Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Tunatiwa Nguvu Ili Kushinda Vishawishi na Kutovunjika Moyo

Tunatiwa Nguvu Ili Kushinda Vishawishi na Kutovunjika Moyo

Tunatiwa Nguvu Ili Kushinda Vishawishi na Kutovunjika Moyo

“Mtapokea nguvu wakati roho takatifu itakapofika juu yenu.”—MDO. 1:8.

1, 2. Yesu aliwaahidi wanafunzi wake msaada gani, na kwa nini wangeuhitaji?

 YESU alijua kwamba wanafunzi wake hawangeweza kutimiza kwa nguvu zao wenyewe mambo yote aliyoamuru. Tukifikiria ukubwa wa kazi yao ya kuhubiri, nguvu za wapinzani wao, na udhaifu wa mwili wa kibinadamu, ilikuwa wazi kwamba walihitaji nguvu zinazozidi za kibinadamu. Kwa hiyo, kabla tu ya kupanda mbinguni, Yesu aliwahakikishia wanafunzi wake hivi: “Mtapokea nguvu wakati roho takatifu itakapofika juu yenu, nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu na pia katika Yudea yote na Samaria na mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.”—Mdo. 1:8.

2 Ahadi hiyo ilianza kutimia wakati wa Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K. roho takatifu ilipowatia nguvu wafuasi wa Yesu Kristo nao wakajaza Yerusalemu na mahubiri yao. Hakuna upinzani ulioweza kusimamisha kazi hiyo. (Mdo. 4:20) “Siku zote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo,” wafuasi waaminifu wa Yesu, kutia ndani sisi, wangehitaji sana nguvu hiyohiyo ya Mungu.—Mt. 28:20.

3. (a) Eleza tofauti iliyopo kati ya roho takatifu na nguvu. (b) Nguvu kutoka kwa Yehova zinaweza kutusaidia kufanya nini?

3 Yesu aliwaahidi wanafunzi wake kwamba ‘wangepokea nguvu wakati roho takatifu ingefika juu yao.’ Maneno “nguvu” na “roho” yana maana tofauti. Roho ya Mungu, yaani, nguvu zake za utendaji, ni nguvu ambazo zinamiminwa na kutumiwa juu ya watu au vitu ili kutimiza mapenzi ya Mungu. Hata hivyo, tunaweza kusema kwamba nguvu ni “uwezo wa kutenda au wa kusababisha matokeo fulani.” Nguvu zinaweza kukaa tu ndani ya mtu au kitu fulani mpaka zinapotumiwa kusababisha matokeo fulani. Kwa hiyo, roho takatifu inaweza kulinganishwa na nguvu za umeme ambazo zinaiongezea betri nguvu mpya, lakini nguvu ni kama tu nishati ambayo haitumiki au imehifadhiwa ndani ya betri. Nguvu ambazo Yehova anawapa watumishi wake kupitia roho takatifu zinamwezesha kila mmoja wetu kutimiza wakfu wetu wa Kikristo na, inapohitajika, zinatuwezesha kushinda nguvu za uovu zinazotumiwa kutupinga.—Soma Mika 3:8; Wakolosai 1:29.

4. Tutachunguza nini katika habari hii, na kwa nini?

4 Nguvu tunazopewa kupitia roho takatifu zinaonekana jinsi gani? Roho takatifu inaweza kutuchochea kutenda jinsi gani? Tunapojitahidi kumtumikia Mungu kwa uaminifu, tunakabili vipingamizi vingi vinavyosababishwa na Shetani, mfumo wake wa mambo, au na mwili wetu wenyewe usio mkamilifu. Ni jambo la maana kushinda vipingamizi hivyo ili tuendelee kuwa Wakristo, kushiriki kwa ukawaida katika huduma, na kudumisha uhusiano mzuri pamoja na Yehova. Acheni basi tuchunguze jinsi roho takatifu inavyotusaidia kushinda vishawishi, kutochoka, na kutovunjika moyo.

