Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Je, Kweli Unathamini Baraka Zako?

Je, Kweli Unathamini Baraka Zako?

Je, Kweli Unathamini Baraka Zako?

BAADA ya kukombolewa kimuujiza kutoka utumwani huko Misri, mwanzoni wana wa Israeli walifurahia kuwa huru kumwabudu Yehova. (Kut. 14:29–15:1, 20, 21) Hata hivyo, baada ya muda mfupi maoni yao yalibadilika. Walianza kulalamika kuhusu hali yao ya maisha. Kwa nini? Kwa sababu waliacha kukazia fikira mambo ambayo Yehova alikuwa amewafanyia na badala yake wakakazia fikira matatizo ya kukaa katika jangwa au nyika. Walimwambia Musa hivi: “Kwa nini mmetutoa Misri ili tufe nyikani? Kwa maana hakuna mkate wala maji, nayo nafsi yetu imeuchukia huu mkate [mana] wa kudharaulika.”—Hes. 21:5.

Karne nyingi baadaye, Mfalme Daudi wa taifa la kale la Israeli aliimba hivi: “Nami nimezitegemea fadhili zako zenye upendo; moyo wangu na ushangilie katika wokovu wako. Nitamwimbia Yehova, kwa maana amenitendea kwa njia ya kunipa thawabu.” (Zab. 13:5, 6) Daudi hakusahau matendo ya fadhili zenye upendo ambayo Yehova alimtendea. Badala ya kusahau matendo hayo, alitafakari kwa ukawaida kuyahusu. (Zab. 103:2) Yehova ametutendea kwa fadhili sisi pia, na ni jambo la hekima kwetu kutopuuza mambo ambayo ametutendea. Acheni sasa tuchunguze baraka fulani kutoka kwa Mungu ambazo tunafurahia leo.

“Urafiki wa Karibu Pamoja na Yehova”

Mtunga-zaburi aliimba hivi: “Urafiki wa karibu pamoja na Yehova ni wa wale wanaomwogopa.” (Zab. 25:14) Ni pendeleo kama nini kwa wanadamu wasio wakamilifu kuwa na uhusiano wa kibinafsi na wa karibu pamoja na Yehova! Hata hivyo, namna gani ikiwa tunajishughulisha sana na mambo ya kila siku ya maisha hivi kwamba tunatumia muda mfupi sana kusali? Hebu fikiria jinsi itakavyokuwa kwa uhusiano wetu mzuri pamoja na Yehova. Akiwa Rafiki yetu, Yehova anatazamia tumtegemee na kumfunulia mambo yaliyo moyoni mwetu kupitia sala, tukimweleza wasiwasi wetu, mambo tunayotamani, na mahangaiko yetu. (Met. 3:5, 6; Flp. 4:6, 7) Basi je, si ni vizuri kufikiri kuhusu uzito wa mambo tunayosema katika sala zetu?

Kijana mmoja Shahidi anayeitwa Paul alipotafakari kuhusu sala zake, alitambua kwamba alihitaji kufanya maendeleo fulani. * Alisema, “Nilikuwa na zoea la kurudia maneno yaleyale niliposali kwa Yehova.” Paul alipofanya utafiti kuhusu sala katika Fahirisi, alijifunza kwamba kuna sala 180 hivi zilizoandikwa katika Biblia. Katika sala hizo, watumishi wa zamani wa Yehova walieleza mambo waliyohisi moyoni. Paul alisema hivi: “Kwa kutafakari kuhusu mifano hiyo iliyo katika Maandiko, nilijifunza kusema mambo waziwazi katika sala zangu. Jambo hilo limenisaidia kumfunulia Yehova mambo yaliyo katika moyo wangu. Sasa ninafurahia kumkaribia katika sala.”

‘Chakula kwa Wakati Unaofaa’

Baraka nyingine ambayo Yehova ametupatia ni kweli nyingi za Kimaandiko. Tunapokula chakula kingi sana cha kiroho chenye kujenga, tuna sababu ya ‘kupiga vigelegele kwa shangwe kwa sababu ya hali nzuri ya moyo.’ (Isa. 65:13, 14) Hata hivyo, ni lazima tujilinde ili tusiruhusu uvutano usiofaa ufanye tupoteze shauku yetu kwa ajili ya kweli. Kwa mfano, kusikiliza habari za uwongo za waasi-imani kunaweza kuharibu kufikiri kwetu na kutuzuia tusione thamani ya ‘chakula kwa wakati unaofaa’ ambacho Yehova anaandaa kupitia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.”—Mt. 24:45-47.

André, ambaye alikuwa amemtumikia Yehova kwa miaka mingi, aliumia sana moyoni alipodanganywa na mawazo ya waasi-imani. Alifikiri kwamba kutazama kwa muda mfupi tu kituo cha Intaneti cha waasi-imani hakungekuwa hatari. Anakumbuka hivi: “Mwanzoni, nilivutiwa na zile zilizoitwa eti kweli ambazo waasi-imani walizungumzia. Kadiri nilivyozidi kuchunguza mambo waliyosema, ndivyo nilivyofikiri kwamba nilikuwa na sababu nzuri ya kutoka katika tengenezo la Yehova. Lakini baadaye, nilipofanya utafiti kuhusu madai ambayo waasi-imani wanatoa ili kupinga Mashahidi wa Yehova, niligundua jinsi walimu hao wa uwongo walivyo wajanja. Walitumia habari iliyopotoshwa wakidai kwamba ni ‘ushahidi wenye nguvu’ wa kutupinga. Hivyo, niliamua kuanza kusoma vichapo vyetu tena na kuhudhuria mikutano. Baada ya muda nilitambua kwamba nilikuwa nimekosa mambo mengi sana.” Inafurahisha kwamba André alirudi katika kutaniko.

