Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Familia za Kikristo—‘Kaeni Macho’

Familia za Kikristo—‘Kaeni Macho’

Familia za Kikristo—‘Kaeni Macho’

“Na tukae macho na kutunza akili zetu.”—1 THE. 5:6.

1, 2. Ni nini kinachohitajiwa ili familia iweze kukaa macho kiroho?

 KUHUSU “ile siku ya Yehova iliyo kuu na yenye kuogopesha,” mtume Paulo aliwaandikia hivi Wakristo huko Thesalonike: “Akina ndugu, hamko gizani, hivi kwamba siku hiyo iwafikie ninyi kama vile ambavyo ingewafikia wezi, kwa maana ninyi nyote ni wana wa nuru na wana wa mchana. Sisi si wa usiku wala si wa giza.” Paulo aliongezea hivi: “Kwa hiyo, basi, na tusiendelee kulala usingizi kama wengine, bali na tukae macho na kutunza akili zetu.”—Yoe. 2:31; 1 The. 5:4-6.

2 Shauri la Paulo kwa Wathesalonike linawafaa kabisa hasa Wakristo wanaoishi “wakati wa mwisho.” (Dan. 12:4) Kadiri mwisho wa mfumo huu mwovu wa mambo unavyozidi kukaribia, ndivyo Shetani anavyoazimia kuwageuza waabudu wengi iwezekanavyo wa kweli ili waache kumtumikia Mungu. Kwa hiyo, tunatenda kwa hekima tunapochukua kwa uzito himizo au shauri la Paulo la kuendelea kukaa macho kiroho. Ili familia ya Kikristo iweze kukaa macho, ni jambo la maana kwa kila mshiriki kutimiza daraka lake la Kimaandiko. Basi, waume, wake, na watoto wanatimiza daraka gani katika kuzisaidia familia zao ‘kukaa macho’?

Waume—Mwigeni “Mchungaji Mwema”

3. Kulingana na andiko la 1 Timotheo 5:8, daraka la mwanamume akiwa kichwa cha familia linatia ndani nini?

3 Biblia inasema “kichwa cha mwanamke ni mwanamume.” (1 Kor. 11:3) Daraka la mwanamume akiwa kichwa cha familia linatia ndani nini? Maandiko yanasema hivi kuhusu daraka moja la kichwa cha familia: “Ikiwa yeyote hawaandalii mahitaji wale walio wake mwenyewe, na hasa wale walio washiriki wa nyumba yake, ameikana imani naye ni mbaya kuliko mtu asiye na imani.” (1 Tim. 5:8) Kwa kweli, mwanamume anapaswa kuiandalia familia yake mahitaji ya kimwili. Hata hivyo, ili aisaidie familia yake kukaa macho kiroho, ni lazima afanye mengi zaidi kuliko tu kuwapa mahitaji ya kimwili. Anahitaji kuijenga familia yake kiroho, na kuwasaidia washiriki wote wa familia kutia nguvu uhusiano wao pamoja na Mungu. (Met. 24:3, 4) Anaweza kufanya hivyo jinsi gani?

4. Ni nini kinachoweza kumsaidia mwanamume afanikiwe kuijenga familia yake kiroho?

4 Kwa kuwa “mume ni kichwa cha mke wake kama vile Kristo pia alivyo kichwa cha kutaniko,” mwanamume aliyeoa anapaswa kuchunguza na kuiga ukichwa wa Yesu juu ya kutaniko. (Efe. 5:23) Fikiria jinsi Yesu alivyoeleza kuhusu uhusiano wake pamoja na wafuasi wake. (Soma Yohana 10:14, 15.) Ni ufunguo gani ambao unaweza kumsaidia mwanamume ambaye anataka kuijenga familia yake kiroho apate matokeo mazuri? Huu ndio ufunguo: Jifunze mambo ambayo Yesu alisema na kutenda akiwa “mchungaji mwema,” na ‘ufuate hatua zake kwa ukaribu.’—1 Pet. 2:21.