Tunatiwa Nguvu Kushinda Vishawishi

5. Sala inaweza kututia nguvu jinsi gani?

5 Yesu aliwafundisha wafuasi wake wasali hivi: “Usituingize katika jaribu, bali utukomboe kutokana na yule mwovu.” (Mt. 6:13) Yehova hatawaacha watumishi wake waaminifu ambao wanamwomba mambo hayo. Katika pindi nyingine, Yesu alisema kwamba “Baba aliye mbinguni [atawapa] roho takatifu wale wanaomwomba.” (Luka 11:13) Inatia moyo kama nini kwamba Yehova anatuahidi kuwa atatupatia roho yake, msaada wenye nguvu ili tutende yaliyo sawa! Bila shaka, hilo halimaanishi kwamba Yehova atazuia tusishawishiwe. (1 Kor. 10:13) Lakini tunaposhawishiwa, huo ndio wakati wa kusali kwa bidii hata zaidi.—Mt. 26:42.

6. Yesu alitegemea nini ili kupinga vishawishi vya Shetani?

6 Ili kupinga vishawishi vya Ibilisi, Yesu alinukuu au kutaja maandiko. Neno la Mungu lilikuwa wazi katika akili ya Yesu alipojibu hivi: “Imeandikwa . . . Tena imeandikwa . . . Nenda zako, Shetani! Kwa maana imeandikwa, ‘Yehova Mungu wako ndiye unayepaswa kumwabudu, na yeye peke yake ndiye unayepaswa kumtolea utumishi mtakatifu.’” Yesu alimpenda Yehova na Neno lake na hilo lilimchochea kupinga vishawishi ambavyo yule Mshawishi aliweka mbele yake. (Mt. 4:1-10) Baada ya Yesu kupinga tena na tena vishawishi hivyo, Shetani alimwacha.

7. Biblia inatusaidia jinsi gani kupinga vishawishi?

7 Kwa kuwa Yesu alitegemea Maandiko ili kupinga vishawishi vya Ibilisi, sisi tunapaswa kuyategemea hata zaidi! Kwa kweli, ili tuweze kumpinga Ibilisi na watumishi wake, ni lazima kwanza tuazimie kujua vizuri viwango vya Mungu na kushikamana navyo kabisa. Watu wengi wamechochewa kuishi kulingana na viwango vya Biblia walipojifunza Maandiko na wakaja kuelewa na kuthamini hekima ya Mungu na uadilifu wake. Kwa kweli, “neno la Mungu” lina nguvu ambayo inaweza kutambua “fikira na makusudio ya moyo.” (Ebr. 4:12) Kadiri mtu anavyosoma na kutafakari juu ya Maandiko, ndivyo anavyoweza kupata ‘ufahamu katika ukweli wa Yehova.’ (Dan. 9:13) Kwa kuwa ndivyo ilivyo, tunapaswa kutafakari juu ya maandiko ambayo yanazungumzia hasa udhaifu wetu.

8. Tunaweza kupata roho takatifu kupitia njia gani?

8 Zaidi ya kuwa na ujuzi wa Maandiko, Yesu alipinga vishawishi kwa sababu alikuwa “amejaa roho takatifu.” (Luka 4:1) Ili tuwe na nguvu na uwezo huohuo, tunahitaji kumkaribia Yehova zaidi kwa kutumia kikamili maandalizi yote ambayo ametupatia ili yatujaze roho yake. (Yak. 4:7, 8) Maandalizi hayo yanatia ndani funzo la Biblia, sala, na ushirika wa waamini wenzetu. Wengi wamethamini pia faida ya kuwa na ratiba au programu kamili ya utendaji mbalimbali wa Kikristo, ambayo inatusaidia kukazia akili mawazo ya kiroho yenye kujenga.

9, 10. (a) Ni vishawishi gani ambavyo ni vya kawaida katika eneo lenu? (b) Kutafakari na kusali kunaweza kukutia nguvu jinsi gani ili ushinde vishawishi hata unapohisi umechoka?

