Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI YA KUJIFUNZA YA 23

Wazazi, Musaidie Watoto Wenu Wamupende Yehova

Wazazi, Musaidie Watoto Wenu Wamupende Yehova

“Unapaswa kumupenda Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote.”​—MT. 22:37.

WIMBO 134 Watoto Ni Zawadi Yenye Mungu Anatupatia

KIFUPI YA HABARI *

1-2. Fasiria namna kanuni fulani za Biblia zinaweza kufikia kuwa za maana zaidi kwetu wakati hali inabadilika.

 SIKU ya ndoa, tunaonaka bwana-arusi na bibi-arusi walishapendeza na wako nafuata kwa uangalifu hotuba ya ndoa. Haikuwake mara ya kwanza kwao kusikia kanuni za Biblia zenye kuzungumziwa mu ile hotuba. Lakini kuanzia ile siku na kuendelea, wataanza kukamata ile mashauri kwa uzito zaidi. Juu ya nini? Juu itaomba waanze kuitumikisha mu maisha yao ya ndoa.

2 Ni vile pia wakati bibi na bwana wanakuwa wazazi. Kwa miaka mingi, pengine walishasikia hotuba mingi zenye kuzungumuzia namna ya kukomalisha watoto. Lakini sasa mashauri yenye kuzungumuziwa mu zile hotuba inaweza kufikia kuwa ya maana zaidi kwao, juu sasa wamekuwa na mutoto mwenye wanapaswa kukomalisha. Ile ni daraka nzito sana! Kusema kweli, wakati hali inabadilika, maandiko fulani yenye tunajua muzuri tunaweza kuanza kuiona kuwa ya maana sana. Njo maana, sawa vile wafalme wa zamani wa Israeli waliombwa kufanya, watumishi wa Yehova leo wanapaswa kusoma na kufikiri sana juu ya maandiko “siku zote” za maisha yao.​—Kum. 17:19.

3. Tutazungumuzia nini mu hii habari?

3 Wazazi, muko na pendeleo ya maana sana kati ya mapendeleo ya maana yenye Mukristo anaweza kuwa nayo. Muko na daraka ya kufundisha watoto wenu juu ya Yehova. Lakini hamupaswe kuwaambia tu mambo mbalimbali kumuhusu Yehova, munapaswa kuwasaidia wamupende sana Yehova. Munaweza kufanya nini juu ya kusaidia watoto wenu wamupende Yehova? Mu hii habari tutazungumuzia kanuni ine zenye zinaweza kuwasaidia. (2 Ti. 3:16) Tutaona pia namna wazazi fulani Wakristo wamepata faida juu walitumikisha kanuni za Biblia.

KANUNI INE ZENYE ZINAWEZA KUSAIDIA WAZAZI

Kama kila mara unatafuta muongozo wa Yehova na kama unawekea watoto wako mufano muzuri, ile itawasaidia namna gani? (Ona fungu ya 4, 8)

4. Ni kanuni gani ya kwanza yenye inaweza kusaidia wazazi wasaidie watoto wao wamupende Yehova? (Yakobo 1:5)

4 Kanuni ya 1: Mutafute muongozo wa Yehova. Mumuombe Yehova awapatie hekima yenye muko nayo lazima juu musaidie watoto wenu wamupende. (Soma Yakobo 1:5.) Hakuna mutu mwenye anaweza kupatia wazazi shauri ya muzuri zaidi kuliko Yehova. Juu ya nini tunasema vile? Kuko sababu za mingi. Lakini tufikirie sababu mbili. Ya kwanza, Yehova njo muzazi mukubwa na mwenye uzoefu zaidi. (Zb. 36:9) Na ya pili, sikuzote mashauri ya hekima yenye anatoa inaletaka faida.​—Isa. 48:17.

5. (a) Tengenezo ya Yehova inatolea wazazi mambo gani? (b) Vile muliona mu video, namna ndugu Amorim na bibi yake walikomalisha watoto wao, inaweza kuwafundisha nini?

5 Kupitia Neno yake na tengenezo yake, Yehova anawatolea nyiye wazazi habari mingi zenye munaweza kutumia juu ya kusaidia watoto wenu wamupende. (Mt. 24:45) Kwa mufano, munaweza kupata mashauri yenye kufaa mu habari mbalimbali zenye kichwa “Musaada kwa Ajili ya Familia,” zenye zilitolewa kwa miaka fulani mu gazeti Amuka! na zenye zinapatikana sasa ku site yetu. Tena, ku jw.org kuko video mbalimbali zenye zinaweza kusaidia wazazi watumikishe kanuni za Biblia juu ya kukomalisha watoto wao. *​—Mez. 2:4-6.

