Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Je, Unatambua Uthibitisho wa Mwongozo wa Mungu?

Je, Unatambua Uthibitisho wa Mwongozo wa Mungu?

Je, Unatambua Uthibitisho wa Mwongozo wa Mungu?

WAISRAELI na hata Wamisri hawakuwa wamewahi kuona kitu kama hicho. Waisraeli walipokuwa wakitoka Misri, nguzo ya wingu ilikuwa ikielea karibu nao na kukaa pamoja nao siku baada ya siku. Usiku, ilikuwa nguzo ya moto. Lilikuwa jambo la kustaajabisha kama nini! Lakini nguzo hiyo ilitoka wapi? Ilikuwa na kusudi gani? Na sisi tunaoishi miaka 3,500 baadaye, tunaweza kujifunza nini kutokana na jinsi Waisraeli walivyoiona ile “nguzo ya moto na wingu”?—Kut. 14:24.

Neno la Mungu linafunua chanzo na kusudi la nguzo hiyo linaposema hivi: “Yehova alikuwa akienda mbele yao wakati wa mchana katika nguzo ya wingu ili kuwaongoza njiani, na wakati wa usiku katika nguzo ya moto ili kuwapa nuru ya kwenda wakati wa mchana na wakati wa usiku.” (Kut. 13:21, 22) Yehova Mungu alitumia nguzo ya moto na wingu kuwaongoza watu wake kutoka Misri na kupitia nyikani. Walipaswa kuwa tayari kuondoka na kuifuata. Vikosi vya Misri vilivyokuwa vinawafuata vilipokuwa karibu kuwashambulia watu wa Mungu, nguzo ile ilisonga na kusimama katikati ya vikundi hivyo viwili, na kuwalinda Waisraeli. (Kut. 14:19, 20) Ingawa nguzo hiyo haikuwaongoza kufuata njia ya moja kwa moja, Waisraeli wangeweza tu kufika katika Nchi ya Ahadi kwa kuifuata nguzo hiyo.

Kuwepo kwa nguzo hiyo kuliwahakikishia watu wa Mungu kwamba Yehova alikuwa pamoja nao. Nguzo hiyo ilimwakilisha Yehova, na nyakati nyingine alizungumza kupitia nguzo hiyo. (Hes. 14:14; Zab. 99:7) Zaidi ya hayo, wingu hilo lilionyesha kwamba Musa ndiye aliyechaguliwa na Yehova kuliongoza taifa hilo. (Kut. 33:9) Vivyo hivyo, Biblia inaonyesha kwamba mara ya mwisho lilipotokea, wingu hilo lilionyesha kwamba Yehova alikuwa amemweka rasmi Yoshua kuwa kiongozi baada ya Musa. (Kum. 31:14, 15) Kwa kweli, ili Waisraeli wafanikiwe katika safari yao ya kutoka Misri, walipaswa kutambua uthibitisho wa mwongozo wa Mungu na kisha kuufuata.

Walipuuza Uthibitisho

Waisraeli walipoona nguzo hiyo kwa mara ya kwanza, bila shaka walistaajabu. Hata hivyo, inasikitisha kwamba muujiza huo ulioonekana waziwazi haukuwasaidia Waisraeli vya kutosha kuwa na uhakika wenye kudumu katika Yehova. Mara kwa mara walitilia shaka mwongozo wa Mungu. Jeshi la Misri lilipowafuata, hawakuonyesha imani katika nguvu za Yehova za kuokoa. Badala yake, walidai kwamba Musa, mtumishi wa Mungu, aliwaongoza ili wafe. (Kut. 14:10-12) Baada ya kukombolewa na kuvuka Bahari Nyekundu, walimnung’unikia Musa, Haruni, na Yehova kwa sababu walidai kwamba walikosa chakula na maji. (Kut. 15:22-24; 16:1-3; 17:1-3, 7) Na baada ya majuma machache, walimsukuma Haruni atengeneze ndama wa dhahabu. Hebu wazia! Katika sehemu moja ya kambi yao, Waisraeli waliona ile nguzo ya moto na wingu—uthibitisho wenye nguvu wa Yule ambaye alikuwa amewaongoza kutoka Misri—na karibu na mahali hapo, wakaanza kuabudu sanamu isiyo na uhai, wakisema: “Huyu ndiye Mungu wako, Ee Israeli, aliyekuongoza kutoka nchi ya Misri.” Yalikuwa “matendo makubwa ya kukosa heshima” kama nini!—Kut. 32:4; Neh. 9:18.

