Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI YA KUJIFUNZA YA 1

WIMBO 2 Jina Yako Ni Yehova

Umupatie Yehova Utukufu

Umupatie Yehova Utukufu

ANDIKO YETU YA MWAKA WA 2025: “Mumupatie Yehova utukufu wenye jina lake linastahili.”ZB. 96:8.

WAZO KUBWA

Kujifunza namna tunaweza kumupatia Yehova utukufu wenye anastahili.

1. Watu wengi leo wanahangaikia nini?

 NA WEYE ulishaona namna watu wengi leo wanajifikiria sana? Kwa mufano, watu fulani wanapitisha wakati mingi ku site za kupashana habari juu tu wengine wawaone na waone mambo yenye walifanya. Lakini, ni watu kidogo tu leo njo wanamupatia Yehova Mungu utukufu. Mu hii habari, tutaona maana ya kumupatia Yehova utukufu na tutaona ni nini inatuchochea kufanya vile. Tutaona pia namna tunaweza kumupatia Mungu utukufu wenye anastahili kabisa na namna yeye mwenyewe atatukuza jina yake hivi karibuni.

KUMUPATIA YEHOVA UTUKUFU MAANA YAKE NINI?

2. Yehova alionyesha utukufu wake namna gani ku Mulima Sinai? (Ona pia picha ku jalada.)

2 Utukufu maana yake nini? Mu Biblia, neno “utukufu” inaweza kumaanisha mambo yote ya ajabu yenye inaweza kushangaza mutu. Wakati kidogo kisha taifa ya Israeli kutoka mu utumwa Misri, Yehova alionyesha utukufu wake mu njia ya ajabu sana. Wazia namna mambo ilikuwa: Mamilioni ya Waisraeli wanakutana chini ya Mulima Sinai juu ya kusikiliza mambo yenye Mungu atawaambia. Wingu yenye giza inafunika mulima. Mara moya kunakuwa tetemeko ya inchi. Udongo unatetemeka kwenye wanasimama na kunatokea pia mwangaza wa radi, mungurumo, na sauti kubwa ya baragumu. (Kut. 19:16-18; 24:17; Zb. 68:8) Wazia namna wale Waisraeli walishangala sana wakati Yehova alionyesha utukufu wake mu ile njia ya ajabu sana.

Ku Mulima Sinai, Yehova alionyesha Waisraeli utukufu wake mu njia ya ajabu (Ona fungu ya 2)


3. Namna gani tunaweza kumupatia Yehova utukufu?

3 Wanadamu wanaweza pia kumupatia Yehova utukufu? Ndiyo. Njia moya ya kumupatia Yehova utukufu ni kuambia wengine juu ya nguvu zake za ajabu na sifa zake zenye kupendeza. Pia tunamupatia Mungu utukufu wakati tunamusifu kwa sababu ya mambo yenye anatuwezesha kufanya. (Isa. 26:12) Mufalme Daudi alimupatia Yehova utukufu. Yeye ni mufano muzuri sana kwetu. Mu sala yenye alitoa mbele ya kutaniko ya Israeli, alimuambia hivi Mungu: “Ee Yehova, ukubwa ni wako na nguvu na uzuri na sifa na utukufu, kwa maana kila kitu mbinguni na duniani ni chako.” Kisha Daudi kumaliza sala yake, “kutaniko lote likamusifu Yehova.”—1 Ny. 29:11, 20.

