Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Penda Uadilifu kwa Moyo Wako Wote

Penda Uadilifu kwa Moyo Wako Wote

Penda Uadilifu kwa Moyo Wako Wote

“Umependa uadilifu.”—ZAB. 45:7.

1. Ni nini kitakachotusaidia kufuata “mapito ya uadilifu”?

 KUPITIA Neno lake na roho yake takatifu, Yehova anawaongoza watu wake katika “mapito ya uadilifu” au haki. (Zab. 23:3) Hata hivyo, kwa kuwa sisi si wakamilifu tuna mwelekeo wa kukengeuka kutoka katika njia hiyo. Ili turudi na kufanya mambo yaliyo sawa tunahitaji kujitahidi kabisa. Ni nini kitakachotusaidia kufanikiwa? Kama Yesu, ni lazima tupende kufanya mambo yaliyo sawa.—Soma Zaburi 45:7.

2. “Mapito ya uadilifu” ni nini?

2 “Mapito ya uadilifu” ni nini? Mapito ni njia nyembamba ya miguu. “Mapito” hayo yanategemea viwango vya Yehova vya uadilifu. Katika Kiebrania na Kigiriki, neno “uadilifu” linamaanisha jambo la “unyoofu,” na neno hilo linaonyesha hali ya kushikamana kabisa na kanuni za maadili. Kwa kuwa Yehova ni “makao ya uadilifu,” waabudu wake wanafurahi kumtegemea ili awaonyeshe njia nyoofu ya maadili ambayo wanapaswa kufuata.—Yer. 50:7.

3. Tunaweza kujifunza jinsi gani mambo mengi kuhusu uadilifu wa Mungu?

3 Tutampendeza Mungu kikamili ikiwa tu tutajitahidi kwa moyo wetu wote kujipatanisha na viwango vyake vya uadilifu. (Kum. 32:4) Ili tufanye hivyo, tunaanza kwa kujifunza yote tunayoweza kumhusu Yehova Mungu katika Neno lake, Biblia. Kadiri tunavyojifunza mengi kumhusu yeye na kumkaribia zaidi kila siku, ndivyo tutakavyozidi kupenda uadilifu wake. (Yak. 4:8) Ni lazima pia tukubali mwongozo wa Neno la Mungu lililoongozwa na roho takatifu tunapohitaji kufanya maamuzi ya maana maishani.

Tafuta Uadilifu wa Mungu

4. Kutafuta uadilifu wa Mungu kunatia ndani nini?

4 Soma Mathayo 6:33. Kutafuta uadilifu wa Mungu kunatia ndani mengi zaidi ya kutumia wakati wetu katika kazi ya kuhubiri habari njema ya Ufalme. Ili utumishi wetu mtakatifu ukubaliwe na Yehova, ni lazima mwenendo wetu wa kila siku upatane na viwango vyake vya juu. Ni lazima watu wote wanaotafuta uadilifu wa Yehova wafanye nini? Ni lazima ‘wavae utu mpya ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli na ushikamanifu.’—Efe. 4:24.