6. Baba moya anasema nini juu ya musaada wenye Yehova anapatia wazazi kupitia tengenezo yake?

6 Wazazi wengi wanafurahia musaada wenye Yehova anatoa kupitia tengenezo yake. Baba moya, mwenye kuitwa Joe, anasema hivi: “Kukomalisha watoto watatu na kuwasaidia wamupende Yehova haiko mwepesi. Sikuzote miye na bibi yangu tunamuombaka Yehova atusaidie. Na tulishakajionea kama mara mingi video ao habari fulani inatokeaka wakati tuko nayo lazima juu ya kutusaidia kupambana na tatizo yenye tuko nayo. Mu mambo yote tunazoea kutafuta muongozo wa Yehova.” Joe na bibi yake wameona kama zile habari na video mbalimbali zimewasaidia wafundishe watoto wao wamupende Yehova.

7. Juu ya nini wazazi wanapaswa kujikaza sana kuwekea watoto wao mufano muzuri? (Waroma 2:21)

7 Kanuni ya 2: Muwawekee mufano muzuri. Watoto wanaangaliaka sana wazazi wao na kuwaiga. Ni kweli kama hakuna muzazi mwenye kukamilika. (Ro. 3:23) Lakini wazazi wenye hekima wanajikazaka sana juu ya kuwekea watoto wao mufano muzuri. (Soma Waroma 2:21.) Baba moya alisemaka hivi juu ya watoto: “Wako sawa sifongo (ao chiffon) yenye inakokotaka kila kitu.” Anasema tena hivi: “Watoto wakiona kama tunafanya mambo yenye iko tofauti na mambo yenye tunawafundishaka wanaweza kutuambia.” Njo maana, kama tunapenda watoto wetu wamupende Yehova, wanapaswa kujionea kama siye wenyewe kwanza tunamupenda sana.

8-9. Wazazi, mambo yenye Andrew na Emma walisema inawafundisha nini?

8 Kuko mambo mingi yenye wazazi wanaweza kufanya juu ya kusaidia watoto wao wamupende Yehova. Ndugu moya wa miaka 17 mwenye kuitwa Andrew, anasema hivi: “Kila mara wazazi wangu walikuwa wanatuambia kama sala ni jambo ya maana sana. Kila usiku, papa alikuwa nasali na miye hata kama nilikuwa nilishasali. Sikuzote wazazi wetu walikuwa natuambia hivi: ‘Munaweza kuzungumuza na Yehova vile munapenda, hata ikuwe mara ngapi.’ Juu wazazi wangu waliona sala kuwa jambo ya maana, ile ilinigusa sana, na imenisaidia nikuwe nasali kwa ukawaida na nimuone Yehova kuwa Baba mwenye upendo.” Wazazi, mukumbuke sikuzote kama mambo yenye munafanya juu ya kuonyesha kama munamupenda Yehova inaweza kusaidia sana watoto wenu wamupende pia.

9 Fikiria pia mufano wa Emma. Wakati baba yake aliwaacha, alimuachia mama yake madeni ya mingi. Emma anasema hivi: “Mara mingi mama alikuwa nakosa makuta, lakini kila mara alikuwa nasema kama Yehova anahangaikiaka watumishi wake. Nilijionea kama mama anaamini kabisa vile kupitia namna alikuwa anaishi. Mama alikuwa natumikisha mambo yenye alikuwa nahubiria wengine.” Wazazi, munajifunza nini? Munaweza kuwekea watoto wenu mufano muzuri hata wakati muko na magumu.​—Gal. 6:9.

10. Wazazi wengi Waisraeli walikuwa na nafasi gani za kuzungumuza na watoto wao? (Kumbukumbu la Torati 6:6, 7)

10 Kanuni ya 3: Muzungumuze na watoto wenu kwa ukawaida. Zamani Yehova aliambia Waisraeli wakuwe nafundisha watoto wao, na wakuwe nafanya vile kwa ukawaida. (Soma Kumbukumbu la Torati 6:6, 7.) Wale wazazi walikuwa na nafasi mingi za kuzungumuza na watoto wao na kuwasaidia wamupende Yehova. Kwa mufano, mutoto mwanaume angeweza kupitisha wakati mingi juu ya kusaidia baba yake mu kazi ya kupanda ao ya kuvuna. Mutoto mwanamuke pia angeweza kupitisha wakati mingi juu ya kusaidia mama yake mu kazi sawa vile kushona manguo, kusuka vitu mbalimbali, na kazi zingine za ku nyumba. Wakati wazazi na watoto walikuwa natumika pamoya wangeweza kuzungumuzia mambo mingi ya maana. Kwa mufano, wangezungumuzia wema wa Yehova na namna alikuwa nasaidia familia yao.