5. Yule Mchungaji Mwema ana ujuzi gani kuhusu kutaniko?

5 Kwa njia ya mfano, uhusiano kati ya mchungaji na kondoo wake unategemea ujuzi na kuaminiana. Mchungaji anajua kila jambo kuhusu kondoo wake, na kondoo wanamjua na kumwamini mchungaji wao. Wanatambua na kutii sauti yake. Yesu alisema hivi: “Ninawajua kondoo wangu na kondoo wangu wananijua.” Yesu hana ujuzi wa kijuu-juu tu kuhusu kutaniko. Neno la Kigiriki ambalo limetafsiriwa ‘kujua’ linamaanisha “ujuzi wa ndani sana kumhusu mtu binafsi.” Ndiyo, yule Mchungaji Mwema anawajua kondoo wake kibinafsi. Anajua mahitaji, udhaifu, na sifa nzuri za kila mmoja wao. Yesu ambaye ni Kielelezo chetu anaona kila jambo linalowahusu kondoo wake. Na kondoo hao wanamjua vizuri kabisa mchungaji wao na wanaamini uongozi wake.

6. Waume wanaweza kumwiga jinsi gani yule Mchungaji Mwema?

6 Ili mume amwige Kristo katika kutumia ukichwa wake, ni lazima ajifunze kufikiria hali yake akiwa mchungaji na kuwafikiria wale ambao anawatunza kama kondoo. Anapaswa kujitahidi kuwa na ujuzi wa ndani kuhusu familia yake. Je, kweli mume anaweza kuwa na ujuzi wa aina hiyo? Ndiyo, anaweza kwa kuzungumza au kuwasiliana vizuri na washiriki wote wa familia yake, kusikiliza mahangaiko yao, kuongoza katika utendaji wa familia, na kujitahidi kabisa kufanya maamuzi mazuri kuhusu mambo kama vile ibada ya familia, kuhudhuria mikutano, utumishi wa shambani, tafrija, na vitumbuizo. Mume Mkristo anapoongoza akiwa na ujuzi si wa Neno la Mungu tu bali pia ujuzi kuhusu wale ambao amepewa daraka la kuwatunza, inaelekea sana kwamba washiriki wa familia yake watakuwa na uhakika katika ukichwa wake naye atafurahi kuona wakiendelea kutumika pamoja katika ibada ya kweli.

7, 8. Mume anaweza kumwiga yule Mchungaji Mwema jinsi gani katika kuwaonyesha upendo wale walio chini ya utunzaji wake?

7 Mchungaji mzuri anawapenda pia kondoo wake. Tunapojifunza masimulizi ya Injili kuhusu maisha na huduma ya Yesu, moyo wetu unatuchochea kuthamini upendo ambao Yesu aliwaonyesha wanafunzi wake. Hata ‘aliitoa nafsi yake kwa ajili ya kondoo.’ Waume wanapaswa kumwiga Yesu kwa kuwaonyesha upendo wale walio chini ya utunzaji wao. Badala ya kumtawala mke wake kwa ukali, mume ambaye anatamani kupata kibali cha Mungu anaendelea kumpenda mke wake “kama vile Kristo pia alivyolipenda kutaniko.” (Efe. 5:25) Mume anapaswa kumwambia mke wake maneno yenye fadhili na ya ufikirio, kwa sababu mke anastahili heshima.—1 Pet. 3:7.

8 Kichwa cha familia anapowazoeza watoto wake, anapaswa kushikamana kabisa na kanuni za kimungu. Hata hivyo, hapaswi kamwe kukosa kuwaonyesha watoto wake upendo. Anapaswa kuwatia nidhamu kwa upendo inapohitajika. Watoto fulani wanaweza kuchukua muda mrefu zaidi kuelewa maagizo ya wazazi kuliko watoto wengine. Baba anapaswa kuwa mwenye subira zaidi anaposhughulika na watoto kama hao. Wanaume wanapoendelea kufuata sikuzote mfano wa Yesu, wanatokeza hali yenye amani na usalama nyumbani. Familia zao zinafurahia usalama wa kiroho ambao mtunga-zaburi aliimba kuuhusu.—Soma Zaburi 23:1-6.

