Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI YA KUJIFUNZA YA 50

Imani na Matendo Inaweza Kufanya Mutu Akuwe Mwenye Haki

Imani na Matendo Inaweza Kufanya Mutu Akuwe Mwenye Haki

“[Tembea] kwa utaratibu katika hatua za imani yenye baba yetu Abrahamu alikuwa nayo.”—RO. 4:12.

WIMBO 119 Tunapaswa Kuwa na Imani

KIFUPI YA HABARI a

1. Wakati tunachunguza mufano wa Abrahamu, tunaweza kujiuliza ulizo gani?

 HATA kama watu wengi wamesikia kuhusu Abrahamu, wengi hawajue habari mingi juu yake. Lakini, weye unajua mambo ya mingi juu ya Abrahamu. Kwa mufano, unajua kama Biblia inamuita “baba ya wale wote wenye kuwa na imani.” (Ro. 4:11) Lakini unaweza kujiuliza: ‘Naweza pia kutembea katika hatua za Abrahamu na kuwa na imani kama yake?’ Ndiyo, unaweza.

2. Juu ya nini ni jambo ya maana kujifunza mufano wa Abrahamu? (Yakobo 2:​22, 23)

2 Njia moya ya kutusaidia tukuwe na imani kama ya Abrahamu ni kujifunza kuhusu mufano wake. Kupatana na vile Mungu alimuomba, Abrahamu alisafiri mu eneo ya mbali, aliishi mu mahema kwa miaka mingi, na alijaribu kumutoa mwana wake Isaka mwenye alipenda sana. Ile matendo ilionyesha kama alikuwa na imani ya nguvu. Imani na matendo ya Abrahamu ilifanya Mungu amukubali na akuwe rafiki yake. (Soma Yakobo 2:​22, 23.) Yehova anapenda na siye, ni kusema na weye, ukubaliwe naye na ukuwe rafiki yake. Ile njo sababu yenye ilifanya aongoze waandikaji wa Biblia Paulo na Yakobo wazungumuzie mufano wa Abrahamu. Acha tuzungumuzie ile mufano, yenye iko mu Waroma sura ya 4 na Yakobo sura ya 2. Wote wawili, Paulo na Yakobo, walisema jambo fulani ya maana sana kuhusu Abrahamu.

3. Paulo na Yakobo walizungumuzia andiko gani?

3 Paulo na Yakobo walirudilia maneno yenye kuwa mu Mwanzo 15:​6, yenye inasema hivi: “[Abrahamu] akakuwa na imani katika Yehova, na Mungu akamuhesabia hilo kuwa haki.” Mara mingi haki ni hali ya mutu mwenye Mungu anakubali, ao mwenye Mungu anaona kuwa bila kosa. Inashangaza vile Mungu anaweza kuona mutu mwenye hakamilike na mutenda-zambi kuwa bila kosa! Bila shaka unapenda Mungu akuone vile pia, na ile inawezekana. Sasa, tuone juu ya nini Yehova alimuona Abrahamu kuwa mwenye haki, na mambo yenye tunapaswa kufanya juu Yehova atuone pia vile.

IMANI NI YA MAANA SANA ILI KUWA MWENYE HAKI

4. Juu ya nini wanadamu hawako wenye haki?

4 Mu barua yake kwa Waroma, Paulo alisema kama wanadamu wote ni watenda-zambi. (Ro. 3:23) Sasa, inawezekana namna gani mutu aonwe kuwa mwenye haki ao mwenye hana kosa na hivyo akubaliwe na Mungu? Juu ya kusaidia Wakristo wote wa kweli wapate jibu ya ile ulizo, Paulo alitumia mufano wa Abrahamu.

5. Juu ya nini Yehova alimuona Abrahamu kuwa mwenye haki? (Waroma 4:​2-4)

5 Yehova alimuita Abrahamu kuwa mweye haki wakati alikuwa angali anaishi mu inchi ya Kanaani. Juu ya nini Yehova alimuona Abrahamu kuwa mwenye haki? Je, ni juu Abrahamu alishika kwa ukamili Sheria ya Musa? Hapana. (Ro. 4:13) Taifa ya Israeli ilipata ile Sheria zaidi ya miaka 400 kisha Mungu kumuona Abrahamu kuwa mwenye haki. Basi, ni juu ya nini Mungu alimuona Abrahamu kuwa mwenye haki? Kwa fazili zake zenye hazistahiliwe, Yehova alimuona Abrahamu kuwa mwenye haki kwa sababu ya imani yake.—Soma Waroma 4:​2-4.

