Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Jinsi ya Kuendelea Kuwa Wanyoofu Katika Ulimwengu Usio na Unyoofu

Jinsi ya Kuendelea Kuwa Wanyoofu Katika Ulimwengu Usio na Unyoofu

Jinsi ya Kuendelea Kuwa Wanyoofu Katika Ulimwengu Usio na Unyoofu

UKOSEFU wa unyoofu umeenea kila mahali kama hewa tunayopumua. Watu wanasema uwongo, wanauza vitu kwa bei ya juu sana, wanaiba, hawalipi madeni, na wanajigamba kwamba wana mbinu za ustadi za kufanya biashara. Kwa kuwa tunaishi katika mazingira hayo, mara nyingi tunapambana na hali ambazo zinajaribu azimio letu la kuwa wanyoofu. Tunaweza jinsi gani kuendelea kupinga mwelekeo wa kukosa unyoofu? Acheni tuchunguze mambo matatu ya maana ambayo yatatusaidia kufanya hivyo. Mambo hayo ni kumwogopa Yehova, kuwa na dhamiri njema, na kuridhika au kutosheka.

Woga Unaofaa Kumwelekea Yehova

Nabii Isaya aliandika hivi: “Yehova ni Mwamuzi wetu, Yehova ni Mpaji-sheria wetu, Yehova ni Mfalme wetu.” (Isa. 33:22) Kutambua cheo cha mamlaka cha Yehova kunafanya tuwe na woga wa kimungu—ambao unatuchochea kuazimia kupinga roho ya kukosa unyoofu. Methali 16:6 inasema hivi: “Mtu huepuka uovu kwa kumwogopa Yehova.” Kumwogopa Mungu hakumaanishi kutetemeka kwa kuwa tunaogopa Mungu atatuadhibu, badala yake ni woga unaofaa wa kutomkosea Baba yetu wa mbinguni, ambaye anapendezwa sana na hali yetu nzuri.—1 Pet. 3:12.

Jambo halisi lililoonwa linaonyesha matokeo mazuri ya kuwa na hangaiko, au woga huo unaofaa. Ricardo na mke wake, Fernanda, walitoa kiasi kinacholingana na dola mia saba za Marekani kutoka katika akaunti yao ya benki. * Fernanda aliweka mabunda hayo ya noti ndani ya mkoba wake bila kuzihesabu. Walipofika nyumbani baada ya kulipa madeni fulani, walishangaa kuona kwamba karibu pesa zote ambazo walikuwa wametoa kwenye benki bado zilikuwa katika mkoba wa Fernanda. Walikata kauli hivi: “Ni lazima mfanyakazi wa benki awe alitupatia pesa nyingi zaidi.” Mwanzoni walishawishiwa kukaa na pesa hizo, kwa kuwa bado walikuwa na madeni mengi ambayo hawakuwa wamelipa. Ricardo anaeleza hivi: “Tulisali kwa Yehova ili tupate nguvu za kurudisha pesa hizo. Tamaa yetu ya kumpendeza kulingana na himizo la Methali 27:11 ilituchochea kurudisha pesa hizo.”

Dhamiri Iliyozoezwa na Biblia

Tunaweza kusitawisha dhamiri inayoitikia haraka kwa kujifunza Biblia na kujitahidi kutumia mambo tunayojifunza. Hivyo, ‘neno la Mungu, ambalo liko hai na lina nguvu,’ halitachochea tu akili zetu bali pia mioyo yetu. Hilo litatuchochea “kujiendesha kwa unyoofu katika mambo yote.”—Ebr. 4:12; 13:18.

Fikiria kisa cha João. Alikuwa na deni kubwa sana, kiasi kinacholingana na dola elfu tano za Marekani. Kisha, akahamia mji mwingine bila kulipa deni lake. Miaka minane baadaye, João alijifunza kweli, na dhamiri yake iliyozoezwa na Biblia ikamchochea kuongea na mtu ambaye alikuwa akimdai lile deni! Kwa kuwa João anatumia mshahara mdogo anaopata ili kumtunza mke na watoto wanne, mtu huyo alikubali amlipe pesa hizo hatua kwa hatua kwa miezi fulani.

