacha Yehova. Napendaka baba yangu, lakini wakati alitengwa kila mara nilikuwa nasikia wasiwasi juu ya hali yake. Na hata nilikuwa na woga sana.”

7. Yehova anajisikiaka namna gani kuhusu kijana mwenye muzazi wake ametengwa?

7 Kijana, ikiwa mumoja kati ya wazazi wako ametengwa, roho yetu na siye inaluma! Lakini ukuwe hakika kama Yehova naye pia anaelewa muzuri maumivu yako. Anakupenda na anasamini sana ushikamanifu wako, na siye pia ndugu na dada zako. Usisahau kama, haiko weye njo ulikamata uamuzi wa muzazi wako. Sawa vile tulisema mbele, Yehova alipatia kila mwanadamu uhuru wa kuchagua. Na kila ndugu ao dada mwenye alishajitoa kwa Yehova na kubatizwa anapaswa ‘kubeba muzigo wa daraka yake mwenyewe.’​—Gal. 6:5, maelezo ya chini.

8. Watu wa familia ya ule mwenye alitengwa wanaweza kufanya nini wakati wako wanachunga mupendwa wao amurudilie Yehova? (Ona kisanduku “ Umurudilie Yehova.”)

8 Wakati mutu mwenye unapenda anaacha kumutumikia Yehova, ni jambo ya kawaida kuwa na tumaini kama kuko siku moja atamurudiliaka. Lakini mbele ile siku ifike, unaweza kufanya nini? Tunza afya yako ya kiroho. Kama unafanya vile, utawekea mufano muzuri watu wengine wa familia yako na pengine hata ule mwenye alitengwa. Tena, utapata nguvu ya kupambana na huzuni yako. Acha tuzungumuzie mambo fulani yenye unaweza kufanya.

MAMBO UNAWEZA KUFANYA JUU UENDELEE KUWA NGUVU KIROHO

9. Ni mu njia gani unaweza kupata nguvu kutoka kwa Yehova? (Ona pia kisanduku “ Maandiko Yenye Inaweza Kukufariji Wakati Mupendwa Wako Anamuacha Yehova.”)

9 Uendelee kutia nguvu imani yako. Ni jambo ya lazima sana uendelee kutia nguvu hali yako ya kiroho na hali ya kiroho ya watu wa familia yako. Unaweza kufanya vile namna gani? Tafuta nguvu kutoka kwa Yehova kwa kuendelea kuheshimia programu yako ya kusoma Biblia, kufikiri sana juu ya mambo yenye uko unajifunza, lakini pia kwa kukusanyika. Joanna, mwenye baba yake na dada yake waliacha kweli, anasema hivi: “Nasikiaka utulivu fulani unakuya wakati nasoma habari ya Biblia juu ya watu sawa vile Abigaili, Esta, Yobu, Yosefu, na Yesu. Mifano yao inanitiaka moyo na inanisaidiaka niendelee kuwa na mawazo ya muzuri, yenye inatulizaka huzuni yangu. Tena, naonaka kama nyimbo zetu za pekee za JW Télédiffusion zinanitiaka moyo sana.”

10. Namna gani Zaburi 32:6-8 inatusaidia kuvumilia wakati tuko na mahangaiko?

10 Umuambie Yehova mahangaiko yako. Wakati uko na mahangaiko usiache kusali kwa Yehova. Umuombe Baba yetu mwenye upendo akusaidie ukuwe na mawazo yenye kufaa juu ya hali yako sawa vile yeye, na akupatie “ufahamu na kukufundisha katika njia yenye unapaswa kufuata.” (Soma Zaburi 32:6-8.) Kwa kweli, inaweza kuwa nguvu sana kumuambia Yehova namna unajisikia kabisa. Lakini ujue kama Yehova anaelewa muzuri sana maumivu ya moyo wako. Anakupenda sana na anakuomba umuambie mambo yote yenye iko mu moyo wako.​—Kut. 34:6; Zb. 62:7, 8.

11. Kulingana na Waebrania 12:11, juu ya nini tunapaswa kutumainia nizamu ya Yehova yenye upendo? (Ona pia kisanduku “ Kutenga Mutenda-Zambi Mwenye Hatubu ni Alama ya Upendo wa Yehova.”)

11 Uunge mukono uamuzi wa wazee. Kutenga mutenda-zambi mwenye hatubu ni mupango wa Yehova. Ni njia ya muzuri ya kusaidia mutu mwenye anaacha kumutumikia Yehova, na pia iko na faida sana kwa siye wote. (Soma Waebrania 12:11.) Watu fulani mu kutaniko wanaweza kusema kama wazee hawakukamata uamuzi wa muzuri. Lakini kumbuka kama, mara mingi, wale watu hawapendake kumusema mubaya ule mutu mwenye alitenda zambi. Kusema kweli, hatukuwake njo na habari zote. Njo maana, ni jambo ya hekima kutumainia uamuzi wenye wazee walikamata, uamuzi wenye ulitegemea kanuni za Biblia. Na ukuwe hakika kama walijikaza kuhumu “kwa ajili ya Yehova.”​—2 Ny. 19:6.

