Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Tunatiwa Nguvu Ili Kushinda Jaribu Lolote

Tunatiwa Nguvu Ili Kushinda Jaribu Lolote

Tunatiwa Nguvu Ili Kushinda Jaribu Lolote

“Kwa mambo yote nina nguvu kupitia yeye anayenipa nguvu.”—FLP. 4:13.

1. Kwa nini watu wa Yehova wanapambana na matatizo mengi?

 KWA KAWAIDA watu wa Yehova wanapambana na matatizo ya aina moja au nyingine. Majaribu fulani yanatokana na kutokamilika kwetu wenyewe au yanasababishwa na mfumo wa mambo tunamoishi. Mengine yanatokana na uadui uliopo kati ya wale wanaomtumikia Mungu na wale ambao hawamtumikii. (Mwa. 3:15) Tangu mwanzoni mwa historia ya wanadamu, Mungu amewasaidia watumishi wake waaminifu kuvumilia mateso ya kidini, kushinda msongo hatari wa marafiki, na kuvumilia matatizo mengine ya kila aina. Roho yake takatifu inaweza kututia nguvu kufanya vivyo hivyo.

Tunasaidiwa Kuvumilia Mateso ya Kidini

2. Ni nini kusudi la mateso ya kidini, na yanaweza kuwa ya aina gani?

2 Mateso ya kidini yanatia ndani kuwasumbua au kuwaumiza watu kimakusudi kwa sababu ya imani au mafundisho yao. Kusudi la mateso hayo ni kukomesha mafundisho hayo, kuyazuia yasienee, au kuvunja utimilifu wa waamini. Mateso yanaweza kuwa ya aina mbalimbali, yanaweza kuwa ya waziwazi au ya ujanja. Biblia inalinganisha mashambulizi ya Shetani na yale ya mwana-simba na pia ya nyoka anayeitwa swila.—Soma Zaburi 91:13.

3. Shetani anashambulia jinsi gani kama simba na kama swila?

3 Akiwa kama simba mkali, mara nyingi Shetani ameshambulia waziwazi na moja kwa moja kwa kutumia jeuri, vifungo vya gereza, au marufuku. (Zab. 94:20) Ripoti za Kitabu cha mwaka zinazoeleza matendo ya Mashahidi wa Yehova katika nyakati za kisasa zina masimulizi mengi ya mbinu kama hizo. Umati wa watu wasiotii sheria, wengine wakiongozwa na makasisi au wanasiasa washupavu, wamewatendea vibaya watu wa Mungu katika maeneo mengi duniani. Mashambulizi hayo yaliyo kama ya simba yamefanya watu wachache wajikwae. Kama nyoka anayeitwa swila, Ibilisi pia anashambulia watu kwa ujanja kutoka mahali anapojificha ili kupotosha akili zao na kuwadanganya wafanye mapenzi yake. Mashambulizi ya aina hiyo yanakusudiwa kutudhoofisha au kutupotosha kiroho. Kupitia roho takatifu ya Mungu, tunaweza kuvumilia mateso hayo ya aina mbili.

4, 5. Ni njia gani iliyo bora zaidi ya kujitayarisha kwa ajili ya mateso, na kwa nini? Toa mfano.

4 Kufikiria mateso mbalimbali ambayo yanaweza kutokea wakati ujao si njia nzuri zaidi ya kujitayarisha kupambana nayo. Ukweli ni kwamba hatuwezi kujua ni mateso ya aina gani tutakayopambana nayo, kwa hiyo hakuna faida ya kuwa na wasiwasi kuhusu mambo ambayo huenda yasitukie kamwe. Hata hivyo, kuna jambo ambalo tunaweza kufanya. Watu wengi wamefaulu kuvumilia mateso kwa kutafakari juu ya mifano ya watu waaminifu walioshika utimilifu ambao wanatajwa katika Maandiko, na pia kutafakari kuhusu mafundisho na mfano wa Yesu. Hilo limewasaidia kumpenda Yehova hata zaidi. Na upendo huo, umewasaidia kushinda majaribu yoyote waliyopata.