“Ushirika Mzima wa Akina Ndugu”

Undugu wetu wenye umoja na upendo ni baraka kutoka kwa Yehova. (Zab. 133:1) Mtume Petro alikuwa na sababu nzuri ya kuandika hivi: “Upendeni ushirika mzima wa akina ndugu.” (1 Pet. 2:17) Tukiwa sehemu ya undugu wa Kikristo, tunafurahia kutegemezwa kwa uchangamfu na wale ambao ni baba, mama, ndugu, na dada zetu wa kiroho katika kweli.—Marko 10:29, 30.

Hata hivyo, nyakati nyingine hali mbalimbali zinaweza kusababisha mkazo katika uhusiano wetu pamoja na ndugu na dada zetu. Kwa mfano, ni rahisi kukasirika kwa sababu ya udhaifu wa mtu fulani na kuwa na mtazamo wa kumchambua mtu huyo. Ikiwa jambo hilo litatokea, ni vizuri kukumbuka kwamba Yehova anawapenda watumishi wake hata ingawa wana udhaifu. Zaidi ya hayo, “kama tukisema: ‘Sisi hatuna dhambi yoyote,’ tunajipotosha wenyewe na kweli haimo ndani yetu.” (1 Yoh. 1:8) Je, si tunapaswa kujitahidi ‘kuendelea kuvumiliana na kusameheana kwa hiari’?—Kol. 3:13.

Msichana mmoja anayeitwa Ann alijifunza kupitia hali ngumu kwamba ushirika wa Kikristo ni wenye thamani. Akitenda kama yule mwana mpotevu katika mfano wa Yesu, msichana huyo alitoka polepole katika kutaniko la Kikristo. Baadaye, alirudiwa tena na fahamu na akarudi katika kweli. (Luka 15:11-24) Ann alijifunza nini kutokana na hali hiyo? Anasema hivi: “Kwa kuwa sasa nimerudi katika tengenezo la Yehova, ninawathamini ndugu na dada zangu wote hata ingawa wana udhaifu. Zamani, nilikimbilia kuwachambua-chambua. Lakini sasa nimeazimia kutoruhusu kitu chochote kinifanye nikose baraka ambazo ninapata nikiwa kati ya waamini wenzangu. Hakuna kitu chochote katika ulimwengu ambacho kinapaswa kutufanya tutoke katika paradiso yetu ya kiroho.”

Uwe Mwenye Shukrani Sikuzote kwa Ajili ya Baraka Zako

Tumaini letu katika Ufalme wa Mungu ambao ni suluhisho la matatizo yote ya wanadamu ni hazina yenye thamani kuliko kitu kingine chochote. Mwanzoni, tulipopata tumaini hilo, mioyo yetu ilijaa uthamini mwingi kama nini! Tulihisi tu kama yule mwanabiashara katika mfano wa Yesu ambaye ‘aliuza vitu vyote alivyokuwa navyo’ ili anunue “lulu moja ya thamani kubwa.” (Mt. 13:45, 46) Yesu hakusema kwamba baadaye mwanabiashara huyo hakuthamini lulu hiyo. Vivyo hivyo, acheni tusipoteze kamwe uthamini wetu kwa tumaini letu zuri ajabu.—1 The. 5:8; Ebr. 6:19.

Fikiria mfano wa Jean, ambaye amekuwa akimtumikia Yehova kwa miaka zaidi ya 60. Dada huyo anasema hivi: “Jambo ambalo limenisaidia kukazia akili Ufalme wa Mungu ni kuzungumza na wengine kuhusu Ufalme huo. Ninapoona macho yao yaking’aa wanapoelewa Ufalme huo ni nini, ninatiwa moyo sana. Ninapoona kweli ya Ufalme ikiboresha maisha ya mwanafunzi wa Biblia ninajiambia hivi: ‘Nina kweli nzuri kama nini za kuwaambia wengine!’”

Tuna sababu nzuri za kuwa wenye shukrani kwa kuwa tuna baraka nyingi za kiroho. Ingawa tunaweza kupata majaribu kama vile upinzani, ugonjwa, uzee, kushuka moyo, kufiwa, na matatizo ya kiuchumi, tunajua kwamba majaribu hayo ni ya muda. Chini ya Ufalme wa Mungu, tutapata baraka za kimwili kuongezea baraka zetu za kiroho. Mateso yoyote ambayo tunavumilia sasa yatakomeshwa kabisa katika mfumo mpya wa mambo.—Ufu. 21:4.

Kwa sasa, acheni tutafakari kuhusu baraka zetu za kiroho na kuonyesha uthamini kama wa mtunga-zaburi ambaye aliimba hivi: “Wewe mwenyewe umefanya mambo mengi, Ee Yehova Mungu wangu, naam, kazi zako za ajabu na mawazo yako kutuelekea; hakuna wa kulinganishwa nawe. Ikiwa ningetaka kueleza na kusema juu yake, zimekuwa nyingi sana kuliko vile ninavyoweza kusimulia.”—Zab. 40:5.

[Maelezo ya Chini]

^ Majina yamebadilishwa.

[Picha katika ukurasa wa 18]

Tumebarikiwa kwa kuwa tunategemezwa kiroho wakati wa majaribu