12. Ni baraka gani wamoja kati yetu walipata juu waliunga mukono nizamu ya Yehova?

12 Wakati unategemeza uamuzi wa wazee wenye ulifanya mupendwa wako atengwe, unaweza kumusaidia amurudilie Yehova. Dada Elizabeth, mwenye tulishataja, anasema hivi: “Ilikuwa nguvu sana kutokuzungumuza tena na mutoto yetu mwanaume. Lakini kisha tu yeye kumurudilia Yehova, alituambia kama alistahili kabisa kutengwa. Kisha wakati fulani, alisema kama alijifunza mambo mingi ya muzuri sana. Nimefikia kusamini sana nizamu ya Yehova.” Bwana yake Mark, anaongezea hivi: “Kisha wakati fulani, mutoto yetu aliniambia kama kati ya mambo yenye ilikuwa inamuchochea kumurudilia Yehova, kulikuwa musimamo wetu wa kutokushirikiana naye. Namushukuru sana Yehova juu alitusaidia tuendelee kuwa watiifu.”

13. Ni nini inaweza kukusaidia upambane na mahangaiko yako?

13 Uzungumuze na marafiki wenye wanaelewa namna unajisikia. Uzungumuze na Wakristo wakomavu wenye wanaweza kukusaidia kuendelea kuwa na mawazo ya muzuri. (Mez. 12:25; 17:17) Joanna, mwenye tulishataja, anasema hivi: “Mu moyo yangu, nilijisikia kuwa miye peke. Lakini kuzungumuza na marafiki wenye kutumainika kulinisaidia kupambana na hali yangu.” Sasa, tuseme nini, kama watu fulani mu kutaniko, wanasema mambo yenye inakufanya ujisikie tena mubaya zaidi?

14. Juu ya nini tunapaswa ‘kuendelea kuvumiliana na kusameheana kwa kupenda’?

14 Uvumilie ndugu na dada zako. Hatuwezi kutazamia kama kila mara watu watakuwa wanasema mambo yenye kufaa. (Yak. 3:2) Siye wote hatukamilike, njo maana usishangae wakati wengine hawajue waseme nini ao hata wanasema mambo yenye inaweza kukuumiza bila wao kujua. Kumbuka shauri yenye mutume Paulo alitupatia: “Muendelee kuvumiliana na kusameheana kwa kupenda hata kama mutu yeyote iko na sababu ya kulalamika juu ya mwingine.” (Kol. 3:13) Dada moja, mwenye mutu fulani wa mu familia yake alitengwa, anasema hivi: “Yehova alinisaidia nisamehe ndugu na dada zangu wenye walipenda kunitia moyo, hata kama walifanya vile mu njia yenye ilinihuzunisha.” Kutaniko inaweza kufanya nini ili kusaidia watu wa familia wenye mupendwa wao alitengwa?

KUTANIKO INAWEZA KUSAIDIA

15. Tunaweza kufanya nini ili kusaidia watu wa familia wenye mupendwa wao alitengwa?

15 Ukaribishe kwa furaha familia ya mwenye alitengwa. Dada Miriam anasema waziwazi kama hakujisikia muzuri sana kuenda ku mikutano kisha ndugu yake kutengwa. Alisema hivi: “Niliogopea mambo yenye watu wangesema. Lakini kulikuwa ndugu na dada wengi wenye walihuzunika sana juu ya hali yenye ilitokea, na hawakukasirika ao kusema jambo fulani ya mubaya juu ya ndugu yangu mwenye alitengwa. Juu walinisaidia, sikujisikia miye peke.” Dada mwingine anasema hivi: “Kisha mutoto yetu mwanaume kutengwa, marafiki walikuja kutufariji. Wengine walisema waziwazi kama hawakujua waseme nini. Tulilia na wengine walinitia moyo kupitia barua. Mambo yenye walifanya ilinisaidia sana!”