11. Wazazi wako na nafasi gani ya kuzungumuza na watoto wao?

11 Leo mambo haiko tena sawa zamani. Mu inchi mingi, ni nguvu kwa wazazi na watoto kukuwa pamoya muchana wote. Pengine wazazi wanatumikaka muchana wote na watoto wanakuwaka ku masomo. Njo maana, wazazi wanapaswa kutafuta wakati wa kuzungumuza nao. (Efe. 5:15, 16; Flp. 1:10) Ibada ya Familia ni nafasi ya muzuri ya kufanya vile. Ndugu moya kijana mwenye kuitwa Alexander anasema hivi: “Baba yangu anafanyaka mipango juu tusikose kufanya ibada ya familia, na haachake jambo yoyote itukoseshe kuifanya. Kisha ibada, mara mingi tunakuwaka tu tunaongea.”

12. Wazazi wanapaswa kukumbuka nini wakati wa ibada ya familia?

12 Kama uko kichwa ya familia, unaweza kufanya nini juu watoto wako wafurahie ibada ya familia? Kuko mambo mingi yenye unaweza kufanya. Kwa mufano, unaweza kujifunza nao kitabu yetu ya mupya Furahia Maisha Milele! Ile itakusaidia ukuwe na mazungumuzo yenye kufurahisha pamoya nao. Tena, juu unapenda watoto wako wakuambie mambo yenye kuwahangaisha na namna wako najisikia, usifanye wakati wa ibada ya familia njo ikuwe wakati wa kuwatolea hotuba ya mashauri ao kuwaambia makosa yao. Zaidi ya ile, usikasirike wakati mutoto anasema mawazo yake hata kama haipatane na Maandiko. Kuliko kukasirika, umushukuru juu amekuambia mawazo yake waziwazi na umutie moyo asikuwe anaogopa kukuambia vile anajisikia. Hauwezi kusaidia watoto wako muzuri kama haujue mambo yenye kuwahangaisha.

Namna gani wazazi wanaweza kutumia uumbaji juu ya kusaidia watoto wao wajue sifa za Yehova? (Ona fungu ya 13)

13. Wazazi wanaweza kutumia nafasi gani zingine juu ya kusaidia watoto wao wamukaribie Yehova?

13 Wazazi, mutafute nafasi mbalimbali za kusaidia watoto wenu wamukaribie Yehova. Musingoye tu wakati wa funzo yenu juu muwaambie mambo fulani kumuhusu Mungu. Ona mambo yenye mama moya mwenye kuitwa Lisa anasema: “Tulisaidiaka watoto wetu wajifunze mambo fulani kupitia uumbaji. Kwa mufano, wakati imbwa wetu alifanyaka jambo fulani yenye kuchekesha, tulitumia ile nafasi juu ya kuonyesha kama Muumbaji wetu ni Mungu mwenye furaha na anapenda na siye tukuwe na furaha.”

Wazazi, munajua marafiki wa watoto wenu? (Ona fungu ya 14) *

14. Juu ya nini ni jambo ya maana wazazi wasaidie watoto wao wakuwe na marafiki wazuri? (Mezali 13:20)

14 Kanuni ya 4: Musaidie watoto wenu wakuwe na marafiki wazuri. Neno ya Mungu inaonyesha wazi kama marafiki wanaweza kufanya tukuwe na sifa za muzuri ao za mubaya. (Soma Mezali 13:20.) Wazazi, munajua muzuri marafiki wa watoto wenu? Mulishakaonana nao na kupitisha wakati pamoya nao? Munaweza kufanya nini juu ya kusaidia watoto wenu wakuwe na marafiki wenye kumupenda Yehova? (1 Ko. 15:33) Kama munapanga kufanya mambo fulani mu familia, munaweza kualika watu wenye wako na hali ya muzuri ya kiroho. Ile itasaidia watoto wenu wapate marafiki wazuri.​—Zb. 119:63.

