Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Familia za Kikristo—“Endeleeni Kuwa Tayari”

Familia za Kikristo—“Endeleeni Kuwa Tayari”

Familia za Kikristo—“Endeleeni Kuwa Tayari”

“Endeleeni kuwa tayari, kwa sababu Mwana wa binadamu atakuja katika saa msiyoitazamia.”—LUKA 12:40.

1, 2. Kwa nini tunapaswa kuchukua kwa uzito himizo la Yesu la ‘kuendelea kuwa tayari’?

 “WAKATI Mwana wa binadamu atakapofika katika utukufu wake” na kuwatenganisha “watu, mmoja kutoka kwa mwenzake,” ni nini kitakachotukia kwako wewe na kwa familia yako? (Mt. 25:31, 32) Kwa kuwa jambo hilo litatukia katika saa tusiyotazamia, ni jambo la maana kama nini kwetu kuchukua kwa uzito himizo au shauri la Yesu la ‘kuendelea kuwa tayari’!—Luka 12:40.

2 Habari iliyotangulia ilizungumzia jinsi kila mshiriki wa familia anavyoweza kuisaidia familia nzima kuendelea kukaa macho kiroho kwa kuchukua kwa uzito daraka lake. Acheni tuzungumzie njia nyingine ambazo tunaweza kuisaidia familia yetu kuwa na hali nzuri ya kiroho.

Endelea Kuwa na Jicho “Rahisi”

3, 4. (a) Familia za Kikristo zinapaswa kujilinda kutokana na nini? (b) Ni nini maana ya kuwa na jicho “rahisi”?

3 Ili washiriki wa familia wawe tayari wakati ambapo Kristo atakuja, ni lazima wawe makini kutokengeushwa kutoka kwa mambo yanayohusu ibada ya kweli. Wanahitaji kujilinda ili wasipotoshwe na mambo yanayokengeusha fikira. Kwa kuwa kufuatia vitu vya kimwili ni mtego ambao umenasa familia nyingi, fikirieni yale ambayo Yesu alisema kuhusu kudumisha jicho “rahisi.” (Soma Mathayo 6:22, 23.) Kama vile tu ambavyo taa inaweza kuangaza njia yetu na kutuwezesha kutembea bila kuanguka, vivyo hivyo mambo tunayotazama kwa ‘macho ya mfano ya moyo wetu’ yanaweza kuangaza njia yetu na kutusaidia kutembea bila kujikwaa.—Efe. 1:18.

4 Ili jicho halisi lione waziwazi, ni lazima lifanye kazi vizuri na kuweza kukazia kitu ambacho linatazama. Ndivyo ilivyo na macho ya moyo. Kuwa na jicho rahisi la mfano kunamaanisha kwamba tunakazia fikira kusudi moja. Badala ya kuishi maisha ambayo yanakazia fikira vitu vya kimwili na kuhangaika kupita kiasi kuhusu kutosheleza mahitaji ya kimwili ya familia yetu, jicho letu linakazia mambo ya kiroho. (Mt. 6:33) Hilo linamaanisha kwamba tunatosheka na mahitaji yetu ya lazima ambayo Mungu anatusaidia kupata na kutanguliza utumishi wake katika maisha yetu.—Ebr. 13:5.