6. Juu ya nini Yehova anaona mutenda-zambi kuwa mwenye haki?

6 Paulo alisema kama wakati mutu iko na imani kwa Mungu, “imani yake inahesabiwa kuwa haki.” (Ro. 4:5) Paulo aliongeza hivi: “Kama vile Daudi pia anasema juu ya furaha ya mutu mwenye Mungu anahesabia kuwa mwenye haki bila matendo: ‘Wenye furaha ni wale wenye matendo yao ya kuvunja sheria yamesamehewa na wenye zambi zao zimefunikwa; mwenye furaha ni mutu mwenye Yehova hatahesabia zambi yake hata kidogo.’” (Ro. 4:​6-8; Zb. 32:​1, 2) Mungu anasamehe ao anafunika zambi za wale wenye kuwa na imani kwake. Anawasamehe kabisa-kabisa na haendelee kuhesabia zambi zao. Kwa musingi ya imani yao, anawaona kuwa wenye hawana kosa na wenye haki.

7. Juu ya nini tunaweza kusema kama watumishi wa zamani wa Yehova walikuwa wenye haki?

7 Hata kama Abrahamu, Daudi, na watumishi wengine waaminifu wa Mungu walionwa kuwa wenye haki, walikuwa wangali watu wenye hawakamilike na wenye wanaweza kufanya zambi. Lakini kwa sababu ya imani yao, Mungu aliwaona kuwa wenye hawana kosa, zaidi sana wakati alikuwa anawalinganisha na watu wengine wenye hawakumutumikia. (Efe. 2:12) Sawa vile Paulo alionyesha mu barua yake, imani ni ya maana sana juu mutu akuwe rafiki ya Mungu. Abrahamu na Daudi walikuwa marafiki wa Mungu juu walikuwa na imani kwake. Siye pia tunaweza kuwa marafiki wa Mungu kama tuko na imani.

KUKO UHUSIANO GANI KATI YA IMANI NA MATENDO?

8-9. Watu fulani walifikia kusema nini kuhusu mambo yenye Paulo na Yakobo waliandika, na juu ya nini walisema vile?

8 Kwa miaka mingi, watu wenye kuwa mu dini zenye zinajiita kuwa za Kikristo wamebishana sana juu ya uhusiano kati ya imani na matendo. Wakubwa fulani wa kidini wanafundisha kama unapaswa tu kuamini Bwana Yesu Kristo juu uokolewe. Pengine ulishaka kuwasikia wakonasema: “Amini Yesu na uokolewe.” Wanaweza hata kutaya hii maneno ya Paulo: “Mungu anahesabia [mutu] kuwa mwenye haki bila matendo.” (Ro. 4:6) Lakini, wakubwa wengine wa kidini wanasema kama unaweza “kujiokoa” kwa kutembelea mahali kwenye dini inaona kuwa takatifu, na kwa kufanya mambo ingine yenye dini inaona kuwa ya muzuri. Ili kujitetea, pengine wanaweza kutumia maneno ya Yakobo 2:24 yenye inasema: “Munaona kwamba mutu anatangazwa kuwa mwenye haki kupitia matendo, hapana kupitia imani tu.”

9 Juu ya ile mawazo mbili tofauti, watu fulani wenye kuandika kuhusu mambo ya kidini wamesema kama Paulo na Yakobo hawakubaliane mu mambo yenye inahusu imani na matendo. Wakubwa wa kidini wanaweza kusema kama Paulo aliamini kwamba mutu anaonwa kuwa mwenye haki kupitia imani hapana matendo, lakini Yakobo yeye alisema kama matendo ni ya maana sana juu mutu akubaliwe na Mungu. Profesa fulani wa mambo ya kidini alifasiria ile jambo kwa kusema hivi: “Yakobo hakuelewa juu ya nini Paulo alikazia kama mutu anaonwa [kuwa mwenye haki] kwa imani tu hapana kwa matendo.” Lakini mambo yote yenye Paulo na Yakobo waliandika iliongozwa na Yehova. (2 Ti. 3:16) Kwa hiyo kunapaswa kuwa njia ingine ya mwepesi ya kuelewa ile mambo yenye walisema. Na ile njia ni kuchunguza mambo ingine yenye walizungumuzia mu barua zao.

