Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Je, Vijana Wanapaswa Kubatizwa?

Je, Vijana Wanapaswa Kubatizwa?

Je, Vijana Wanapaswa Kubatizwa?

“NINAFURAHI sana kwamba binti yangu sasa ni mtumishi wa Yehova, ninajua kuwa yeye pia anafurahi,” akasema Carlos, * baba Mkristo huko Ufilipino. Baba mwingine kutoka Ugiriki aliandika hivi: “Mimi na mke wangu tunafurahi kwamba watoto wetu watatu walibatizwa na kuwa Mashahidi wa Yehova walipokuwa wakibalehe. Wanafanya maendeleo ya kiroho na wanafurahia kumtumikia Yehova.”

Wazazi Wakristo wana sababu ya kushangilia wakati watoto wao wanapobatizwa, lakini nyakati nyingine wanashangilia na wakati uleule wanakuwa na wasiwasi. Mama mmoja alisema hivi: “Nilikuwa na furaha nyingi na pia wasiwasi mwingi.” Kwa nini mama huyo alifurahi na pia kuwa na wasiwasi? “Nilijua kwamba mwana wangu sasa alikuwa na daraka kamili mbele za Yehova.”

Vijana wote wanapaswa kuwa na mradi wa kumtumikia Yehova wakiwa Mashahidi wake waliobatizwa. Hata hivyo, huenda wazazi wanaomwogopa Mungu wakajiuliza, ‘Ninajua kwamba mtoto wangu amefanya maendeleo mazuri, lakini je, ana nguvu za kutosha kushinda mikazo ya upotovu wa maadili na kubaki safi mbele za Yehova?’ Huenda wazazi wengine wakajiuliza, ‘Je, mtoto wangu ataendelea kumtumikia Mungu kwa shangwe na bidii hata akishawishiwa kufuatia vitu vya kimwili?’ Hivyo basi, ni mwongozo gani wa Biblia unaoweza kuwasaidia wazazi kujua ikiwa watoto wao wako tayari kubatizwa?

Kuwa Mwanafunzi wa Kristo Ni Takwa la Maana Zaidi

Badala ya kutaja umri fulani ambao mtu anapaswa kubatizwa, Neno la Mungu linaeleza kuhusu hali ya kiroho ya wale ambao wanastahili kuchukua hatua hiyo. Yesu aliwaagiza wafuasi wake hivi: ‘Mfanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, mkiwabatiza.’ (Mt. 28:19) Hivyo, wale wanaopaswa kubatizwa ni wale ambao tayari ni wanafunzi wa Kristo.

Mwanafunzi ni nani? Kitabu Insight on the Scriptures (Étude perspicace des Écritures) kinaeleza hivi: “Neno hilo linawahusu hasa wale wote ambao hawaamini tu mafundisho ya Kristo bali pia wanayafuata kwa ukaribu.” Je, vijana wenye umri mdogo wanaweza kuwa wanafunzi wa kweli wa Kristo? Dada mmoja ambaye ametumika akiwa mmishonari huko Amerika ya Latini kwa miaka zaidi ya 40 anaandika hivi kujihusu na kuhusu dada zake wawili: “Tulikuwa na umri wa kutosha kujua kwamba tulitaka kumtumikia Yehova na kuishi katika Paradiso. Wakfu wetu ulitusaidia kuwa na nguvu tulipopambana na vishawishi vya ujanani. Hatujuti kwamba tulijiweka wakfu kwa Mungu tukiwa na umri mdogo.”

Unaweza kujua jinsi gani ikiwa mtoto wako amekuwa mwanafunzi wa Kristo? Biblia inasema hivi: “Kwa matendo yake, mvulana hujitambulisha kama utendaji wake ni safi na mnyoofu.” (Met. 20:11) Fikiria mazoea fulani ambayo yanaonyesha kwamba kijana anafanya ‘maendeleo yake yawe wazi’ akiwa mwanafunzi.—1 Tim. 4:15.

Mambo Yanayoonyesha Kwamba Mtoto Ni Mwanafunzi wa Kristo

Je, mtoto wako anakutii? (Kol. 3:20) Je, anafanya kazi ambazo amegawiwa afanye nyumbani? Biblia inasema hivi kumhusu Yesu akiwa na umri wa miaka 12: “Akaendelea kujitiisha [kwa wazazi wake].” (Luka 2:51) Bila shaka, leo hakuna mtoto ambaye anaweza kuwatii wazazi wake kikamilifu. Lakini Wakristo wa kweli wanapaswa ‘kufuata hatua za Yesu kwa ukaribu.’ Kwa hiyo, vijana ambao wangependa kubatizwa wanapaswa kujulikana kuwa vijana wanaowatii wazazi wao.—1 Pet. 2:21.

Fikiria maswali au maulizo yanayofuata: Je, mtoto wako ‘anaendelea kuutafuta kwanza Ufalme’ kwa kushiriki katika huduma? (Mt. 6:33) Je, yuko tayari kuwahubiria wengine habari njema, au ni lazima umhimize sana ili aende katika utumishi wa shambani na kuhubiri milangoni? Je, anajitahidi kutimiza daraka lake akiwa mhubiri ambaye hajabatizwa? Je, anatamani kuwarudia watu wanaopendezwa ambao anakutana nao katika eneo? Je, anawajulisha walimu na wanafunzi wenzake kwamba yeye ni Shahidi wa Yehova?