5. Msichana fulani tineja alionyesha jinsi gani kwamba “jicho” lake lilikazia kumtumikia Mungu?

5 Matokeo yanaweza kuwa mazuri kama nini watoto wakizoezwa kuendelea kuwa na jicho rahisi! Fikiria mfano wa msichana mmoja tineja katika nchi ya Ethiopia. Alifanya vizuri sana shuleni hivi kwamba alipomaliza masomo yake ya msingi, alipewa nafasi ya kulipiwa masomo ili apate elimu zaidi. Hata hivyo, kwa sababu jicho lake lilikazia kumtumikia Yehova, alikataa nafasi hiyo. Baada ya muda mfupi, alipewa nafasi ya kufanya kazi ambayo angelipwa mshahara wa dola za Marekani 4,200 kwa mwezi, pesa nyingi sana zikilinganishwa na mishahara ambayo watu wengi wanapata katika nchi yake. Lakini “jicho” la msichana huyo lilikazia utumishi wa painia. Hakuhitaji kuzungumza na wazazi wake kabla ya kukataa kazi hiyo. Wazazi wake walihisi namna gani waliposikia kuhusu jambo ambalo binti yao alifanya? Kwa kweli, walifurahi pamoja naye na kumwambia jinsi walivyojivunia yeye kuwa binti yao!

6, 7. Tunapaswa ‘kuendelea kufungua macho yetu’ ili tuone hatari gani?

6 Katika andiko la Mathayo 6:22, 23, Yesu anatoa onyo lisilo la moja kwa moja kuhusu pupa. Yesu hakusema kwamba kinyume cha jicho “rahisi” ni jicho “linalokazia mambo mengi,” badala yake alisema kinyume chake ni jicho “bovu.” ‘Jicho bovu’ ni jicho baya; lenye wivu, yaani, lina pupa au linatamani. (Mt. 6:23) Yehova anahisi namna gani kuhusu kutamani au pupa? Biblia inasema: “Uasherati na ukosefu wa usafi wa kila namna au pupa [au, kutamani] visitajwe hata kidogo katikati yenu.”—Efe. 5:3.

7 Ingawa inaweza kuwa rahisi kugundua kwamba wengine wana pupa, ni vigumu zaidi kugundua kwamba sisi wenyewe tuna pupa. Hivyo, ni jambo la hekima kwetu kutii shauri hili la Yesu: “Endeleeni kufungua macho yenu na mjilinde na kila namna ya tamaa.” (Luka 12:15) Ili tufanye hivyo ni lazima tujichunguze na kuona tunakazia nini katika mioyo yetu. Familia za Kikristo zinapaswa kufikiria kwa uzito wakati na pesa ambazo wanatumia katika vitumbuizo, tafrija, na kununua vitu vya kimwili.

8. Inapohusu kununua vitu, tunaweza jinsi gani ‘kuendelea kufungua macho yetu’?

8 Kabla ya kununua kitu, unapaswa kufikiria mambo mengi zaidi kuliko tu kuamua ikiwa unaweza kukinunua au huwezi. Fikiria mambo kama haya: ‘Je, nitakuwa na wakati wa kutumia kitu hicho kwa ukawaida na kukitunza? Nitahitaji muda mrefu kadiri gani kujifunza kukitumia vizuri?’ Enyi vijana, msiamini mambo yote ambayo matangazo ya kibiashara ulimwenguni yanasema kuhusu vitu vinavyouzwa na kuwafanya mnunue mitindo ya mavazi ya bei ghali na vitu vingine ambavyo si vya lazima. Mjizuie. Pia, fikiria ikiwa kupata kitu fulani kutaisaidia familia yako kujitayarisha kwa ajili ya kuja kwa Mwana wa binadamu. Uwe na imani katika ahadi hii ya Yehova: “Sitakuacha wala kukutupa hata kidogo.”—Ebr. 13:5.

Fuatia Miradi ya Kiroho

9. Kufuatia miradi ya kiroho kunaweza kuisaidia familia jinsi gani?

9 Njia nyingine ambayo washiriki wa familia wanaweza kutia nguvu imani yao na kuisaidia familia nzima kuwa na hali nzuri ya kiroho ni kujiwekea miradi ya kiroho na kuifuatia. Kufanya hivyo kunaweza kuzisaidia familia kutambua maendeleo wanayofanya katika kutimiza kusudi lao la kumpendeza Yehova na pia kuamua ikiwa utendaji fulani ni wa maana au si wa maana sana.—Soma Wafilipi 1:10.

10, 11. Mnafuatia miradi gani ya kiroho mkiwa familia, na mngependa kujiwekea miradi gani ya wakati ujao?