Matendo ya Waisraeli ya uasi yalionyesha wazi kwamba walipuuza mwongozo wa Yehova. Si kwamba walikuwa vipofu kihalisi, badala yake hawakuona mambo kwa njia ya kiroho. Waliiona ile nguzo, lakini walisahau maana ya nguzo hiyo. Ingawa matendo yao ‘yalimtia uchungu Mtakatifu wa Israeli,’ kwa rehema Yehova aliendelea kutoa mwongozo kupitia ile nguzo mpaka Waisraeli walipofika katika Nchi ya Ahadi.—Zab. 78:40-42, 52-54; Neh. 9:19.

Ona Uthibitisho wa Mwongozo wa Mungu Leo

Vivyo hivyo leo, Yehova hajawaacha kamwe watu wake bila mwongozo ulio wazi. Kama vile tu ambavyo hakutazamia Waisraeli wajitafutie njia yao wenyewe, sisi pia hatuambiwi tujitafutie wenyewe njia ya kuingia katika ulimwengu mpya ulioahidiwa. Yesu Kristo ndiye amepewa mgawo wa kuwa Kiongozi wa kutaniko. (Mt. 23:10; Efe. 5:23) Ameikabidhi kiasi fulani cha mamlaka jamii ya mtumwa mwaminifu, ambayo ni jamii ya Wakristo waaminifu waliotiwa mafuta kwa roho ya Mungu. Kisha jamii hiyo ya mtumwa, inaweka rasmi waangalizi katika kutaniko la Kikristo.—Mt. 24:45-47; Tito 1:5-9.

Tunaweza jinsi gani kuwa na uhakika kuhusu utambulisho wa jamii hiyo ya mtumwa mwaminifu au msimamizi-nyumba? Ona jinsi Yesu mwenyewe anavyoeleza kuhusu jamii hiyo: “Ni nani kwa kweli aliye msimamizi-nyumba mwaminifu, mwenye busara, ambaye bwana wake atamweka rasmi juu ya watumishi wake kuendelea kuwapa kipimo chao cha chakula katika wakati unaofaa? Mwenye furaha ni mtumwa huyo, ikiwa bwana wake anapofika anamkuta akifanya hivyo!”—Luka 12:42, 43.

Hivyo, jamii ya msimamizi-nyumba inatenda kwa ‘uaminifu,’ bila kumsaliti au kumwacha kamwe Yehova, Yesu, kweli za Biblia, au watu wa Mungu. Kwa kuwa wana “busara,” washiriki wa jamii ya msimamizi-nyumba wanafanya maamuzi kwa hekima wanapoongoza kazi ya maana zaidi ya kuhubiri “habari njema ya ufalme” na kufanya “wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.” (Mt. 24:14; 28:19, 20) “Katika wakati unaofaa,” jamii ya msimamizi-nyumba inagawa kwa utii chakula cha kiroho kinachofaa na chenye kujenga. Kibali cha Yehova kinaonekana kupitia jinsi anavyowabariki watu wake kwa ongezeko, kuwaongoza wanapofanya maamuzi ya maana, kuelewa vizuri zaidi kweli za Biblia, kuwalinda wasiangamizwe na maadui wao, na kuwapa amani ya akilini na moyoni.—Isa. 54:17; Flp. 4:7.

Fuata Mwongozo wa Mungu

Tunaweza kuonyesha jinsi gani kwamba tunathamini mwongozo wa Mungu? Mtume Paulo alisema hivi: “Watiini wale wanaoongoza katikati yenu na mnyenyekee.” (Ebr. 13:17) Huenda nyakati nyingine ikawa vigumu kufanya hivyo. Kwa mfano: Jiweke katika hali ya Mwisraeli aliyeishi katika siku za Musa. Wazia kwamba baada ya wewe kutembea kwa muda fulani, ile nguzo inasimama. Itasimama mahali hapo kwa muda gani? Siku moja? Juma moja? Miezi fulani? Unajiuliza, ‘Je, ninahitaji kufungua mizigo yangu yote?’ Kwanza, huenda ukafungua vitu ambavyo unahitaji zaidi. Hata hivyo, baada ya siku chache, ukiwa umechoka kutafuta-tafuta vitu ndani ya mizigo yako, unaanza kufungua kila kitu. Lakini mara tu unapokaribia kumaliza kufungua kila kitu, unaona nguzo ikiinuka—na hivyo unalazimika kufunga mizigo yako tena! Hilo halingekuwa jambo rahisi wala lenye kupendeza. Ingawa hivyo, bado Waisraeli walipaswa ‘kuondoka mara moja baada ya’ wingu kuinuka.—Hes. 9:17-22.

