Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Kujitahidi Kunaleta Faida!

Kujitahidi Kunaleta Faida!

Kujitahidi Kunaleta Faida!

IBADA YA FAMILIA na funzo la Biblia ni mambo ya maana ili kuwalea watoto “katika nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova.” (Efe. 6:4) Hata hivyo, ikiwa wewe ni mzazi, unajua kwamba watoto wanaweza kuchoshwa haraka na mambo. Unaweza kufanya nini ili waendelee kukaza fikira? Chunguza mambo ambayo wazazi fulani wamefanya.

George anayeishi California, Marekani, anasema hivi: “Watoto walipokuwa na umri mdogo zaidi, mimi na mke wangu tulijitahidi kufanya funzo la Biblia la familia lifurahishe sikuzote. Nyakati nyingine sote tulivaa kama watu wanaotajwa katika Biblia na kuiga simulizi tulilokuwa tukisoma katika Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia. Hata tulitengeneza vifaa vya kufanya michezo hiyo kama vile, mapanga, fimbo za watawala, vikapu, na vitu vingine. Pia, tulicheza michezo ya Biblia ya kitendawili tuliyoiita ‘mimi ni nani’ na tukatengeneza mchezo wa ubao wenye maswali magumu ya Biblia na pia maswali rahisi. Tulikuwa pia na miradi, kama vile, kujenga mfano wa safina ya Noa au kuandika mfuatano wa matukio ya Biblia. Nyakati nyingine tulikuwa na vipindi vya kuchora ambapo tulichora watu wanaotajwa katika Biblia au picha za hadithi za Biblia. Kwa sasa, tuna mradi wa kuchora silaha za kiroho zinazotajwa katika Waefeso 6:11-17, na kila mmoja wetu amepewa mgawo wa kueleza kile kinachofananishwa na silaha fulani. Njia hizo zimetusaidia kufurahia funzo letu la familia.”

Debi, mama anayeishi huko Michigan, Marekani, anasema hivi: “Halikuwa jambo rahisi kwa mimi na mume wangu kumfanya binti yetu apendezwe na funzo alipokuwa na umri wa miaka mitatu hivi. Kisha, siku moja nilipokuwa nikimsomea kwa sauti hadithi kuhusu Isaka na Rebeka katika Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia, nilichukua sanamu mbili za kuchezea za watoto (wanasesere) na kuanza kuzitumia kusimulia hadithi hiyo. Sasa alisikiliza kila neno kwa makini! Katika miezi miwili iliyofuata, tulitumia sanamu hizo mbili kuigiza watu wengi mbalimbali wanaotajwa katika Biblia. Baada ya kusoma simulizi fulani, binti yetu alitafuta vitu vya kuchezea au vitu vingine katika nyumba ambavyo tungetumia kufanya mchezo kuhusu hadithi hiyo. Ni kana kwamba alikuwa akitafuta hazina! Tulitumia sanduku la kubebea viatu na uzi mwekundu kufananisha nyumba ya Rahabu yenye kamba nyekundu. Nyoka bandia wa kuchezea mwenye urefu wa mita 1.5 aliyezungushwa kwenye mti wa ufagio alifananisha yule nyoka wa shaba anayetajwa katika Hesabu 21:4-9. Tuliweka vitu hivyo vya kuchezea ndani ya mfuko mkubwa. Tulifurahi kumwona binti yetu akiwa ameketi sebuleni akipekua-pekua ‘mfuko wake wa hadithi za Biblia.’ Ni shangwe kama nini kumwona akiigiza hadithi hizo katika njia yake mwenyewe ya pekee!”

Kulea watoto si jambo rahisi, muda zaidi unahitajiwa mbali na vipindi vya kila juma, ili kukuza ndani yao tamaa ya kumtumikia Yehova. Lakini mnaweza kutumia ibada ya familia na funzo la Biblia kama msingi wa kufundisha mambo mengine ya kiroho. Bila shaka, kujitahidi kunaleta faida!