10 Hata mnaweza kupata baraka nyingi mkijiwekea miradi midogo inayofaa ambayo karibu kila mshiriki wa familia anaweza kuifikia. Kwa mfano, fikiria mradi wa kuzungumzia andiko la siku kila siku. Maelezo yanayotolewa na washiriki wa familia yanaweza kumsaidia kichwa cha familia kutambua kiwango cha hali yao ya kiroho. Mradi wa kusoma Biblia pamoja kwa ukawaida mkiwa familia unawapa watoto nafasi nzuri sana ya kuboresha uwezo wao wa kusoma na pia kuelewa vizuri zaidi ujumbe wa Biblia. (Zab. 1:1, 2) Na je, hatupaswi kujiwekea mradi wa kuboresha sala zetu? Kusitawisha kwa kadiri kubwa zaidi sifa za tunda la roho kunaweza pia kuwa mradi mzuri sana wa kufuatia. (Gal. 5:22, 23) Au je, mnaweza kutafuta njia za kuwatendea kwa huruma watu mnaokutana nao katika huduma? Kujitahidi kufanya hivyo mkiwa familia kunaweza kuwasaidia watoto kujifunza kuwa wenye huruma, na inaelekea sana kwamba watakuza tamaa ya kutumika wakiwa mapainia wa kawaida au wamishonari.

11 Kwa nini usifikirie miradi fulani ambayo wewe na familia yako mnaweza kufuatia? Je, familia yako inaweza kujiwekea mradi wa kutumia muda zaidi katika huduma? Je, mnaweza kujiwekea mradi wa kuwa na ujasiri wa kutoa ushahidi barabarani, katika maeneo ya kibiashara, au kwa kutumia simu? Je, mnaweza kwenda kuhubiri katika maeneo yenye uhitaji mkubwa zaidi wa wahubiri wa Ufalme? Je, mshiriki mmoja wa familia yenu anaweza kujifunza lugha ya kigeni ili awahubirie habari njema watu wa nchi nyingine?

12. Vichwa vya familia wanaweza kufanya nini ili kuzisaidia familia zao kukua kiroho?

12 Ukiwa kichwa cha familia, angalia mambo ambayo familia yako inaweza kutimiza ili ifanye maendeleo kiroho. Kisha, mjiwekee miradi hususa yenye kujenga ya kuwasaidia kutimiza kusudi hilo. Miradi ambayo mnajiwekea mkiwa familia inapaswa kuwa inayofaa na ambayo mnaweza kuifikia kulingana na uwezo na hali zenu. (Met. 13:12) Bila shaka, muda unahitajika ili kujitahidi kufikia mradi fulani wa maana. Kwa hiyo, nunueni wakati ambao mnatumia kutazama televisheni na kuutumia kufuatia mambo ya kiroho. (Efe. 5:15, 16) Ujitahidi kufikia miradi ambayo unaiwekea familia yako. (Gal. 6:9) Familia ambayo inafuatia miradi ya kiroho itafanya maendeleo yake “yawe wazi kwa watu wote.”—1 Tim. 4:15.

Endeleeni Kuwa na Jioni ya Ibada ya Familia

13. Ni badiliko gani ambalo lilifanywa katika ratiba ya kila juma ya mikutano ya kutaniko, na ni maswali au maulizo gani tunayopaswa kutafakari?

13 Badiliko kubwa ambalo lilifanywa kuanzia Januari 1, 2009 (1/1/2009) katika ratiba au programu ya kila juma ya mikutano ni mpango mzuri zaidi wa kuzisaidia familia ‘kuendelea kuwa tayari’ kwa ajili ya kuja kwa Mwana wa binadamu. Hatuhitaji tena kukutana pamoja katika siku tofauti kwa ajili ya mkutano ambao ulikuwa ukiitwa Funzo la Kitabu la Kutaniko kwa sababu mkutano huo uliunganishwa na Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na Mkutano wa Utumishi. Badiliko hilo lilifanywa ili familia za Kikristo zipate nafasi ya kujenga hali yao ya kiroho kwa kutenga jioni moja kila juma ili kuwa na ibada ya familia. Sasa kwa kuwa muda fulani umepita tangu badiliko hilo lilipofanywa, tunaweza kujiuliza hivi: ‘Je, ninatumia vizuri wakati ambao umetengwa ili kuwa na jioni ya Ibada ya Familia au kuwa na funzo la kibinafsi? Je, nimefanikiwa kutimiza kusudi la mpango huo?’

