Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

“Mwangalizi Mzuri Ajabu na Rafiki Mpendwa”

“Mwangalizi Mzuri Ajabu na Rafiki Mpendwa”

“Mwangalizi Mzuri Ajabu na Rafiki Mpendwa”

JOHN (JACK) BARR, ambaye alitumika akiwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, alikufa Jumamosi asubuhi (Siku ya Posho), Desemba 4, 2010 (4/12/2010) akiwa na tumaini la kwenda mbinguni. Alikuwa na umri wa miaka 97. Wengi wanasema kwamba alikuwa “mwangalizi mzuri ajabu na rafiki mpendwa.”

Ndugu Jack Barr alizaliwa huko Aberdeen, Scotland, akiwa mtoto wa mwisho katika familia ya watoto watatu. Wazazi wake wote wawili walikuwa watiwa-mafuta. Mara nyingi Ndugu Barr alizungumza kwa hisia kuhusu maisha yake ya mapema ya familia; alithamini sana mfano bora kabisa ambao baba na mama yake walimwekea.

Jack alipoingia katika miaka yake ya utineja, ilikuwa vigumu sana kwake kuzungumza na watu asiowajua. Hata hivyo, alijitahidi sana kushinda tatizo hilo, na Jumapili moja alasiri (Siku ya Yenga) mwaka wa 1927, akiwa na umri wa miaka 14, alimwambia baba yake kwamba alikuwa tayari kwenda naye kuhubiri nyumba kwa nyumba. Hivyo ndivyo alivyoanza. Kuanzia siku hiyo mpaka alipokufa, Ndugu Barr aliendelea kuwa mhubiri mwenye bidii wa habari njema.

Aksidenti mbaya sana ambayo karibu imuue mama yake mpendwa ilifanya kijana Jack afikirie kwa uzito kuhusu kusudi la maisha, na mwaka wa 1929 akajiweka wakfu kwa Yehova, na kuonyesha wakfu wake mwaka wa 1934 alipopata nafasi ya kufanya hivyo. Kisha, mwaka wa 1939, akawa mshiriki wa familia ya Betheli huko London, Uingereza. Hivyo, akaanza kazi ya utumishi wa wakati wote ambayo alifanya kwa miaka 71.

Mnamo Oktoba 29, 1960 (29/10/1960), Ndugu Barr aliingia katika uhusiano ambao aliuita “uhusiano wenye thamani kubwa sana” alipomwoa Mildred Willet, ambaye alikuwa ametumika kwa miaka mingi akiwa painia na mmishonari mwenye bidii. Ndugu na Dada Barr walijulikana kuwa wenzi wa ndoa wenye mfano mzuri ambao walikuwa wamejitoa, na waliendelea kuwa hivyo mpaka Mildred alipokufa Oktoba mwaka wa 2004. Ndugu na Dada Barr walisoma sehemu ya Biblia pamoja kila siku kwa muda wote wa maisha yao ya ndoa.

Kwa wale waliomjua, jina Jack Barr litawakumbusha kuhusu mwanamume ambaye alitoa mashauri yenye hekima—ambayo kila wakati yalikuwa yenye usawaziko, yenye fadhili, na yaliyotegemea kabisa Maandiko. Alikuwa mfanyakazi mwenye bidii na mwangalizi anayejali na mwenye upendo na vilevile rafiki mshikamanifu. Maelezo yake, hotuba zake, na sala zake zilifunua jinsi alivyopenda kweli sana na pia uhusiano wake wa karibu pamoja na Yehova.

Ingawa tutamkosa sana Ndugu yetu mpendwa Barr, tunashangilia pamoja naye kwa sababu amepokea zawadi ya uhai usioweza kufa—pendeleo ambalo alitazamia kwa hamu na kulizungumzia mara nyingi. Ndilo jambo pekee ambalo alitazamia kwa hamu.—1 Kor. 15:53, 54. *

[Maelezo ya Chini]

^ Unaweza kupata simulizi la maisha ya John E. Barr katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Julai 1, 1987, ukurasa wa 26-31.