Paulo aliambia Wakristo Wayahudi wenye kuwa Roma kama ni imani njo ya maana sana, hapana matendo yenye Sheria ya Musa inaomba (Ona fungu ya 10) b

10. Paulo anazungumuzia ”‏matendo”‏ gani? (Waroma 3:​21, 28) (Ona pia picha.)

10 Paulo anazungumuzia ”‏matendo”‏ gani mu Waroma 3 na 4? Alikuwa anazungumuzia zaidi sana “matendo ya sheria,” ni kusema sheria ya Musa yenye ilitolewa ku Mulima Sinai. (Soma Waroma 3:​21, 28.) Inaonekana kama, mu wakati wa Paulo ilikuwa nguvu kwa Wakristo fulani Wayahudi kukubali kama haikukuwa tena lazima wafuate Sheria ya Musa na matendo yenye ile Sheria iliomba. Kwa hiyo, Paulo alitumia mufano wa Abrahamu ili kuhakikisha kama haiko “matendo ya sheria” njo inafanya mutu kuwa mwenye haki mbele ya Mungu. Ni imani njo inafanya mutu kuwa mwenye haki. Ile inatutia moyo, juu inatufundisha kama ikiwa tuko na imani kwa Mungu na kwa Kristo, tunaweza kukubaliwa na Mungu.

Yakobo anatia moyo Wakristo waonyeshe imani yao kupitia “matendo,” sawa vile kutendea watu muzuri bila ubaguzi (Ona fungu ya 11-12) c

11. Yakobo anazungumzia ”‏matendo”‏ gani?

11 Kwa upande mwengine, “matendo” yenye inazungumuziwa mu sura ya 2 ya Yakobo haiko ile “matendo ya sheria” yenye Paulo alizungumuzia. Yakobo yeye anazungumuzia matendo, ao mambo yenye Wakristo wanafanyaka mu maisha yao ya kila siku. Ni ile matendo njo inaonyesha kama Mukristo iko na imani ya kweli kwa Mungu ao hapana. Tuzungumuzie mifano mbili yenye Yakobo alitumia.

12. Yakobo alionyesha namna gani uhusiano kati ya imani na matendo? (Ona pia picha.)

12 Mu mufano wake wa kwanza, Yakobo alionyesha juu ya nini ni jambo ya maana Wakristo wasikuwe na ubaguzi mu uhusiano wao na wengine. Alionyesha ile kwa kuzungumuzia habari ya mutu mwenye alipendelea tajiri lakini akazarau maskini. Yakobo alionyesha kama mutu wa vile anaweza kusema kama iko na imani; lakini, je, matendo yake inaonyesha imani kabisa? (Yak. 2:​1-5, 9) Mu mufano wa pili, Yakobo anazungumuzia mutu mwenye anaona ‘ndugu ao dada anakosa nguo ao chakula’ lakini hamutolee musaada wenye iko nao lazima. Hata kama ule mutu anasema kama iko na imani, ile imani haionekane kupitia matendo; kwa hiyo, ile imani ni ya bure. Sawa tu vile Yakobo aliandika, “imani yenyewe bila matendo imekufa.”—Yak. 2:​14-17.

13. Yakobo alitumia mufano gani juu ya kuonyesha uhusiano kati ya imani na matendo? (Yakobo 2:​25, 26)

13 Yakobo alizungumuzia Rahabu kuwa mufano muzuri wa kuonyesha imani kupitia matendo. (Soma Yakobo 2:​25, 26.) Rahabu alisikia habari kuhusu Yehova na akaamini kama ni Yehova njo alikuwa anategemeza Waisraeli. (Yos. 2:​9-11) Alionyesha imani yake kupitia matendo. Alilinda wapelelezi wawili Waisraeli wakati uzima wao ulikuwa mu hatari. Ile ilikuwa na matokeo gani? Ule mwanamuke, mwenye hakamilike na mwenye hakukuwa Muisraeli, alionwa kuwa mwenye haki sawa vile tu Abrahamu. Mufano wake unaonyesha ulazima wa kuwa na imani yenye inaonekana kupitia matendo.

14. Juu ya nini tunaweza kusema kama Paulo na Yakobo walikuwa tu nafasiria imani na matendo mu njia mbili tofauti?

14 Paulo na Yakobo, hawa waandikaji mbili wa Biblia, walikuwa tu nafasiria imani na matendo mu njia mbili tofauti. Paulo alikuwa anawaambia Wakristo Wayahudi kama hawawezi kukubaliwa na Yehova juu tu wanafanya mambo yenye Sheria ya Musa inaomba. Yakobo alikuwa anakazia kwamba ni jambo ya lazima sana kwa Wakristo wote kuonyesha imani yao kwa kutendea wengine mambo ya muzuri.

