Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI YA KUJIFUNZA YA 52

Dada Vijana​—⁠Mujikaze Kuwa Wakristo Wenye Kukomaa Kiroho

Dada Vijana​—⁠Mujikaze Kuwa Wakristo Wenye Kukomaa Kiroho

“Vilevile wanamuke wanapaswa [kuwa] . . . na kiasi katika tabia zao, na waaminifu katika mambo yote.”—1 TI. 3:11.

WIMBO 133 Umuabudu Yehova Wakati Ungali Kijana

KIFUPI YA HABARI a

1. Tunapaswa kufanya nini ili tukomae kiroho?

 INASHANGAZA sana kuona namna watoto wanakomaa haraka sana na kuwa watu wazima. Ni sawa vile hakuna kitu yenye mutoto anafanyaka juu akomae. Lakini, juu mutu akomae kiroho inaomba ajikaze. b (1 Ko. 13:11; Ebr. 6:1) Ili tufikie kukomaa kiroho, tunapaswa kuwa na urafiki wa sana pamoya na Yehova. Tuko pia na lazima ya roho yake takatifu ili tuweze kuwa na sifa zenye zinamupendeza, ili tujifunze ufundi fulani, na ili kujitayarisha kwa ajili ya madaraka yenye tunaweza kuwa nayo wakati wenye kuja.—Mez. 1:5.

2. Tunajifunza nini mu Mwanzo 1:​27, na tutazungumuzia nini mu hii habari?

2 Yehova aliumba wanadamu mwanaume na mwanamuke. (Soma Mwanzo 1:27.) Wanaume na wanamuke hawako tu tofauti kimwili, wako pia tofauti mu mambo ingine. Kwa mufano, kuko kazi zenye Yehova alipatia wanaume na kazi zenye alipatia wanamuke. Kwa hiyo, kila mutu iko na lazima ya sifa na ufundi fulani wenye utamusaidia kutimiza madaraka yake. (Mwa. 2:18) Mu hii habari, tutazungumuzia mambo yenye dada kijana anaweza kufanya ili kufikia kuwa Mukristo mwenye kukomaa kiroho. Mu habari yenye kufuata, tutazungumuzia mambo yenye ndugu kijana anapaswa kufanya.

KOMALISHA SIFA ZENYE KUMUFURAHISHA MUNGU

Kuiga sifa za wanamuke waaminifu sawa vile Rebeka, Esta, na Abigaili, kutakusaidia ukuwe mwanamuke Mukristo mwenye kukomaa kiroho (Ona fungu ya 3-4)

3-4. Dada vijana wanaweza kupata wapi mifano ya muzuri ya kuiga? (Ona pia picha.)

3 Biblia inazungumuzia mifano mingi ya wanamuke wa pekee wenye walimupenda na kumutumikia Yehova. (Ona ku jw.org habari “Wanamuke Wenye Kuzungumuziwa mu Biblia Wanatufundisha Nini?”) Kama vile andiko yetu ya musingi inaonyesha, walikuwa “na kiasi katika tabia zao, na waaminifu katika mambo yote.” Zaidi ya ile, dada vijana wanaweza kupata mu kutaniko yao dada Wakristo wenye kukomaa kiroho wenye kuwa mifano mizuri ya kuiga.

4 Dada vijana, hamuone kama itakua muzuri mutafute mu kutaniko yenu dada fulani wenye kukomaa kiroho wenye munaweza kuiga? Mutambue sifa zao za muzuri, kisha muone namna munaweza pia kuzionyesha. Mu fungo zenye kufuata, tuzungumuzie sifa tatu za maana zenye dada mwenye kukomaa kiroho iko nazo lazima.