5. Ni nini kitakachotusaidia kushinda hali ya kuvunjika moyo?

5 Tunapojitahidi kuishi kulingana na viwango vya Mungu vya uadilifu, huenda nyakati nyingine tukavunjika moyo kwa sababu ya makosa yetu. Ni nini kinachoweza kutusaidia kushinda hali ya kuvunjika moyo inayodhoofisha sana na kujifunza kupenda na kutenda mambo ya uadilifu? (Met. 24:10) Ni lazima tusali kwa Yehova kwa ukawaida “tukiwa na mioyo ya kweli katika uhakikisho kamili wa imani.” (Ebr. 10:19-22) Iwe sisi ni Wakristo watiwa-mafuta au tuna tumaini la kuishi duniani, tunaonyesha imani katika dhabihu ya ukombozi au fidia ya Yesu Kristo na katika utumishi wake akiwa Kuhani wetu Mkuu sana. (Rom. 5:8; Ebr. 4:14-16) Gazeti la kwanza kabisa la Mnara wa Mlinzi lilitoa mfano ambao unaonyesha uwezo wa damu ya Yesu iliyomwagwa. (1 Yoh. 1:6, 7) Gazeti hilo lilisema hivi: “Ni jambo la hakika kabisa kwamba [wakati] kitu chekundu kabisa [kinapotazamwa] kupitia kioo chekundu katika mwangaza, kitu hicho kinaonekana kuwa cheupe; kwa hiyo, hata dhambi zetu zikiwa nyekundu sana, tunapokuja mahali ambapo Mungu anaweza kuziona kupitia damu ya Kristo, zinaonekana kuwa nyeupe.” (Julai [Mwezi wa 7] 1879, uku. 6) Yehova ametuandalia mpango mzuri ajabu kama nini kupitia dhabihu ya ukombozi ya Mwana wake mpendwa!—Isa. 1:18.

Chunguza Silaha Zako za Kiroho

6. Kwa nini ni jambo la maana kwetu kuchunguza silaha zetu za kiroho?

6 Nyakati zote, tunahitaji kuvaa “bamba la kifuani la uadilifu,” kwa sababu ni sehemu ya maana ya silaha za kiroho kutoka kwa Mungu. (Efe. 6:11, 14) Iwe tumejiweka wakfu kwa Yehova hivi karibuni au tumekuwa tukishiriki katika utumishi mtakatifu kwa makumi ya miaka, ni jambo la maana sana kwetu kuchunguza silaha zetu za kiroho kila siku. Kwa nini? Kwa sababu Ibilisi na roho wake waovu wametupwa chini katika ujirani wa dunia. (Ufu. 12:7-12) Shetani ana hasira, naye anajua kwamba ana wakati mfupi. Hivyo, amezidisha mashambulizi yake kuelekea watu wa Mungu. Je, tunathamini umuhimu wa kuvaa “bamba la kifuani la uadilifu”?

7. Tutajiendesha jinsi gani tukitambua kwamba tunahitaji “bamba la kifuani la uadilifu”?

7 Bamba la kifuani linalinda moyo halisi. Kwa sababu ya hali yetu ya kutokamilika, moyo wetu wa mfano ni hatari na una mwelekeo wa kuwa wenye hila au udanganyifu. (Yer. 17:9) Kwa kuwa moyo wetu una mwelekeo wa kufanya mambo yasiyofaa, ni jambo la maana sana kwetu tuuzoeze na kuutia nidhamu. (Mwa. 8:21) Tukitambua kwamba tunahitaji “bamba la kifuani la uadilifu,” hatutavua bamba hilo kwa muda kwa kuchagua kuburudishwa na mambo ambayo Mungu anachukia; wala hatutajiruhusu tutafakari kuhusu kutenda mambo yasiyofaa. Hatutapoteza wakati mwingi sana wenye thamani tukitazama televisheni. Badala yake, tutaendelea kujitahidi kufanya mambo yanayompendeza Yehova. Hata tukijikwaa kwa muda baada ya kushawishiwa na mawazo ya kimwili yasiyo ya uadilifu, tutasimama tena kwa msaada wa Yehova.—Soma Methali 24:16.

8. Kwa nini tunahitaji “ngao kubwa ya imani”?

8 “Ngao kubwa ya imani” ni kati ya silaha zetu za kiroho. Inatuwezesha “kuizima mishale yote inayowaka moto ya yule mwovu.” (Efe. 6:16) Kisha, kuwa na imani na kumpenda Yehova kwa moyo wetu wote kunatusaidia kutenda mambo ya uadilifu na kubaki katika barabara inayoongoza kwenye uzima wa milele. Kadiri tunavyojifunza kumpenda Yehova, ndivyo tutakavyothamini zaidi uadilifu wake. Lakini namna gani kuhusu dhamiri yetu? Inatusaidia jinsi gani tunapojitahidi kuupenda uadilifu?

