Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI YA KUJIFUNZA YA 9

WIMBO 75 “Miye Huyu! Unitume!”

Uko Tayari Kujitoa kwa Yehova?

Uko Tayari Kujitoa kwa Yehova?

“Nitamulipa Yehova nini kwa mema yote yenye amenitendea?”ZB. 116:12.

WAZO KUBWA

Hii habari itakusaidia ukuwe na urafiki wa karibu pamoya na Yehova na ile itafanya upende kujitoa kwake na kubatizwa.

1-2. Mutu anapaswa kufanya nini mbele ya kubatizwa?

 KWA miaka tano yenye imepita, zaidi ya watu milioni moya wamebatizwa na kuwa Mashahidi wa Yehova. Kama mwanafunzi Timoteo wa mu karne ya kwanza, wengi wao walijifunza kweli “tangu utoto.” (2 Ti. 3:​14, 15) Wengine walijifunza wakati walikuwa walishakuwa watu wazima, na wengine wakati walikuwa wamezeeka. Miaka fulani yenye imepita, mwanamuke mumoja mwenye alijifunza Biblia pamoya na Mashahidi wa Yehova, alibatizwa na miaka 97!

2 Kama uko mwanafunzi wa Biblia ao ulikomalishwa na wazazi wenye kuwa Mashahidi, je, uko nafikiria kubatizwa? Kama ni vile, unastahili pongezi! Lakini, mbele ya kubatizwa unapaswa kujitoa kwa Yehova. Hii habari itafasiria maana ya kujitoa kwa Yehova. Itakusaidia pia ujue juu ya nini haupaswe kujizuia kujitoa kwa Yehova na kubatizwa wakati uko tayari kufanya vile.

KUJITOA KWA YEHOVA MAANA YAKE NINI?

3. Toa mifano yenye kuzungumuziwa mu Biblia ya watu wenye walijitoa kwa Yehova.

3 Mu Biblia, kujitoa maana yake kuwekwa pembeni kwa ajili ya kusudi fulani takatifu. Waisraeli walikuwa taifa yenye ilitolewa kwa Yehova. Lakini watu fulani mu ile taifa walijitoa kwa Yehova mu njia fulani ya pekee. Kwa mufano, Haruni alivaa bamba lenye kungaa la zahabu upande wa mbele wa kilemba chake, yenye ilikuwa “alama takatifu ya kuwekwa pembeni kwa ajili ya kusudi la pekee.” Ile bamba ya zahabu ilionyesha kama aliwekwa pembeni ili kumutumikia Yehova mu njia ya pekee, ni kusema, kuwa kuhani mukubwa wa taifa ya Israeli. (Law. 8:9) Wanaziri pia walijitoa kwa Yehova mu njia ya pekee. Neno “Munaziri,” yenye inatokana na neno ya Kiebrania nazirʹ, maana yake “Mwenye Alitengwa” ao “Mwenye Alitolewa kwa Mungu.” Sawa vile Sheria ya Musa ilionyesha, Wanaziri walipaswa kuepuka mambo fulani.—Hes. 6:​2-8.

4. (a) Ni mu njia gani wale wenye wamejitoa kwa Yehova wamewekwa pembeni kwa ajili ya kusudi takatifu? (b) ‘Kujikana’ mwenyewe maana yake nini? (Ona pia picha.)

4 Wakati unajitoa kwa Yehova, unachagua kuwa mwanafunzi wa Yesu Kristo, na kufanya mapenzi ya Mungu njo inakuwa jambo ya maana zaidi mu maisha yako. Wakati Mukristo anajitoa kwa Yehova, ile inaonyesha kama iko tayari kufanya nini? Yesu alisema hivi: “Kama mutu yeyote anataka kunifuata, lazima ajikane mwenyewe.” (Mt. 16:24) Musemwa ya Kigiriki wenye kutafsiriwa “lazima ajikane mwenyewe” unaweza pia kutafsiriwa “anapaswa kujiambia hapana.” Juu umejitoa sasa kwa Yehova na umekuwa mutumishi wake, unapaswa kusema hapana kwa kila kitu yenye inapingana na mapenzi yake. (2 Ko. 5:​14, 15) Ile inatia ndani kusema hapana ku “matendo ya mwili” sawa vile uasherati. (Gal. 5:​19-21; 1 Ko. 6:18) Kuepuka ile mambo kutafanya maisha yako ikuwe nguvu? Hapana, haitakuwa nguvu kama unamupenda Yehova na uko hakika kama sheria zenye anatoa zinakuletea faida. (Zb. 119:97; Isa. 48:​17, 18) Ndugu mwenye kuitwa Nicholas alisema hivi juu ya ile jambo: “Unaweza kuona kanuni za Yehova sawa vile ukuta wa gereza wenye kukuzuia kufanya mambo yenye unapenda, ao sawa vile lupango ya machuma-machuma yenye inakulinda ili simba asikushambulie.”