Je, kuhudhuria mikutano ya kutaniko ni jambo la maana kwake? (Zab. 122:1) Je, anafurahia kutoa maelezo katika Funzo la Mnara wa Mlinzi na Funzo la Biblia la Kutaniko? Je, anashiriki kwa uchangamfu katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi?—Ebr. 10:24, 25.

Je, mtoto wako anajitahidi kubaki safi kimaadili kwa kuepuka mashirika mabaya shuleni na sehemu nyingine? (Met. 13:20) Anapendelea muziki, sinema, vipindi vya televisheni, na michezo ya video ya aina gani, na anatumia Intaneti jinsi gani? Je, maneno na matendo yake yanaonyesha kwamba anataka kuishi kulingana na viwango vya Biblia?

Mtoto wako anaijua Biblia vizuri kadiri gani? Je, anaweza kueleza kwa maneno yake mwenyewe mambo anayojifunza katika jioni ya Ibada ya Familia? Je, anaweza kueleza kweli za msingi za Biblia? (Met. 2:6-9) Je, anafurahia kusoma Biblia na kujifunza vichapo vya jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara? (Mt. 24:45) Je, anauliza maswali kuhusu mafundisho na mistari ya Biblia?

Maswali hayo yanaweza kukusaidia kupima maendeleo ya kiroho ya mtoto wako. Baada ya kuyachunguza, huenda ukaamua kwamba anapaswa kufanya maendeleo katika mambo fulani kabla ya kubatizwa. Hata hivyo, ikiwa maisha yake yanaonyesha kwamba yeye ni mwanafunzi na kwamba kwa kweli ameweka maisha yake wakfu kwa Mungu, unaweza kuamua kumruhusu abatizwe.

Vijana Wanaweza Kumsifu Yehova

Watumishi wengi wa Mungu walionyesha uaminifu na ushikamanifu wakati wa kubalehe au wakiwa na umri mdogo zaidi. Mfikirie Yosefu, Samweli, Yosia, na Yesu. (Mwa. 37:2; 39:1-3; 1 Sam. 1:24-28; 2:18-20; 2 Nya. 34:1-3; Luka 2:42-49) Na ni wazi kwamba binti wanne wa Filipo, ambao walikuwa wakitoa unabii, walizoezwa vizuri tangu utotoni.—Mdo. 21:8, 9.

Shahidi mmoja huko Ugiriki alisema hivi: “Nilibatizwa nikiwa na umri wa miaka 12. Sijawahi kamwe kujuta kwa sababu ya uamuzi wangu. Sasa, miaka 24 imepita, na miaka 23 kati ya miaka hiyo nimeshiriki katika utumishi wa wakati wote. Upendo wangu kwa Yehova ulinisaidia sikuzote kupambana na matatizo ya ujanani. Nikiwa na umri wa miaka 12, sikujua Maandiko kama ninavyoyajua sasa. Lakini nilijua kwamba nilimpenda Yehova na nilitaka kumtumikia milele. Ninafurahi kwamba amenisaidia kuendelea katika utumishi wake.”

Iwe mtu ni kijana au ana umri mkubwa, akionyesha wazi kwamba ni mwanafunzi wa kweli wa Kristo anapaswa kubatizwa. Mtume Paulo aliandika hivi: “Kwa moyo mtu huonyesha imani kwa ajili ya uadilifu, lakini kwa kinywa mtu hufanya tangazo la hadharani kwa ajili ya wokovu.” (Rom. 10:10) Kijana ambaye ni mwanafunzi wa Kristo anapochukua hatua muhimu ya kubatizwa, yeye na wazazi wake wanatimiza mradi wa maana sana. Usiache kitu chochote kikuzuie wewe au watoto wako kupata shangwe iliyo mbele yenu.

[Maelezo ya Chini]

^ Baadhi ya majina yamebadilishwa.

[Sanduku katika ukurasa wa 5]

Maoni Yanayofaa Kuhusu Ubatizo

Wazazi fulani wanaona kwamba ubatizo wa watoto wao ni hatua yenye faida ambayo ni hatari kwa njia fulani, kama vile kupata leseni au cheti cha kuendesha gari. Lakini je, ubatizo na utumishi mtakatifu unahatarisha kwa njia yoyote mafanikio ya mtu ya wakati ujao? Jibu la Biblia ni hapana. Andiko la Methali 10:22 linasema: “Baraka ya Yehova—hiyo ndiyo hutajirisha, naye haongezi maumivu pamoja nayo.” Naye Paulo alimwandikia hivi kijana Timotheo: “Kwa hakika, huo ni njia ya kupata faida kubwa, huu ujitoaji-kimungu pamoja na ujitoshelevu.”—1 Tim. 6:6.