Dumisha Dhamiri Njema

9. Tunafaidika jinsi gani kwa kudumisha dhamiri njema?

9 Wakati tulipobatizwa, tulitoa ombi kwa Yehova la kupata “dhamiri njema.” (1 Pet. 3:21) Kwa sababu tuna imani katika dhabihu ya ukombozi, damu ya Yesu inafunika dhambi zetu na hivyo tunakuwa na msimamo safi mbele za Mungu. Hata hivyo, ili tuendelee kuwa na msimamo huo safi, tunahitaji kudumisha dhamiri njema. Ikiwa nyakati nyingine dhamiri yetu inatushtaki na kutoa maonyo, tunapaswa kushukuru kwamba inafanya kazi vizuri. Maonyo hayo yanaonyesha kwamba dhamiri yetu haijakufa ganzi kuhusiana na njia za Yehova za uadilifu. (1 Tim. 4:2) Lakini dhamiri inaweza kutimiza daraka la ziada kwa ajili ya wale wanaotaka kupenda uadilifu.

10, 11. (a) Simulia jambo ambalo linaonyesha kwa nini tunapaswa kuisikiliza dhamiri yetu iliyozoezwa na Biblia. (b) Kwa nini tunaweza kupata furaha kubwa tukipenda uadilifu?

10 Tunapofanya makosa, dhamiri yetu inaweza kutuhukumu au kutusumbua. Kijana mmoja aliacha kufuata “mapito ya uadilifu.” Akawa na zoea la kutazama ponografia (picha au habari za ngono) na kisha akaanza kuvuta bangi. Alijihisi akiwa na hatia alipoenda katika mikutano na alijiona kuwa mnafiki aliposhiriki katika utumishi wa shambani, kwa hiyo, aliacha kushiriki katika utendaji huo wa Kikristo. Alisema hivi: “Lakini, sikujua kamwe kwamba dhamiri yangu ingenisumbua kwa sababu ya matendo yangu.” Akaongezea hivi: “Niliendelea kuishi maisha hayo ya upumbavu kwa miaka minne hivi.” Kisha akaanza kufikiria kurudi katika kweli. Ingawa alifikiri kwamba Yehova hangesikiliza sala yake, alisali tu na kuomba msamaha. Kabla ya dakika kumi kupita, mama yake alimtembelea na kumtia moyo aanze tena kuhudhuria mikutano. Alienda katika Jumba la Ufalme na kumwomba mzee mmoja ajifunze pamoja naye. Baada ya muda, alibatizwa, na sasa anamshukuru Yehova kwa sababu aliokoa uhai wake.

11 Je, hatujaona kwamba tunapata furaha kubwa tunapofanya mambo yaliyo sawa? Kadiri tunavyojifunza kupenda uadilifu na kutenda matendo ya uadilifu kwa ukamili zaidi, ndivyo tunavyopata shangwe zaidi tunapofanya mambo yanayompendeza Baba yetu wa mbinguni. Hebu fikiria jambo hili! Siku inakuja wakati ambapo wanadamu wote watakuwa na dhamiri ambayo inawaletea furaha tu; wataiga sifa za Mungu kwa ukamilifu. Kwa hiyo, acheni tusitawishe sasa ndani kabisa ya mioyo yetu sifa ya kupenda uadilifu na hivyo kumfanya Yehova ashangilie.—Met. 23:15, 16.

12, 13. Tunaweza kuzoeza dhamiri yetu namna gani?