4. Namna gani Yesu alimupatia Yehova utukufu?

4 Wakati Yesu alikuwa ku dunia, alitukuza Baba yake kwa kuonyesha kama ni Baba yake njo alimupatia nguvu ya kufanya miujiza. (Mk. 5:18-20) Yesu alimutukuza Baba yake mu njia ingine. Alimutukuza kupitia namna alitendea wengine, na kupitia mambo yenye alisema juu ya Baba yake. Siku moya, Yesu alikuwa nafundisha mu sinagogi. Kati ya wenye walikuwa namusikiliza, kulikuwa mwanamuke moya mwenye alikuwa na pepo muchafu kwa miaka 18. Ule pepo muchafu alifanya mwili wa ule mwanamuke ukunjame mara mbili na hangeweza kusimama wima. Ile ilikuwa hali ya kuhuzunisha sana! Juu Yesu alimusikilia huruma, alimukaribia na akamuambia hivi kwa upole: “Mwanamuke, umefunguliwa kutoka katika uzaifu wako.” Kisha akamugusa na mara moya akasimama wima na “kuanza kumutukuza Mungu.” Ule mwanamuke alikuwa sasa na afya ya muzuri! (Lu. 13:10-13) Alikuwa na sababu ya muzuri ya kumupatia Yehova utukufu, na siye tuko na sababu za kufanya vile.

NI NINI INATUCHOCHEA KUMUPATIA YEHOVA UTUKUFU?

5. Juu ya nini tunamuheshimia Yehova?

5 Tunamupatia Yehova utukufu juu tunamuheshimia sana. Tuko na sababu mingi za kumuheshimia Yehova. Yeye ni Mweza-Yote; nguvu zake hazina mipaka. (Zb. 96:4-7) Hekima yake ya ajabu inaonekana wazi mu vitu vyenye aliumba. Ametupatia uzima na kila kitu yenye tuko nayo lazima juu tuendelee kuishi. (Ufu. 4:11) Ni mushikamanifu. (Ufu. 15:4) Mambo yote yenye anafanya inakuwaka na matokeo ya muzuri, na anatimiza mambo yote yenye anaahidi. (Yos. 23:14) Njo maana hatushangale kuona mambo yenye Yeremia alisema juu ya Yehova. Alisema hivi: “Kati ya watu wote wenye hekima wa mataifa na kati ya falme zao zote, hakuna mutu yeyote hata kidogo mwenye kuwa kama wewe.” (Yer. 10:6, 7) Bila shaka, tuko na sababu za muzuri za kuheshimia Baba yetu wa mbinguni. Lakini zaidi ya kustahili heshima yetu, anastahili pia upendo wetu. Juu ya nini?

6. Juu ya nini tunamupenda Yehova?

6 Tunamupatia Yehova utukufu juu tunamupenda sana. Fikiria sifa mingi zenye Yehova iko nazo zenye zinafanya tumupende. Iko na rehema na huruma. (Zb. 103:13; Isa. 49:15) Anajitia pa nafasi yetu; wakati tunaumia yeye pia anaumia. (Zek. 2:8) Anafanya ikuwe mwepesi kwetu kumukaribia na kuwa marafiki wake. (Zb. 25:14; Mdo. 17:27) Ni munyenyekevu; “anainama ili aangalie mbingu na dunia, anainua mutu wa hali ya chini kutoka katika mavumbi.” (Zb. 113:6, 7) Juu ya ile mambo yote, tunapenda kabisa kumupatia Mungu wetu Mukubwa utukufu.—Zb. 86:12.

7. Tuko na nafasi gani ya pekee?

7 Tunamupatia Yehova utukufu juu tunapenda wengine wamujue. Watu wengi hawajue kweli juu ya Yehova. Juu ya nini? Juu Shetani amepofusha akili zao kwa kueneza habari za bongo juu ya Yehova. (2 Ko. 4:4) Shetani amefanya watu waamini kama Yehova analipishaka kisasi, haangaikie watu, na ni yeye njo ameleta mateso mingi mu dunia. Lakini siye tunajua kweli juu ya Mungu wetu! Tuko na nafasi ya kuelezea watu ile kweli, na kwa kufanya vile tunamutukuza Yehova. (Isa. 43:10) Zaburi 96 inazungumuzia zaidi sana kuhusu kumupatia Yehova utukufu. Wakati tutakuwa nazungumuzia maneno fulani yenye kuwa mu ile zaburi yenye iliongozwa na roho ya Mungu, fikiria ni mu njia gani mbalimbali unaweza kumupatia Yehova utukufu wenye anastahili kabisa.