5 Fikiria mfano wa dada zetu wawili huko Malawi. Katika jitihada za kuwashawishi wanunue kadi za chama cha kisiasa, umati wa watu wenye jeuri uliwapiga, ukawavua nguo, na kutisha kuwalala kinguvu. Watu hao waliwadanganya dada hao kwamba hata washiriki wa familia ya Betheli walikuwa wamenunua kadi za chama. Dada hao walitenda jinsi gani? “Tunamtumikia Yehova Mungu peke yake. Kwa hiyo, ikiwa ndugu katika ofisi ya tawi wamenunua kadi, hilo halitafanya tununue kadi hizo. Hatutalegeza msimamo wetu, hata mkituua!” Baada ya kuchukua msimamo huo wa ujasiri, dada hao waliachiliwa huru.

6, 7. Yehova anawatia nguvu jinsi gani watumishi wake ili wapambane na mateso?

6 Mtume Paulo aliandika kwamba Wakristo huko Thesalonike walikubali ujumbe wa kweli “chini ya dhiki nyingi,” lakini “pamoja na shangwe ya roho takatifu.” (1 The. 1:6) Kwa kweli, Wakristo wengi, wa zamani na wa sasa, ambao wamepambana na mateso na kuyashinda wanasema kwamba walipojaribiwa vikali zaidi, walipata amani ya moyoni, ambayo ni sehemu ya tunda la roho takatifu ya Mungu. (Gal. 5:22) Hivyo, amani hiyo ilisaidia kulinda mioyo yao na nguvu zao za akili. Ndiyo, Yehova anatumia nguvu yake ya utendaji ili kuwatia nguvu watumishi wake kushinda majaribu na kutenda kwa hekima matatizo yanapotokea. *

7 Watazamaji wanashangaa kuona jinsi watu wa Mungu wanavyoazimia kudumisha utimilifu wao hata wanapokabili mateso makali. Mashahidi wanaonekana kuwa na nguvu nyingi zinazozidi zile za kibinadamu, na kwa kweli wana nguvu hizo. Mtume Petro anatuhakikishia hivi: “Ikiwa mnashutumiwa kwa ajili ya jina la Kristo, ninyi ni wenye furaha, kwa sababu ile roho ya utukufu, yaani roho ya Mungu, inatulia juu yenu.” (1 Pet. 4:14) Uhakika wa kwamba tunateswa kwa sababu tunafuata viwango vya uadilifu unaonyesha kwamba tunakubaliwa na Mungu. (Mt. 5:10-12; Yoh. 15:20) Tunapata shangwe kama nini tunapoona uthibitisho huo wa baraka za Yehova!

Tunasaidiwa Kushinda Msongo wa Marafiki

8. (a) Ni nini kilichowawezesha Yoshua na Kalebu kupinga msongo wa wapelelezi wenzao? (b) Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Yoshua na Kalebu?

8 Upinzani usio wa wazi zaidi ambao Wakristo wanapaswa kuvumilia ni msongo mbaya wa marafiki. Hata hivyo, kwa sababu roho ya Yehova ni yenye nguvu zaidi kuliko roho ya ulimwengu, tunaweza kuwapinga watu wanaotudhihaki, wanaoeneza uwongo kutuhusu, au wanaojaribu kutulazimisha tufuate viwango vyao. Kwa mfano, ni nini kilichowawezesha Yoshua na Kalebu kupinga maoni ya wale wapelelezi wengine kumi ambao walitumwa katika nchi ya Kanaani? Roho takatifu iliwachochea kuwa na “roho” tofauti, au mwelekeo tofauti wa akili.—Soma Hesabu 13:30; 14:6-10, 24.

9. Kwa nini ni lazima Wakristo wawe tayari kuwa tofauti na watu wengi?

9 Vivyo hivyo, roho takatifu iliwatia nguvu mitume wa Yesu kumtii Mungu badala ya wale ambao watu wengi waliwaheshimu na kuwaona kuwa walimu wa dini ya kweli. (Mdo. 4:21, 31; 5:29, 32) Watu wengi wanapendelea kufuata umati ili kuepuka mapambano au ugomvi. Lakini, mara nyingi Wakristo wa kweli wamelazimika kusimama imara kwa ajili ya yale ambayo wanajua kuwa ni sawa. Hata hivyo, kwa sababu nguvu ya utendaji ya Mungu inawatia nguvu, hawaogopi kuwa tofauti na wengine. (2 Tim. 1:7) Ona njia moja ambayo tunapaswa kuepuka kusongwa na marafiki.