Hivyo basi, tunatenda jinsi gani tunapopata mwongozo kutoka kwa Mungu? Je tunajaribu kuufuata ‘mara moja baada ya’ kutolewa? Au je, tunaendelea kufanya mambo kama vile tu tulivyozoea kufanya? Je, tunaelewa mwongozo uliorekebishwa, kama vile kuhusu kuongoza mafunzo ya Biblia ya nyumbani, kuwahubiria watu wanaozungumza lugha ya kigeni, kushiriki katika ibada ya familia kwa ukawaida, kushirikiana na Halmashauri za Uhusiano na Hospitali, na kujiendesha vizuri tunapokuwa katika makusanyiko? Pia, tunaonyesha kwamba tunathamini mwongozo wa Mungu kwa kukubali mashauri. Tunapofanya maamuzi mazito, hatutegemei hekima yetu wenyewe badala yake tunatafuta mwongozo kutoka kwa Yehova na tengenezo lake. Na kama vile tu mtoto anavyotafuta ulinzi kutoka kwa mzazi wake kunapokuwa na dhoruba, tunatafuta ulinzi katika tengenezo la Yehova wakati matatizo ya ulimwengu huu yanayofanana na mvua ya mawe yanapotupata.

Bila shaka, wale wanaoongoza katika sehemu ya kidunia ya tengenezo la Mungu si wakamilifu—hata Musa hakuwa mkamilifu. Hata hivyo, sikuzote ile nguzo ilitoa uthibitisho wa kwamba alikuwa amewekwa rasmi na Mungu na alikuwa na kibali cha Mungu. Ona pia kwamba halikuwa daraka la kila Mwisraeli kujiamulia wakati wa kuondoka. Badala yake watu walifuata “agizo la Yehova kupitia Musa.” (Hes. 9:23) Hivyo, inaelekea kwamba Musa, ambaye alitumiwa na Mungu kutoa mwongozo, ndiye aliyetoa ishara ya kuondoka.

Leo, jamii ya msimamizi-nyumba ya Yehova inatoa ishara iliyo wazi kila mara kunapokuwa na uhitaji wa kuchukua hatua fulani. Msimamizi-nyumba huyo anafanya hivyo jinsi gani? Kupitia makala katika Mnara wa Mlinzi, Huduma Yetu ya Ufalme, vichapo vipya, na hotuba katika makusanyiko. Mwongozo unatolewa pia kwa makutaniko kupitia waangalizi wanaosafiri au kupitia barua au vipindi vya mazoezi ambavyo vinahudhuriwa na ndugu walio na mapendeleo katika kutaniko.

Je, unatambua waziwazi uthibitisho wa mwongozo wa Mungu? Yehova anatumia tengenezo lake kutuongoza sisi, watu wake, ‘katika nyika’ au jangwa wakati huu wa siku za mwisho za ulimwengu mwovu wa Shetani. Matokeo ni kwamba tunafurahia umoja, upendo, na usalama.

Waisraeli walipofika katika Nchi ya Ahadi, Yoshua alisema hivi: “Mnajua vema kwa mioyo yenu yote na kwa nafsi zenu zote kwamba halikukosa kutimia hata neno moja kati ya maneno yote mema ambayo Yehova Mungu wenu amewaambia ninyi. Yote yametimia kwenu.” (Yos. 23:14) Vivyo hivyo, leo watu wa Mungu bila shaka watafika katika ulimwengu mpya ulioahidiwa. Hata hivyo, ili sisi wenyewe tuwe huko itategemea sana ikiwa tutatii mwongozo wa Mungu kwa unyenyekevu. Kwa hiyo, acheni sisi sote tuendelee kutambua uthibitisho wa mwongozo wa Yehova!

[Picha katika ukurasa wa 5]

Tunaongozwa na tengenezo la Yehova leo

Vichapo vinavyotolewa katika makusanyiko

Shule za kitheokrasi

Mazoezi kwenye mikutano ya utumishi wa shambani