NAMNA GANI TUNAWEZA KUMUPATIA YEHOVA UTUKUFU WENYE ANASTAHILI?

8. Tunaweza kumupatia Yehova utukufu mu njia gani? (Zaburi 96:1-3)

8 Soma Zaburi 96:1-3.Tunaweza kumupatia Yehova utukufu kupitia mambo yenye tunasema juu yake. Mu hii andiko, watu wa Yehova wanaombwa ‘kumuimbia Yehova,’ ‘kusifu jina lake,’ ‘kutangaza habari njema za wokovu wake,’ na ‘kutangaza utukufu wake kati ya mataifa.’ Tunaweza kumupatia Baba yetu wa mbinguni utukufu mu zile njia zote. Wayahudi waaminifu na Wakristo wa mu karne ya kwanza hawakujizuia kuambia wengine kuhusu mambo ya muzuri yenye Yehova alikuwa amewafanyia na kuhusu sifa zake. (Da. 3:16-18; Mdo. 4:29) Na siye tunaweza kufanya vile namna gani?

9-10. Mufano wa Angelena unakufundisha nini? (Ona pia picha.)

9 Ona mufano wa dada Angelena, a mwenye kuishi mu Amerika. Kwa uhodari, alimutetea Yehova ku kazi. Angelena alikuwa mufanyakazi mupya na alialikwa ku mukutano fulani. Ku ule mukutano, wafanyakazi wote wapya waliombwa kusema jambo fulani kuhusu maisha yao. Angelena alitayarisha picha mbalimbali zenye zinaonyesha furaha yenye iko nayo juu iko Shahidi wa Yehova. Lakini, mbele tu wakati yake ya kusema ifike, mufanyakazi mwingine alijitambulisha na kusema kama alikomalia mu familia ya Mashahidi wa Yehova. Alianza kusema mambo ya mubaya juu ya imani yetu. Angelena anasema hivi: “Moyo ulianza kunipiga mbiombio. Lakini nilijiuliza hivi: ‘Nitaacha huyu mutu aseme bongo juu ya Yehova? Ao nitamutetea Yehova?’”

10 Wakati ule mufanyakazi alimaliza kusema, Angelena alitoa sala ya mufupi mu moyo. Kisha kwa upole akamuambia hivi: “Hali yangu inafanana na yako. Na miye nilikomalia mu familia ya Mashahidi wa Yehova, na niko Shahidi mupaka leo.” Hata kama hali haikukuwa mwepesi, Angelena alibakia mwenye kutulia na alionyesha wafanyakazi wenzake picha fulani zenye zilionyesha namna yeye na marafiki wake walikuwa na furaha mu kazi ya Yehova, na kwa heshima alitetea mambo yenye anaamini. (1 Pe. 3:15) Matokeo ilikuwa nini? Wakati Angelena alimaliza kuzungumuza, ule mwanaume alitulia. Na hata alisema kama anakumbuka mambo ya muzuri yenye alijionea wakati alikuwa nakomalia mu familia ya Mashahidi wa Yehova. Angelena anasema hivi: “Yehova anastahili kutetewa. Ni pendeleo kutetea jina yake.” Siye pia tuko na pendeleo ya kumusifu Yehova na kumutukuza, hata wakati wengine wanamukosea heshima.

