Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI YA KUJIFUNZA YA 11

WIMBO 129 Tutaendelea Kuvumilia

Unaweza Kuendelea Kuvumilia Hata Ukivunjika Moyo

Unaweza Kuendelea Kuvumilia Hata Ukivunjika Moyo

“Umeendelea kuvumilia kwa ajili ya jina langu.”UFU. 2:3.

WAZO KUBWA

Tunaweza kuendelea kumutumikia Yehova hata tukipambana na hali zenye kuvunja moyo.

1. Ni baraka gani fulani zenye tunapata kwa sababu tuko mu tengenezo ya Yehova?

 MU HIZI siku za mwisho zenye kuwa nguvu, tunapata baraka mingi juu tuko mu tengenezo ya Yehova. Kadiri hali zinaendelea kuharibika mu huu ulimwengu, Yehova anatupatia familia ya kiroho yenye umoja ya ndugu na dada. (Zb. 133:1) Anatufundisha namna ya kuendelea kuwa wenye furaha mu familia. (Efe. 5:33–6:1) Na anatupatia utambuzi na hekima yenye tuko nayo lazima ili tukuwe na amani ya moyo.

2. Tunapaswa kufanya nini, na juu ya nini?

2 Lakini, tunapaswa kuendelea kujikaza sana ili tuendelee kumutumikia Yehova kwa uaminifu. Juu ya nini? Juu wakati fulani makosa ya wengine inaweza kutukwaza. Tunaweza pia kuvunjika moyo kwa sababu ya makosa yetu wenyewe, zaidi sana kama tunarudilia kosa ileile tena na tena. Tunapaswa kuendelea kuvumilia mu utumishi wetu kwa Yehova (1) wakati muabudu mwenzetu anatukwaza, (2) wakati bibi ao bwana yetu anatuvunja moyo, na (3) wakati makosa yetu wenyewe inafanya tuvunjike moyo. Mu kila habari tutazungumuzia zile hali tatu. Tutaona pia mambo yenye tunaweza kujifunza kupitia mufano wa mutu fulani muaminifu mwenye kuzungumuziwa mu Biblia.

ENDELEA KUVUMILIA WAKATI MUABUDU MWENZAKO ANAKUKWAZA

3. Watu wa Yehova wanapambana na tatizo gani?

3 Tatizo. Pengine Wakristo fulani wako na tabia zenye zinatukwazaka. Wengine wanaweza kutuvunja moyo ao kututendea mu njia yenye haiko ya muzuri. Pia wale wenye kuongoza wanaweza kufanya makosa. Ile mambo yote inaweza kufanya mutu aanze kujiuliza ikiwa hii ni tengenezo ya Mungu kabisa. Kuliko kuendelea kumutumikia Mungu “bega kwa bega” pamoya na ndugu na dada, anaweza kuanza kuepuka wale wenye wamemukosea ao hata kuacha kukusanyika. (Sef. 3:9) Ni jambo ya hekima kufanya vile? Tuone mambo yenye tunaweza kujifunza kupitia mufano wa mutu fulani mwenye kuzungumuziwa mu Biblia mwenye alipatwa na magumu sawa ile.

4. Mutume Paulo alipambana na magumu gani?

4 Mutu mwenye kuzungumuziwa mu Biblia. Mutume Paulo alijua kama Wakristo wenzake hawakukuwa wakamilifu. Kwa mufano, muda mufupi kisha Paulo kuingia mu kutaniko ya Kikristo, Wakristo fulani walikuwa na mawazo ya mubaya juu yake. (Mdo. 9:26) Kisha, Wakristo wengine walikuwa nasema mubaya kumuhusu juu ya kumuharibishia sifa. (2 Ko. 10:10) Paulo aliona namna ndugu fulani mwenye alikuwa na madaraka mu kutaniko alikamata uamuzi wenye ungekwaza wengine. (Gal. 2:​11, 12) Na Marko, mumoja kati ya marafiki wake wa karibu, alifanya avunjike moyo sana. (Mdo. 15:​37, 38) Paulo angeacha ile mambo imufanye aepuke Wakristo wenye walimukwaza. Lakini hakufanya vile. Aliendelea kuwa na mawazo ya muzuri juu ya wale ndugu na dada, na aliendelea kumutumikia Yehova kwa bidii. Nini njo ilimusaidia aendelee kuvumilia?