Imani yako inakuchochea kufanya matendo yenye Yehova anakubali? (Ona fungu ya 15)

15. Ni mu njia gani mbalimbali tunaweza kuonyesha imani kupitia matendo? (Ona pia picha.)

15 Yehova haseme kama ikiwa tunapenda atuone kuwa wenye haki tunapaswa kufanya mambo ileile yenye Abrahamu alifanya. Kuko mambo ingine ya mingi yenye tunaweza kufanya juu ya kuonyesha kama tuko na imani. Kwa mufano, tunaweza kukaribisha wapya mu kutaniko, kusaidia ndugu na dada wenye kuwa mu uhitaji, na kutendea muzuri watu wa familia yetu. Ile mambo yote Mungu anaifurahia na kuibariki. (Ro. 15:7; 1 Ti. 5:​4, 8; 1 Yoh. 3:18) Njia moya ya muzuri sana ya kuonyesha waziwazi imani yetu ni kuhubiri kwa bidii habari njema ya Ufalme. (1 Ti. 4:16) Siye wote tunaweza kuonyesha kupitia matendo yetu kama tunaamini kwamba ahadi za Yehova zitatimia, na kwamba namna yake ya kufanya mambo njo ya muzuri zaidi. Tukifanya vile, tutakuwa hakika kama Mungu atatuona kuwa wenye haki na atatuita marafiki wake.

TUMAINI NI YA MAANA SANA ILI KUWA NA IMANI YENYE NGUVU

16. Namna gani tumaini ya Abrahamu ilitia imani yake nguvu?

16 Mu Waroma sura ya 4 muko somo ingine ya maana sana yenye mufano wa Abrahamu unaweza kutufundisha, ile somo ni ulazima wa kuwa na tumaini. Yehova aliahidi kwamba, kupitia Abrahamu “mataifa mengi” ingebarikiwa. Ni tumaini ya muzuri sana yenye Abrahamu alikuwa nayo! (Mwa. 12:3; 15:5; 17:4; Ro. 4:17) Lakini, hata wakati Abrahamu alikuwa na miaka 100 na Sarah miaka 90, ule mutoto mwenye aliahidiwa alikuwa hayazaliwa tu. Ku macho ya wanadamu, ilionekana sawa vile haiwezekane Abrahamu na Sara wazale mutoto. Ile ilikuwa kabisa jaribu kwa Abrahamu. “Lakini kwa kutegemea tumaini, alikuwa na imani kwamba angekuwa baba ya mataifa mengi.” (Ro. 4:​18, 19) Na mwishowe, ile jambo yenye alikuwa anatumainia ilitimia. Alifikia kuwa baba wa Isaka, ule mutoto mwenye alingojea kwa miaka mingi!—Ro. 4:​20-22.

17. Tunajua namna gani kama inawezekana Mungu atuone kuwa wenye haki na marafiki wake?

17 Kama Abrahamu, Mungu anaweza kutukubali, kutuona kuwa wenye haki, na tunaweza kuwa marifiki wake. Paulo alikazia ile jambo wakati aliandika hivi: “Maneno ‘ikahesabiwa kwake’ hayakuandikwa kwa ajili yake [Abrahamu] tu, lakini pia kwa ajili yetu, sisi wenye itahesabiwa kwetu, kwa sababu tunamuamini Yeye mwenye alimufufua Yesu.” (Ro. 4:​23, 24) Kama Abrahamu, tuko na lazima ya imani, imani yenye inaonekana kwa matendo, na pia tumaini. Mu Waroma sura ya 5, Paulo aliendelea kuzungumuzia tumaini. Tutaona ile mu habari yenye kufuata.

WIMBO 28 Rafiki ya Yehova Ni Nani?

a Tunapenda kukubaliwa na Mungu na tunapenda atuone kuwa wenye haki. Kwa kutumia mambo yenye Paulo na Yakobo waliandika, hii habari itazungumuzia namna ile inawezekana na namna imani yenye inaonekana kupitia matendo ni ya maana sana juu tuweze kukubaliwa na Yehova.

b MAFASIRIO YA PICHA: Paulo anatia moyo Wakristo Wayahudi wakazie imani, hapana “matendo ya sheria” sawa vile kuvala nguo yenye kuwa na uzi ya rangi ya bleu, kufanya sikukuu ya Pasaka, ao kunawa kulingana na desturi.

c MAFASIRIO YA PICHA: Yakobo alitia moyo watu waonyeshe imani kwa kutendea wengine mambo ya muzuri, sawa vile kwa kusaidia maskini.