Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI YA KUJIFUNZA YA 39

Jina Yako Iko mu “Kitabu cha Uzima”?

Jina Yako Iko mu “Kitabu cha Uzima”?

“Kitabu cha kumbukumbu kikaandikwa mbele yake kwa ajili ya wale wenye kumuogopa Yehova.”​—MAL. 3:16.

WIMBO 61 Tuende Mbele

KIFUPI YA HABARI *

Kwa miaka mingi, Yehova ameendelea kuongeza majina mu “kitabu cha uzima” (Ona fungu ya 1-2)

1. Kulingana na Malaki 3:16, ni kitabu gani Yehova ameendelea kuandika kwa miaka mingi, na munapatikana nini?

 KWA miaka mingi, Yehova ameendelea kuandika kitabu fulani ya pekee sana. Mu ile kitabu muko liste ya majina kuanzia jina ya Abeli, shahidi muaminifu wa kwanza. * (Lu. 11:50, 51) Tangu ile wakati, Yehova ameendelea kuongeza majina mu ile kitabu, na leo munapatikana mamilioni ya majina. Mu Biblia, ile kitabu inaitwa “kitabu cha kumbukumbu,” “kitabu cha uzima,” na “kitabu cha kukunjwa cha uzima.” Mu hii habari, tutatumia maneno “kitabu cha uzima.”​—Soma Malaki 3:16; Ufu. 3:5; 17:8.

2. Ni majina ya wanani njo imeandikwa mu kitabu ya uzima, na tunapaswa kufanya nini juu majina yetu iandikwe mu ile kitabu?

2 Mu ile kitabu ya pekee munapatikana majina ya wale wote wenye kumuogopa Yehova na kupenda jina yake. Wako na tumaini ya kupata uzima wa milele. Juu na siye majina yetu iandikwe mu ile kitabu, tunapaswa kuwa na urafiki wa pekee pamoya na Yehova na kuamini bei ya ukombozi ya Mwana wake, Yesu Kristo. (Yoh. 3:16, 36) Ikuwe tuko na tumaini ya kuishi mbinguni ao ku dunia, siye wote tunapenda majina yetu iandikwe mu ile kitabu.

3-4. (a) Wale wote wenye kwa sasa majina yao imeandikwa mu kitabu ya uzima watapata uzima wa milele? Fasiria. (b) Tutajibia maulizo gani mu hii habari na mu habari yenye kufuata?

3 Ile inamaanisha kama wale wote wenye majina yao imeandikwa mu ile kitabu watapata uzima wa milele? Tunapata jibu ya ile ulizo mu maneno yenye Yehova alimuambia Musa mu Kutoka 32:33. Yehova alisema hivi: “Kila mutu mwenye amenitendea zambi, nitamufuta katika kitabu changu.” Kwa hiyo, Yehova anaweza kufuta, ao kuzimisha majina yenye kwa sasa inapatikana mu ile kitabu. Ni sawa vile Yehova ameiandika kwanza na kreyo. (Ufu. 3:5) Tunapaswa kujikaza juu majina yetu iendelee kubakia mu ile kitabu mupaka wakati Yehova ataiandika na bike, ni kusema, wakati ataiandika kwa lote.

4 Ile inaweza kufanya tujiulize maulizo fulani. Kwa mufano, Biblia inasema nini kuhusu wale wenye majina yao imeandikwa mu kitabu ya uzima na pia kuhusu wale wenye majina yao haiyaandikwa ndani? Ni wakati gani wale wenye majina yao imeandikwa mu ile kitabu watapata uzima wa milele? Mambo itakuwa namna gani kuhusu wale wenye walikufa bila kupata nafasi ya kumujua Yehova? Itawezekana majina yao iandikwe pia mu ile kitabu? Tutajibia ile maulizo mu hii habari na mu habari yenye kufuata.

NI WANANI NJO MAJINA YAO IKO MU ILE KITABU?

5-6. (a) Vile Wafilipi 4:3 inaonyesha, ni wanani njo majina yao iko kati ya majina yenye kuandikwa mu kitabu ya uzima? (b) Ni wakati gani njo majina yao itaandikwa kwa lote mu kitabu ya uzima?