5. Ni nini njo ilisaidia Paulo aendelee kuwa karibu na ndugu na dada zake? (Wakolosai 3:​13, 14) (Ona pia picha.)

5 Paulo alipenda ndugu na dada zake. Juu Paulo alipenda wengine, ile ilimusaidia akazie akili sifa zao za muzuri, hapana makosa yao. Upendo ulimusaidia pia afanye mambo yenye yeye mwenyewe aliandika mu Wakolosai 3:​13, 14. (Soma.) Namna alimutendea Marko inaonyesha kabisa-kabisa kama alifuata maneno ya ile andiko. Hata kama Marko aliacha Paulo mu safari yake ya kwanza ya umisionere, Paulo hakuendelea kukasirika. Kisha wakati fulani, wakati Paulo aliandikia barua kutaniko ya Kolosai, alimusifu Marko kwa kusema kama alikuwa mufanyakazi mwenzake na “chanzo cha faraja nyingi.” (Kol. 4:​10, 11) Wakati Paulo alikuwa amefungwa katika Roma, aliomba Marko akuye kumusaidia. (2 Ti. 4:11) Kwa kweli, Paulo alibakia karibu na ndugu na dada zake. Mufano wa Paulo unaweza kutufundisha nini?

Kulikuwa tatizo fulani yenye ilihusu Paulo, Barnaba, na Marko. Lakini mutume Paulo hakuendelea kuifikiria na alifikia kutumika kwa furaha pamoya na Marko (Ona fungu ya 5)


6-7. Namna gani tunaweza kuendelea kuonyesha ndugu na dada zetu upendo hata kama wanafanya makosa? (1 Yohana 4:7)

6 Jambo yenye tunajifunza. Yehova anapenda tuendelee kuonyesha ndugu na dada zetu upendo. (Soma 1 Yohana 4:7.) Tunaweza kujiambia kama ndugu ao dada yetu anapenda kufuata kanuni za Biblia, na kama alitenda tu bila kufikiri. (Mez. 12:18) Mungu anapenda watumishi wake waaminifu hata kama wanafanyaka makosa. Yehova hatukatae wakati tunafanya makosa na haendelee kutukasirikia. (Zb. 103:9) Bila shaka, ni jambo ya maana sana tuige Baba yetu mwenye kusamehe!—Efe. 4:32–5:1.

7 Kumbuka pia kama kadiri mwisho unakaribia, tunapaswa kuendelea kutia nguvu uhusiano wetu pamoya na ndugu na dada. Tunaweza kuwa hakika kama mateso itaongezeka. Tunaweza hata kujikuta mu gereza kwa sababu ya imani yetu. Kama ile inatokea, tutakuwa na lazima ya ndugu na dada zetu kuliko wakati mwingine wowote. (Mez. 17:17) Fikiria mambo yenye ilimufikia Josep, a muzee wa kutaniko katika Uhispania. Yeye na ndugu wengine walifungwa mu gereza pamoya kwa sababu walikatala kuunga mukono upande wowote. Anasema hivi: “Mu gereza, ni mwepesi kukwazika kwa sababu ya Mukristo mwenzetu juu tunaishi pamoya fasi ya kidogo. Tulipaswa kuvumiliana na kuwa tayari kusameheana. Ile ilitusaidia tuendelee kuwa na umoja na ilitulinda. Tulizungukwa na wafungwa wenye hawakumutumikia Yehova. Wakati fulani niliumia ku mukono na singeweza kujifanyia kitu. Lakini ndugu yangu fulani alifula nguo zangu, na kunihangaikia mu njia zingine. Nilionyeshwa upendo wa kweli wakati nilikuwa nao lazima kabisa.” Bila shaka, tuko na sababu za muzuri za kumaliza leo matatizo yenye tuko nayo pamoya na Wakristo wenzetu!