Kutaniko inaweza kutegemeza watu wa familia ya ule mutu mwenye alitengwa (Ona fungu ya 17) *

16. Namna gani kutaniko inaweza kuendelea kusaidia na kufariji familia ya mwenye alitengwa?

16 Endelea kutegemeza familia ya ule mwenye alitengwa. Wako na lazima ya upendo wako na vitia-moyo vyako sana kuliko hata zamani. (Ebr. 10:24, 25) Wakati fulani, watu wa familia ya mwenye alitengwa wanajisikiaka sawa vile nao pia walitengwa na kutaniko. Hatupende wajisikie vile! Zaidi sana vijana wenye wazazi wao walitengwa wako na lazima sana ya vitia-moyo na kupongezwa. Maria, mwenye bwana yake alitengwa na kisha akaacha familia, anasema hivi: “Marafiki wangu fulani walikuya ku nyumba na walipika chakula na walinisaidia kujifunza pamoja na watoto wangu. Walihuzunika pamoja na miye na tulilia pamoja. Walinitetea wakati watu wengine walisema mambo yenye haiko ya kweli juu yangu. Kusema kweli, walinitia moyo sana!”​—Ro. 12:13, 15.

17. Wazee wanaweza kufanya nini ili kufariji wale wenye walipatwa na magumu?

17 Wazee, mutumie nafasi mbalimbali ili kutia nguvu familia ya ule mwenye alitengwa. Muko na daraka ya pekee ya kufariji Wakristo wenzenu wenye mupendwa wao aliacha Yehova. (1 Te. 5:14) Muwatie moyo mbele na kisha mikutano. Muwatembelee kwao na musali pamoja nao. Muhubiri pamoja nao, ao wakati fulani muwaalike wakuje ku ibada yenu ya familia. Kama vile Yehova, wachungaji wa kiroho wanapaswa kuonyesha huruma, upendo, na kuhangaikia kondoo wenye wako mu magumu.​—1 Te. 2:7, 8.

USIPOTEZE TUMAINI NA UENDELEE KUMUTUMAINIA YEHOVA

18. Kulingana na 2 Petro 3:9, Mungu anataka wale wenye walishamuacha wafanye nini?

18 Yehova “hataki mutu yeyote aharibiwe lakini anataka wote wafikie kutubu.” (Soma 2 Petro 3:9.) Hata kama mutu anaweza kutenda zambi nzito, uzima wake ungali tu wa maana ku macho ya Mungu. Usisahau kama Yehova alitoa uzima wa mwana wake mupendwa kwa ajili ya kila mumoja wetu. Kwa upendo, Yehova anajaribu kusaidia wale wenye walishamuacha ili wamurudilie. Anatumainia kama watafanya yao yote ili kumurudilia, sawa vile mufano wa Yesu wa mwana mupotevu unaonyesha. (Lu. 15:11-32) Wengi wenye waliacha kweli walifikia kumurudilia Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo na kutaniko iliwakaribisha kwa furaha sana. Elizabeth, mwenye tulishataja, alijionea na macho yake furaha ya kuona mutoto yake mwanaume anarudishwa mu kutaniko. Anasema hivi: “Niko na furaha sana juu walitutia moyo tusipoteze tumaini.”

19. Juu ya nini tunapaswa kuendelea kumutumainia Yehova?

19 Kila siku tunaweza kuendelea kumutumainia Yehova. Kila mara, mashauri yake inakuwaka tu kwa faida yetu. Iko mukarimu na Baba mwenye huruma mwenye anapenda sana wale wote wenye wanamupenda na kumuabudu. Ukuwe hakika kama Yehova hatakuacha wakati uko mu magumu. (Ebr. 13:5, 6) Mark, mwenye tulishataja, anasema hivi: “Hakuna siku Yehova alituacha. Hakuwake mbali na siye wakati tuko mu magumu.” Yehova ataendelea kukupatia “nguvu zenye kupita zile za kawaida.” (2 Ko. 4:7) Ndiyo, unaweza kubakia muaminifu na kuendelea kuwa na tumaini hata kama mupendwa wako anamuacha Yehova.

WIMBO 44 Sala ya Mutu wa Hali ya Chini

^ fu. 5 Inaletaka huzuni sana wakati mupendwa wetu anamuacha Yehova! Hii habari inaonyesha vile Yehova anajisikiaka wakati ile hali inatokea. Tena, inaonyesha mambo yenye watu wa familia ya ule mwenye alitengwa wanaweza kufanya ili kupambana na ile huzuni na pia namna wanaweza kubakia nguvu kiroho. Mu hii habari, tutaona pia namna kutaniko yote inaweza kufariji na kutegemeza familia ya ule mwenye alitengwa.

^ fu. 1 Majina fulani mu hii habari imebadilishwa.

^ fu. 79 MAFASIRIO YA PICHA: Wakati ndugu moja anaacha familia yake na anaacha Yehova, bibi na watoto wake wanateseka.

^ fu. 81 MAFASIRIO YA PICHA: Wazee wawili wanatembelea familia moja ya mu kutaniko yao ili kuwatia moyo.