Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Je, Kweli Unapendezwa na Neno la Mungu?

Je, Kweli Unapendezwa na Neno la Mungu?

Je, Kweli Unapendezwa na Neno la Mungu?

LORRAINE anasema hivi: “Nilipoanza kusoma Biblia kwa ukawaida, niliona jambo hilo kuwa la kidesturi na sikulifurahia. Ilikuwa vigumu kuelewa, kwa hiyo, mara nyingi mawazo yangu yalitangatanga.”

Wengine wanakubali kwamba walipoanza kusoma Biblia wao pia hawakufurahia kuisoma. Hata hivyo, hawakuacha kwa sababu walijua kwamba kusoma Maandiko Matakatifu ni jambo linalofaa. Marc anasema hivi: “Ni rahisi kukengeushwa unaposoma Biblia au unapojifunza kibinafsi. Nilisali na kujitahidi sana ili nifanikiwe kufanya usomaji wa Biblia kila siku uwe sehemu ya ratiba au programu yangu.”

Unaweza kufanya nini ili uthamini zaidi Neno la Mungu lililoandikwa, yaani, Biblia? Unaweza kufanya nini ili ufurahie kuisoma? Fikiria mapendekezo yafuatayo.

Miradi na Njia za Kujifunza

Sali na ukaze fikira unaposoma Biblia. Mwombe Yehova akusaidie kusitawisha hamu ya kujifunza Neno lake. Msihi afungue akili na moyo wako ili uelewe hekima yake kikamili zaidi. (Zab. 119:34) Bila kuwa na mtazamo kama huo, ni rahisi sana kuanza kujifunza Biblia kidesturi tu, na unaweza kupoteza hamu yako ya kuendelea. Lynn anasema hivi: “Nyakati nyingine ninasoma haraka sana na hivyo ninakosa kabisa kuona habari za ziada zenye kupendeza. Mara nyingi, sielewi kikamili mawazo makuu. Hata hivyo, ninasali ili niweze kujizuia na hilo linafanya akili yangu isitange-tange.”

Thamini mambo unayojifunza. Kumbuka kwamba uhai wako unategemea kuelewa na kutumia kweli za Biblia. Kwa hiyo, jitahidi kabisa kupata habari za maana na uzitumie. Chris anasema hivi: “Ninatafuta habari ambazo zinanisaidia kutambua mitazamo na mielekeo mibaya iliyo ndani yangu. Inaburudisha kuona jinsi ambavyo Biblia na vichapo vyetu vingi vina habari ambazo zinanifaidi mimi mwenyewe, hata ingawa sijawahi kamwe kukutana na waandikaji hao.”

Jiwekee miradi unayoweza kufikia. Jaribu kujifunza jambo jipya kuhusu watu wanaotajwa katika Biblia. Unaweza kupata mambo yenye kusisimua kuhusu wengi wao kwa kuchunguza mabuku ya Insight on the Scriptures au Fahirisi. Unapoendelea kuwajua wanaume na wanawake wanaotajwa katika Biblia na kuwaona kuwa watu halisi wenye nyutu na hisia, utafaidika zaidi na mambo unayosoma kuwahusu.

Tafuta njia mpya za kufafanua au kueleza Maandiko. (Mdo. 17:2, 3) Sophia anajifunza akiwa maoni hayo akilini. Anasema hivi: “Tamaa yangu ni kujifunza na kusitawisha njia mpya za kufafanua Maandiko ambazo ninaweza kutumia katika huduma na katika pindi nyingine, ili niweze kueleza waziwazi kweli za Biblia. Gazeti la Mnara wa Mlinzi ni kifaa bora cha kufanya hivyo.”—2 Tim. 2:15.

Wazia au piga picha akilini kuhusu masimulizi ya Biblia. Andiko la Waebrania 4:12 linasema hivi: “Neno la Mungu liko hai.” Unaposoma Maandiko, acha ujumbe wa Mungu uwe halisi katika akili yako kwa kuwazia mambo ambayo watu wanaotajwa katika Biblia walikuwa wakiona. Jaribu kusikia mambo waliyokuwa wakisikia na uhisi jinsi walivyokuwa wakihisi. Husianisha mambo yaliyowapata na hali fulani katika maisha yako. Jifunze kutokana na jinsi walivyoshughulikia hali mbalimbali. Hilo litakusaidia kuelewa vizuri zaidi na kuweka akilini masimulizi ya Biblia.

Tenga wakati wa kuchunguza maandiko magumu na ufafanuzi wake ili uyaelewe vizuri. Tenga wakati mwingi kwa ajili ya kila kipindi cha kujifunza. Huenda ukapata maswali yenye kusisimua sana ambayo yanahitaji ufanye utafiti wa ziada. Angalia maana ya maneno magumu, chunguza maelezo ya chini, na uangalie marejeo ya pambizoni katika Biblia. Kadiri unavyoelewa na kutumia mambo unayosoma, ndivyo utakavyopendezwa zaidi na Neno la Mungu lililoandikwa. Kisha utasema kama mtunga-zaburi alivyosema: “Nimevichukua vikumbusho vyako [Yehova] kuwa ni urithi mpaka wakati usio na kipimo, kwa maana hivyo ni furaha ya moyo wangu.”—Zab. 119:111.

