Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Ni Nani Mtu wa Maana Zaidi Katika Maisha Yako?

Ni Nani Mtu wa Maana Zaidi Katika Maisha Yako?

Ni Nani Mtu wa Maana Zaidi Katika Maisha Yako?

“Wewe peke yako ndiye Uliye Juu Zaidi, juu ya dunia yote.”—ZAB. 83:18.

1, 2. Kuhusu wokovu wetu sisi wenyewe, kwa nini haitoshi tu kulijua jina la Yehova?

 LABDA uliona jina la Yehova kwa mara ya kwanza wakati ulipoonyeshwa jina hilo kwenye Zaburi 83:18. Huenda ulishangaa uliposoma maneno haya: “Ili watu wajue kwamba wewe, ambaye jina lako ni Yehova, wewe peke yako ndiye Uliye Juu Zaidi, juu ya dunia yote.” Tangu wakati huo, bila shaka umetumia andiko hilohilo ili kuwasaidia wengine kumjua Mungu wetu mwenye upendo, Yehova.—Rom. 10:12, 13.

2 Ingawa ni jambo la maana kwa watu kulijua jina la Yehova, ujuzi huo peke yake hautoshi. Ona jinsi mtunga-zaburi anavyokazia ukweli mwingine wa maana ambao unahusu wokovu wetu anaposema hivi: “Wewe peke yako ndiye Uliye Juu Zaidi, juu ya dunia yote.” Ndiyo, Yehova ndiye Mtu wa maana zaidi katika ulimwengu wote. Akiwa Muumba wa vitu vyote, ana haki ya kutazamia viumbe wake wote wajitiishe kikamili kwake. (Ufu. 4:11) Hivyo basi, tuna sababu nzuri ya kujiuliza, ‘Ni nani mtu wa maana zaidi katika maisha yangu?’ Ni jambo la maana sana kuchunguza kwa uangalifu jibu letu kwa swali au ulizo hilo!

Suala Katika Bustani ya Edeni

3, 4. Shetani alifanikiwa kumdanganya Hawa jinsi gani, na matokeo yalikuwa nini?

3 Mambo yaliyotukia zamani katika bustani ya Edeni yanaonyesha waziwazi uzito wa swali hilo. Katika bustani hiyo, malaika mwasi ambaye baadaye aliitwa Shetani Ibilisi alimshawishi mwanamke wa kwanza, Hawa, atangulize tamaa zake mwenyewe badala ya kutii amri ya Yehova ya kutokula tunda la mti fulani. (Mwa. 2:17; 2 Kor. 11:3) Alishindwa na kishawishi hicho na hivyo akakosa kuheshimu enzi kuu ya Yehova. Hawa hakumtambua Yehova kuwa Mtu wa maana zaidi katika maisha yake. Lakini Shetani alifanikiwa jinsi gani kumdanganya Hawa?

4 Shetani alitumia njia mbalimbali za ujanja katika mazungumzo yake pamoja na Hawa. (Soma Mwanzo 3:1-5.) Kwanza, Shetani hakutumia jina la kibinafsi la Yehova. Alitumia tu neno “Mungu.” Kinyume na hilo, mwandikaji wa kitabu cha Mwanzo alitumia jina la kibinafsi la Yehova katika mstari wa kwanza wa sura hiyo. Pili, badala ya kusema kuhusu “amri” ya Mungu, Shetani aliuliza tu kuhusu yale ambayo Mungu “alisema.” (Mwa. 2:16) Kupitia njia hiyo ya ujanja, huenda Shetani alijaribu kupunguza uzito wa amri hiyo. Tatu, ingawa alikuwa akizungumza na Hawa peke yake, Shetani alitumia neno “nanyi” ambalo linawakilisha nafsi katika hali ya wingi. Kwa kufanya hivyo, huenda alijaribu kuchochea kiburi cha Hawa, huku akijitahidi kumfanya ajione kuwa mtu wa maana, kana kwamba Hawa alikuwa msemaji wake mwenyewe na pia wa mume wake. Matokeo yakawa nini? Ni wazi kwamba, kwa kimbelembele Hawa aliamua kusema kwa ajili yake na kwa ajili ya mume wake kwa kumwambia nyoka hivi: “Tunaweza kula matunda ya miti ya bustani.”