Unaona kanuni za Yehova sawa vile ukuta wa gereza wenye kukuzuia kufanya mambo yenye unapenda, ao sawa vile lupango ya machuma-machuma yenye inakulinda ili simba asikushambulie? (Ona fungu ya 4)


5. (a) Unaweza kujitoa kwa Yehova namna gani? (b) Kuko tofauti gani kati ya kujitoa kwa Yehova na kubatizwa? (Ona pia picha.)

5 Unaweza kujitoa kwa Yehova namna gani? Unajitoa kwa Yehova wakati unamuahidi katika sala kama utamuabudu yeye tu na kama utatia mapenzi yake pa nafasi ya kwanza katika maisha yako. Unamuahidi Yehova kama utaendelea kumupenda “kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote na kwa nguvu zako zote.” (Mk. 12:30) Ile ahadi ya kujitoa kwa Yehova ni kati yako weye na Yehova tu. Lakini ubatizo unafanywa mbele ya watu wengi, unaonyesha watu wengine kama umejitoa kwa Yehova. Kujitoa kwa Yehova ni naziri takatifu, na Yehova anatazamia kama utaheshimia ile naziri; na weye pia unapaswa kuazimia kufanya vile.—Muh. 5:​4, 5.

Unajitoa kwa Yehova wakati unamuahidi katika sala ya kipekee kama utamuabudu yeye tu na kama utatia mapenzi yake pa nafasi ya kwanza katika maisha yako (Ona fungu ya 5)


JUU YA NINI UJITOE KWA YEHOVA?

6. Ni nini inachochea mutu ajitoe kwa Yehova?

6 Sababu kubwa yenye inakuchochea ujitoe kwa Yehova ni juu unamupenda. Ule upendo hautegemee tu namna unajisikia. Lakini unategemea “ujuzi wenye hauna makosa” na “uelewaji wa kiroho” wa mambo yenye umejifunza juu ya Yehova, mambo yenye imefanya upendo wako kwake ukomae. (Kol. 1:9) Mambo yenye umejifunza mu Maandiko imekuhakikishia kama (1) Yehova ni mutu wa kweli kabisa, (2) Biblia ni Neno yake yenye kuongozwa na roho, na (3) anatumia tengenezo yake ili kutimiza mapenzi yake.

7. Tunapaswa kufanya nini mbele ya kujitoa kwa Mungu?

7 Wale wenye wanajitoa kwa Yehova wanapaswa kujua mafundisho ya musingi ya Biblia na kuishi kulingana na kanuni zake. Wanaelezea wengine kuhusu imani yao kadiri hali yao inawaruhusu. (Mt. 28:​19, 20) Upendo wao kwa Yehova umekomaa, na wanapenda sana kumuabudu yeye tu. Na weye unajisikia vile? Kama na weye unamupenda Yehova, hautajitoa kwake na kubatizwa juu tu ya kufurahisha mwalimu wako wa Biblia ao wazazi wako; na hautafanya vile juu tu marafiki wako wako nafanya vile.

8. Namna gani kuwa wenye shukrani kunatuchochea tujitoe kwa Yehova? (Zaburi 116:​12-14)

8 Wakati unafikiria mambo yote yenye Yehova alishafanya kwa ajili yako, unajisikia tu ujitoe kwake. (Soma Zaburi 116:​12-14.) Bila shaka Biblia haikosee wakati inamuita Yehova Mupaji wa “kila zawadi ya muzuri na kila zawadi kamilifu.” (Yak. 1:17) Zawadi kubwa zaidi kati ya zawadi zenye Yehova ametutolea ni zabihu ya Mwana wake Yesu. Waza kidogo! Bei ya ukombozi imefanya iwezekane ukuwe na urafiki wa karibu pamoya na Yehova. Na inafanya ukuwe na tumaini ya kuishi milele. (1 Yo. 4:​9, 10, 19) Kujitoa kwa Yehova ni njia ya kuonyesha shukrani juu ya ile tendo kubwa zaidi ya upendo, na juu ya baraka zingine za mingi zenye amekupatia. (Kum. 16:17; 2 Ko. 5:15) Nukta ya 4 ya somo ya 46 ya kitabu Furahia Maisha Milele! inazungumuzia namna ya kuonyesha shukrani na iko na video ya dakika tatu yenye kichwa Umutolee Mungu Zawadi.