5. Juu ya nini unyenyekevu ni sifa ya maana ili kuwa dada Mukristo mwenye kukomaa kiroho?

5 Unyenyekevu ni sifa ya maana ili kuwa Mukristo mwenye kukomaa kiroho. Kama dada iko munyenyekevu, atakuwa na uhusiano muzuri pamoya na Yehova na pamoya na wengine. (Yak. 4:6) Kwa mufano, mwanamuke mwenye anamupenda Yehova anategemeza kwa unyenyekevu mupango wa ukichwa wenye Baba yake wa mbinguni aliweka. (1 Ko. 11:3) Kuko mambo yenye anaweza kufanya juu ya kuonyesha kama anategemeza ule mupango wa ukichwa mu kutaniko, na mambo ingine yenye anaweza kufanya juu ya kuonyesha kama anategemeza ule mupango mu familia. c

6. Mufano wa unyenyekevu wa Rebeka unaweza kufundisha nini dada vijana?

6 Tuzungumuzie mufano wa Rebeka. Alikuwa mwanamuke mwenye hekima mwenye mu maisha yake yote alijua namna ya kukamata maamuzi ya muzuri. Alijua pia wakati wa kutenda na namna ya kutenda. (Mwa. 24:58; 27:​5-17) Hata vile, alikuwa na heshima na alikuwa tayari kufuata muongozo. (Mwa. 24:​17, 18, 65) Kama unategemeza kwa unyenyekevu mupango ya Yehova kama vile Rebeka alifanya, utakuwa mufano muzuri mu familia yako na mu kutaniko.

7. Dada vijana wanaweza kuiga namna gani kiasi ya Esta?

7 Kiasi ni sifa ingine ya maana yenye Wakristo wote wenye kukomaa kiroho wako nayo lazima. Biblia inasema kama “wenye kiasi wako na hekima.” (Mez. 11:2) Esta alikuwa mwanamuke mwenye kiasi na mutumishi muaminifu wa Mungu. Juu alikuwa na kiasi, ile ilimusaidia asitende kwa kimbelembele. Alisikiliza na kufuata mashauri ya binamu yake Mordekai mwenye alikuwa amekomaa. (Est. 2:​10, 20, 22) Unaweza pia kuonyesha sifa ya kiasi kwa kutafuta mashauri ya muzuri na kuifuata.—Tit. 2:​3-5.

8. Kulingana na 1 Timoteo 2:​9, 10, namna gani sifa ya kiasi inasaidia dada akamate maamuzi ya hekima kuhusu namna ya kuvaa na kujipamba?

8 Esta alionyesha kiasi mu njia ingine. Alikuwa na “umbo ya muzuri na sura yenye kupendeza;” lakini, hakupenda kujionyesha. (Est. 2:​7, 15) Mufano wa Esta unaweza kusaidia namna gani dada Wakristo? 1 Timoteo 2:​9, 10 inaonyesha jambo yenye wanaweza kufanya. (Soma.) Paulo aliambia wanamuke Wakristo wavae kwa kiasi na akili ya muzuri. Neno ya kigiriki yenye kutumiwa mu hii andiko inaonyesha kama nguo zenye mwanamuke Mukristo anavaa zinapaswa kuonyesha kama anaheshimia wengine na anahangaikia mawazo yao. Tunawafurahia sana nyiye dada zetu Wakristo wenye kukomaa kiroho juu munavaa kwa kiasi!

9. Mufano wa Abigaili unaweza kutufundisha nini?

9 Utambuzi ni sifa ingine yenye dada wote wenye kukomaa kiroho wanaonyesha. Utambuzi ni nini? Ni uwezo wa kutofautisha jambo ya muzuri na ya mubaya na kuchagua kufanya jambo ya muzuri. Tuchunguze mufano wa Abigaili. Bwana yake alikamata uamuzi wa mubaya wenye ungekuwa na matokeo ya mubaya sana juu ya watu wote wa nyumba yake. Abigaili alitenda bila kukawia. Juu alitambua jambo ya muzuri ya kufanya, aliokoa maisha ya watu wengi. (1 Sa. 25:​14-23, 32-35) Utambuzi unatusaidia pia kujua wakati wa kusema na wakati wa kunyamaza. Na unatusaidia tuhangaikie wengine bila kuingia mu mambo yao ya kipekee.—1 Te. 4:11.

UJIFUNZE UFUNDI MBALIMBALI

Kujua kusoma na kuandika muzuri kumekusaidia namna gani? (Ona fungu ya 11)

10-11. Namna gani kujua kusoma na kuandika muzuri kutakuletea faida weye na wengine pia? (Ona pia picha.)