5. (a) Shetani alifanikiwa kumfanya Hawa aanze kukazia fikira nini? (b) Hawa alionyesha nini kwa kula tunda lililokatazwa?

5 Pia, Shetani alipotosha ukweli. Alidai kwamba Mungu hakutenda kwa haki kwa kuwakataza Adamu na Hawa ‘wasile matunda ya kila mti wa bustani.’ Kisha, Shetani alimfanya Hawa aanze kujifikiria mwenyewe na jinsi ambavyo angefanya maisha yake yawe eti mazuri zaidi na kuwa “kama Mungu.” Mwishowe, alifaulu kumfanya Hawa aanze kufikiria ule mti na matunda yake badala ya kufikiria uhusiano wake pamoja na Yule aliyempa kila kitu. (Soma Mwanzo 3:6.) Inasikitisha kwamba kwa kula lile tunda, Hawa alionyesha kwamba Yehova hakuwa Mtu wa maana zaidi katika maisha yake.

Suala Katika Siku za Ayubu

6. Shetani alitilia shaka jinsi gani maisha ya Ayubu ya utimilifu, na hivyo Ayubu alipewa nafasi gani?

6 Karne nyingi baadaye, mwanamume mwaminifu Ayubu alipata nafasi ya kuonyesha ni nani aliyekuwa Mtu wa maana zaidi katika maisha yake. Yehova alipomwambia Shetani kuhusu jinsi Ayubu alivyoishi maisha ya utimilifu, Shetani alijibu hivi kwa hasira: “Je, Ayubu amemwogopa Mungu bure?” (Soma Ayubu 1:7-10.) Shetani hakupinga kwamba Ayubu alimtii Mungu. Badala yake, alitilia shaka nia ya Ayubu. Kwa ujanja alidai kwamba Ayubu anamtumikia Yehova kwa sababu ya faida za kichoyo bali si kwa sababu anampenda. Ayubu tu ndiye angeweza kujibu shtaka hilo, na alipewa nafasi ya kufanya hivyo.

7, 8. Ayubu alipambana na majaribu gani, na alionyesha nini alipovumilia kwa uaminifu?

7 Yehova alimruhusu Shetani amshambulie Ayubu kwa misiba iliyofuatana, mmoja baada ya mwingine. (Ayu. 1:12-19) Ayubu alitenda jinsi gani kwa sababu ya mabadiliko hayo? Tunaambiwa kwamba “hakutenda dhambi, wala kumhesabia Mungu jambo lolote lisilofaa.” (Ayu. 1:22) Lakini bado Shetani hakunyamaza. Aliendelea kulalamika hivi: “Ngozi kwa ngozi, na kila kitu alicho nacho mtu atakitoa kwa ajili ya nafsi yake.” * (Ayu. 2:4) Shetani alidai kwamba ikiwa Ayubu mwenyewe angeteseka, hangemwona Yehova kuwa Mtu wa maana zaidi katika maisha yake.

8 Mwili wa Ayubu uliharibiwa sana na ugonjwa wenye kuchukiza na kisha mke wake akamkaza sana amlaani Mungu na kufa. Baadaye, wafariji watatu wa uwongo walidai kwamba alikuwa na mwenendo mbaya. (Ayu. 2:11-13; 8:2-6; 22:2, 3) Hata hivyo, katika mateso yake yote, Ayubu alikataa kukana utimilifu wake. (Soma Ayubu 2:9, 10.) Alivumilia kwa uaminifu na hivyo kuonyesha kwamba Yehova alikuwa Mtu wa maana zaidi katika maisha yake. Pia, Ayubu alionyesha kwamba mwanadamu asiye mkamilifu anaweza kujibu, hata kwa kiasi kidogo, mashtaka ya uwongo ya Ibilisi.—Linganisha na Methali 27:11.

Jibu Kamilifu la Yesu

9. (a) Shetani alijaribu jinsi gani kumshawishi Yesu kwa kutumia tamaa yake ya mwili? (b) Yesu alitenda jinsi gani alipojaribiwa?