5 Ni wanani njo majina yao imeandikwa mu ile kitabu ya mufano? Juu ya kujibia ile ulizo, tutazungumuzia vikundi tano vya watu. Kuko vikundi vya wale wenye majina yao imeandikwa mu kitabu ya uzima, na vingine hapana.

6 Kikundi ya kwanza ni ya wale wenye wamechaguliwa juu ya kutawala na Yesu mbinguni. Tunaweza kusema kama kwa sasa majina yao imeandikwa mu kitabu ya uzima? Ndiyo. Maneno yenye Mutume Paulo aliandikia ‘wafanyakazi wenzake’ katika Filipi inaonyesha kama majina ya watiwa-mafuta wenye wamechaguliwa ili kutawala na Yesu mbinguni inapatikana kwa sasa mu kitabu ya uzima. (Soma Wafilipi 4:3.) Lakini juu majina yao iendelee kubakia mu ile kitabu ya mufano, wanapaswa kuendelea kuwa waaminifu. Kama wanafanya vile, wakati watatiwa muhuri wa mwisho, majina yao itaandikwa kwa lote mu ile kitabu. Na wanatiwa muhuri wa mwisho mbele wakufe ao mbele taabu kubwa ianze.​—Ufu. 7:3.

7. Kulingana na Ufunuo 7:16, 17 ni wakati gani majina ya kondoo wengine itaandikwa kwa lote mu kitabu ya uzima?

7 Kikundi ya pili ni ya kundi kubwa ya kondoo wengine. Tunaweza kusema kama kwa sasa majina yao imeandikwa mu kitabu ya uzima? Ndiyo. Majina yao itaendelea kuwa mu kitabu ya uzima kisha wao kuokoka Armagedoni? Ndiyo. (Ufu. 7:14) Yesu alisema kama wale watumishi wa Yehova wenye kufananishwa na kondoo “wataingia katika uzima wa milele.” (Mt. 25:46) Lakini hawatapata uzima wa milele kisha tu kuokoka Armagedoni. Majina yao itaendelea kuwa mu kitabu ya uzima. Lakini itakuwa sawa vile majina yenye kuandikwa na kreyo. Mu Utawala wa Miaka Elfu, Yesu “atawachunga na kuwaongoza kwenye chemchemi za maji ya uzima.” Wale wenye watatii muongozo wa Kristo na wenye ku mwisho wataonekana kuwa waaminifu kwa Yehova, majina yao itaandikwa kwa lote katika kitabu ya uzima.​—Soma Ufunuo 7:16, 17.

8. Ni wanani njo majina yao haiko mu kitabu ya uzima, na watapata nini?

8 Kikundi ya tatu inafanyizwa na mbuzi, ni kusema, wale wenye wataharibiwa ku Armagedoni. Majina yao haiko mu kitabu ya uzima. Yesu alisema kama “watakatiliwa mbali milele.” (Mt. 25:46) Paulo alisema kama “watu hao watahukumiwa azabu ya uharibifu wa milele.” (2 Te. 1:9; 2 Pe. 2:9) Ni vile pia kuhusu wale wenye mupaka leo wanatenda zambi juu ya roho takatifu. Kusema kweli, hawatafufuliwa. (Mt. 12:32; Mk. 3:28, 29; Ebr. 6:4-6) Tuchunguze sasa vikundi mbili vya wale wenye watafufuliwa ku dunia.

WALE WENYE WATAFUFULIWA

9. Vile Matendo 24:15 inaonyesha, ni vikundi gani mbili vya watu wenye watafufuliwa, na kuko tofauti gani kati ya vile vikundi mbili?

9 Biblia inazungumuzia vikundi mbili vya watu wenye watafufuliwa juu waishi milele ku dunia. Kuko “wenye haki” na “wenye hawako wenye haki.” (Soma Matendo 24:15.) “Wenye haki” ni wale wenye walimutumikia Yehova kwa uaminifu wakati walikuwa wazima. Lakini “wenye hawako wenye haki” ni wale wenye hawakumutumikia Yehova kwa uaminifu. Wengi kati yao walikuwa na mwenendo mubaya. Juu wenye haki na wenye hawako wenye haki watafufuliwa, tunaweza kusema kama majina yao imeandikwa mu kitabu ya uzima? Juu ya kupata jibu tuzungumuzie kila kikundi.

