Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Kwa nini Musa aliwakasirikia Eleazari na Ithamari, wana wa Haruni, baada ya vifo vya ndugu zao Nadabu na Abihu, na hasira yake ilitulizwa jinsi gani?—Law. 10:16-20.

Muda mfupi baada ya kuanzishwa kwa ukuhani kwa ajili ya utumishi wa maskani, Yehova aliwaangamiza Nadabu na Abihu, wana wa Haruni kwa sababu walikuwa wamemtolea Yehova moto haramu. (Law. 10:1, 2) Musa aliagiza wana waliobaki wa Haruni wasiwaombolezee ndugu zao waliokufa. Muda si muda, Musa aliwakasirikia Eleazari na Ithamari kwa sababu hawakuwa wamemla mbuzi wa toleo la dhambi. (Law. 9:3) Kwa nini Musa alitenda hivyo?

Sheria ambazo Yehova alikuwa amempa Musa zilisema waziwazi kwamba kuhani ambaye alitoa toleo la dhambi alipaswa kula sehemu ya toleo hilo katika ua wa hema la mkutano. Kufanya hivyo kulionwa kuwa kulipia dhambi za wale waliotoa dhabihu hiyo. Hata hivyo, ikiwa sehemu ya damu ya dhabihu hiyo ilipelekwa ndani ya Mahali Patakatifu, katika chumba cha kwanza cha patakatifu, toleo hilo halikupaswa kuliwa. Badala yake, lilipaswa kuteketezwa kwa moto.—Law. 6:24-26, 30.

Inaonekana kwamba baada ya matukio hayo yaliyosababisha msiba siku hiyo, Musa aliona kulikuwa na uhitaji wa kuhakikisha kwamba amri zote za Yehova zilifuatwa. Alipogundua kwamba mbuzi wa toleo la dhambi alikuwa ameteketezwa, kwa hasira aliwauliza Eleazari na Ithamari kwa nini hawakumla mbuzi huyo kama walivyoagizwa, kwa sababu damu ya mbuzi huyo haikuwa imetolewa mbele za Yehova katika Mahali Patakatifu.—Law. 10:17, 18.

Haruni alijibu swali la Musa, kwa kuwa ni wazi kwamba makuhani waliobaki walitenda hivyo kwa sababu alikuwa amewaruhusu. Baada ya wanawe wawili kuuawa, huenda Haruni alikuwa na shaka ikiwa kuhani yeyote angeweza kula kwa dhamiri njema toleo la dhambi siku hiyo. Labda alihisi kwamba hawangempendeza Yehova kwa kula toleo hilo, hata ingawa si wao waliosababisha moja kwa moja kosa lililofanywa na Nadabu na Abihu.—Law. 10:19.

Huenda Haruni alifikiri hasa kwamba siku ambayo washiriki wa familia yake walitimiza kazi yao ya kikuhani kwa mara ya kwanza, walipaswa kuwa waangalifu sana ili wampendeze Mungu hata katika mambo madogo zaidi. Hata hivyo, Nadabu na Abihu walikuwa wamelitia unajisi jina la Yehova na hasira ya Mungu iliwaka juu yao. Kwa hiyo, huenda Haruni alifikiri kwamba washiriki wa familia ya kikuhani ambayo ilihusianishwa na dhambi hiyo hawakupaswa kula toleo takatifu.

Inaonekana kwamba Musa alikubali jibu la ndugu yake, kwa kuwa simulizi hilo linamalizia hivi: “Musa aliposikia hilo, ndipo hilo likawa jema machoni pake.” (Law. 10:20) Inaonekana kwamba Yehova alitosheka pia na jibu la Haruni.