Epuka kupitia habari hiyo haraka-haraka. Uwe na usawaziko kuhusu muda unaotenga kwa ajili ya funzo la kibinafsi. Sawazisha wakati huo na wakati ambao unatumia kutayarisha mikutano ya kutaniko. Raquel anasema hivi: “Mara nyingi ninakuwa na wasiwasi sana hivi kwamba ninashindwa kukaza fikira. Kwa hiyo, ninaona kwamba vipindi vifupi vya kujifunza vina faida. Vinanisaidia kufaidika zaidi na funzo langu.” Chris anasema hivi: “Ninapojifunza haraka-haraka, dhamiri yangu inanisumbua kwa sababu ninakumbuka habari chache sana. Kwa kawaida, habari hiyo haigusi moyo wangu.” Kwa hiyo, tumia muda wa kutosha.

Kuza tamaa kubwa zaidi kwa ajili ya neno la Mungu. Mtume Petro alisema hivi: “Kama watoto wachanga waliozaliwa hivi karibuni, kuzeni tamaa kwa ajili ya maziwa yasiyochanganywa kitu ambayo ni ya lile neno, ili kupitia hayo mkue kufikia wokovu.” (1 Pet. 2:2) Watoto hawahitaji kusitawisha tamaa ya maziwa. Wanazaliwa wakiwa na tamaa hiyo. Lakini Maandiko yanasema kwamba tunapaswa kukuza tamaa kwa ajili ya neno la Mungu. Ukisoma ukurasa mmoja tu wa Biblia kila siku, baada ya muda mfupi utakuwa na tamaa hiyo. Jambo ambalo huenda mwanzoni lilionekana kuwa gumu sana linaweza kuwa lenye kupendeza baada ya muda mfupi.

Tafakari kuhusu masimulizi ya Kimaandiko. Kutafakari pia kuhusu mambo unayosoma kunaleta faida kubwa. Kufanya hivyo kutakusaidia kuona jinsi habari za kiroho ambazo umechunguza zinavyohusiana. Baada ya muda utapata habari za kiroho zinazohusiana ambazo ni kama lulu za kiroho—mali yenye kupendeza.—Zab. 19:14; Met. 3:3.

Muda Unaotumiwa Vizuri

Kuendelea kuwa na mazoea mazuri ya kujifunza kunahitaji jitihada, lakini kunaleta baraka nyingi sana. Na utaelewa vizuri zaidi mambo ya kiroho. (Ebr. 5:12-14) Utambuzi na hekima unayopata kutokana na Maandiko yaliyoongozwa na roho ya Mungu inaleta furaha, hali nzuri, na amani. Hekima inayopatikana katika Neno la Mungu lililoongozwa na roho yake ni “mti wa uzima” kwa wale wanaoipata na kuitumia.—Met. 3:13-18.

Ukijifunza Neno la Mungu kwa undani unaweza kupata moyo wa uelewaji. (Met. 15:14) Hilo litakuwezesha kutoa mashauri yanayotoka moyoni ambayo yanategemea kabisa Biblia. Ukiruhusu maamuzi yako yaongozwe na mambo unayosoma katika Maandiko na katika vichapo vya “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” utafurahia hali yenye kuburudisha na kutia nguvu ambayo inaletwa na Neno la Yehova lililoongozwa na roho yake. (Mt. 24:45) Utakuwa na mtazamo unaofaa zaidi, utakuwa na uhakika zaidi, na utakuwa mtu wa kiroho. Zaidi ya hayo, mambo yote ambayo yanahusu uhusiano wako pamoja na Mungu yatafanikiwa.—Zab. 1:2, 3.

Moyo uliojaa upendo kwa Mungu utakuchochea kushiriki na wengine mambo unayoamini. Hilo pia linaweza kukuridhisha sana. Sophia anajitahidi kukumbuka na kutumia maandiko mbalimbali ili kuvuta uangalifu wa wenye-nyumba na kufanya huduma yake ya Kikristo iwe yenye kusisimua na yenye matokeo. Anasema hivi: “Kuona jinsi watu wanavyoitikia wanaposikia ujumbe wa Biblia kunasisimua.”

Hata hivyo, faida kubwa zaidi ya kupendezwa na Neno la Mungu ni kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova. Kujifunza Biblia kunakuwezesha kujua viwango vyake na kuthamini upendo, ukarimu, na haki yake. Hakuna jambo lingine ambalo ni la maana zaidi au lenye kuthawabisha zaidi kuliko hilo. Jitoe kabisa kujifunza Neno la Mungu kwa moyo wote. Kwa kweli, kufanya hivyo ni kutumia wakati vizuri.—Zab. 19:7-11.

[Sanduku/​Picha katika ukurasa wa 5]

KUSOMA NENO LA MUNGU: MIRADI NA NJIA ZA KUJIFUNZA

▪ Sali na ukaze fikira unaposoma Biblia.

▪ Thamini mambo unayojifunza.

▪ Jiwekee miradi unayoweza kufikia.

▪ Tafuta njia mpya za kufafanua au kueleza Maandiko.

▪ Wazia au piga picha akilini kuhusu masimulizi ya Biblia.

▪ Tenga wakati wa kuchunguza maandiko magumu na ufafanuzi wake ili uyaelewe vizuri.

▪ Epuka kupitia habari hiyo haraka-haraka.

▪ Kuza tamaa kubwa zaidi kwa ajili ya neno la Mungu.

▪ Tafakari kuhusu masimulizi ya Kimaandiko.

[Picha katika ukurasa wa 4]

Unaposoma simulizi fulani la Biblia, jiwazie ukiwa katika hali kama hiyo