10. Ni hali gani inayoweza kuwatatanisha Wakristo fulani?

10 Vijana fulani wanaweza kushindwa jambo la kufanya wanapojua kwamba rafiki yao amekuwa na mwenendo usiopatana na maandiko. Huenda wakahisi kwamba kuwaomba wazee wamsaidie rafiki yao ni kukosa kuwa mwaminifu kwa rafiki yao; kwa hiyo, wanakataa kuzungumza kuhusu jambo hilo kwa sababu ya kuwa na ushikamanifu usiofaa. Mkosaji anaweza hata kuwasonga marafiki wake ili wafiche dhambi yake. Bila shaka, si vijana tu walio na tatizo kama hilo. Inaweza pia kuwa vigumu kwa watu fulani wazima kuwafikia wazee wa kutaniko na kuwaeleza kuhusu rafiki au mshiriki wa familia aliyetenda dhambi. Lakini Wakristo wa kweli wanapaswa kutenda jinsi gani wanaposongwa hivyo?

11, 12. Ni njia gani nzuri zaidi ya kumjibu mshiriki wa kutaniko anayekuomba usifunue dhambi yake, na kwa nini?

11 Fikiria hali hii. Tuseme kwamba ndugu kijana anayeitwa Alex anapata habari kwamba Steve, rafiki yake katika kutaniko, amezoea kutazama ponografia. Alex anamwambia Steve kwamba ana wasiwasi sana kuhusu zoea lake. Hata hivyo, Steve anapuuza maneno ya rafiki yake. Alex anapomhimiza rafiki yake azungumze na wazee kuhusu jambo hilo, Steve anamwambia kwamba ikiwa kwa kweli yeye ni rafiki yake, basi hatawaambia wazee jambo hilo. Je, Alex anapaswa kuogopa kumpoteza rafiki yake? Huenda akafikiria kwamba wazee hawatamwamini ikiwa Steve atakana kabisa jambo hilo. Hata hivyo, hali hiyo haitabadilika na kuwa nzuri ikiwa Alex atanyamaza. Kwa kweli, inaweza kuharibu uhusiano wa Steve pamoja na Yehova. Itakuwa vizuri Alex akikumbuka kwamba “kutetemeshwa na wanadamu ndiko huleta mtego, lakini yeye anayemtegemea Yehova atalindwa.” (Met. 29:25) Alex anaweza kufanya jambo gani lingine? Kwa upendo, anaweza kumfikia tena Steve na kuzungumza naye waziwazi kuhusu tatizo lake. Anahitaji ujasiri ili kufanya hivyo. Hata hivyo, huenda ikawa kwamba wakati huu Steve atatumia nafasi hiyo kuzungumza kuhusu tatizo lake. Alex anapaswa tena kumtia moyo Steve azungumze na wazee na kumwambia kwamba ikiwa hatafanya hivyo haraka, basi Alex atawajulisha wazee.—Law. 5:1.

12 Ikiwa utahitaji kushughulikia hali kama hiyo, huenda mwanzoni rafiki yako asifurahie jitihada zako za kumsaidia. Lakini baada ya muda huenda akatambua kwamba unafanya hivyo kwa faida yake. Mkosaji akipokea na kukubali msaada, basi huenda akakushukuru daima kwa sababu ya ujasiri na ushikamanifu wako. Kwa upande mwingine, akikukasirikia, je, kweli ungependa kuwa na rafiki kama huyo? Sikuzote, jambo linalofaa ambalo tunapaswa kufanya ni kumpendeza Rafiki yetu mkuu zaidi, Yehova. Tunapomtanguliza, wengine ambao wanampenda watatuheshimu kwa sababu ya ushikamanifu wetu na watakuwa marafiki wa kweli. Hatupaswi kamwe kumpa Ibilisi nafasi katika kutaniko la Kikristo. Ikiwa tungefanya hivyo, tungeihuzunisha kwelikweli roho takatifu ya Yehova. Hata hivyo, tunatenda kulingana na roho hiyo tunapojitahidi kudumisha usafi wa kutaniko la Kikristo.—Efe. 4:27, 30.