UKO TAYARI KUJITOA KWA YEHOVA NA KUBATIZWA?

9. Juu ya nini mutu hapaswe kujisikia kama anakazwa kujitoa kwa Yehova?

9 Unaweza kujisikia kama hauko tayari kujitoa kwa Yehova na kubatizwa. Pengine unapaswa kufanya mabadiliko fulani mu maisha yako ili kujipatanisha na kanuni za Yehova, ao pengine uko na lazima ya wakati zaidi ili kutia imani yako nguvu. (Kol. 2:​6, 7) Kila mwanafunzi iko na mwendo wake wa kufanya maendeleo, na haiko vijana wote njo wanakuwa tayari kujitoa kwa Yehova na kubatizwa ku ileile miaka. Pima kufikiria maendeleo yako ya kiroho kulingana na mambo yenye unaweza kufanya, hapana kwa kujilinganisha na mutu mwingine.—Gal. 6:​4, 5.

10. Unaweza kufanya nini ikiwa unaona kuwa hauko tayari kujitoa kwa Yehova na kubatizwa? (Ona pia kisanduku “ Kwa Wale Wenye Wanakomalishwa Katika Kweli.”)

10 Hata kama unatambua kama hauko tayari kujitoa kwa Yehova, endelea kufanya ile jambo kuwa muradi wako. Umuombe Yehova abariki mambo yote yenye uko nafanya ili kufanya mabadiliko yenye inaombwa. (Flp. 2:13; 3:16) Unaweza kuwa hakika kama atasikiliza sala zako na atakujibu.—1 Yo. 5:14.

JUU YA NINI WATU FULANI WANAJIZUIA?

11. Namna gani Yehova atatusaidia tubakie waaminifu kwake?

11 Watu fulani wenye kuwa tayari kujitoa kwa Yehova na kubatizwa wanajizuia kufanya vile. Wanaweza kuogopa kama, kisha kubatizwa watafanya zambi nzito na watatengwa. Kama na weye uko na ile woga, ukuwe hakika kama Yehova atakupatia kila kitu yenye uko nayo lazima ili ‘utembee kwa namna yenye kumustahili ili kumupendeza kwa ukamili.’ (Kol. 1:10) Atakupatia pia nguvu ya kufanya mambo ya muzuri. Yehova ameonyesha kama anaweza kufanya vile kupitia namna amesaidia wengine. (1 Ko. 10:13) Njo maana ni watu kidogo tu njo wanatengwa na kutaniko. Yehova anasaidiaka watu wake waendelee kuwa waaminifu.

12. Tunaweza kufanya nini ili kuepuka zambi nzito?

12 Wanadamu wote wenye hawakamilike wanajaribiwa kufanya mambo ya mubaya. (Yak. 1:14) Lakini, weye njo wa kuamua namna utatenda wakati unajaribiwa. Kusema kweli, ni weye tu njo uko na uwezo wa kuamua namna utaishi. Hata kama watu fulani wanasema kama haiwezekane mutu azuie hisia na matendo yake, unaweza kujifunza kuzuia tamaa za mubaya. Hata kama unaweza kujaribiwa, unaweza kujizuia na kukatala kutenda kulingana na zile tamaa. Ili uweze kufanya vile, sali kila siku. Ukuwe na programu ya muzuri ya kujifunza kipekee Neno ya Mungu. Huzuria mikutano ya Kikristo. Ambia wengine mambo yenye unaamini. Kufanya ile mambo kwa ukawaida kutakupatia nguvu ya kuheshimia naziri yako ya kujitoa kwa Mungu. Na usisahau hata siku moya kama Yehova atakusaidia kufanya vile.—Gal. 5:16.

13. Yosefu alituachia mufano gani muzuri?

13 Itakuwa mwepesi zaidi kwako kuheshimia naziri yako ya kujitoa kwa Mungu kama unaamua mbele ya wakati namna utatenda wakati utakutana na majaribu. Biblia inazungumuzia watu wengi wenye walifanya vile, hata kama walikuwa wanadamu wenye hawakamilike. Kwa mufano, bibi ya Potifa alimushawishi Yosefu mara kwa mara ili alale naye. Lakini Yosefu alikuwa hakika kabisa na mambo yenye alipaswa kufanya. Biblia inatuambia kama ‘alikataa,’ na alisema hivi: “Ninaweza namna gani kufanya ubaya huu mukubwa na kwa kweli nimutendee Mungu zambi?” (Mwa. 39:​8-10) Ni wazi kama, Yosefu alijua namna atatenda mbele hata bibi ya Potifa amushawishi. Ile ilifanya ikuwe mwepesi zaidi kwake wakati alipambana na ile jaribu.