Ni kweli kwamba kumtumikia Yehova si jambo rahisi. Yeremia alipata matatizo mengi katika kazi yake akiwa nabii wa Mungu. Hata hivyo, aliandika hivi kuhusu ibada aliyomtolea Mungu wa kweli: “Neno lako linakuwa kwangu furaha na kushangilia kwa moyo wangu; kwa maana jina lako limeitwa juu yangu, Ee Yehova Mungu wa majeshi.” (Yer. 15:16) Yeremia alijua kwamba utumishi wa Mungu ndio uliomletea shangwe. Ulimwengu wa Shetani unasababisha matatizo. Wazazi wanahitaji kuwasaidia watoto wao kutambua tofauti hiyo.—Yer. 1:19.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 6]

Je, Mtoto Wangu Anapaswa Kungoja Wakati Upite Kabla ya Kubatizwa?

Nyakati nyingine, hata watoto wanapostahili kubatizwa, wazazi wao wanaweza kuamua watoto wangoje wakati upite kabla ya kubatizwa. Huenda wakatoa sababu gani?

Ninaogopa kwamba mtoto wangu akibatizwa, huenda baadaye akaanguka katika dhambi nzito na kutengwa na ushirika. Je, ni jambo la hekima kuamini kwamba kijana anayekataa kubatizwa hatatozwa hesabu na Mungu kwa ajili ya mwenendo wake? Sulemani aliwaambia vijana maneno yafuatayo: “Ujue kwamba kwa ajili ya mambo yote hayo [matendo yako], Mungu wa kweli atakuleta hukumuni.” (Mhu. 11:9) Naye Paulo alitoa kikumbusho hiki kwa watu wa kila umri: “Kila mmoja wetu atatoa hesabu kwa Mungu kwa ajili yake mwenyewe.”—Rom. 14:12.

Waabudu waliobatizwa na wale ambao hawajabatizwa watatoa hesabu mbele za Mungu. Usisahau kwamba Yehova anawalinda watumishi wake kwa ‘kutoacha wajaribiwe kupita wanavyoweza kuhimili.’ (1 Kor. 10:13) Maadamu watumishi hao ‘wanatunza akili zao’ na kupambana na kishawishi, wanaweza kuwa na hakika kwamba Mungu atawategemeza. (1 Pet. 5:6-9) Mama mmoja Mkristo anaandika hivi: “Watoto ambao wamebatizwa wana sababu nyingi za kuepuka mambo mabaya ya ulimwengu. Mwana wangu, aliyebatizwa akiwa na umri wa miaka 15, anahisi kwamba ubatizo ni ulinzi. Alisema hivi: ‘Hufikirii kufanya jambo ambalo ni kinyume cha sheria ya Yehova.’ Ubatizo ni kichocheo chenye nguvu cha kutenda uadilifu.”

Ikiwa umewazoeza watoto wako kumtii Yehova kwa maneno na mfano wako, unaweza kuwa na hakika kwamba wataendelea kufanya hivyo baada ya kubatizwa. Andiko la Methali 20:7 linasema: “Mwadilifu anatembea kwa utimilifu wake. Wanawe watakuwa na furaha baada yake.”

Ningependa kumwona mtoto wangu akitimiza miradi fulani kwanza. Vijana wanapaswa kujifunza kufanya kazi ili, baada ya muda, waweze kutimiza mahitaji yao. Lakini kuna hatari ya kuwatia moyo kufuatia maisha yanayokazia elimu na kupata usalama wa kifedha badala ya ibada ya kweli. Yesu alisema hivi kuhusu neno la Ufalme au “mbegu” ambayo haikui: “Na yule aliyepandwa katikati ya miiba, huyo ndiye anayelisikia neno, lakini mahangaiko ya mfumo huu wa mambo na nguvu za udanganyifu wa utajiri hulisonga neno, naye huwa asiyezaa matunda.” (Mt. 13:22) Ikiwa mzazi anamtia moyo mtoto kufuatia miradi ya ulimwengu na kuona miradi ya kiroho si ya maana, anaweza kupunguza tamaa ya kijana ya kumtumikia Mungu.

Mzee mmoja mwenye uzoefu alisema hivi kuhusu vijana ambao wanastahili kubatizwa lakini wazazi wao wanakataa wabatizwe: “Kumzuia kijana asibatizwe kunaweza kumzuia kufanya maendeleo ya kiroho na kumfanya avunjike moyo.” Na mwangalizi mmoja anayesafiri aliandika hivi: “Kijana anaweza kuanza kuhisi kwamba hastahili au hafai kiroho. Huenda akaamua kuingia katika ulimwengu ili kuhisi kwamba anafanikiwa.”

[Picha]

Je, tunapaswa kutafuta kwanza elimu ya chuo kikuu?

[Picha katika ukurasa wa 3]

Kijana mwenye umri mdogo anaweza kuonyesha kwamba yeye ni mwanafunzi wa Kristo

[Picha katika ukurasa wa 3]

Kutayarisha na kutoa maelezo katika mikutano

[Picha katika ukurasa wa 4]

Kuwatii wazazi

[Picha katika ukurasa wa 4]

Kushiriki katika huduma

[Picha katika ukurasa wa 4]

Kusali kibinafsi