9. Kama Noa, aliyekuwa mzee wa ukoo, wanaume Wakristo wana daraka gani, na ni nini kitakachowasaidia kubeba daraka hilo?

9 Noa, aliyekuwa mzee wa ukoo, aliishi katika kipindi cha mwisho cha ulimwengu wa siku zake. Lakini Yehova alimlinda “akiwa salama pamoja na wengine saba alipoleta gharika juu ya ulimwengu wa watu wasiomwogopa Mungu.” (2 Pet. 2:5) Noa alikuwa na daraka la kuisaidia familia yake kuokoka Gharika. Wanaume Wakristo ambao ni vichwa vya familia wanakabili hali kama hiyo katika siku hizi za mwisho. (Mt. 24:37) Ni jambo la maana kama nini kwamba wajifunze mfano wa yule “mchungaji mwema” na kujitahidi kumwiga!

Wake—‘Mjenge Nyumba Zenu’

10. Inamaanisha nini mke kujitiisha chini ya mume wake?

10 Mtume Paulo aliandika hivi: “Wake na wajitiishe kwa waume zao kama kwa Bwana.” (Efe. 5:22) Maneno hayo hayaonyeshi kwa njia yoyote kwamba cheo cha wake si cha heshima. Kabla ya kumuumba Hawa, mwanamke wa kwanza, Mungu wa kweli alitangaza hivi: “Si vema huyo mwanamume aendelee kuwa peke yake. Nitamfanyia msaidizi, awe kikamilisho chake.” (Mwa. 2:18) Daraka la “msaidizi” na “kikamilisho,” yaani, kumuunga mkono mume wake anapotimiza madaraka yake katika familia, ni daraka lenye heshima kwelikweli.

11. Mke ambaye ni mfano mzuri ‘anaijenga nyumba yake’ jinsi gani?

11 Mke ambaye ni mfano mzuri anajitahidi kuijenga familia yake. (Soma Methali 14:1.) Tofauti na mwanamke mpumbavu ambaye haheshimu mpango wa ukichwa, mwanamke mwenye hekima anaheshimu sana mpango huo. Badala ya kuonyesha mtazamo wa ulimwengu wa kutotii na kujitegemea, mwanamke mwenye hekima anajitiisha chini ya mume wake. (Efe. 2:2) Mke ambaye ni mpumbavu haogopi kusema mabaya kumhusu mume wake, lakini mwanamke mwenye hekima anajitahidi kuongeza heshima ambayo mume wake anapata kutoka kwa watoto wake na watu wengine. Mke kama huyo anajitahidi sana kutodharau ukichwa wa mume wake kwa kumsumbua-sumbua au kubishana naye. Pia, anajitahidi kutumia pesa vizuri. Inaelekea kwamba mwanamke mpumbavu anatumia vibaya pesa ambazo familia yake inapata kwa shida. Mwanamke anayemuunga mkono mume wake hayuko hivyo. Anashirikiana na mume wake katika mambo ya kifedha. Anafanya mambo kwa busara na kutumia pesa kwa uangalifu. Hamsukumi mume wake afanye kazi nyingine ya ziada.

12. Mke anaweza kufanya nini ili kuisaidia familia yake ‘kukaa macho’?

12 Mke ambaye ni mfano mzuri anaisaidia familia ‘kukaa macho’ kwa kumsaidia mume wake katika kuwafundisha watoto mambo ya kiroho. (Met. 1:8) Anaunga mkono kwa bidii programu ya Ibada ya Familia. Zaidi ya hayo, anamuunga mkono mume wake anapowashauri na kuwatia nidhamu watoto wao. Yuko tofauti kabisa na mwanamke ambaye hashirikiani na mume wake, na hivyo watoto wake wanateseka kimwili na kiroho!