10 Mwanamuke Mukristo iko na lazima ya kujifunza kazi mbalimbali zenye zinaweza kumusaidia mu maisha yake ya kila siku. Mambo fulani yenye watoto wanamuke wanajifunza itawasaidia maisha yao yote. Tuone mifano fulani.

11 Ujifunze kusoma na kuandika muzuri. Mu desturi fulani, watu wanaona kama haiko lazima mwanamuke ajifunze kusoma na kuandika. Lakini, ile ni ya maana sana kwa Wakristo wote. d (1 Ti. 4:13) Kwa hiyo usiache kitu yoyote ikuzuie kujifunza kusoma muzuri na kuandika. Utapata faida gani? Kama unajua kusoma na kuandika, ile inaweza kukusaidia kupata kazi. Itakusaidia pia ukuwe unajifunza Neno ya Mungu na kuifundisha muzuri. Zaidi ya yote, itakusaidia ukuwe karibu sana na Yehova kadiri unaendelea kusoma sana Neno yake na kuifikiria sana.—Yos. 1:8; 1 Ti. 4:15.

12. Mezali 31:26 inaweza kukusaidia namna gani ujue kuzungumuza muzuri?

12 Ujifunze kuzungumuza muzuri na wengine. Ni jambo ya maana Wakristo wajifunze kufanya vile. Kuhusu ile jambo, Yakobo alitupatia hii shauri ya muzuri: “Kila mutu anapaswa kuwa mwepesi wa kusikiliza, hapana mwepesi wa kusema.” (Yak. 1:19) Wakati unasikiliza wengine kwa uangalifu wakati wako wanasema, unaonyesha kama ‘unajitia pa nafasi ya wengine.’ (1 Pe. 3:8) Ikiwa hauko hakika kwamba unaelewa mambo yenye mutu iko anasema ao namna iko anajisikia, umuulize maulizo yenye kufaa. Kisha ukamate wakati wa kuwaza mbele ya kusema. (Mez. 15:​28, maelezo ya chini.) Ujiulize hivi: ‘Mambo yenye ninataka kusema ni ya kweli na yenye kujenga? Ni ya heshima na ya muzuri? Ujifunze kupitia mufano wa dada wenye kukomaa kiroho wenye wanajua kuzungumuza muzuri. (Soma Mezali 31:26.) Chunguza kwa uangalifu mambo yenye wanasema na namna wanaisema. Vile uko unajifunza kuzungumuza muzuri na wengine, ni vile uhusiano wako nao utakuwa muzuri zaidi.

Mwanamuke mwenye amejifunza kushugulikia nyumba ni baraka kwa familia yake na kwa kutaniko yote (Ona fungu ya 13)

13. Unaweza kujifunza namna gani kushugulikia nyumba? (Ona pia picha.)

13 Ujifunze kushugulikia nyumba. Mu ma eneo ya mingi, wanamuke njo wanafanyaka kazi mingi za ku nyumba. Mama yako ao dada mwengine mwenye uzoefu anaweza kukufundisha namna ya kufanya kazi. Dada mwenye kuitwa Cindy anasema hivi: “Moya kati ya zawadi za maana sana zenye mama yangu amenipatia ni kunifundisha kufurahia kutumika sana. Kujifunza kazi sawa vile kupiga chakula, kufanya usafi, kushona, na kununua vitu, kumenisaidia mu maisha na kumenipatia nafasi ya kumutumikia Yehova zaidi. Mama alinifundisha pia namna ya kukaribisha wageni, na ile ilinisaidia nikutane na ndugu na dada wenye kuwa na sifa za muzuri zenye naweza kuiga.” (Mez. 31:​15, 21, 22) Mwanamuke mwenye anatumikaka sana, mukarimu, na mwenye amejifunza kushugulikia nyumba, ni baraka kwa familia yake na kwa kutaniko yote.—Mez. 31:​13, 17, 27; Mdo. 16:15.