9 Ni vishawishi gani vya kutenda dhambi unavyohitaji kupinga? Je, umewahi kushawishiwa kumchezea kimapenzi mtu ambaye si mwenzi wako wa ndoa? Ikiwa wewe hujafunga ndoa, je, umewahi kushawishiwa kukubali kufanya matembezi ya kimapenzi na mtu ambaye si mwamini? Wanapotazama televisheni au kutumia Intaneti, Wakristo wanaweza kwa ghafula kushawishiwa kutazama jambo fulani lisilo safi. Je, umewahi kujikuta katika hali hiyo, ikiwa ndivyo, ulitenda jinsi gani? Ni jambo la hekima kufikiria jinsi tendo moja baya linavyoweza kuongoza kwenye tendo lingine baya na baadaye kwenye kosa zito. (Yak. 1:14, 15) Fikiria jinsi ambavyo tendo moja la kukosa uaminifu linavyoweza kumtia uchungu Yehova, kutaniko, na familia yako. Kwa upande mwingine, dhamiri safi inatokana na kuendelea kudumisha ushikamanifu kwa kanuni za Mungu. (Soma Zaburi 119:37; Methali 22:3.) Wakati wowote unapopambana na majaribu kama hayo, azimia kusali na kuomba nguvu za kuyapinga.

10 Kuna jambo lingine la kukumbuka kuhusu vishawishi kutoka kwa Ibilisi. Shetani alimjia Yesu baada ya Yeye kufunga kwa siku 40 nyikani. Bila shaka, Ibilisi alifikiri kwamba huo ulikuwa ndio ‘wakati unaofaa’ kabisa wa kujaribu utimilifu wa Yesu. (Luka 4:13) Shetani anatafuta pia nyakati zinazofaa za kujaribu utimilifu wetu. Hivyo, ni jambo la maana kwamba tuendelee kuwa wenye nguvu kiroho. Mara nyingi Shetani anashambulia wakati anapoona kwamba windo lake liko dhaifu zaidi. Kwa hiyo, wakati wowote tunapohisi tumechoka au kuvunjika moyo, ni lazima tuazimie zaidi kuliko wakati mwingine wowote kumwomba Yehova msaada na ulinzi wake na pia roho yake takatifu.—2 Kor. 12:8-10.

Tunatiwa Nguvu Ili Tusichoke na Kuvunjika Moyo

11, 12. (a) Kwa nini watu wengi leo wamevunjika moyo? (b) Ni nini kinachoweza kututia nguvu ili tusivunjike moyo?

11 Tukiwa wanadamu wasio wakamilifu, mara kwa mara tunavunjika moyo. Inaweza kuwa hivyo hasa leo kwa sababu wakati tunamoishi ni wenye mikazo mingi. Tunaishi katika nyakati ambazo labda ndizo nyakati ngumu zaidi ambazo wanadamu kwa ujumla wamewahi kupambana nazo. (2 Tim. 3:1-5) Har–Magedoni inapokaribia, mikazo ya kiuchumi, kihisia, na mikazo mingine inaongezeka. Basi, hatupaswi kushangaa kwamba inazidi kuwa vigumu kwa watu fulani kutimiza madaraka yao ya kutunza familia zao na kutosheleza mahitaji yao. Wanahisi wamechoka, wamelemewa, wamepondeka, na hata wako hoi kabisa. Ikiwa hivyo ndivyo unavyohisi, unaweza kushinda jinsi gani mikazo hiyo?

12 Kumbuka Yesu aliwahakikishia wanafunzi wake kwamba angewapa msaidizi, yaani, roho takatifu ya Mungu. (Soma Yohana 14:16, 17.) Roho takatifu ni nguvu zenye uwezo zaidi katika ulimwengu wote. Kwa kutumia roho hiyo, Yehova anaweza kutupatia “kwa wingi zaidi” nguvu ambazo tunahitaji ili kuvumilia jaribu lolote. (Efe. 3:20) Tunapoitegemea roho takatifu, mtume Paulo alisema kwamba tunapokea “nguvu zinazopita zile za kawaida,” hata ingawa “tunakazwa katika kila njia.” (2 Kor. 4:7, 8) Yehova haahidi kuondoa mikazo, lakini anatuhakikishia kwamba kupitia roho yake, atatupatia nguvu za kupambana na mikazo hiyo.—Flp. 4:13.