12 Tunaweza kuizoeza namna gani dhamiri yetu? Tunapojifunza Maandiko na vichapo vyetu vinavyotegemea Biblia, ni jambo la maana kukumbuka kwamba “moyo wa mwadilifu hutafakari ili kujibu.” (Met. 15:28) Fikiria jinsi jambo hilo linavyotusaidia tunapokuwa na maswali au maulizo kuhusu kazi ya kuajiriwa, yaani, kazi ya mshahara. Ikiwa kazi fulani inapingana moja kwa moja na matakwa ya Kimaandiko, wengi wetu tunafuata haraka mwongozo ambao umetolewa kupitia jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara. Hata hivyo, ikiwa hakuna jibu la wazi kwa swali fulani kuhusu kazi, tunapaswa kusali na kufikiria kanuni za Biblia. * Tunapaswa kufikiria kanuni kama ile ya kuepuka kuumiza dhamiri za wengine. (1 Kor. 10:31-33) Tunapaswa kufikiria hasa kanuni zinazohusu uhusiano wetu pamoja na Mungu. Ikiwa tunamwona Yehova kuwa halisi, tutajiuliza hivi kwanza: ‘Je, nikifanya kazi hii nitamhuzunisha Yehova na kumtia uchungu?’—Zab. 78:40, 41.

13 Tunapotayarisha Funzo la Mnara wa Mlinzi au Funzo la Biblia la Kutaniko, tunapaswa kukumbuka kwamba tunahitaji kutafakari kuhusu habari hiyo. Je, sikuzote tunajikuta tukipiga mistari haraka-haraka jibu la swali katika funzo na kuendelea na fungu linalofuata? Inaelekea kwamba kujifunza kwa njia hiyo hakuwezi kuongeza upendo wetu kwa ajili ya uadilifu au kutusaidia kusitawisha dhamiri inayotoa maonyo haraka. Ili tupende uadilifu, tunahitaji kujifunza kwa bidii na kutafakari kuhusu mambo tunayosoma katika Neno la Mungu lililoandikwa. Hakuna njia fupi au za mkato inapohusu kujifunza kupenda uadilifu kwa moyo wetu wote!

Njaa na Kiu kwa Ajili ya Uadilifu

14. Yehova Mungu na Yesu Kristo wanataka tuhisi jinsi gani kuhusu utumishi wetu mtakatifu?

14 Yehova Mungu na Yesu Kristo wanataka tuwe na furaha tunapofanya utumishi wetu mtakatifu. Ni nini kitakachochangia furaha yetu? Ni kupenda uadilifu! Katika Mahubiri ya Mlimani, Yesu alisema hivi: “Wenye furaha ni wale walio na njaa na walio na kiu kwa ajili ya uadilifu, kwa kuwa watashibishwa.” (Mt. 5:6) Maneno hayo yana maana gani kwa wale ambao wanatamani kupenda uadilifu?

15, 16. Kiu na njaa ya kiroho inaweza kutoshelezwa kwa njia gani?

15 Ulimwengu ambamo tunaishi unatawaliwa na yule mwovu. (1 Yoh. 5:19) Tunaposoma gazeti kutoka katika nchi yoyote, tunapata habari kuhusu ukatili na jeuri ambayo haijawahi kamwe kutokea! Mtu mwadilifu anaumia sana moyoni anapoona unyama ambao mwanadamu anamtendea mwanadamu mwenzake. (Mhu. 8:9) Sisi ambao tunampenda Yehova, tunajua kwamba ni yeye peke yake anayeweza kutosheleza kiu na njaa ya kiroho ya watu ambao wanatamani kujifunza uadilifu. Watu wasiomwogopa Mungu wataondolewa hivi karibuni, na wale wanaopenda uadilifu hawatateseka tena kwa sababu ya watu wanaokaidi au kuvunja sheria na kwa sababu ya matendo yao maovu. (2 Pet. 2:7, 8) Watapata kitulizo kikubwa kama nini!

16 Tukiwa watumishi wa Yehova na wafuasi wa Yesu Kristo, tunatambua kwamba wote walio na kiu na njaa kwa ajili ya uadilifu “watashibishwa.” Watatoshelezwa kabisa kupitia mpango wa Mungu wa kuleta mbingu mpya na dunia mpya ambamo “uadilifu utakaa.” (2 Pet. 3:13) Basi, acheni tusivunjike moyo au kushangazwa kwamba uonevu na jeuri imetwaa au kuondoa kabisa uadilifu katika ulimwengu huu wa kishetani. (Mhu. 5:8) Yehova, Aliye Juu Zaidi, anajua mambo yanayotukia na hivi karibuni atawakomboa wale wanaopenda uadilifu.

