Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

‘Leta Vitabu vya Kukunjwa, Hasa Vile vya Ngozi’

‘Leta Vitabu vya Kukunjwa, Hasa Vile vya Ngozi’

‘Leta Vitabu vya Kukunjwa, Hasa Vile vya Ngozi’

MTUME Paulo alisema maneno hayo alipomhimiza mmishonari mwenzake Timotheo amletee vitabu fulani vyenye maandishi. Paulo alikuwa akimaanisha vitabu gani vya kukunjwa na vya ngozi? Kwa nini alisema maneno hayo? Nasi tunaweza kujifunza nini kutokana na ombi hilo?

Kufikia katikati ya karne ya kwanza W.K. wakati Paulo alipoandika maneno hayo, vile vitabu 39 vya Maandiko ya Kiebrania vilikuwa vimegawanywa katika vitabu 22 au 24, na inaelekea kwamba vingi vya vitabu hivyo vilikuwa kitabu kimoja-kimoja cha kukunjwa. Profesa Alan Millard alisema kwamba vitabu hivyo vya kukunjwa, hata ingawa vilikuwa ghali, ‘vingeweza kununuliwa na watu matajiri.’ Wengine wao wangeweza kupata angalau kitabu kimoja. Kwa mfano, yule towashi Mwethiopia alikuwa na kitabu cha kukunjwa katika gari lake na alikuwa “akimsoma kwa sauti kubwa nabii Isaya.” Alikuwa “na mamlaka chini ya Kandake malkia wa Waethiopia, na ambaye alikuwa juu ya hazina yote ya malkia.” Ni wazi kwamba alikuwa tajiri vya kutosha kuwa na vitabu fulani vya Maandiko.—Mdo. 8:27, 28.

Paulo aliandika hivi katika ombi kwa Timotheo: “Utakapokuja, ilete ile kanzu niliyomwachia Karpo kule Troa, na vile vitabu vya kukunjwa, hasa vile vya ngozi.” (2 Tim. 4:13) Maneno hayo yanaonyesha kwamba Paulo alikuwa na hesabu fulani ya vitabu. Bila shaka, Neno la Mungu ndicho kitabu kilichokuwa cha maana zaidi katika maktaba ya Paulo. Msomi wa Biblia A. T. Robertson alisema hivi kuhusu maneno ‘vitabu vya ngozi’ katika mstari huo: “Inaelekea kwamba vitabu hivyo vilikuwa nakala za vitabu vya Maandiko ya Agano la Kale, ngozi ilikuwa na bei ya juu kuliko mafunjo.” Tangu akiwa kijana na kuendelea, Paulo ‘alielimishwa miguuni pa Gamalieli,’ ambaye alifundisha Sheria ya Musa na aliheshimiwa sana na watu wote. Kwa hiyo, ni jambo linaloeleweka kwamba Paulo angeweza kupata nakala za kibinafsi za vitabu vya kukunjwa vya Neno la Mungu.—Mdo. 5:34; 22:3.

Jinsi Wakristo Walivyotumia Vitabu vya Kukunjwa

Hata hivyo, ni watu wachache sana ambao walikuwa na vitabu vya kukunjwa vya Maandiko Matakatifu. Basi, Wakristo wengi siku hizo walipata jinsi gani Neno la Mungu? Barua ambayo Paulo alimwandikia Timotheo mapema inatusaidia kupata jibu. Aliandika hivi: “Ninapokuwa nikija, endelea kufanya bidii katika kusoma mbele ya watu wote.” (1 Tim. 4:13) Programu ya makutaniko ya Kikristo ilitia ndani kusoma mbele ya watu wote, na tangu siku za Musa watu wa Mungu walikuwa na zoea hilo.—Mdo. 13:15; 15:21; 2 Kor. 3:15.

Akiwa mzee wa kutaniko, Timotheo alihitaji ‘kufanya bidii’ katika kusoma kwa sauti, na hivyo kuwafaidi wale ambao hawakuwa na nakala zao wenyewe za Maandiko. Bila shaka, wakati Neno la Mungu lilipokuwa likisomwa mbele ya watu, wote walisikiliza kwa makini ili wasikose neno lolote, na bila shaka wazazi na watoto walizungumza nyumbani kuhusu mambo yaliyosomwa katika mikutano.