9 Muda mfupi baada ya Yesu kubatizwa, Shetani alijaribu kumshawishi afuatie tamaa za kichoyo badala ya kuendelea kumwona Yehova kuwa Mtu wa maana zaidi katika maisha yake. Ibilisi alimjaribu Yesu kwa njia tatu. Kwanza, alijaribu kuchochea tamaa yake ya mwili kwa kumshawishi Yesu ageuze mawe yawe mkate. (Mt. 4:2, 3) Yesu alikuwa ametoka tu kufunga kwa muda wa siku 40 na alikuwa na njaa sana. Kwa hiyo, Ibilisi alimhimiza atumie vibaya nguvu zake za kufanya miujiza ili kutosheleza njaa yake. Yesu alitenda jinsi gani? Tofauti na Hawa, Yesu alikazia fikira Neno la Yehova na papo hapo akapinga jaribu hilo.—Soma Mathayo 4:4.

10. Kwa nini Shetani alimshawishi Yesu alijitupe kutoka juu ya mnara wa hekalu?

10 Pia, Shetani alijaribu kumshawishi Yesu atende kwa kichoyo. Alimshawishi Yesu ajitupe kutoka juu ya mnara wa hekalu. (Mt. 4:5, 6) Shetani alitaka kutimiza nini? Shetani alidai kwamba ikiwa Yesu hangeumia baada ya kuanguka, hilo lingeonyesha kwamba alikuwa “mwana wa Mungu.” Bila shaka, Ibilisi alitaka Yesu ahangaikie sana sifa yake mwenyewe, hata kufikia hatua ya kuonyesha uwezo wake. Shetani alijua kwamba mtu anaweza kukubali kufanya jambo hatari kama hilo kwa sababu ya kiburi na tamaa ya kutaka kuheshimiwa na wengine. Shetani alitumia vibaya andiko fulani, lakini Yesu alionyesha kwamba Alielewa kikamili Neno la Yehova. (Soma Mathayo 4:7.) Yesu alipopinga jaribu hilo alionyesha kwamba Yehova ni Mtu wa maana zaidi katika maisha yake.

11. Kwa nini Yesu alikataa toleo la Ibilisi la falme zote za ulimwengu?

11 Katika jaribu lake la mwisho kabisa, Shetani alitaka kumpa Yesu falme zote za ulimwengu. (Mt. 4:8, 9) Yesu alikataa papo hapo toleo hilo. Alitambua kwamba kukubali toleo hilo kungemaanisha kuwa anakataa enzi kuu ya Yehova, yaani, haki ya Mungu ya kuwa Aliye Juu Zaidi. (Soma Mathayo 4:10.) Katika kila jaribu, Yesu alimjibu Shetani kwa kunukuu au kutaja maandiko ambayo yalikuwa na jina la kibinafsi la Yehova.

12. Ni uamuzi gani mgumu ambao Yesu alipaswa kufanya alipokaribia mwisho wa maisha yake duniani, na tunajifunza nini kutokana na jinsi alivyohisi kuhusu uamuzi huo?

12 Alipokaribia mwisho wa maisha yake duniani, Yesu alipaswa kufanya uamuzi mgumu sana. Katika huduma yake yote, alionyesha kwamba alikuwa tayari kutoa uhai wake kuwa dhabihu. (Mt. 20:17-19, 28; Luka 12:50; Yoh. 16:28) Hata hivyo, Yesu alitambua pia kwamba angeshtakiwa kwa uwongo na kuhukumiwa chini ya mfumo wa sheria wa Kiyahudi na kuuawa kama mtu aliyekufuru. Aliteseka sana kwa sababu ya shtaka hilo la uwongo ambalo lingefanya auawe. Alisali hivi: “Baba yangu, ikiwezekana, kikombe hiki na kipitilie mbali kutoka kwangu.” Hata hivyo, aliendelea kusema hivi: “Lakini, si kulingana na mapenzi yangu, bali kulingana na mapenzi yako.” (Mt. 26:39) Ndiyo, bila shaka yoyote, uaminifu wa Yesu mpaka kifo ulionyesha ni nani aliyekuwa Mtu wa maana zaidi katika maisha yake!

Jibu Letu kwa Swali Hilo

13. Kufikia hapa, ni masomo gani ambayo tumejifunza kutokana na mfano wa Hawa, Ayubu, na Yesu Kristo?

13 Tumejifunza nini kufikia hapa? Katika kisa cha Hawa, tunajifunza kwamba wale wanaoshindwa na tamaa za kichoyo au hisia za kujiona kuwa watu wa maana sana wanafunua kwamba Yehova si Mtu wa maana zaidi katika maisha yao. Kinyume na hilo, kutokana na maisha ya Ayubu ya kushika utimilifu, tunajifunza kwamba hata wanadamu wasio wakamilifu wanaweza kuonyesha kuwa wanamtanguliza Yehova kwa kuvumilia kwa uaminifu matatizo, hata wakati ambapo hawaelewi kikamili chanzo cha matatizo hayo. (Yak. 5:11) Mwishowe, mfano wa Yesu unatufundisha tuwe tayari kuaibishwa au kufedheheshwa na kutojiona wenyewe kuwa watu wa maana sana. (Ebr. 12:2) Lakini tunaweza kutumia jinsi gani masomo hayo?