Kutosheka

Mtume Paulo aliandika hivi: “Ni njia ya kupata faida kubwa, huu ujitoaji-kimungu pamoja na ujitoshelevu. . . . Tukiwa na chakula na kitu cha kujifunika, tutaridhika na vitu hivyo.” (1 Tim. 6:6-8) Kuchukua shauri hilo lenye hekima kwa uzito kutatusaidia tuepuke kunaswa na mtego wa kufanya biashara kwa kutumia mbinu zinazochochewa na pupa, na ambazo si za unyoofu au miradi ya uwongo ya kutajirika haraka. (Met. 28:20) Kufuata shauri la Paulo kutatusaidia pia kutanguliza Ufalme wa Mungu, tukiwa na hakika kwamba tutapata mahitaji yetu ya lazima.—Mt. 6:25-34.

Hata hivyo, kwa sababu ya “nguvu za udanganyifu wa utajiri,” hatupaswi kamwe kupuuza hatari ya kulemewa na pupa na kutamani. (Mt. 13:22) Kumbuka mwanamume aliyeitwa Akani. Alikuwa amejionea Waisraeli wakivuka Mto Yordani kimuujiza. Hata hivyo, kwa sababu ya kulemewa na pupa, hakushinda tamaa ya kuiba kiasi fulani cha fedha na dhahabu na vazi lenye thamani kutoka kwa vitu vilivyokuwa vimechukuliwa katika jiji la Yeriko. Alipoteza uhai wake kwa sababu ya tendo hilo. (Yos. 7:1, 20-26) Haishangazi kwamba karne nyingi baadaye, Yesu alionya hivi: “Endeleeni kufungua macho yenu na mjilinde na kila namna ya tamaa”!—Luka 12:15.

Uwe Mnyoofu Kazini

Acheni sasa tuchunguze hali fulani ambazo zinaweza kujaribu azimio letu la kuendelea kuwa wanyoofu katika mambo yote. Kuwa wanyoofu kazini kunatia ndani ‘kuepuka kuiba’—hata kama watu wengi wanaona kwamba kufanya hivyo ni jambo la kawaida. (Tito 2:9, 10) Jurandir, ambaye anafanya kazi katika shirika la kiserikali, alikuwa akiripoti kwa unyoofu kuhusu gharama zake za usafiri. Hata hivyo, wafanyakazi wenzake walikuwa wakiomba kiasi kikubwa zaidi cha pesa kuliko walichotumia. Walikuwa wakifanya hivyo kwa sababu msimamizi wa idara yao alikuwa akiwaficha wafanyakazi ambao hawakuwa wanyoofu. Msimamizi huyo hata alimkemea Jurandir kwa sababu ya kuwa mnyoofu na akaacha kumtuma kwa safari za kikazi. Hata hivyo, baada ya muda hesabu za shirika hilo zilikaguliwa, na Jurandir akapongezwa kwa sababu ya unyoofu wake. Vilevile alipandishwa cheo.

André, ambaye ni muuzaji, aliambiwa na mkubwa wake wa kazi alipishe huduma fulani mara mbili kwenye akaunti za wateja. Ndugu yetu alisali kwa Yehova ili apate ujasiri wa kushikamana na kanuni za Biblia. (Zab. 145:18-20) Alijaribu pia kumweleza mkubwa wake wa kazi kwa nini hangefuata maagizo yake, lakini hakumsikiliza. Kwa hiyo, André akaamua kuacha kazi yake ya mshahara mkubwa. Hata hivyo, karibu mwaka mmoja baadaye, mkubwa wake wa zamani alimwita arudi kazini, na kumhakikishia kwamba wateja hawakuwa tena wakilipishwa kupita kiasi. André alipandishwa cheo na kuwa meneja.

Lipa Madeni

Mtume Paulo aliwashauri Wakristo hivi: “Msiwe na deni la hata jambo moja la mtu yeyote.” (Rom. 13:8) Huenda tukajaribu kujitetea kwa nini hatujalipa deni, kwa kusema kwamba mtu anayetudai ana pesa nyingi na hahitaji pesa hizo. Hata hivyo Biblia inaonya hivi: “Mwovu anakopa lakini halipi.”—Zab. 37:21.

