Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Utafuata Kanuni za Yehova juu ya Haki?

Utafuata Kanuni za Yehova juu ya Haki?

“Nitatangaza jina la Yehova . . . , Mungu wa uaminifu, ambaye hana ukosefu wowote wa haki.”—KUMBUKUMBU LA TORATI 32:3, 4.

NYIMBO: 110, 2

1, 2. (a) Namna gani Nabothi na watoto wake walitendewa bila haki? (b) Tutazungumuzia sifa gani mbili katika habari hii?

WANAUME wawili wabaya wanashitaki mwanaume mumoja kuwa amefanya kosa kubwa. Mambo yenye wanasema ni ya uongo. Lakini mwanaume huyo anahukumiwa kuwa mwenye kosa na anapaswa kuuawa. Wazia namna watu wenye kupenda haki walijisikia wakati walikuwa wanaona namna mwanaume huyo mwenye hakukuwa na kosa pamoja na watoto wake wanaume wanapigwa majiwe na kuuawa! Hiyo haiko hadisi tu. Mambo hayo yalimupata kabisa mutumishi mumoja wa Yehova mwenye kuitwa Nabothi, mwenye aliishi wakati Mufalme Ahabu alikuwa anatawala Israeli.—1 Wafalme 21:11-13; 2 Wafalme 9:26.

2 Katika habari hii, tutazungumuzia mambo yenye yalimupata Nabothi. Tutazungumuzia pia kosa nzito lenye muzee mumoja muaminifu wa kutaniko moja la Kikristo la wakati wa mitume alifanya. Mifano hiyo mbili itatuonyesha namna sifa ya unyenyekevu na ya kuwa tayari kusamehe ni za lazima ikiwa tunapenda kufuata kanuni za Yehova juu ya haki.

TENDO LA MUBAYA SANA LA UKOSEFU WA HAKI

3, 4. Nabothi alikuwa mutu wa namna gani, na sababu gani alikataa kuuzisha shamba lake kwa Mufalme Ahabu?

3 Nabothi alikuwa muaminifu kwa Yehova wakati Waisraeli wengi walikuwa wanafuata mufano mubaya wa Mufalme Ahabu na bibi yake Yezebeli, malkia mubaya. Waliabudu Baali, mungu wa uongo na hawakuheshimia Yehova ao sheria zake. Lakini, Nabothi aliona urafiki wake pamoja na Yehova kuwa wa maana zaidi kuliko hata uzima wake.

4 Soma 1 Wafalme 21:1-3. Wakati Ahabu alipenda kuuza shamba la mizabibu la Nabothi ao kumupatia shamba lingine la muzuri zaidi pa nafasi ya shamba hilo, Nabothi alikataa. Sababu gani? Alieleza hivi kwa heshima: ‘Ni jambo lisilowaziwa kwangu, kwa maoni ya Yehova, kwamba mimi nikupe fungu la uriti la mababu zangu.’ Nabothi alikataa ombi la Mufalme Ahabu kwa sababu sheria ya Yehova ilikataza kuuzisha uriti wa familia milele. (Mambo ya Walawi 25:23; Hesabu 36:7) Kwa kweli, Nabothi alikuwa anamutii Yehova.

5. Yezebeli alifanya nini ili apate shamba la mizabibu la Nabothi?

5 Wakati Nabothi alikataa kuuzisha shamba lake la mizabibu, Mufalme Ahabu na bibi yake walifanya mambo ya mubaya sana. Ili kupata shamba hilo, Malkia Yezebeli aliomba wanaume wawili wamushitaki Nabothi juu ya kosa lenye hakufanya. Kwa hiyo, Nabothi na watoto wake wanaume waliuawa. Yehova alifanya nini juu ya tendo hilo la mubaya sana la ukosefu wa haki?

HAKI YA MUNGU

6, 7. Namna gani Yehova alionyesha kuwa anapenda haki, na sababu gani hilo lilipaswa kutia moyo familia ya Nabothi na marafiki wake?

6 Bila kukawia Yehova alimutuma Eliya aende kukutana na Ahabu. Eliya alimuambia Ahabu kuwa alikuwa muuaji na mwizi. Yehova alichukua uamuzi gani? Ahabu, bibi yake, na watoto wake wangeuawa kama vile Nabothi na watoto wake walikuwa wameuawa.​—1 Wafalme 21:17-25.

