Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Kumfuata Kristo, Kiongozi Mkamilifu

Kumfuata Kristo, Kiongozi Mkamilifu

Kumfuata Kristo, Kiongozi Mkamilifu

MARA nyingi wale wanaofuata viongozi wa kibinadamu wanavunjwa moyo. Hata hivyo, wale wanaojitiisha chini ya uongozi wa Kristo wanapata matokeo yaliyo tofauti kabisa. Yesu alisema hivi: “Njooni kwangu, nyote mnaotaabika na kulemewa na mizigo, nami nitawaburudisha ninyi. Chukueni nira yangu na mjifunze kutoka kwangu, kwa maana mimi ni mwenye tabia-pole na mnyenyekevu moyoni, nanyi mtapata burudisho kwa ajili ya nafsi zenu.” (Mt. 11:28, 29) Uongozi wa Yesu ni wenye kuburudisha na kujenga. Anapendezwa sana na watu wa hali ya chini na wanaodharauliwa, na anawaalika wachukue nira yake yenye fadhili. Hata hivyo, ni nini kinachohusika katika kufuata uongozi wa Yesu?

Mtume Petro aliandika hivi: “Kristo aliteseka kwa ajili yenu, akiwaachia ninyi kielelezo ili mfuate hatua zake kwa ukaribu.” (1 Pet. 2:21) Ni jambo la maana kadiri gani kufuata hatua za Yesu? Wazia kwamba uko katika kikundi cha watu ambao wanataka kuvuka eneo lililotegwa mabomu ya ardhini na ni mtu mmoja tu kati yenu ambaye anajua jinsi ya kuvuka eneo hilo kwa usalama. Je, hungefuata hatua zake kwa ukaribu, labda hata kukanyaga mahali anapokanyaga? Vivyo hivyo, ili tuwe na wakati ujao salama ni lazima tufuate mfano wa Yesu katika maisha yetu. Kufanya hivyo kunatia ndani kumsikiliza na kumtii na kushirikiana na wale wanaomwakilisha.

Sikiliza na Utii

Alipokuwa akikaribia mwisho wa Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu alisema hivi: “Kila mtu anayesikia maneno yangu haya na kuyatenda atafananishwa na mtu mwenye busara, aliyejenga nyumba yake juu ya mwamba. Na mvua ikanyesha na mafuriko yakaja na pepo zikavuma na kuipiga nyumba hiyo, lakini haikuporomoka, kwa maana msingi wake ulikuwa umejengwa juu ya mwamba.”—Mt. 7:24, 25.

Hivyo, Yesu alisema kwamba mtu anayemsikiliza na kutii maneno yake ni mwenye “busara.” Je, tunatii kutoka moyoni na hivyo kuonyesha kwamba tunaheshimu na kuthamini mfano wa Kristo, au je, tuna mwelekeo wa kuchagua amri za Kristo ambazo ni rahisi au si vigumu kutii? Yesu alisema: “Sikuzote mimi hufanya mambo yanayompendeza [Mungu].” (Yoh. 8:29) Acheni tujitahidi kuiga mfano huo.

Katika karne ya kwanza, mitume waliweka mfano mzuri wa kujitiisha chini ya uongozi wa Kristo. Pindi moja Petro alimwambia Yesu hivi: “Tazama! Sisi tuliacha vitu vyote na tumekuwa tukikufuata wewe.” (Marko 10:28) Kwa kweli, mitume waliona uongozi wa Yesu kuwa wenye thamani sana hivi kwamba waliacha vitu vingine kwa kupenda ili wamfuate.—Mt. 4:18-22.