Namna gani ikiwa hatuwezi kulipa deni kwa sababu ya “tukio lisilotazamiwa”? (Mhu. 9:11) Francisco alikopa kiasi cha pesa kinacholingana na dola elfu saba za Marekani kutoka kwa Alfredo ili amalize kulipa mkopo wa nyumba. Lakini kwa sababu ya matatizo fulani ya kibiashara, Francisco alishindwa kulipa deni lake kufikia tarehe ambayo walikuwa wamekubaliana. Alichukua hatua ya kumfikia Alfredo ili wazungumzie jambo hilo, na Alfredo akakubali kulipwa deni hilo hatua kwa hatua.

Epuka Kudanganya Kuhusu Hali Yako

Kumbuka mfano mbaya wa Anania na Safira, wenzi wa ndoa katika kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza. Baada ya kuuza shamba, waliwaletea mitume kiasi kidogo cha pesa walizopata na kudai kwamba kilikuwa kiasi chote cha pesa walizopata baada ya kuuza shamba. Walitaka kuwavutia wengine kwa kujifanya wakarimu sana. Hata hivyo, akiongozwa na roho takatifu ya Mungu, mtume Petro alifunua udanganyifu wao, na Yehova akawapiga wakafa.—Mdo. 5:1-11.

Tofauti na Anania na Safira ambao hawakuwa wanyoofu, waandikaji wa Biblia waliandika mambo waziwazi na kwa unyoofu. Musa alieleza kwa unyoofu jinsi alivyokasirika na hivyo kuzuiwa kuingia katika Nchi ya Ahadi. (Hes. 20:7-13) Vivyo hivyo, Yona hakuficha udhaifu ambao alionyesha kabla na baada ya kuwahubiria Waninawi. Badala yake, aliandika kuhusu udhaifu huo.—Yona 1:1-3; 4:1-3.

Bila shaka, mtu anahitaji ujasiri ili aseme ukweli hata kama hilo litafanya upoteze kitu fulani, kama inavyoonyeshwa na jambo lililompata shuleni msichana mwenye umri wa miaka 14 anayeitwa Nathalia. Aliangalia mtihani aliokuwa amefanya na kutambua kwamba mwalimu wake alikuwa ametia alama ya kuonyesha kwamba jibu fulani lenye makosa lilikuwa sahihi. Ingawa alijua kwamba jambo hilo lingebadili sana matokeo ya mtihani wake, Nathalia hakusita kumwambia mwalimu wake. Alisema hivi: “Sikuzote wazazi wangu wamenifundisha kwamba ili nimpendeze Yehova, ni lazima niwe mnyoofu. Dhamiri yangu ingenisumbua ikiwa singemwambia mwalimu wangu.” Mwalimu huyo alithamini unyoofu wa Nathalia.

Unyoofu—Sifa Inayomletea Yehova Utukufu

Giselle, msichana mwenye umri wa miaka 17 aliokota mfuko uliokuwa na hati mbalimbali na kiasi cha pesa kinacholingana na dola 35 za Marekani. Alifanya mipango pamoja na wasimamizi wa shule ili mfuko huo urudishiwe mwenyewe. Mwezi mmoja baadaye, msaidizi wa mwalimu mkuu wa shule hiyo alisoma mbele ya darasa barua ya kumsifu Giselle kwa sababu ya unyoofu wake na kuipongeza familia yake kwa sababu ya kumzoeza vizuri na kumlea kulingana na dini. ‘Matendo yake mazuri’ yalimletea Yehova utukufu.—Mt. 5:14-16.

Tunapaswa kujitahidi ili tuwe wanyoofu tunapoishi kati ya wale ambao ni ‘wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda pesa, wenye kujidai, wenye majivuno, na wasio washikamanifu.’ (2 Tim. 3:2) Ingawa hivyo, woga unaofaa kumwelekea Yehova, dhamiri iliyozoezwa na Biblia, na kutosheka kunatusaidia kuendelea kuwa wanyoofu katika ulimwengu usio na unyoofu. Tunasitawisha pia urafiki wa karibu zaidi pamoja na Yehova, ambaye ‘ni mwadilifu na anapenda matendo ya uadilifu.’—Zab. 11:7.

[Maelezo ya Chini]

^ Baadhi ya majina yamebadilishwa.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Woga unaofaa kumwelekea Yehova unatia nguvu azimio letu la kuwa wanyoofu

[Picha katika ukurasa wa 8]

Tabia yetu ya unyoofu inamletea Yehova utukufu