Faidika kwa Kupenda Uadilifu

17. Taja faida fulani ambazo tunapata kwa sababu ya kupenda uadilifu.

17 Zaburi ya 146:8 inakazia faida kubwa ya kufuata mapito ya uadilifu. Mtunga-zaburi aliimba hivi: “Yehova anawapenda waadilifu.” Hebu wazia! Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu wote mzima anatupenda kwa sababu tunapenda uadilifu! Kwa sababu ya upendo wa Yehova, tuna hakika kwamba atatosheleza mahitaji yetu tunapotanguliza mambo ya Ufalme katika maisha yetu. (Soma Zaburi 37:25; Methali 10:3.) Mwishowe, wale wanaopenda uadilifu ndio watakaofurahia dunia hii yote. (Met. 13:22) Idadi kubwa ya watu wa Mungu watathawabishwa kwa kupewa shangwe nyingi sana na uzima bila mwisho katika dunia maridadi itakayokuwa paradiso kwa sababu walitenda mambo ya uadilifu. Hata sasa, wale ambao wanapenda uadilifu wa Mungu wanapata thawabu ya kuwa na amani moyoni ambayo inachangia umoja katika familia zao na katika makutaniko yao.—Flp. 4:6, 7.

18. Ni mambo gani mazuri ambayo tunaweza kufanya tunapongojea siku ya Yehova?

18 Tunapongojea siku kuu ya Yehova ifike, ni lazima tuendelee kutafuta uadilifu wake. (Sef. 2:2, 3) Kwa hiyo, acheni tuonyeshe kwamba tunapenda kikweli njia za uadilifu za Yehova Mungu. Hilo linatia ndani kuvaa kikamili kabisa “bamba la kifuani la uadilifu” ili tuulinde moyo wetu wa mfano. Pia, tunahitaji kudumisha dhamiri njema, ambayo itatuletea furaha na kuufanya moyo wa Mungu wetu ushangilie.—Met. 27:11.

19. Tunapaswa kuazimia kufanya nini, na habari inayofuata itazungumzia nini?

19 ‘Macho ya Yehova yanaenda huku na huku duniani kote ili aonyeshe nguvu zake kwa ajili ya wale ambao moyo wao ni mkamilifu kumwelekea yeye.’ (2 Nya. 16:9) Maneno hayo yanatufariji kama nini tunapofanya mambo yaliyo sawa huku tukipambana na ukosefu wa usalama, jeuri, na uovu ambao unazidi kuongezeka katika ulimwengu huu wenye misukosuko! Ni kweli kwamba huenda matendo yetu ya uadilifu yakawashangaza wanadamu wengi ambao wametengwa mbali na Mungu. Lakini tunajifaidi wenyewe sana tunaposhikamana na uadilifu wa Yehova. (Isa. 48:17; 1 Pet. 4:4) Kwa hiyo basi, acheni tuazimie kwa moyo kamili kuendelea kupata shangwe kwa kupenda na kutenda mambo ya uadilifu kwa moyo wetu wote. Hata hivyo, kuwa na moyo kamili kunatia ndani pia kuchukia uasi-sheria. Habari inayofuata itatuonyesha hilo linamaanisha nini.

[Maelezo ya Chini]

^ Kwa maelezo zaidi juu ya kanuni za Biblia zinazohusu maswali ya kazi ya kuajiriwa, ona gazeti la Mnara wa Mlinzi la Aprili 15, 1999, ukurasa wa 28-30.

Ungesema Nini?

• Kwa nini tunahitaji kuthamini dhabihu ya ukombozi ili tuweze kupenda uadilifu?

• Kwa nini ni jambo la maana kwetu kuvaa “bamba la kifuani la uadilifu”?

• Tunaweza kuzoeza dhamiri yetu jinsi gani?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 26]

Dhamiri iliyozoezwa inatusaidia kutatua maswali kuhusu kazi ya kuajiriwa