Kitabu cha Kukunjwa cha Bahari ya Chumvi cha Isaya ambacho kinajulikana sana kina urefu wa futi 24 (mita 7.3) hivi. Kitabu cha kukunjwa kilikuwa kizito kwa sababu kilikuwa na mpini kila upande na mara nyingi kilifunikwa na jalada ili kisiharibike. Labda Wakristo wengi hawangeweza kubeba vitabu vingi vya kukunjwa walipoenda kuhubiri. Hata ikiwa Paulo alikuwa na vitabu fulani vya kukunjwa vya Maandiko vya kutumia kibinafsi, inaelekea kwamba aliposafiri hangeweza kubeba vitabu vyote vya kukunjwa alivyokuwa navyo. Inaonekana kwamba alimwachia rafiki yake Karpo vitabu fulani huko Troa.

Tunajifunza Nini Kutokana na Mfano wa Paulo?

Kabla tu ya kutoa ombi lake, Paulo, ambaye alikuwa amefungwa katika gereza kwa mara ya pili huko Roma, aliandika hivi: “Nimepigana pigano zuri, nimekimbia mwendo mpaka mwisho . . . Tangu wakati huu na kuendelea nimewekewa akiba ya taji la uadilifu.” (2 Tim. 4:7, 8) Inaelekea kwamba aliandika maneno hayo karibu mwaka wa 65 W.K. wakati wa mateso yaliyosababishwa na Nero. Wakati huu kifungo hicho cha gereza kilikuwa kibaya sana. Kwa kweli, alihisi kwamba alikuwa karibu kuuawa. (2 Tim. 1:16; 4:6) Inaeleweka kwa nini Paulo alitamani sana kupata vitabu vyake vya kukunjwa. Ingawa alikuwa na uhakika kwamba alikuwa amepigana pigano zuri mpaka mwisho, alikuwa na hamu kubwa ya kuendelea kujitia nguvu kwa kujifunza Neno la Mungu.

Huenda bado Timotheo alikuwa Efeso wakati alipopata ombi la Paulo. (1 Tim. 1:3) Kutoka Efeso mpaka Roma kupitia Troa ni umbali wa kilomita 1,600 hivi. Katika barua hiyohiyo, Paulo alimhimiza hivi Timotheo: “Fanya kabisa yote unayoweza ili ufike kabla ya majira ya baridi kali.” (2 Tim. 4:21) Biblia haisemi ikiwa Timotheo alipata meli ya kumpeleka Roma ili afike wakati ambapo Paulo alitaka afike.

Tunajifunza nini kutokana na ombi la Paulo la kutaka aletewe “vitabu vya kukunjwa, hasa vile vya ngozi”? Aliendelea kuwa na hamu ya kusoma Neno la Mungu wakati huo mgumu zaidi wa maisha yake. Je, huoni kwamba hiyo ndiyo siri iliyomsaidia sikuzote kuwa na bidii na kuwa hai kiroho na pia kuwa chanzo cha kuwatia moyo watu wengi?

Leo, ni baraka kama nini ikiwa tuna nakala yetu binafsi ya Biblia nzima! Wengine wetu hata wana nakala na tafsiri mbalimbali za Biblia. Kama Paulo, tunahitaji kusitawisha hamu ya kuyaelewa Maandiko kwa undani zaidi. Kati ya barua 14 zilizoongozwa na roho ya Mungu ambazo Paulo alikuwa na pendeleo la kuandika, barua ambayo aliandika mwisho ni ile barua ya pili kwa Timotheo. Ombi lake binafsi la vitabu vya kukunjwa linaonekana karibu mwishoni mwa kitabu hicho. Kwa kweli, moja kati ya mambo aliyoomba mwishoni na yakaandikwa ni kumwomba Timotheo ‘amletee vitabu vya kukunjwa, hasa vile vya ngozi.’

Je, unatamani kwa bidii kupigana pigano zuri la imani mpaka mwisho, kama Paulo alivyofanya. Je, unataka kuendelea kuwa na nguvu kiroho na kujitayarisha kushiriki katika kazi ya kutoa ushahidi maadamu Bwana anataka tuendelee kufanya hivyo? Basi, kwa nini usifanye kama Paulo alivyowahimiza Wakristo wafanye? “Jiangalie daima wewe mwenyewe na kufundisha kwako” kwa kujifunza sikuzote Biblia kwa bidii, ambayo watu wengi sasa wanaweza kuipata katika njia mbalimbali ambazo ni bora kuliko vitabu vya kukunjwa.—1 Tim. 4:16.

[Ramani/​Picha katika ukurasa wa 18, 19]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Efeso

Troa

Roma