ENDELEA KUVUMILIA WAKATI BIBI AO BWANA YAKO ANAKUVUNJA MOYO

8. Wale wenye wamefunga ndoa wanapambana na magumu gani?

8 Tatizo. Ndoa zote ziko na magumu. Biblia inasema kama wale wenye wamefunga ndoa watakuwa na “taabu katika mwili wao.” (1 Ko. 7:28) Juu ya nini? Juu ndoa inaunganisha watu wawili wenye hawakamilike. Kila mumoja wao iko na tabia yake, iko na mambo yenye anapendaka, na yenye anachukiaka. Pengine walikomalia mu desturi tofauti. Wanaweza kuonyesha tabia fulani zenye hazikuonekana mbele wafunge ndoa. Jambo yoyote kati ya ile mambo inaweza kuleta magumu. Kuliko bibi ao bwana kukubali kama naye iko na kosa kwa kadiri fulani na kujikaza kumaliza magumu yao, anaweza kuanza kulaumu mwenzake. Bibi na bwana wanaweza hata kuona kama kuachana ao kuvunja ndoa njo kutamaliza magumu. Lakini kuvunja ndoa njo kutamaliza magumu yao? b Tuone basi mutu fulani mwenye kuzungumuziwa mu Biblia mwenye aliendelea kuvumilia mu ndoa yenye ilikuwa na magumu mingi.

9. Abigaili alipambana na magumu gani?

9 Mutu mwenye kuzungumuziwa mu Biblia. Abigaili alikuwa bibi ya Nabali. Biblia inasema kama Nabali alikuwa mukali na mwenye tabia ya mubaya. (1 Sa. 25:3) Inawezekana haikukuwa mwepesi kwa Abigaili kuishi na mwanaume wa vile. Abigaili alipata nafasi ya kuvunja ndoa yake? Alipata ile nafasi wakati Daudi, mwenye angekuwa mufalme wa Israeli, alikuya kuua bwana yake kwa sababu alimutukana yeye na wanaume wake. (1 Sa. 25:​9-13) Abigaili angekimbia na kuacha Daudi aue Nabali. Lakini kuliko kufanya vile alikamata hatua fulani na kuomba Daudi aache Nabali aishi, na Daudi alimusikiliza. (1 Sa. 25:​23-27) Inawezekana nini njo ilimuchochea kufanya vile?

10. Inawezekana ni nini ilimusaidia Abigaili aendelee kuvumilia hata kama ndoa yake ilikuwa na magumu?

10 Abigaili alimupenda Yehova na aliheshimia kanuni zake kuhusu ndoa. Bila shaka alijua mambo yenye Mungu aliambia Adamu na Eva wakati alianzisha ndoa ya kwanza. (Mwa. 2:24) Abigaili alijua kama Yehova aliona ndoa kuwa mupango takatifu. Alipenda kumufurahisha Mungu. Na ile ilimuchochea afanye yote yenye angeweza ili kuokoa nyumba yake, kutia ndani bwana yake. Alitenda haraka ili kumuzuia Daudi asimuue Nabali. Pia alikuwa tayari kuomba musamaha juu ya makosa yenye hakufanya. Ni wazi kama Yehova alipenda sana ule mwanamuke mwenye uhodari na mwenye kuhangaikia wengine. Mufano wa Abigaili unaweza kufundisha bibi na bwana nini?

11. (a) Yehova anapenda bibi na bwana wafanye nini? (Waefeso 5:33) (b) Unajifunza nini wakati unafikiria namna Carmen alijikaza sana ili kuokoa ndoa yake? (Ona pia picha.)

11 Jambo yenye tunajifunza. Yehova anaomba wale wenye wamefunga ndoa waheshimie mupango wa ndoa hata kama haiko mwepesi kuishi na bibi ao bwana yao. Yehova anafurahi sana wakati anaona bibi na bwana wanafanya yao yote ili kumaliza magumu yao na kuonyeshana upendo wa kweli na heshima. (Soma Waefeso 5:33.) Fikiria mufano wa Carmen. Miaka sita kisha kuolewa alianza kujifunza Biblia pamoya na Mashahidi wa Yehova, na kisha akafikia kubatizwa. Carmen anasema hivi: “Bwana yangu hakufurahia uamuzi wangu. Alimusikilia Yehova wivu. Alikuwa nanitukana na kuniogopesha kama ataniacha.” Lakini Carmen aliendelea kuvumilia mu ndoa yake. Kwa miaka 50 alijikaza sana kuonyesha upendo na heshima mu ndoa yake. Anasema tena hivi: “Vile miaka ilikuwa napita nilijifunza kuwa na utambuzi zaidi na kuzungumuza na bwana yangu kwa busara zaidi. Juu nilijua kama Yehova anaona ndoa kuwa takatifu, nilifanya yangu yote ili kuilinda. Sikujaribu hata siku moya kumuacha bwana yangu kwa sababu ninamupenda Yehova.” c Kama magumu inatokea mu ndoa yako, unaweza kuwa hakika kama Yehova atakutegemeza na atakusaidia uendelee kuvumilia.