14. Mufano wa Crystal unatufundisha nini, na ni nini itakusaidia kukazia mambo ya kiroho?

14 Ujifunze kujitimizia mahitaji. Ni jambo ya maana kwa Wakristo wote wakomavu kujifunza kujitimizia mahitaji yao. (Flp. 4:11) Dada mwenye kuitwa Crystal anasema hivi: “Wazazi wangu walinisaidia kuchagua mambo yenye ningesoma ku segondere yenye ingeweza kunisaidia nikuwe na ufundi fulani wenye utanisaidia mu maisha yangu. Baba yangu alinitia moyo nijifunze comptabilité, na ile imenisaidia sana.” Zaidi ya kujifunza ufundi wenye utakusaidia upate kazi fulani, ujikaze pia kujifunza namna ya kutumikisha makuta. (Mez. 31:​16, 18) Kama unaepuka madeni yenye haina lazima na unatosheka na maisha mepesi, ile itakusaidia kukazia mambo ya kiroho.—1 Ti. 6:8

UJITAYARISHE KWA AJILI YA MADARAKA YA WAKATI WENYE KUYA

15-16. Juu ya nini dada wenye hawayaolewa ni wa maana sana? (Marko 10:​29, 30)

15 Wakati unakomalisha sifa za kiroho na ufundi mbalimbali, ile itakusaidia mu wakati wenye kuya. Tuone mifano fulani ya mambo yenye unaweza kufanya.

16 Unaweza kuamua kubakia bila kuolewa kwa wakati fulani. Kupatana na maneno ya Yesu, dada fulani wanachagua kubakia bila kuolewa, hata kama desturi za kwao hazitie watu moyo kufanya vile. (Mt. 19:​10-12) Hali fulani inaweza pia kufanya mutu abakie bila kuolewa. Ukuwe hakika kama Yehova na Yesu hawazarau Wakristo wenye hawana bibi ao bwana. Mu dunia yote, dada wenye hawayaolewa wanafanya mambo mingi ya muzuri mu kutaniko. Juu hawa dada Wakristo wanapenda sana wengine na kuwahangaikia kabisa, ile inawachochea wakuwe dada na mama wa kiroho kwa ndugu na dada wengi.—Soma Marko 10:​29, 30; 1 Ti. 5:2

17. Dada kijana anaweza kujitayarisha namna gani leo juu afikie kuwa mutumishi wa wakati wote?

17 Unaweza kuwa mutumishi wa wakati wote. Dada Wakristo wanafanya mengi mu kazi ya kuhubiri mu dunia yote. (Zb. 68:11) Unaweza kujiwekea muradi wa kuingia mu utumishi wa wakati wote? Unaweza kuwa painia, unaweza kusaidia mu kazi ya ujenzi, ao kuwa Mwanabeteli. Sali kwa ajili ya muradi wako. Zungumuza na wengine wenye walifikia ule muradi, na uone ni nini yenye unapaswa kufanya ili ustahili kuwa mutumishi wa wakati wote. Kisha ukamate mipango yenye inaweza kukusaidia kufikia ule muradi. Kuwa mutumishi wa wakati wote kutakusaidia kufanya mambo mengi yenye kufurahisha mu kazi ya Yehova.

Kama unapenda kuolewa, unapaswa kuchagua kwa uangalifu sana mutu wa kuolewa naye (Ona fungu ya 18)

18. Juu ya nini dada anapaswa kuchagua kwa uangalifu sana mutu wa kuolewa naye? (Ona pia picha.)

18 Unaweza kuamua kuolewa. Sifa na ufundi fulani-fulani wenye tulizungumuzia utakusaidia ukuwe bibi muzuri. Lakini, kama uko nafikiria kuolewa, ujue kama unapaswa kuchagua muzuri mutu wa kuolewa naye. Ile ni moja kati ya maamuzi ya maana sana yenye utakamata mu maisha yako. Kumbuka kama utakuwa chini ya ukichwa wa mutu mwenye utachagua kuolewa naye. (Ro. 7:2; Efe. 5:​23, 33) Kwa hiyo ujiulize hivi: ‘Huyu ndugu ni wa kiroho? Je, anatia pa nafasi ya kwanza mambo ya kiroho mu maisha yake? Anakamataka maamuzi ya hekima? Anaweza kukubali makosa yake? Anaheshimiaka wanamuke? Iko na uwezo wa kunihangaikia kiroho, kimwili, na anaweza kuwa rafiki muzuri kwangu? Anatimizaka muzuri madaraka yake? Kwa mufano, anafanya kazi gani mu kutaniko na ile kazi anaifanya namna gani?’ (Lu. 16:10; 1 Ti. 5:8) Kusema kweli, kama unapenda upate ndugu mwenye atakuwa bwana muzuri, na weye unapaswa kujikaza kuwa dada mwenye atakuwa bibi muzuri.