7 Watu wa familia ya Nabothi na marafiki wake walihuzunika juu ya mambo ya mubaya sana yenye Ahabu alikuwa amefanya. Lakini Yehova aliona ukosefu huo wa haki na akatenda bila kukawia. Hilo lilipaswa kuwafariji. Lakini, pengine unyenyekevu wao na tumaini lao kwa Yehova vilijaribiwa na mambo yenye yalitokea kisha hapo.

8. Ahabu alitenda namna gani wakati alisikia ujumbe wa Yehova, na matokeo yalikuwa nini?

8 Wakati Ahabu alisikia mambo yenye Yehova alikuwa ameamua kumufanyia, “akayararua [akapasua] mavazi yake, akavaa nguo za magunia mwilini mwake; naye akaanza kufunga, akaendelea kulala katika nguo za magunia, akatembea kwa huzuni.” Ahabu alijinyenyekeza. Matokeo yalikuwa nini? Yehova alimwambia Eliya hivi: ‘Kwa sababu amejinyenyekeza kwa ajili yangu, sitauleta ule musiba katika siku zake. Katika siku za mwana wake nitauleta musiba ule juu ya nyumba yake.’ (1 Wafalme 21:27-29; 2 Wafalme 10:10, 11, 17) Yehova, ‘muchunguzaji wa mioyo,’ mwenye anaweza kuona namna mutu iko kabisa, alionyesha Ahabu rehema.​—Methali 17:3.

UNYENYEKEVU NI ULINZI

9. Sababu gani unyenyekevu ungekuwa ulinzi kwa familia ya Nabothi na marafiki wake?

9 Wakati watu wa familia ya Nabothi na marafiki wake walisikia kama familia ya Ahabu ingepewa malipizi kisha kifo cha Ahabu, pengine hilo lilijaribu imani yao kwa Mungu. Lakini unyenyekevu ungewasaidia kulinda imani yao. Sababu gani? Ikiwa walikuwa wanyenyekevu, wangeendelea kumuabudu Yehova, na kutumaini kuwa Mungu hawezi hata kidogo kutenda bila haki. (Soma Kumbukumbu la Torati 32:3, 4.) Wakati unaokuja, watu wa familia ya Nabothi watapata baraka ya kuona wapendwa wao wakati wa ufufuo. Kutakuwa haki kamilifu kwa Nabothi na watoto wake. (Ayubu 14:14, 15; Yohana 5:28, 29) Mutu munyenyekevu anajua kama ‘Mungu wa kweli ataleta kila kazi katika hukumu, kuhusiana na kila jambo lililofichwa, liwe njema ao mbaya.’ (Mhubiri 12:14) Yehova anachunguza mambo yenye sisi hatujue. Kwa hiyo, unyenyekevu unatulinda ili tusipoteze imani yetu katika Yehova.

10, 11. (a) Ni hali gani zinaweza kujaribu namna yetu ya kuona haki? (b) Ni katika njia gani unyenyekevu utatulinda?

10 Utatenda namna gani ikiwa wazee wanakamata uamuzi wenye hauelewe ao wenye haukubaliane nao? Kwa mufano, utafanya nini ikiwa wewe ao mutu mwenye unapenda anapoteza daraka fulani katika utumishi wa Yehova? Utafanya nini ikiwa bibi ao bwana yako, ao mutoto wako, ao rafiki yako, anatengwa na kutaniko na haukubaliane na uamuzi wa wazee? Utafanya nini ikiwa unafikiri kuwa wazee walifanya kosa kwa kuonyesha rehema mutu fulani mwenye alifanya zambi? Hali hizo zinaweza kujaribu imani yetu katika Yehova na katika namna amepanga kutaniko leo. Namna gani unyenyekevu utakulinda ikiwa unajaribiwa katika hali moja kati ya hali hizo? Tuchunguze basi njia mbili.