Tunatiwa Nguvu Kuvumilia Matatizo ya Kila Aina

13. Watu wa Yehova wanakabili matatizo ya aina gani, na kwa nini mambo kama hayo yameenea sana leo?

13 Majaribu yanaweza kuwa ya aina mbalimbali, kama vile matatizo ya kiuchumi, kupoteza kazi, misiba ya asili, kifo cha mpendwa, ugonjwa, na kadhalika. Kwa kuwa tunaishi katika “nyakati za hatari,” tunatambua kwamba muda si muda sisi sote tutakabiliana na jaribu fulani. (2 Tim. 3:1) Ikiwa hilo litatukia, ni jambo la maana kutoogopa. Roho takatifu inaweza kututia nguvu kuvumilia tatizo lolote.

14. Ni nini kilichomtia Ayubu nguvu kuvumilia matatizo yake?

14 Ayubu alipatwa na tatizo moja baada ya lingine. Alipoteza mali ambayo ilimletea riziki, alipoteza watoto, marafiki, na afya yake, na mke wake akaacha kumtegemea Yehova. (Ayu. 1:13-19; 2:7-9) Hata hivyo, Ayubu alimwona Elihu kuwa mfariji wa kweli. Ujumbe wa Elihu, na pia jambo kuu ambalo Yehova alikuwa akimwambia Ayubu ni hili: “Simama tuli na ukazie fikira kazi za ajabu za Mungu.” (Ayu. 37:14) Ni nini kilichomsaidia Ayubu kuvumilia majaribu yake? Na ni nini kinachoweza kutusaidia kuvumilia majaribu yetu? Ni kukumbuka na kutafakari juu ya matendo mbalimbali ya roho takatifu ya Yehova na nguvu zake. (Ayu. 38:1-41; 42:1, 2) Labda tunakumbuka nyakati fulani katika maisha yetu tulipoona uthibitisho wa kwamba Mungu anapendezwa nasi binafsi. Bado anapendezwa nasi.

15. Ni nini kilichomtia mtume Paulo nguvu za kuvumilia majaribu?

15 Mtume Paulo alivumilia matatizo mengi yaliyohatarisha uhai wake kwa ajili ya imani yake. (2 Kor. 11:23-28) Alidumisha jinsi gani usawaziko na utulivu wa moyoni katika hali hizo zenye kujaribu? Kwa kumtegemea Yehova katika sala. Wakati wa jaribu ambalo inaelekea lilifanya auawe kwa sababu ya imani yake, Paulo aliandika: “Bwana alisimama karibu nami na kutia nguvu ndani yangu, ili kupitia mimi kazi ya kuhubiri itimizwe kwa ukamili na mataifa yote yaisikie; nami nilikombolewa kutoka katika kinywa cha simba.” (2 Tim. 4:17) Kwa hiyo, kutokana na mambo yaliyompata yeye binafsi, Paulo aliwahakikishia waamini wenzake kwamba hawakuhitaji ‘kuhangaika juu ya kitu chochote.’Soma Wafilipi 4:6, 7, 13.

16, 17. Toa mfano unaoonyesha jinsi Yehova anavyowatia watu wake nguvu ili wakabiliane na matatizo leo.