Tunaweza kumupatia Yehova utukufu kupitia maneno yetu, vitu vyetu, na mwenendo wetu (Ona fungu ya 9-10, 12, 14) b


11. Tangu zamani, namna gani waabudu wa kweli wamefuata kanuni yenye kuwa mu Zaburi 96:8?

11 Soma Zaburi 96:8. Tunaweza kumupatia Yehova utukufu kupitia vitu vyetu. Tangu zamani, waabudu wa kweli wanamupatia Yehova utukufu mu ile njia. (Mez. 3:9) Kwa mufano, Waisraeli walitoa michango juu ya kusaidia kujenga na kutunza hekalu. (2 Fa. 12:4, 5; 1 Ny. 29:3-9) Wanafunzi fulani wa Yesu walimuhangaikia na kumutumikia yeye na mitume wake “kwa kutumia mali zao.” (Lu. 8:1-3) Wakristo wa karne ya kwanza pia walitoa misaada kwa ajili ya ndugu na dada zao. (Mdo. 11:27-29) Leo, siye pia tunaweza kumupatia Yehova utukufu kwa kutoa michango ya kujipendea.

12. Namna gani michango yetu inamuletea Yehova utukufu? (Ona pia picha.)

12 Fikiria mufano moya tu yenye inaonyesha kama michango yetu inamuletea Yehova utukufu. Ripoti fulani mu 2020 ilionyesha matokeo yenye kipwa ya muda murefu ilikuwa nayo mu inchi ya Zimbabwe. Watu wengi sana walikosa chakula. Dada yetu Prisca naye alikosa chakula. Hata kama hali kaikukuwa muzuri, Prisca aliendelea na programu yake ya kuhubiri kila Siku ya Tatu na Siku ya Tano. Alikuwa nafanya vile hata mu kipindi ya kulima. Majirani wake walimucheka juu alikuwa naenda mu mahubiri kuliko kuenda ku shamba. Walikuwa namuambia: “Utakufa na njala.” Prisca alikuwa nawajibia: “Yehova hayaachaka watumishi wake hata siku moya.” Kisha wakati kidogo, Prisca alipata musaada wenye tengenezo yetu ilitoa. Michango yetu ya kujipendea njo ilifanya ile misaada iweze kutolewa. Majirani wa Prisca walishangala sana na walimuambia hivi: “Mungu hayakuachiliaka, njo maana tunapenda kujua mambo mingi juu yake.” Watu saba kati ya majirani wake walianza kukusanyika.

Tunaweza kumupatia Yehova utukufu kupitia vitu vyetu (Ona fungu ya 12) c


13. Namna gani mwenendo wetu unaweza kumuletea Yehova utukufu? (Zaburi 96:9)

13 Soma Zaburi 96:9.Tunaweza kumupatia Yehova utukufu kupitia mwenendo wetu. Makuhani wenye walikuwa natumika ku hekalu walipaswa kuwa safi kimwili. (Kut. 40:30-32) Lakini, zaidi ya kuwa safi kimwili ni jambo ya maana sana kuwa na mwenendo safi. (Zb. 24:3, 4; 1 Pe. 1:15, 16) Tunapaswa kufanya nguvu yetu yote juu ya kutosha “utu wa zamani,” ni kusema kuacha mawazo na matendo machafu, kisha tunapaswa kuvala “utu mupya,” ni kusema kuwaza na kutenda mu njia yenye inaonyesha kama tunaiga sifa za Yehova zenye kupendeza. (Kol. 3:9, 10) Kwa musaada wa Yehova, hata mutu mwenye kuwa na mwenendo muchafu sana na mwenye kupenda jeuri, anaweza kubadilika na kuvala utu mupya.