Utatenda namna gani ikiwa wazee wanatangaza uamuzi wenye haukubaliane nao? (Picha hii inapatana na fungu la 10, 11)

11 Kwanza, ikiwa tuko wanyenyekevu tutakubali kama hatujue mambo yote. Hata kama tunafikiri kuwa tunajua mambo yote juu ya hali fulani, ni Yehova tu ndiye anajua mambo yenye kuwa ndani ya moyo wa mutu. (1 Samweli 16:7) Ikiwa tunakumbuka jambo hilo, tutakubali kwa unyenyekevu kuwa tuko na mipaka na kuwa tunapaswa kubadilisha mawazo yetu. Pili, ikiwa tumetendewa bila haki ao tumeona mutu mwengine ametendewa hivyo, unyenyekevu utatusaidia kutii na kuvumilia na kungojea Yehova atengeneze mambo. Biblia inasema hivi: ‘Mambo yatawaendea vyema [muzuri] wale wanaomuogopa Mungu wa kweli.’ Biblia inasema pia hivi: ‘Lakini mambo hayatakuwa mema kwa muovu, wala hatarefusha siku zake.’ (Mhubiri 8:12, 13) Ikiwa tunaendelea kuwa wanyenyekevu, tutapata faida sisi wenyewe na watu wote wenye kuhusika.—Soma 1 Petro 5:5.

HALI YA UNAFIKI KATIKA KUTANIKO

12. Tutazungumuzia sasa habari gani, na sababu gani?

12 Wakristo wa kwanza-kwanza katika Antiokia ya Siria walipatwa na hali fulani yenye ilijaribu sifa yao ya unyenyekevu na ya kuwa tayari kusamehe. Tuzungumuzie basi habari hiyo na tuitumie ili kuchunguza mawazo yetu juu ya kusamehe wengine. Inaweza kutusaidia kuelewa sababu gani Yehova anaweza kutumia watu wenye hawakamilike bila kuregeza kanuni zake.

13, 14. Mutume Petro alikuwa na migawo gani, na namna gani alionyesha kama alikuwa na ujasiri?

13 Mutume Petro alikuwa muzee mwenye alijulikana muzuri sana na Wakristo wengi wa kwanza-kwanza. Alikuwa rafiki wa sana wa Yesu na alikuwa amepewa migawo ya maana. (Mathayo 16:19) Kwa mufano, katika mwaka wa 36, Petro alipewa mugawo wa kuhubiria Kornelio na watu wote wa nyumba yake. Sababu gani jambo hilo lilikuwa la pekee? Kwa sababu Kornelio hakukuwa Muyahudi; alikuwa mutu wa Mataifa mwenye hatahiriwe. Wakati Kornelio na watu wa nyumba yake walipokea roho takatifu, Petro alitambua kwamba wangeweza kubatizwa na kuwa Wakristo. Alisema hivi: ‘Je, mutu yeyote anaweza kuyakataza maji kwamba hawa wasibatizwe ambao wameipokea roho takatifu kama vile sisi tulivyoipokea?’ —Matendo 10:47.

14 Katika mwaka wa 49, mitume na wazee katika Yerusalemu walikutana ili kuamua ikiwa Wakristo wenye hawakukuwa Wayahudi walipaswa kutahiriwa. Kwenye mukutano huo, Petro alikumbusha kwa ujasiri ndugu hao kwamba alikuwa amejionea namna watu wa Mataifa wenye hawatahiriwe walipokea roho takatifu. Jambo hilo lenye Petro alijionea ndilo lilisaidia baraza lenye kuongoza kukamata uamuzi. (Matendo 15:6-11, 13, 14, 28, 29) Wakristo Wayahudi na wenye hawakukuwa Wayahudi, wote walipaswa kuwa wenye shukrani kwa sababu Petro alipata ujasiri wa kueleza mambo hayo. Ilipaswa kuwa mwepesi kwa Wakristo wa kwanza-kwanza kutumainia mwanaume huyo muaminifu mwenye kukomaa kiroho!—Waebrania 13:7.

15. Petro alifanya kosa gani wakati alikuwa katika Antiokia ya Siria? (Ona picha kwenye mwanzo wa habari hii.)

15 Muda mufupi kisha mukutano huo katika Yerusalemu, Petro alitembelea Antiokia ya Siria. Wakati alikuwa huko, alipitisha wakati pamoja na ndugu na dada wenye hawakukuwa Wayahudi. Wazia namna walifurahia kujifunza mambo fulani kupitia ujuzi na uzoefu wa Petro. Lakini, walipaswa kushangaa sana na kuumia wakati Petro aliacha mara moja kula pamoja nao. Petro alichochea Wakristo wengine Wayahudi, kutia ndani Barnaba, wafanye hivyo. Sababu gani Mukristo huyo mwenye kukomaa kiroho alifanya kosa hilo kubwa, lenye lingeleta mugawanyiko katika kutaniko? Na zaidi ya hilo, kosa la Petro linaweza kutufundisha jambo gani lenye linaweza kutusaidia ikiwa maneno ao matendo ya muzee fulani yanatuumiza?