14. (a) Ni nini kusudi kuu la kuendelea kuwa na jioni ya Ibada ya Familia au funzo la kibinafsi? (b) Kwa nini ni jambo la maana kutenga jioni moja kwa ajili ya kujifunza?

14 Kusudi kuu la kuendelea kuwa na jioni ya Ibada ya Familia au wakati wa funzo la kibinafsi ni kumkaribia Mungu zaidi. (Yak. 4:8) Tunapotumia wakati kujifunza Biblia kwa ukawaida na kuongeza ujuzi wetu kumhusu Muumba, uhusiano wetu pamoja naye unatiwa nguvu. Kadiri tunavyozidi kumkaribia Yehova, ndivyo tunavyochochewa zaidi kumpenda ‘kwa moyo wetu wote, kwa nafsi yetu yote, kwa akili yetu yote, na kwa nguvu zetu zote.’ (Marko 12:30) Bila shaka, tunatamani kumtii Mungu na kumwiga. (Efe. 5:1) Basi, kuendelea kuwa na jioni ya Ibada ya Familia kwa ukawaida, ni jambo la maana linalowasaidia washiriki wote wa familia yetu ‘kuendelea kuwa tayari’ kiroho tunapongojea “dhiki kuu” iliyotabiriwa. (Mt. 24:21) Hilo ni jambo la maana ili tuokolewe.

15. Jioni ya Ibada ya Familia inaweza kuwasaidia washiriki wa familia wawe na hisia gani kuelekea washiriki wenzao wa familia?

15 Mpango wa Ibada ya Familia unatimiza pia kusudi lingine—kuwasaidia washiriki wa familia kuwa na uhusiano wa karibu kati yao. Kutumia wakati pamoja kuzungumzia mambo ya kiroho kila juma kunaboresha sana jinsi washiriki wa familia wanavyohisi kuhusu wengine katika familia. Wenzi wa ndoa wanakuwa na uhusiano wa karibu sana wanaposikia mwenzi wao akishangilia wanapopata wakiwa pamoja hazina ya kiroho katika funzo! (Soma Mhubiri 4:12.) Inaelekea kwamba wazazi na watoto wanaoabudu pamoja wanaunganishwa na upendo, ambao ni “kifungo kikamilifu cha muungano.”—Kol. 3:14.

16. Simulia jinsi dada watatu kiroho wanavyofaidika kwa kutenga jioni moja ya kujifunza Biblia.

16 Fikiria jinsi ambavyo dada watatu wa kiroho wamefaidika kupitia mpango wa kutenga jioni moja kwa ajili ya funzo la Biblia. Ingawa dada hao hawana uhusiano wa kiukoo, wajane hao watatu waliozeeka wanaishi katika mji mmoja na wamekuwa marafiki wa karibu kwa miaka mingi. Kwa kuwa walitaka sana kushirikiana zaidi pamoja na wakati huohuo kufaidika kiroho badala ya kufurahia ushirika tu wa kirafiki, waliamua kutenga jioni moja ili wakutane na kujifunza Biblia. Walianza kujifunza wakitumia kitabu “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu. Mmoja wao anasema hivi: “Tunafurahia sana wakati huo hivi kwamba kwa kawaida tunajifunza kwa zaidi ya saa nzima. Tunajaribu kuwazia akilini hali za ndugu zetu wa karne ya kwanza, na tunazungumzia jinsi ambavyo tungetenda katika hali kama hizo. Kisha tunajaribu kutumia katika huduma mambo tuliyojifunza kutokana na mazungumzo yetu. Hilo limefanya kazi yetu ya kuhubiri kuhusu Ufalme na kufanya wanafunzi iwe yenye kufurahisha zaidi na yenye matokeo zaidi kuliko mwanzoni.” Mpango huo umewajenga kiroho marafiki hao watatu na zaidi ya hilo umewasaidia kuwa na uhusiano wa karibu hata zaidi. Wanasema hivi: “Tunathamini sana mpango huo.”