14. Mufano wa Jack unakufundisha nini? (Ona pia picha.)

14 Ona mufano wa Jack. Alikuwa mutu hatari na wa jeuri sana, mupaka watu walimupanga jina Shetani. Juu ya mambo ya mubaya sana yenye alifanya, Jack alihukumiwa kifo. Lakini, wakati alikuwa nangoya siku ya kifo yake, alikubali kujifunza Biblia pamoya na ndugu mwenye alikuwa natembelea gereza. Hata kama zamani alikuwa na maisha ya mubaya sana, Jack alitosha utu wake wa zamani, na kisha wakati alistahili kubatizwa. Jack alibadilika sana. Siku yenye alipaswa kuuawa, walinzi fulani wa gereza walikuwa na machozi mu macho wakati walikuwa namulaga. Askari fulani mwenye alikuwa natumika ku ile gereza alisema hivi: “Zamani Jack njo alikuwa mufungwa mwenye tabia ya mubaya sana hapa. Sasa iko kati ya wafungwa wenye wako na tabia ya muzuri zaidi.” Juma yenye ilifuata kisha kifo ya Jack, ndugu mwenye alikuya kuongoza mikutano ya kila juma mu gereza, alikutana na mufungwa mwenye alifika ku mikutano kwa mara ya kwanza. Nini ilichochea ule mufungwa akuye ku mikutano? Alishangala kuona namna Jack alibadilisha mwenendo wake na alipenda kujua jambo yenye na yeye anaweza kufanya juu amuabudu Yehova. Kwa kweli, mwenendo wetu unaweza kumuletea Baba yetu wa mbinguni utukufu!—1 Pe. 2:12.

Tunaweza kumupatia Yehova utukufu kupitia mwenendo wetu (Ona fungu ya 14) d


NAMNA YEHOVA ATATUKUZA JINA YAKE HIVI KARIBUNI

15. Yehova atatukuza namna gani jina yake hivi karibuni? (Zaburi 96:10-13)

15 Soma Zaburi 96:10-13.Mistari ya mwisho-­mwisho ya Zaburi 96 inaonyesha kama Yehova ni Muamuzi na Mufalme mwenye haki. Namna gani Yehova atatukuza jina yake hivi karibuni? Kwa kuhukumu kwa haki. Hivi karibuni, Yehova ataharibu Babiloni Mukubwa juu imechafua jina yake takatifu. (Ufu. 17:5, 16; 19:1, 2) Watu fulani wenye wataona vile Babiloni Mukubwa inaharibiwa wanaweza kujiunga na siye mu ibada ya kweli. Ku mwisho, wakati wa Armagedoni, Yehova ataharibu ulimwengu wote wa Shetani, ni kusema wote wenye kumupinga na kutukana jina yake; lakini ataokoa wote wenye kumupenda na kumutii na wenye wanafurahia kumupatia utukufu. (Mk. 8:38; 2 Te. 1:6-10) Kisha jaribu ya mwisho yenye itakuwa kisha Miaka Elfu ya Utawala wa Kristo, Yehova atatakasa kabisa-kabisa jina yake. (Ufu. 20:7-10) Ile wakati, “dunia itajaa ujuzi juu ya utukufu wa Yehova kama vile maji yanafunika bahari.”—Hab. 2:14.

16. Tunaazimia kufanya nini? (Ona pia picha.)

16 Itafurahisha sana wakati kila mutu mwenye kuishi atapatia Yehova utukufu wenye jina yake inastahili! Lakini mbele ile wakati ifike, tutumie kila nafasi juu ya kupatia Mungu wetu utukufu. Ili kukazia ile jambo ya maana sana, Baraza Yenye Kuongoza imechagua Zaburi 96:8 kuwa andiko yetu ya mwaka wa 2025: Mumupatie Yehova utukufu wenye jina lake linastahili.”

Ku mwisho, kila mutu mwenye kuishi atamupatia Yehova utukufu wenye jina yake inastahili! (Ona fungu ya 16)

WIMBO 12 Yehova Ni Mungu Mukubwa

a Majina fulani imebadilishwa.

b MAFASIRIO YA PICHA: Ku Mulima Sinai, Yehova alionyesha Waisraeli utukufu wake mu njia ya ajabu. Picha zenye kuonyesha mambo yenye ilifikia Angelena, Prisca, na Jack. Picha yenye kuonyesha mambo yenye ilifikia Angelena.

c MAFASIRIO YA PICHA: Picha yenye kuonyesha mambo yenye ilifikia Prisca.

d MAFASIRIO YA PICHA: Picha yenye kuonyesha mambo yenye ilifikia Jack.