16. Petro alikaripiwa namna gani, na tunaweza kujiuliza maulizo gani?

16 Soma Wagalatia 2:11-14. Petro aliogopa wanadamu. (Methali 29:25) Petro alijua mawazo ya Yehova juu ya watu wenye hawakukuwa Wayahudi. Lakini aliogopa kwamba Wayahudi wenye kutahiriwa wenye waliwatembelea kutoka Yerusalemu, hawangemuheshimia tena kwa sababu alikuwa anajiunga na Wakristo hao wenye hawakukuwa Wayahudi. Mutume Paulo aliambia Petro kwamba alikuwa anatenda kwa unafiki. Sababu gani? Kwa sababu Paulo alikuwa amesikia namna Petro alitetea Wakristo wenye hawakukuwa Wayahudi kwenye mukutano katika Yerusalemu katika mwaka wa 49. (Matendo 15:12; Wagalatia 2:13) Wakristo wenye hawakukuwa Wayahudi wenye Petro alikuwa amekosea wangetenda namna gani? Wangeacha jambo hilo liwakwaze? Petro angepoteza madaraka yake kwa sababu ya kosa hilo?

UKUWE MWENYE KUSAMEHE

17. Ni nini inaonyesha kama Yehova alimusamehe Petro?

17 Petro alikuwa munyenyekevu na alikubali karipio la mutume Paulo. Maandiko hayaseme kuwa Petro alipoteza daraka fulani. Na hata alifikia kuandika barua mbili zenye ziliongozwa na roho ya Mungu zenye zilifikia kuwa kati ya vitabu vya Biblia. Katika barua yake ya pili, wakati alikuwa anazungumuzia juu ya Paulo alimuita ‘ndugu yetu mupendwa Paulo.’ (2 Petro 3:15) Kosa la Petro lilipaswa kuwaumiza Wakristo wenye hawakukuwa Wayahudi. Lakini Yesu, mwenye kuwa kichwa cha kutaniko aliendelea kumutumikisha. (Waefeso 1:22) Ndugu na dada katika kutaniko walikuwa na nafasi ya kuiga Yesu na Baba yake kwa kusamehe Petro. Jambo la kufurahisha ni kwamba, hakuna mutu mwenye alikwazika kwa sababu ya kosa la mwanaume huyo mwenye hakukamilika.

18. Ni wakati gani tuko na lazima ya kufuata kanuni za Yehova juu ya haki?

18 Hakukuwa wazee wakamilifu katika kutaniko la Kikristo la kwanza-kwanza, na hakuna wazee wakamilifu katika kutaniko la Kikristo leo. Biblia inasema hivi: ‘Sisi sote tunajikwaa [tunafanya makosa] mara nyingi.’ (Yakobo 3:2) Ni vyepesi kukubali jambo hilo, lakini tutafanya nini wakati ndugu ao dada fulani anatukosea? Tutafuata kanuni za Yehova juu ya haki? Kwa mufano, utafanya nini ikiwa muzee fulani wa kutaniko anatoa maelezo yenye kuonekana kuwa na ubaguzi? Utakwazika ikiwa muzee anasema bila kufikiri jambo fulani lenye kukuumiza? Kuliko kufikiri mara moja kama ndugu huyo hastahili kuwa muzee, utavumilia na kuacha mambo katika mikono ya Yesu, kichwa cha kutaniko? Kuliko kukazia kosa lake, utakumbuka miaka mingi yenye ndugu huyo ametumikia Yehova kwa uaminifu? Ikiwa ndugu mwenye amekukosea anaendelea kuwa muzee ao hata anapewa madaraka mengine, utafurahi? Ikiwa uko tayari kusamehe, unaonyesha kuwa unafuata kanuni za Yehova juu ya haki.—Soma Mathayo 6:14, 15.

19. Tunapaswa kuazimia kufanya nini?

19 Kwa sababu tunapenda haki, tunangojea kwa hamu wakati Yehova atamaliza kabisa ukosefu wote wa haki wenye Shetani na ulimwengu wake wameleta. (Isaya 65:17) Mbele wakati huo ufike, ikiwa tunatendewa bila haki, tukubali kwa unyenyekevu kuwa pengine hatujue mambo yote na tukuwe tayari kusamehe wale wenye wanatukosea. Ikiwa tunafanya hivyo, tutaonyesha kuwa tunafuata kanuni ya Yehova juu ya haki.