10. Juu ya nini “wenye haki” watafufuliwa, na wamoja kati yao watapewa pendeleo gani? (Ona pia mu hii gazeti habari “Maulizo ya Wasomaji Wetu” kuhusu ufufuo wenye utafanyika ku dunia.)

10 “Wenye haki” njo kikundi ya ine ya wale wenye majina yao imeandikwa mu kitabu ya uzima. Mbele wakufe, majina yao iliandikwa mu kitabu ya uzima. Majina yao ilifutwa mu ile kitabu wakati walikufa? Hapana. Wangali “wazima” mu kumbukumbuku ya Yehova juu yeye “haiko Mungu wa wafu, lakini ni Mungu wa wenye kuwa wazima, kwa maana kwake wote ni wazima.” (Lu. 20:38) Ile inamaanisha kama wakati wenye haki watafufuliwa ku dunia, majina yao itapatikana mu kitabu ya uzima. Lakini itakuwa sawa vile majina yenye kuandikwa na “kreyo,” ni kusema, itakuwa haiyaandikwa kwa lote. (Lu. 14:14) Bila shaka, watu fulani kati ya wale wenye watafufuliwa watapewa pendeleo ya kuwa “wakubwa katika dunia yote.”​—Zb. 45:16.

11. “Wenye hawako wenye haki” watakuwa na lazima ya kufundishwa nini juu majina yao iandikwe mu kitabu ya uzima?

11 Tuchunguze kikundi ya tano, ni kusema, wale “wenye hawako wenye haki.” Pengine hawakujiendesha kwa njia ya haki mbele wakufe juu hawakujua sheria za Yehova. Njo maana, majina yao haikuandikwa mu kitabu ya uzima. Lakini, Mungu atawafufua na kuwapatia nafasi ya kuonyesha ikiwa wanapenda majina yao iandikwe mu kitabu ya uzima. “Wenye hawako wenye haki” watakuwa na lazima ya kusaidiwa sana. Wamoja kati yao walikuwa nafanya mambo ya mubaya sana mbele wakufe. Njo maana, watakuwa na lazima ya kufundishwa namna ya kutumikisha kanuni za haki za Yehova mu maisha yao. Juu ya kufanya vile, Ufalme wa Mungu utaanzisha kazi kubwa ya kufundisha watu yenye haiyafanyikaka ku dunia.

12. (a) Wanani njo watafundisha wale wenye hawako wenye haki? (b) Nini njo itafikia wale wenye watakatala kutumikisha mambo yenye wamejifunza?

12 Wanani njo watafundisha wenye hawako wenye haki? Ni kundi kubwa na wenye haki wenye watafufuliwa. Juu majina yao iandikwe mu kitabu ya uzima, itaomba wale wenye hawako wenye haki wakuwe na uhusiano na Yehova na wajitoe kwake. Mbinguni, Yesu Kristo na watiwa-mafuta watakuwa wanachunguza kwa uangalifu namna wale wenye hawako wenye haki wako natumikisha mambo yenye wako nafundishwa. (Ufu. 20:4) Ule mwenye atakatala kutumikisha mambo yenye atafundishwa, ataharibiwa hata akuwe na miaka 100. (Isa. 65:20) Yehova na Yesu wako na uwezo wa kujua mambo yenye iko mu moyo wa mutu na hawataruhusu mutu yeyote alete muvurugo mu dunia mupya.​—Isa. 11:9; 60:18; 65:25; Yoh. 2:25.

UFUFUO WA UZIMA NA UFUFUO WA HUKUMU

13-14. (a) Zamani, tulielewa namna gani maneno ya Yesu mu Yohana 5:29? (b) Lakini wakati tunaangalia muzuri maneno ya Yesu, tunatambua nini?

13 Yesu alizungumuzia pia wale wenye watafufuliwa hapa ku dunia. Kwa mufano, alisema hivi: “Saa inakuja yenye wale wote wenye kuwa katika makaburi ya ukumbusho watasikia sauti yake na watatoka, wale wenye walitenda mambo ya muzuri kwenye ufufuo wa uzima, na wale wenye walizoea kutenda mambo maovu kwenye ufufuo wa hukumu.” (Yoh. 5:28, 29) Yesu alipenda kusema nini?