Shirikiana na Wale Wanaomwakilisha Kristo

Muda mfupi kabla ya kifo chake, Yesu alitaja njia nyingine ambayo tunaweza kufuata uongozi wake. Alisema hivi: “Yule anayempokea yeyote ninayemtuma hunipokea mimi pia.” (Yoh. 13:20) Kwa kweli, Yesu alisema kwamba wawakilishi wake ambao wametiwa mafuta kwa roho ni “ndugu” zake. (Mt. 25:40) Baada ya Yesu kufufuliwa na kurudi mbinguni, “ndugu” zake waliwekwa rasmi kumwakilisha, ‘wakiwa badala ya Kristo’ kama mabalozi wanaowaalika wengine wapatanishwe na Yehova Mungu. (2 Kor. 5:18-20) Njia moja ambayo tunaonyesha kwamba tunatambua uongozi wa Kristo ni kujitiisha chini ya “ndugu” zake.

Ni vizuri kuchunguza jinsi tunavyoitikia mashauri ya Kimaandiko yanayochapishwa kwa wakati katika vichapo vyetu vinavyotegemea Biblia. Tunapojifunza Maandiko na kuhudhuria mikutano ya kutaniko, tunakumbushwa mafundisho ya Kristo. (2 Pet. 3:1, 2) Tunaonyesha kwamba tunathamini kutoka moyoni maandalizi hayo ya chakula cha kiroho kwa kukitumia kwa ukawaida. Hata hivyo, tunapaswa kuhisi jinsi gani ikiwa mashauri fulani yanarudiwa tena na tena? Kwa mfano, Neno la Mungu linawashauri Wakristo waoe au kuolewa “katika Bwana tu.” (1 Kor. 7:39) Kwa zaidi ya karne moja, habari hiyo imezungumziwa mara kwa mara katika gazeti la Mnara wa Mlinzi. Bila shaka, ndugu za Kristo wanaonyesha kwamba wanajali hali yetu ya kiroho kwa kuchapisha makala kuhusu jambo hilo na mashauri mengine yaliyoongozwa na roho ya Mungu. Kusikiliza vikumbusho hivyo ni njia moja ya kuonyesha kwamba tunamfuata Kiongozi wetu mkamilifu, Yesu Kristo.

Andiko la Methali 4:18 linasema hivi: “Njia ya waadilifu ni kama nuru inayong’aa, inayozidi kuongezeka mpaka mchana mkamilifu.” Ndiyo, uongozi wa Yesu unaendelea kusonga mbele, haujasimama. Njia nyingine ya kushirikiana na “ndugu” za Kristo ni kuwa na mtazamo unaofaa kuhusu marekebisho katika uelewaji wetu wa kweli za Kimaandiko zinazochapishwa na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.”—Mt. 24:45.

Tunaonyesha pia kwamba tunajitiisha chini ya “ndugu” za Kristo kwa kushirikiana na waangalizi waliowekwa rasmi katika kutaniko la Kikristo. Mtume Paulo alisema hivi: “Watiini wale wanaoongoza katikati yenu na mnyenyekee, kwa maana wanaendelea kuzilinda nafsi zenu.” (Ebr. 13:17) Kwa mfano, huenda mzee akatutia moyo kuhusu umuhimu wa kuwa na jioni ya Ibada ya Familia kwa ukawaida au anaweza kutoa mapendekezo kuhusu sehemu fulani ya huduma yetu ya shambani. Mwangalizi anayesafiri anaweza kutupatia mashauri ya Kimaandiko yanayofaa kuhusu sehemu fulani ya maisha yetu ya Kikristo. Tunapotumia mashauri kama hayo kwa kupenda, tunaonyesha kwamba tunamfuata Yesu akiwa Kiongozi wetu.

Inasikitisha kwamba ulimwengu hauna kiongozi anayefaa. Lakini inaburudisha kama nini kufuata uongozi wa Kristo wenye upendo! Acheni tuazimie kabisa kumtii Kiongozi wetu na kushirikiana na wale anaowatumia leo.

[Picha katika ukurasa wa 27]

Je, unakubali mashauri ya Kimaandiko kuhusu kutofungwa nira pamoja na mtu ambaye si mwamini?