13. (a) Msichana mmoja ametiwa nguvu jinsi gani ili kupambana na hali ngumu? (b) Je, unajua watu wengine walio katika hali kama hiyo?

13 Fikiria mfano wa Stephanie, painia wa kawaida mwenye umri wa miaka 19. Akiwa na umri wa miaka 12, alipatwa na ugonjwa wa kupooza au kiharusi, na ikagunduliwa kwamba alikuwa na uvimbe kwenye ubongo. Tangu wakati huo, amefanyiwa upasuaji mara mbili, akatibiwa kwa kutumia miali, na akapooza tena mara mbili. Wakati huu mwili wake ulidhoofika sana upande wa kushoto na hangeweza kuona vizuri. Stephanie anatumia nguvu zake kwa ajili tu ya mambo ambayo anaona kuwa ya maana zaidi, kama vile mikutano ya Kikristo na utumishi wa shambani. Hata hivyo, anaona jinsi roho ya Yehova inavyomsaidia kuvumilia katika njia nyingi. Vichapo vinavyotegemea Biblia ambavyo vina masimulizi ya Wakristo wenzetu vinamtia nguvu anaposhuka moyo. Ndugu na dada wamemtegemeza kwa kumtumia barua au kwa kuzungumza naye maneno yanayotia moyo kabla na baada ya mikutano. Watu wanaopendezwa pia wameonyesha kwamba wanathamini yale ambayo Stephanie anawafundisha kwa kwenda nyumbani kwake ili awafundishe Biblia. Stephanie anamshukuru sana Yehova kwa ajili ya mambo yote hayo. Andiko analopenda sana ni Zaburi 41:3, ambalo anaamini kwamba limetimia kwake.

14. Ni nini tunachopaswa kuepuka tunapovunjika moyo, na kwa nini?

14 Tunapochoka au tunapokuwa chini ya mikazo fulani, hatupaswi kamwe kufikiri kwamba njia ya kushughulika na mikazo ni kupunguza utendaji wa kiroho. Ni jambo baya sana kufanya hivyo. Kwa nini? Kwa sababu tunapokea roho takatifu inayotutia nguvu mpya tunaposhiriki katika utendaji wa kiroho kama vile funzo la kibinafsi, funzo la Biblia la familia, utumishi wa shambani, na kuhudhuria mikutano. Sikuzote utendaji wa Kikristo unaburudisha. (Soma Mathayo 11:28, 29.) Ni mara ngapi ndugu na dada wanafika kwenye mikutano wakiwa wamechoka, lakini wakati wa kurudi nyumbani, wanahisi wametiwa nguvu mpya, ni kana kwamba betri zao za kiroho zimetiwa nguvu tena.

15. (a) Je, Yehova anaahidi kwamba atafanya maisha ya Mkristo yawe rahisi? Eleza kulingana na Maandiko. (b) Mungu anatuahidi nini, na hilo linatokeza swali au ulizo gani?

15 Bila shaka, hilo halimaanishi kwamba mzigo wa kuwa mwanafunzi Mkristo ni mwepesi. Jitihada zinahitajiwa ili kuwa Mkristo mwaminifu. (Mt. 16:24-26; Luka 13:24) Hata hivyo, kupitia roho takatifu, Yehova anaweza kumpa nguvu yule ambaye amechoka. Nabii Isaya aliandika hivi: “Wale wanaomtumaini Yehova watapata nguvu mpya. Wataruka juu kwa mabawa kama tai. Watakimbia wala hawatazimia; watatembea wala hawatachoka.” (Isa. 40:29-31) Kwa hiyo, tunapaswa kujiuliza, Kwa kweli ni nini kinachomfanya mtu achoke kiroho?