17. Ni mambo gani yanayosaidia jioni ya Ibada ya Familia iwe yenye matokeo mazuri?

17 Namna gani wewe? Unafaidika jinsi gani kwa kutenga jioni ya kuwa na ibada ya familia au funzo la kibinafsi? Mpango huo usipofuatwa kwa ukawaida, hauwezi kutimiza kusudi lake. Kila mshiriki wa familia anapaswa kuwa tayari kujifunza wakati uliowekwa. Mambo madogo-madogo hayapaswi kuruhusiwa kuvuruga jioni hiyo. Zaidi ya hayo, mnapaswa kuchagua mambo ya kujifunza ambayo yanafanya pindi hiyo iwe yenye kujenga familia yenu. Mnaweza kufanya nini ili vipindi hivyo vya kujifunza viwe vyenye kufurahisha? Tumieni njia mbalimbali za kujifunza zenye matokeo mazuri, na mdumishe mazingira matulivu na yenye heshima.—Yak. 3:18. *

‘Kaa Macho’ na ‘Uendelee Kuwa Tayari’

18, 19. Kujua kwamba Mwana wa binadamu yuko karibu kuja kunapaswa kukuchochea jinsi gani wewe na familia yako?

18 Hali za ulimwengu ambazo zinazidi kuwa mbaya katika siku zetu zinaonyesha waziwazi kwamba tangu mwaka wa 1914, ulimwengu mwovu wa Shetani uliingia katika siku zake za mwisho. Mawingu ya dhoruba ya Har–Magedoni yako karibu sana. Hivi karibuni Mwana wa binadamu atakuja kutekeleza hukumu ya Yehova juu ya watu waovu. (Zab. 37:10; Met. 2:21, 22) Je, kujua hivyo hakupaswi kukuchochea wewe na familia yako?

19 Je, unatii shauri la Yesu la kuendelea kuwa na jicho “rahisi”? Ingawa huenda watu wa ulimwengu huu wakajitahidi kupata utajiri, umashuhuri, au mamlaka, je, familia yako inafuatia miradi ya kiroho? Je, mpango wa jioni ya Ibada ya Familia au wakati wa funzo la kibinafsi unakusaidia? Je, unatimiza vizuri makusudi ya mpango huo? Kama tulivyozungumzia katika habari iliyotangulia, je, unatimiza madaraka yako ya Kimaandiko ukiwa mume, mke, au mtoto, na hivyo kuisaidia familia nzima ‘kukaa macho’? (1 The. 5:6) Ikiwa unafanya hivyo, ‘utaendelea kuwa tayari’ kwa ajili ya kuja kwa Mwana wa binadamu.

[Maelezo ya Chini]

^ Ili kupata mapendekezo kuhusu mambo ya kujifunza na jinsi ya kufanya jioni za Ibada ya Familia ziwe zenye faida na zenye kufurahisha, ona gazeti la Mnara wa Mlinzi, la Oktoba 15, 2009, ukurasa wa 29-31.

Ulijifunza Nini?

• Eleza jinsi familia za Kikristo zinavyoweza ‘kuendelea kuwa tayari’ kwa . . .

kuwa na jicho “rahisi.”

kujiwekea na kufuatia miradi ya kiroho.

kuendelea kuwa na jioni ya Ibada ya Familia.

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 13]

Jicho “rahisi” litatuchochea kupinga mambo ya ulimwengu yanayokengeusha fikira