15. Wazazi wanaweza kufanya nini juu ya kusaidia watoto wao wakuwe na marafiki wazuri?

15 Fikiria mufano wa baba mwenye kuitwa Tony. Anafasiria mambo yenye yeye na bibi yake wamefanya juu ya kusaidia watoto wao wakuwe na marafiki wazuri. Anasema hivi: “Kwa miaka mingi, tumealika kwetu ndugu na dada wa miaka mbalimbali na wenye wanatoka mu desturi mbalimbali. Ile wakati, tunakula pamoya nao na kufanya ibada ya familia pamoya nao. Ile ni njia ya muzuri ya kutusaidia tufahamiane na watu wenye wanamupenda Yehova na wenye wanamutumikia kwa furaha. Tulishakaalika kwetu waangalizi wa muzunguko, wamisionere, na watu wengine. Ile ni baraka kubwa! Mambo yenye wamejionea, bidii yao, na namna wanaonyesha roho ya kujitoa mu kazi ya Yehova imesaidia sana watoto wetu mu njia mbalimbali na imesaidia wamukaribie Yehova.” Wazazi, mujikaze sana kusaidia watoto wenu wakuwe na marafiki wazuri.

MUSIPOTEZE TUMAINI!

16. Utafanya nini kama mutoto wako anasema kama hatamutumikia Yehova?

16 Sasa mutafanya nini kama kisha kufanya yenu yote, mutoto wenu anasema kama hatamutumikia Yehova? Musiwaze kama mumeshindwa kutimiza daraka yenu. Yehova alitupatia siye wote uhuru wa kuamua kama tutamutumikia ao hapana. Watoto pia wako na ule uhuru. Kwa hiyo, kama mutoto wako anaamua kumuacha Yehova, uendelee kutumainia kama siku moya atamurudilia. Ukumbuke mufano wa mwana mupotevu. (Lu. 15:11-19, 22-24) Ule kijana alifanyaka mambo mingi ya mubaya, lakini kisha, alirudia. Watu fulani wanaweza kusema hivi: “Ile ilikuwaka tu mufano. Lakini kweli mutu anaweza kumurudilia Yehova?” Ndiyo, bila shaka! Na ile njo mambo yenye ilifikiaka kijana moya mwenye kuitwa Elie.

17. Habari ya Elie inakutia moyo namna gani?

17 Elie anasema hivi juu ya wazazi wake: “Walifanya yote yenye waliweza juu ya kunisaidia nimupende Yehova na Neno yake Biblia. Lakini, wakati nilikuwa kijana, nilianza kuasi.” Elie alianza kuishi maisha ya unafiki, na hata kama wazazi wake walijikaza sana juu ya kumusaidia, hakuwasikiliza. Kisha alitoka ku nyumba na akakuwa na tabia za mubaya. Hata vile, wakati fulani alikuwa anazungumuza na wengine juu ya Biblia. Elie anasema hivi: “Kadiri nilikuwa nazungumuza na rafiki yangu juu ya Yehova, ni vile nilikuwa nawaza zaidi juu ya Yehova. Polepole, mbegu ya kweli za Biblia yenye wazazi wangu walijikazaka sana kupanda mu moyo wangu, ilianza kukomala.” Kisha, Elie alifikia kumurudilia Yehova. * Waza namna wazazi wake walifurahi juu walijikazaka kumusaidia amupende Yehova wakati alikuwa angali mudogo!​—2 Ti. 3:14, 15.

18. Uko na mawazo gani juu ya wazazi wenye wanajikaza sana ili kusaidia watoto wao wamupende Yehova?

18 Wazazi, Yehova amewapatia pendeleo ya pekee sana. Muko na daraka ya kukomalisha watumishi wake wa kesho. (Zb. 78:4-6) Ile ni daraka nzito, na tunawashukuru sana juu munaendelea kujikaza sana kusaidia watoto wenu! Kama munaendelea kufanya yote yenye munaweza juu ya kuwasaidia wamupende Yehova na kumutii, mukuwe hakika kama Baba yenu wa mbinguni atafurahi sana.​—Efe. 6:4.

WIMBO 135 Yehova Anakuomba “Ukuwe na Hekima”

^ Wazazi Wakristo wanapendaka watoto wao sana. Wanafanyaka yao yote juu watoto wao wasikose mambo yenye wako nayo lazima na wakuwe na furaha. Zaidi ya yote, wanajikazaka sana juu ya kusaidia watoto wao wamupende sana Yehova. Hii habari itazungumuzia kanuni ine za Biblia zenye zinaweza kusaidia wazazi wafanye vile.

^ Ona habari yenye kichwa “Biblia Inabadili Maisha” mu Munara wa Mulinzi wa tarehe 1 Mwezi wa 4, 2012.

^ MAFASIRIO YA PICHA: Baba anapenda kujua marafiki wa mutoto wake, kwa hiyo, iko anacheza basket pamoya na mutoto wake na rafiki ya mutoto wake.