14. Namna gani tunaweza kujifunza kusema hapana wakati tunajaribiwa?

14 Namna gani unaweza kumuiga Yosefu kwa kusema hapana wakati unajaribiwa? Unaweza kuamua sasa mambo yenye utafanya wakati jaribu itatokea. Ujifunze kukatala palepale mambo yenye Yehova anachukia na hata uepuke kabisa kuifikiria. (Zb. 97:10; 119:165) Kama unafanya vile hautatenda zambi wakati unajaribiwa. Utajua tayari namna utatenda. Utakuwa ulishaamua njia yenye utafuata.

15. Namna gani mutu anaweza kuonyesha kama ‘anamutafuta kwa bidii’ Yehova? (Waebrania 11:6)

15 Pengine unajua kama umepata kweli na unapenda kumutumikia Yehova kwa moyo wako wote, lakini kuko jambo fulani yenye ingali inakuzuia kujitoa kwake na kubatizwa. Unaweza kufanya jambo yenye Mufalme Daudi alifanya. Unaweza kumulilia Yehova hivi: “Unichunguze kabisa, Ee Mungu, na ujue moyo wangu. Unichunguze, na ujue mawazo yangu yenye kuhangaisha. Angalia kama kuko njia yoyote yenye kuumiza ndani yangu, na uniongoze katika njia ya milele.” (Zb. 139:​23, 24) Yehova anabariki wale wenye “wanamutafuta kwa bidii.” Wakati unajikaza sana ili ufikie muradi wako wa kujitoa kwa Yehova na kubatizwa, unaonyesha kama uko namutafuta kwa bidii.—Soma Waebrania 11:6.

ENDELEA KUMUKARIBIA YEHOVA

16-17. Yehova anavuta namna gani wale wenye kukomalishwa katika kweli? (Yohana 6:44)

16 Yesu alisema kama ni Yehova njo anavuta wanafunzi wake. (Soma Yohana 6:44.) Fikiria ile wazo ya maana sana na uone namna inakuhusu. Yehova anaona jambo ya muzuri yenye kuwa mu moyo wa kila mutu mwenye anavuta kwake. Anaona kila mumoja wao kuwa “mali yake ya pekee” ao “mali yake yenye anapendezwa nayo sana.” (Kum. 7:6; maelezo ya chini) Ni vile anakuona pia.

17 Lakini, pengine uko kijana na wazazi wako ni Mashahidi wa Yehova. Unaweza kuwaza kama uko mu tengenezo juu tu wazazi wako ni Mashahidi wa Yehova. Lakini Biblia inasema hivi: “Mumukaribie Mungu, naye atawakaribia ninyi.” (Yak. 4:8; 1 Ny. 28:9) Wakati weye unakamata hatua ya kumukaribia Yehova, Yehova naye anakukaribia. Yehova haone tu kama uko mu kikundi fulani. Anavuta kila mumoja wetu kipekee—hata wale wenye walikomalishwa katika kweli. Kama mutu mwenye alikomalishwa katika kweli anakamata hatua ya kumukaribia Yehova, Yehova naye anamukaribia, sawa vile Yakobo 4:8 inasema.—Linganisha na 2 Watesalonike 2:13.

18. Tutazungumuzia nini mu habari yenye kufuata? (Zaburi 40:8)

18 Wakati unajitoa kwa Yehova na kubatizwa, unaiga Yesu. Kwa kupenda, alijitoa kwa Baba yake ili kufanya mambo yote yenye alimuomba. (Soma Zaburi 40:8; Ebr. 10:7) Mu habari yenye kufuata, tutazungumuzia mambo yenye itakusaidia uendelee kumutumikia Yehova kwa uaminifu kisha kubatizwa.

UTAJIBU NAMNA GANI?

  • Kujitoa kwa Yehova maana yake nini?

  • Namna gani kuwa wenye shukrani kunaweza kutuchochea tujitoe kwa Yehova?

  • Nini njo itakusaidia uepuke zambi nzito?

WIMBO 38 Atakupatia Nguvu