Unajifunza nini wakati unafikiria namna Abigaili alikuwa tayari kufanya yake yote ili kuokoa nyumba yake? (Ona fungu ya 11)


ENDELEA KUVUMILIA WAKATI MAKOSA YAKO INAKUVUNJA MOYO

12. Tunaweza kupambana na magumu gani wakati tunafanya zambi nzito?

12 Tatizo. Tunaweza kuvunjika moyo sana kama tunafanya zambi nzito. Biblia inaonyesha wazi kama zambi zetu zinaweza kufanya ‘tuvunjike na kupondwa.’ (Zb. 51:17) Ndugu fulani mwenye kuitwa Robert alitumika sana kwa miaka mingi ili astahili kuwa mutumishi wa huduma. Lakini alifanya zambi nzito, na alitambua kama amemusaliti Yehova. Anasema hivi: “Zamiri yangu ilinisumbua sana, ilikuwa sawa vile jiwe kubwa sana inaniangukia. Kisha nilisikia mubaya sana. Nililia na kusali kwa Yehova. Ninakumbuka kama niliwaza Mungu hawezi tena kunisikiliza. Juu ya nini anasikilize? Nilikuwa nimemuhuzunisha.” Kama tunafanya zambi tunaweza kuvunjika moyo sana juu moyo wetu wenye kuumia unaamini kama Yehova ametuacha. (Zb. 38:4) Kama unajisikia vile, fikiria mufano wa mutu fulani mwenye kuzungumuziwa mu Biblia mwenye aliendelea kumutumikia Yehova hata kama alifanya zambi nzito.

13. Petro alifanya zambi gani nzito, na nini njo ilimufikisha ku ile zambi?

13 Mutu mwenye kuzungumuziwa mu Biblia. Usiku mbele Yesu auawe, mutume Petro alifanya makosa mbalimbali. Na ile ilimufanya aangukie mu zambi nzito. Kwanza, Petro alijitumainia kupita kiasi kwa kusema kama yeye angeendelea kuwa muaminifu hata mitume wengine wamuache Yesu. (Mk. 14:​27-29) Kisha, wakati walikuwa mu bustani ya Getsemane, Petro alishindwa tena na tena kuendelea kubakia macho. (Mk. 14:​32, 37-41) Kisha, Petro alimuacha Yesu wakati watu wengi walikuya kumukamata. (Mk. 14:50) Ku mwisho, mara tatu Petro alikana Yesu, na hata alilapa kama hamujue. (Mk. 14:​66-71) Petro alitenda namna gani wakati alitambua uzito wa zambi yake? Alishindwa kujizuia na akaanza kulia sana. Pengine zamiri yake ilimuhukumu sana. (Mk. 14:72) Wazia huzuni kubwa yenye Petro alisikia saa fulani kisha pale wakati rafiki yake Yesu aliuawa. Bila shaka, Petro alijiona kuwa hastahili hata kidogo!

14. Ni nini ilimusaidia Petro aendelee kumutumikia Yehova? (Ona picha ku .)

14 Kuko sababu mbalimbali zenye zilimusaidia Petro aendelee kumutumikia Yehova. Hakubakia peke yake. Alienda kwa ndugu zake wa kiroho na bila shaka walimufariji. (Lu. 24:33) Zaidi ya ile, kisha kufufuliwa Yesu alimutokea Petro, inawezekana ili kumutia moyo. (Lu. 24:34; 1 Ko. 15:5) Kisha pale, kuliko kumukemea Petro kwa sababu ya makosa yenye alifanya, Yesu aliambia ule rafiki yake kama atapata madaraka zaidi. (Yoh. 21:​15-17) Petro alijua kama alikuwa amefanya zambi nzito, lakini hakuendelea kuvunjika moyo. Juu ya nini? Juu alikuwa hakika kama Bwana wake, Yesu, hakumuacha. Na ndugu zake wa kiroho waliendelea kumutegemeza. Mufano wa Petro unaweza kutufundisha nini?