16. Ni nini tunachoweza kufanya ili kuondoa mambo yanayoweza kutufanya tuchoke au kuvunjika moyo?

16 Neno la Yehova linatuhimiza ‘tuhakikishe mambo yaliyo ya maana zaidi.’ (Flp. 1:10) Akilinganisha maisha ya Kikristo na mashindano marefu ya mbio za miguu, chini ya mwongozo wa roho ya Mungu mtume Paulo alipendekeza hivi: “Acheni sisi pia tuondoe kila uzito . . . , na acheni tukimbie kwa uvumilivu shindano la mbio lililowekwa mbele yetu.” (Ebr. 12:1) Wazo lake lilikuwa kwamba ni lazima tuepuke kufuatilia mambo yasiyo ya maana, mizigo mizito isiyo ya lazima, ambayo itatuchosha. Huenda wengine wetu wanajaribu tu kutimiza mambo mengi sana ingawa tayari maisha yao yana shughuli nyingi. Hivyo, ikiwa kwa kawaida unahisi kwamba umechoka na una mikazo, unaweza kufaidika kwa kuchunguza unatumia muda gani katika kazi yako ya kimwili, unasafiri mara ngapi ili kujifurahisha, na unafuatilia sana michezo au vitumbuizo vingine kwa kadiri gani. Sifa za usawaziko na kiasi zinapaswa kutuchochea sisi sote kutambua udhaifu wetu na kupunguza mambo yasiyo ya maana.

17. Kwa nini huenda wengine wakavunjika moyo, lakini Yehova ametuhakikishia nini kuhusu hilo?

17 Pia, huenda ikawa kwamba wengine wetu tunavunjika moyo kwa kiasi fulani kwa sababu mwisho wa mfumo huu wa mambo haujafika haraka kama tulivyotazamia. (Met. 13:12) Hata hivyo, yeyote anayehisi hivyo, anaweza kutiwa moyo na maneno ya Habakuki 2:3: “Maono hayo bado ni ya wakati uliowekwa, nayo yanafanya haraka kuelekea mwisho, wala hayatasema uwongo. Hata yakikawia, endelea kuyatarajia; kwa maana bila shaka yatatimia. Hayatachelewa.” Yehova ametuhakikishia kwamba mwisho wa mfumo huu wa mambo utakuja kwa wakati kamili uliowekwa!

18. (a) Ni ahadi gani ambazo zinakutia nguvu? (b) Habari inayofuata itatufaidi jinsi gani?

18 Bila shaka, watumishi wote waaminifu wa Yehova wanatamani sana kuona siku ambayo watu hawatachoka wala kuvunjika moyo tena, wakati ambapo watu wote walio hai watafurahia “nguvu za ujana.” (Ayu. 33:25) Hata sasa tunaweza kufanywa kuwa na uwezo ndani yetu kupitia utendaji wa roho takatifu tunaposhiriki katika utendaji wa kiroho unaotutia nguvu mpya. (2 Kor. 4:16; Efe. 3:16) Usiruhusu hali ya kuchoka ikuzuie kupata baraka za milele. Kila jaribu, iwe linasababishwa na kishawishi, hali ya kuchoka, au kuvunjika moyo, litapita, hata ikiwa si sasa, basi litapitilia mbali katika ulimwengu mpya wa Mungu. Katika habari inayofuata, tutachunguza jinsi roho takatifu inavyowatia nguvu Wakristo wavumilie mateso, washinde msongo hatari wa marafiki, na kuvumilia majaribu mengine mbalimbali.

Ungesema Nini?

• Usomaji wa Biblia unatutia nguvu jinsi gani?

• Sala na kutafakari kunatutia nguvu jinsi gani?

• Unaweza kufanya nini ili kuondoa mambo yanayoweza kukufanya uvunjike moyo?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 24]

Mikutano ya Kikristo inaweza kututia nguvu kiroho