14 Zamani, tulielewa kama Yesu alikuwa nazungumuzia mambo yenye wale wenye watafufuliwa watafanya kisha kufufuliwa: Wamoja watafufuliwa na kufanya mambo ya muzuri, na wengine watafufuliwa na kufanya mambo ya mubaya sana. Lakini ukiangalia muzuri, Yesu hakusema kama wale wenye wametoka mu makaburi ya ukumbusho watatenda mambo ya muzuri ao watazoea kutenda mambo maovu. Hakutumia wakati yenye kuya, lakini alitumia wakati yenye imepita. Alizungumuzia wale wenye “walitenda mambo ya muzuri” na “wale wenye walizoea kutenda mambo maovu.” Ile inamaanisha kama walifanya ile mambo mbele wakufe. Ile inaeleweka, hauone vile? Juu hakuna mutu mwenye ataruhusiwa kuzoea kutenda mambo maovu mu dunia mupya. Wale wenye hawako wenye haki walizoea kutenda mambo maovu mbele wakufe. Sasa, Yesu alipenda kusema nini wakati alizungumuzia “ufufuo wa uzima” na “ufufuo wa hukumu”?

15. Nani njo watapata “ufufuo wa uzima,” na juu ya nini?

15 Wenye haki, ni kusema, wale wenye walifanya mambo ya muzuri mbele wakufe, watapata “ufufuo wa uzima” juu majina yao itakuwa tayari imeandikwa mu kitabu ya uzima. Ile inamaanisha kama ufufuo wa “wale wenye walitenda mambo ya muzuri” yenye Yohana 5:29 inazungumuzia njo tu ufufuo wa “wenye haki” wenye Matendo 24:15 inazungumuzia. Ile mafasirio inapatana na mawazo ya Waroma 6:7, yenye inasema hivi: “Ule mwenye amekufa ameondolewa zambi yake.” Kwa hiyo, wakati wale wenye haki walikufa, zambi zao ziliishia pale. Lakini, Yehova aliendelea kukumbuka matendo yao ya uaminifu. (Ebr. 6:10) Kwa kweli, wale wenye haki wenye watafufuliwa watakuwa na lazima ya kuendelea kuwa waaminifu juu majina yao iendelee kubakia mu kitabu ya uzima.

16. “Ufufuo wa hukumu” maana yake nini?

16 Halafu wale wenye walizoea kutenda mambo maovu mbele wakufe? Hata kama zambi zao ziliondolewa wakati walikufa, hawakumutumikia Yehova kwa uaminifu wakati walikuwa wazima. Majina yao haiandikwe mu kitabu ya uzima. Kwa hiyo, ufufuo wa wale “wenye walizoea kutenda mambo maovu” njo tu ufufuo wa wale wenye hawako wenye haki yenye Matendo 24:15 inazungumuzia. Ni “ufufuo wa hukumu.” * Ni kusema wale wenye hawako wenye haki watahukumiwa. Namna gani? Yesu atakuwa nawachunguza ili kuona namna wako najiendesha. (Lu. 22:30) Kisha wakati fulani kupita, Yesu ataamua ikiwa majina yao inastahili kuandikwa mu kitabu ya uzima. Majina ya wale wenye hawako wenye haki itaandikwa mu kitabu ya uzima kama tu wanaachana na mambo ya mubaya yenye walifanyaka zamani na kujitoa kwa Yehova.

17-18. Wale wote wenye watafufuliwa ili kuishi ku dunia watakuwa na lazima ya kufanya nini, na ni “matendo” gani njo yenye inazungumuziwa mu Ufunuo 20:12, 13?

17 Ikuwe walikuwa wenye haki ao wenye hawako wenye haki mbele wakufe, itaomba wale wote wenye watafufuliwa watii sheria zenye zitapatikana mu vitabu vya kukunjwa vyenye vitafunguliwa mu miaka 1 000. Kuhusu ile mambo yenye aliona mu maono, mutume Yohana anasema hivi: “Nikaona wafu, wakubwa na wadogo, wamesimama mbele ya kile kiti cha ufalme, na vitabu vya kukunjwa vikafunguliwa. Lakini kitabu kingine cha kukunjwa kikafunguliwa; hicho ni kitabu cha kukunjwa cha uzima. Wafu wakahukumiwa kupatana na yale mambo yenye kuandikwa katika vile vitabu vya kukunjwa kulingana na matendo yao.”​—Ufu. 20:12, 13.