13. Kwa nini ni jambo la maana kwa mke kumuunga mkono mume wake anaposhiriki kwa bidii katika shughuli za kiroho?

13 Mke anayemuunga mkono mume wake anahisi jinsi gani anapomwona akitimiza madaraka yake kwa bidii katika kutaniko la Kikristo? Anakuwa na shangwe kwelikweli! Iwe mume wake ni mtumishi wa huduma, mzee, au labda mshiriki wa Halmashauri ya Uhusiano na Hospitali au Halmashauri ya Ujenzi ya Mkoa, mke huyo anafurahia pendeleo la mume wake. Bila shaka, atahitaji kujidhabihu ili amuunge mkono kwa bidii mume wake kupitia maneno na matendo yake. Lakini anajua kwamba mume wake anaposhiriki kwa bidii katika shughuli za kiroho anaisaidia familia yote kukaa macho kiroho.

14. (a) Ni hali gani inayoweza kuwa ngumu kwa mke anayemuunga mkono mume wake, naye anaweza kukabiliana jinsi gani na hali hiyo? (b) Mke anaweza kusaidia jinsi gani ili familia nzima iwe na hali njema?

14 Si rahisi kwa mke kuweka mfano mzuri katika kumuunga mkono mume wake wakati anapofanya uamuzi ambao mke hakubaliani nao. Hata wakati huo, mke anaonyesha “roho ya utulivu na ya upole” na kushirikiana naye ili uamuzi wake ufanikiwe. (1 Pet. 3:4) Mke mwema anajaribu kuiga mifano mizuri ya wanawake waliomwogopa Mungu nyakati za kale, kama vile, Sara, Ruthu, Abigaili, na Maria, mama ya Yesu. (1 Pet. 3:5, 6) Pia, anawaiga wanawake wenye umri mkubwa leo “wenye tabia ya kumhofu Mungu.” (Tito 2:3, 4) Kwa kumpenda na kumheshimu mume wake, mwanamke ambaye ni mfano mzuri anasaidia sana katika kufanikisha ndoa yao na kuchangia hali njema ya familia nzima. Nyumba yake ni mahali salama na penye kustarehesha. Mwanamume wa kiroho anamthamini sana mke anayemuunga mkono!—Met. 18:22.

Vijana—‘Endeleeni Kukaza Macho Yenu Juu ya Vitu Visivyoonekana’

15. Vijana wanaweza kushirikiana jinsi gani na wazazi wao ili familia ‘ikae macho’?

15 Ninyi vijana mnaweza jinsi gani kushirikiana na wazazi wenu ili familia yenu ‘ikae macho’ kiroho? Fikirieni zawadi ambayo Yehova ameweka mbele yenu. Labda tangu mlipokuwa watoto, wazazi wenu waliwaonyesha picha zinazoonyesha jinsi maisha yatakavyokuwa katika Paradiso. Mlipoendelea kukua, inaelekea kwamba walitumia Biblia na vichapo vya Kikristo kuwasaidia kuwazia katika akili zenu jinsi uzima wa milele utakavyokuwa katika ulimwengu mpya. Kukazia macho yenu utumishi wa Yehova na kupanga maisha yenu vizuri kutawasaidia ‘kukaa macho.’

16, 17. Vijana wanaweza kufanya nini ili wafanikiwe kukimbia mbio ya uzima?

16 Chukueni kwa uzito maneno ya mtume Paulo yaliyo katika andiko la 1 Wakorintho 9:24. (Soma.) Kimbieni mbio ya uzima mkiwa na kusudi moja tu la kushinda. Chagueni maisha ambayo yatawasaidia kupata zawadi ya uzima wa milele. Vijana wengi wameruhusu kufuatia vitu vya kimwili kuwakengeushe na hivyo wameacha kukazia macho yao ile zawadi. Hilo ni jambo la upumbavu kama nini! Kupanga kutumia maisha yetu kutafuta utajiri hakuleti furaha ya kweli. Vitu ambavyo vinaweza kununuliwa kwa pesa ni vya muda tu. Hata hivyo, endeleeni kukaza macho yenu juu ya “vitu visivyoonekana.” Kwa nini? Kwa sababu “vitu visivyoonekana ni vya milele.”—2 Kor. 4:18.