19. Juu ya nini kuwa “musaidizi” ni daraka ya kuheshimisha?

19 Biblia inasema kama bibi muzuri ni “musaidizi” kwa bwana yake na ni “kikamilisho” chake. (Mwa. 2:18) Ile inaonyesha kama bibi ni wa hali ya chini? Hapana! Daraka ya kuwa musaidizi inamuheshimisha bibi. Juu ya nini? Juu mu Biblia hata Yehova anaitwa mara mingi “musaidizi.” (Zb. 54:4; Ebr. 13:6) Bibi ni musaidizi wa kweli wakati anamutegemeza bwana yake, na wakati anamusaidia kutimiza maamuzi yenye alikata juu ya familia. Juu anamupenda Yehova, anafanya yake yote ili kuheshimisha bwana yake. (Mez. 31:​11, 12; 1 Ti. 3:11) Unaweza kujitayarisha kuwa bibi muzuri kwa kutia nguvu upendo wako kwa Yehova na kwa kusaidia wengine ku nyumba na mu kutaniko.

20. Namna gani mama anaweza kusaidia familia yake?

20 Unaweza kuwa mama. Kisha ndoa, weye na bwana yako munaweza kuwa na watoto. (Zb. 127:3) Kwa hiyo, ni jambo ya lazima kufikiria ile mbele ya wakati. Sifa na ufundi mbalimbali wenye tulizungumuzia mu hii habari unaweza kukusaidia ukuwe bibi na mama muzuri. Upendo wako, fazili, na uvumilivu wako vitachangia ili mu nyumba yako mukuwe hali ya muzuri, mwenye watoto watajisikia salama na watakomaa mu hali ya muzuri.—Mez. 24:3.

Vijana wanamuke wengi wenye wamefundishwa kupitia maandiko na kutumikisha mambo yenye wamejifunza, wamekuwa Wakristo wenye kukomaa kiroho (Ona fungu ya 21)

21. Namna gani tunaona dada zetu, na juu ya nini? (Ona picha ku jalada.)

21 Dada, tunawapenda sana kwa sababu ya mambo yote yenye munafanya kwa ajili ya Yehova na watu wake. (Ebr. 6:10) Munatumika nguvu ili kukomalisha sifa za kiroho na kujifunza ufundi mbalimbali. Ile inafanya maisha yenu na ya wale wenye kuwazunguka ikuwe ya kufurahisha, na inawasaidia mujitayarishe muzuri kwa ajili ya madaraka yenu ya wakati wenye kuya. Dada, muko wa maana sana mu tengenezo ya Yehova!

WIMBO 137 Wanamuke Wenye Imani

a Dada vijana wapendwa, muko wa maana sana mu kutaniko. Munaweza kuwa Wakristo wenye kukomaa kiroho kwa kukomalisha sifa zenye kumufurahisha Mungu, kwa kujifunza ufundi mbalimbali, na kwa kujitayarisha kwa ajili ya madaraka yenye kuya. Mukifanya vile, mutapata baraka mingi mu utumishi wa Yehova.

b MAFASIRIO YA MANENO FULANI: Mutu mwenye amekomaa kiroho anaongozwa na roho ya Mungu, hapana hekima ya ulimwengu. Anafuata mufano wa Yesu, anapenda kubakia na uhusiano wa karibu pamoya na Yehova na anajitoa kwa upendo kwa ajili ya wengine.

d Ili kujua juu ya nini kusoma ni jambo ya maana ona ku jw.org habari “Juu ya Nini Kusoma Ni Jambo ya Maana kwa Watoto—Sehemu ya 1: Kusoma ao Kuangalia?