14, 15. Tofauti na Hawa, Yesu alikabiliana jinsi gani na majaribu, na tunaweza kumwiga namna gani? (Toa maelezo kuhusu picha iliyo kwenye ukurasa wa 18.)

14 Usiruhusu kamwe vishawishi vifanye umsahau Yehova. Hawa aliruhusu macho yake yavutiwe na kishawishi kilichokuwa mbele yake. Aliona kwamba tunda hilo ‘lilikuwa zuri kwa chakula na kwamba lilikuwa kitu cha kutamanika kwa macho, ndiyo, mti huo ulikuwa wenye kupendeza kuutazama.’ (Mwa. 3:6) Ni tofauti kama nini na jinsi Yesu alivyotenda alipojaribiwa mara tatu! Kila mara, hakukazia fikira tu jaribu, aliona kwa mbali matokeo ya matendo yake. Alitegemea Neno la Mungu na pia alitumia jina la Yehova.

15 Tunaposhawishiwa kufanya mambo yasiyompendeza Yehova, tunakazia fikira zetu juu ya nini? Kadiri tunavyozidi kukazia fikira kishawishi, ndivyo tamaa mbaya inavyokuwa yenye nguvu zaidi. (Yak. 1:14, 15) Tunahitaji kuchukua hatua ya haraka ili kung’oa tamaa hiyo, hata ikiwa hatua hiyo huenda ikaonekana kuwa kali, kama vile kuondoa kiungo fulani cha mwili wetu. (Mt. 5:29, 30) Kama Yesu, tunahitaji kukazia fikira matokeo ya matendo yetu, yaani, jinsi yatakavyokuwa na uvutano juu ya uhusiano wetu pamoja na Yehova. Ni lazima tukumbuke yale ambayo Neno lake, Biblia, linasema. Ni katika njia hiyo tu tunaweza kuonyesha kwamba Yehova ndiye Mtu wa maana zaidi katika maisha yetu.

16-18. (a) Ni nini kinachoweza kutufanya tuvunjike moyo? (b) Ni nini kitakachotusaidia kuvumilia hali ngumu?

16 Usiruhusu kamwe misiba inayokupata ifanye uwe mwenye uchungu kumwelekea Yehova. (Met. 19:3) Tunapozidi kukaribia mwisho wa ulimwengu huu mwovu, watu wengi wa Yehova wanazidi kupatwa na misiba ya asili na misiba mingine. Hatutazamii kulindwa kimuujiza wakati huu. Hata hivyo, kama Ayubu, huenda tukavunjika moyo wakati wapendwa wetu wanapokufa au tunapopatwa na matatizo ya kibinafsi.

17 Ayubu hakuelewa kwa nini Yehova aliruhusu mambo fulani yatukie, na nyakati nyingine huenda pia tusielewe kwa nini mambo mabaya yanatukia. Labda tumesikia kuhusu ndugu fulani waaminifu ambao walikufa katika tetemeko la nchi, kama vile huko Haiti, au katika msiba mwingine wa asili. Au huenda tunamjua ndugu au dada fulani aliyeshika utimilifu ambaye alitendewa kijeuri au kufa katika aksidenti mbaya. Au tunaweza hata kujikuta katika hali fulani ngumu sana au kuona kwamba tunatendewa isivyo haki. Huenda mioyo yetu yenye huzuni ikatufanya tuulize hivi kwa uchungu: ‘Kwa nini, Yehova. Kwa nini ni mimi? Nilifanya jambo gani baya?’ (Hab. 1:2, 3) Ni nini kitakachotusaidia kuvumilia katika nyakati kama hizo?