17 “Vitu visivyoonekana” vinatia ndani baraka za Ufalme. Panga kuishi maisha yako kwa njia ambayo itakuwezesha kupata baraka hizo. Furaha ya kweli inatokana na kutumia maisha yako katika utumishi wa Yehova. Tunapomtumikia Mungu wa kweli tunapata nafasi za kujitahidi kufikia miradi ya muda mfupi na pia miradi ya muda mrefu. * Kujiwekea miradi ya kiroho unayoweza kutimiza kunaweza kukusaidia kukazia macho kumtumikia Mungu ukiwa na kusudi la kupata zawadi ya uzima wa milele.—1 Yoh. 2:17.

18, 19. Kijana anaweza kujua namna gani ikiwa amefanya kweli iwe mali yake mwenyewe?

18 Enyi vijana, hatua ya kwanza katika barabara ya uzima ni kufanya kweli iwe mali yenu. Je, umechukua hatua hiyo? Jiulize hivi: ‘Je, mimi ni mtu wa kiroho, au ninashiriki katika utendaji wa kiroho kwa sababu tu ya wazazi wangu? Je, ninasitawisha sifa ambazo zinafanya nimpendeze Mungu? Je, ninajitahidi kuwa na programu ya kawaida ya kushiriki katika utendaji unaohusiana na ibada ya kweli, kama vile kusali kwa ukawaida, kujifunza, kuhudhuria mikutano, na kushiriki katika utumishi wa shambani? Je, ninamkaribia Mungu kwa kusitawisha uhusiano wa kibinafsi pamoja naye?’—Yak. 4:8.

19 Tafakari kuhusu mfano wa Musa. Hata ingawa alifundishwa utamaduni wa kigeni, alichagua kutambuliwa kuwa mwabudu wa Yehova badala ya kuitwa mwana wa binti ya Farao. (Soma Waebrania 11:24-27.) Enyi vijana Wakristo, ninyi pia mnahitaji kuazimia kumtumikia Yehova kwa uaminifu. Mkifanya hivyo, mtapata furaha ya kweli, maisha mazuri kabisa sasa, na tumaini la ‘kuushika imara uzima ulio wa kweli.’—1 Tim. 6:19.

20. Katika mbio ya uzima, ni nani wanaopokea zawadi?

20 Katika michezo ya zamani, mkimbiaji mmoja tu ndiye aliyeshinda mashindano ya mbio. Hali ni tofauti katika mbio ya uzima. Ni mapenzi ya Mungu kwamba “watu wa namna zote waokolewe na kupata ujuzi sahihi wa kweli.” (1 Tim. 2:3, 4) Watu wengi walioishi kabla yako wamekimbia kwa mafanikio, na wengi wanaendelea kukimbia pamoja nawe. (Ebr. 12:1, 2) Wote ambao hawachoki watapata zawadi. Kwa hiyo, azimia kushinda!

21. Habari inayofuata itazungumzia nini?

21 Hatuwezi kuepuka “kuja kwa ile siku ya Yehova iliyo kuu na yenye kuogopesha.” (Mal. 4:5) Siku hiyo haipaswi kuzipata familia za Kikristo kwa ghafula. Ni jambo la maana kwa wote katika familia kubeba daraka lao la Kimaandiko. Ni nini kingine unachoweza kufanya ili uendelee kukaa macho kiroho na kutia nguvu uhusiano wako pamoja na Mungu? Habari inayofuata itazungumzia mambo matatu ambayo yanaweza kuisaidia familia nzima iwe na hali njema ya kiroho.

[Maelezo ya Chini]

^ Ona Mnara wa Mlinzi, Novemba 15, 2010 (15/11/2010), ukurasa wa 12-16; Julai 15, 2004, ukurasa wa 21-23.

Umejifunza Nini?

• Kwa nini ni jambo la maana kwa familia za Kikristo kuendelea ‘kukaa macho’?

• Mume anaweza kumwiga jinsi gani yule Mchungaji Mwema?

• Mke ambaye ni mfano mzuri anaweza kufanya nini ili amuunge mkono mume wake?

• Vijana wanaweza jinsi gani kusaidia familia zao kukaa macho kiroho?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 9]

Mwanamume wa kiroho anamthamini sana mke anayemuunga mkono