Yohana 21:​15-17 inaonyesha kama Yesu hakumuachilia Petro, na ile ilimutia moyo Petro aendelee kumutumikia Yehova (Ona fungu ya 14)


15. Yehova anapenda tukuwe hakika na jambo gani? (Zaburi 86:5; Waroma 8:​38, 39) (Ona pia picha.)

15 Jambo yenye tunajifunza. Yehova anapenda tukuwe hakika kama anatupenda na iko tayari kutusamehe. (Soma Zaburi 86:5; Waroma 8:​38, 39.) Wakati tunafanya zambi, zamiri inatusumbuaka. Ile ni jambo ya kawaida na ni muzuri. Lakini hatupaswe kuwaza kama Yehova hawezi tena kutupenda ao kutusamehe. Tunapaswa kutafuta musaada bila kukawia. Robert, mwenye tumezungumuzia, anasema hivi: “Niliangukia mu zambi juu nilitegemea nguvu yangu mwenyewe ili kupambana na jaribu.” Robert alielewa kama alipaswa kuzungumuza na wazee. Anasema tena hivi: “Wakati nilikamata ile hatua, niliona upendo wa Yehova kupitia wale wazee. Wazee pia waliendelea kunionyesha upendo. Walinisaidia kuelewa kama Yehova hayaniacha.” Siye pia tunaweza kuwa hakika kama Yehova anatupenda kabisa na anatusamehe ikiwa tunatubu zambi zetu, tunatafuta musaada, na tunajikaza kwa moyo wote ili tusirudilie tena ile makosa. (1 Yo. 1:​8, 9) Kuwa hakika na ile jambo kutatusaidia tusiendelee kuvunjika moyo ikiwa tunajikwaa ao kuanguka.

Unajisikia namna gani ao utajisikia namna gani wakati wazee wenye kutumika kwa bidii wanakutolea musaada? (Ona fungu ya 15)


16. Juu ya nini unaazimia kuendelea kuvumilia mu utumishi wako kwa Yehova?

16 Yehova anafurahia sana namna tunajikaza kumutumikia mu hizi siku za mwisho zenye kuwa nguvu. Kwa musaada wa Yehova, tunaweza kuendelea kuvumilia, hata wakati tunavunjika moyo. Tunaweza kupenda zaidi ndugu na dada zetu na kuwasamehe wakati wanatukosea. Tunaweza kuonyesha kama tunamupenda sana Mungu na tunaheshimia mipango yake, kwa kufanya yetu yote ili kumaliza matatizo yenye inatokea mu ndoa yetu. Na kama tunafanya zambi, tunaweza kutafuta musaada wa Yehova, kukubali upendo wake na musamaha wake, na kuendelea kumutumikia. Tunaweza kuwa hakika kama tutapata baraka za mingi kama ‘hatuache kufanya mema.’—Gal. 6:9.

NAMNA GANI TUNAWEZA KUENDELEA KUVUMILIA MU UTUMISHI WETU KWA YEHOVA WAKATI . . .

  • muabudu mwenzetu anatukosea?

  • bibi ao bwana yetu anatuvunja moyo?

  • tunavunjika moyo kwa sababu ya makosa yetu wenyewe?

WIMBO 139 Wazia Uko mu Dunia Mupya

a Majina fulani imebadilishwa.

b Neno ya Mungu inaonyesha kama haiko muzuri bibi na bwana waachane. Kama wanafanya vile, ile haiwapatie ruhusa ya kuoa ao kuolewa tena. Lakini kuko hali fulani za nguvu zenye zimefanya Wakristo fulani wafikirie kuachana na bibi ao bwana yao. Ona maelezo ingine ya 5 “Kutengana” mu kitabu Furahia Maisha Milele!

c Ili kuona mufano ingine, fungua jw.org na uangalie video Amani ya Uongo Isikudanganye!—Darrel Freisinger na Deborah Freisinger.