18 Wale wenye watafufuliwa watahukumiwa kulingana na “matendo” gani? Matendo yenye walitenda mbele wakufe? Hapana! Usisahau kama wakati walikufa, zambi zao za zamani ziliishia pale. Kwa hiyo, “matendo yao” haiwezi kuwa mambo yenye walifanyaka mbele wakufe. Lakini, inapaswa kuwa mambo yenye watafanya kisha mafundisho yenye watapewa mu dunia mupya. Na hata wanaume waaminifu sawa vile Noa, Samweli, Daudi, na Danieli watakuwa na lazima ya kujifunza juu ya Yesu Kristo na kuonyesha kama wanaamini bei yake ya ukombozi. Sasa, kama wale wanaume waaminifu watakuwa na lazima ya kujifunza mambo mingi, tuseme nini kuhusu wale wenye hawako wenye haki?

19. Nini njo itapata wale wenye watakatala kutumikisha mambo yenye watafundishwa?

19 Nini njo itapata wale wenye watakatala kutumikisha mambo yenye watafundishwa? Ufunuo 20:15 inatuambia hivi: “Kila mutu mwenye hakupatikana ameandikwa katika kile kitabu cha uzima alitupwa ndani ya lile ziwa la moto.” Ni kusema wataharibiwa kabisa milele. Njo maana, inaomba tujikaze sana juu jina yetu iandikwe mu kitabu ya uzima na ibakie ndani!

Ndugu moya iko nashiriki mu kazi kubwa ya kufundisha watu yenye itafanywa mu kipindi ya Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo (Ona fungu ya 20)

20. Ni kazi gani kubwa yenye itafanywa mu kipindi ya Utawala wa Miaka Elfu wa Yesu? (Ona picha ku jalada.)

20 Utawala wa Miaka Elfu wa Yesu utakuwa kipindi ya furaha sana! Kutakuwa kazi kubwa ya kufundisha watu yenye haiyafanyikaka ku dunia. Lakini itakuwa pia wakati yenye mwenendo wa wenye haki na wale wenye hawako wenye haki utachunguzwa. (Isa. 26:9; Mdo. 17:31) Ile kazi kubwa ya kufundisha watu itafanywa namna gani? Habari yenye kufuata itatusaidia kuelewa namna mambo itakuwa.

WIMBO 147 Ahadi ya Uzima wa Milele

^ Hii habari iko na mafasirio ya mupya ya maneno ya Yesu yenye kupatikana mu Yohana 5:28, 29 kuhusu “ufufuo wa uzima” na “ufufuo wa hukumu.” Tutajifunza maana ya “ufufuo wa uzima” na “ufufuo wa hukumu,” na tutaona nani njo atapata “ufufuo wa uzima” na nani njo atapata “ufufuo wa hukumu.”

^ Ile kitabu ilianza kuandikwa tangu “kuwekwa musingi wa ulimwengu.” Hapa ulimwengu unamaanisha watu wenye wanaweza kukombolewa katika zambi. (Mt. 25:34; Ufu. 17:8) Kwa hiyo, inaonekana kama, jina yenye ilikuwa ya kwanza kuandikwa mu kitabu ya uzima ni jina ya Abeli, mwenye haki.

^ Zamani, tulifasiria kama neno “hukumu” yenye kutumiwa mu Yohana 5:28, 29 inamaanisha kupewa azabu ao malipizi. Ni kweli, neno “hukumu” inaweza kuwa na ile maana. Lakini mu ile andiko, inaonekana Yesu hakutumia neno “hukumu” katika maana fulani ya pekee. Yesu alitumia ile neno juu ya kuzungumuzia namna mutu fulani anachunguzwa ili kuona ikiwa anastahili, ao sawa vile diksionere fulani ya Kigiriki inasema, “kuchunguza kabisa mwenendo wa mutu.”