18 Tunahitaji kuwa waangalifu ili tusifikiri kwamba matukio kama hayo yanaonyesha kuwa hatuna kibali cha Yehova. Yesu alikazia ukweli huo alipozungumza kuhusu misiba miwili iliyotukia katika siku zake. (Soma Luka 13:1-5.) Misiba mingi inasababishwa na “wakati na tukio lisilotazamiwa.” (Mhu. 9:11) Lakini hata matatizo yetu yawe yanasababishwa na nini, tunaweza kuvumilia ikiwa tunamkazia fikira “Mungu wa faraja yote.” Atatupatia nguvu tunazohitaji ili kuendelea kuwa waaminifu.—2 Kor. 1:3-6.

19, 20. Ni nini kilichomsaidia Yesu kuvumilia hali zenye kufedhehesha, na ni nini kinachoweza kutusaidia kufanya hivyo?

19 Usiruhusu kamwe kiburi au kuogopa kuaibishwa kuwe jambo la maana zaidi kwako. Unyenyekevu wa Yesu ulimwezesha ‘kujiondolea mwenyewe hali yake na kuchukua umbo la mtumwa.’ (Flp. 2:5-8) Aliweza kuvumilia hali nyingi zenye kufedhehesha kwa sababu alimtegemea Yehova. (1 Pet. 2:23, 24) Kwa kufanya hivyo, Yesu alitanguliza mapenzi ya Yehova, na matokeo yalikuwa kwamba alipandishwa kwenye cheo cha juu zaidi. (Flp. 2:9) Yesu alipendekeza wanafunzi wake wafuate njia hiyohiyo ya maisha.—Mt. 23:11, 12; Luka 9:26.

20 Nyakati nyingine, majaribu fulani ya imani yetu yanaweza kusababisha aibu. Hata hivyo, tunapaswa kuwa na uhakika kama mtume Paulo, aliyeandika hivi: “Kwa sababu hii ninavumilia pia mambo haya, lakini sioni aibu. Kwa maana namjua yule ambaye nimemwamini, nami nina hakika anaweza kukilinda kile ambacho nimeweka amana kwake mpaka siku ile.”—2 Tim. 1:12.

21. Ingawa ulimwengu una mtazamo wa kichoyo, umeazimia kufanya nini?

21 Biblia ilitabiri kwamba katika wakati wetu watu wangekuwa “wenye kujipenda wenyewe.” (2 Tim. 3:2) Haishangazi kwamba tunazungukwa na kizazi cha watu wanaojifikiria tu. Na tusichafuliwe kamwe na mtazamo kama huo wa kichoyo! Badala yake, iwe tunapambana na kishawishi, misiba, au tunakabiliana na watu wanaojaribu kufanya tuaibike, acheni kila mmoja wetu aazimie kuonyesha kwamba kwa kweli Yehova ndiye Mtu wa maana zaidi katika maisha yetu!

[Maelezo ya Chini]

^ Wasomi fulani wa Biblia wanafikiri kwamba huenda maneno “ngozi kwa ngozi” yanamaanisha kwamba Ayubu angekuwa tayari kuruhusu kwa uchoyo watoto na wanyama wake wapoteze ngozi zao, au uhai, ikiwa tu yeye angeendelea kuwa na ngozi yake, au uhai. Wengine wanafikiri maneno hayo yanakazia kwamba mtu angekuwa tayari kupoteza sehemu fulani ya ngozi ikiwa hilo lingemaanisha kuokoa uhai wake. Kwa mfano, mtu anaweza kuinua mkono wake ili ajikinge asipigwe kichwa, na hivyo kupoteza sehemu fulani ya ngozi yake. Haidhuru maneno hayo ya mfano yana maana gani, bila shaka yanamaanisha kwamba Ayubu alikuwa tayari kutoa kila kitu ili aendelee kuwa hai.

Tunaweza Kujifunza Nini Kutokana na . . .

• jinsi Shetani alivyomdanganya Hawa?

• jinsi Ayubu alivyotenda alipopatwa na misiba?

• jambo kuu ambalo Yesu alikazia fikira?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 17]

Hawa alishindwa kukazia fikira uhusiano wake pamoja na Yehova

[Picha katika ukurasa wa 18]

Yesu alipinga majaribu ya Shetani na akakazia fikira kufanya mapenzi ya Yehova

[Picha katika ukurasa wa 20]

Kuhubiri ndani ya mahema baada ya tetemeko la nchi huko Haiti

Katika nyakati za taabu, tunaweza kumkazia fikira “Mungu wa faraja yote”