16 Painia mmoja anayeitwa Roxana ameona jinsi Yehova anavyowasaidia watu wake. Alipomwomba mkubwa wake wa kazi ruhusa ya kuhudhuria kusanyiko letu kwa siku fulani, mkubwa huyo alimjibu kwa hasira kwamba ikiwa angeenda, angemfuta kazi. Hata hivyo, Roxana alienda kusanyikoni na akasali kwa bidii ili asipoteze kazi yake. Baada ya hapo, alihisi ametulia moyoni. Kama tu alivyokuwa ametishwa, mkubwa wake alimfuta kazi Jumatatu (Siku ya Kwanza) baada ya kusanyiko. Roxana alivurugika. Roxana alihitaji kazi hiyo ili kuitegemeza familia yake, ingawa ilikuwa kazi ya mshahara mdogo. Kwa mara nyingine tena alisali, na akatafakari juu ya ukweli wa kwamba Mungu alitosheleza mahitaji yake ya kiroho katika kusanyiko, hivyo, bila shaka, angeweza pia kutosheleza mahitaji yake ya kimwili. Alipokuwa akitembea kuelekea nyumbani, Roxana aliona tangazo lenye maneno “Tunahitaji Wafanyakazi” ambalo lilieleza kwamba mafundi wenye uzoefu wa kuendesha mashini za kushona viwandani walihitajiwa, hivyo akatuma maombi ya kazi. Msimamizi wa kampuni hiyo alitambua kwamba Roxana hakuwa na uzoefu lakini akaamua tu kumpa kazi na kumlipa mshahara ambao ulikuwa karibu mara mbili ya ule ambao alikuwa akilipwa mbeleni. Roxana aliona kwamba sala zake zilijibiwa. Hata hivyo, baraka kubwa zaidi ilikuwa kwamba aliweza kuwahubiria habari njema wafanyakazi wenzake wengi. Watano kati yao, kutia ndani yule msimamizi, walikubali kweli nao wakabatizwa.

17 Nyakati nyingine, inaweza kuonekana kwamba sala zetu hazijibiwi papo hapo au kwa njia ambayo tunatazamia. Ikiwa ndivyo ilivyo, bila shaka kuna sababu nzuri. Yehova anajua sababu hiyo, lakini huenda tu sababu hiyo ikawa wazi zaidi kwetu wakati ujao. Tunaweza kuwa na hakika kuhusu jambo moja, Mungu hawaachi waaminifu wake.—Ebr. 6:10.

Tunasaidiwa Kushinda Majaribu na Vishawishi

18, 19. (a) Kwa nini tunaweza kutarajia kupata majaribu na vishawishi? (b) Unaweza kukabiliana na majaribu jinsi gani kwa mafanikio?

18 Watu wa Yehova hawashangai wanaposhawishiwa, kuteswa, kuvunjika moyo, na kusongwa na marafiki. Kwa ujumla, ulimwengu unatuchukia. (Yoh. 15:17-19) Hata hivyo, roho takatifu inaweza kutusaidia kushinda tatizo lolote ambalo tunaweza kupata katika utumishi wetu kwa Mungu. Yehova hatatuacha tujaribiwe kupita tunavyoweza kuvumilia. (1 Kor. 10:13) Hatatuacha kamwe wala kututupa hata kidogo. (Ebr. 13:5) Kutii Neno lake lililoongozwa na roho kunatulinda na kututia nguvu. Zaidi ya hayo, roho ya Mungu inaweza kuwachochea waamini wenzetu watupatie msaada wakati tunapouhitaji zaidi.

19 Acheni sisi sote tuendelee kutafuta roho takatifu kwa kusali na kujifunza Maandiko. Na tuendelee ‘kufanywa kuwa na nguvu kwa nguvu zote kwa kadiri ya uwezo wa Mungu wenye utukufu ili kuvumilia kikamili na kuwa wenye ustahimilivu pamoja na shangwe.’—Kol. 1:11.

[Maelezo ya Chini]

^ Unaweza kupata mifano katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Mei 1, 2001 (1/5/2001), ukurasa wa 16; na gazeti la Amkeni! la Februari 8, 1993, ukurasa wa 21 na 22.

Ungesema Nini?

• Unaweza kujitayarisha jinsi gani kuvumilia mateso?

• Unapaswa kutenda jinsi gani ikiwa mtu fulani anakuomba usifunue dhambi yake?

• Unaweza kuwa na uhakika gani unapokabiliana na tatizo lolote?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 28]

Tunaweza kujifunza nini kutokana na Yoshua na Kalebu?

[Picha katika ukurasa wa 29]

Unaweza kumsaidia jinsi gani rafiki ambaye ametenda dhambi?