Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Je, Utafuata Mwongozo wa Yehova Wenye Upendo?

Je, Utafuata Mwongozo wa Yehova Wenye Upendo?

Je, Utafuata Mwongozo wa Yehova Wenye Upendo?

“Nimechukia kila njia ya uwongo.”—ZAB. 119:128.

1, 2. (a) Unapotafuta mwongozo wa kukusaidia kufika mahali fulani, ungefurahi kupata maonyo ya aina gani, na kwa nini? (b) Yehova anawapatia maonyo ya aina gani wale wanaomtumikia, na kwa nini?

 WAZIA hali hii: Unahitaji kusafiri kwenda mahali fulani. Ili kupata mwongozo, unazungumza na rafiki unayemwamini ambaye anajua njia vizuri. Anapokupatia mwongozo, anaweza kusema hivi: “Uwe mwangalifu kwa sababu ya kona iliyo hapo mbele. Ishara ya barabarani inadanganya watu. Watu wengi ambao wanafuata ishara hiyo wanapotea njia.” Je, ungethamini msaada wake na kutii onyo? Kwa njia fulani, Yehova ni kama rafiki huyo. Anatupatia mwongozo mzuri sana kuhusu jinsi ya kupata uzima wa milele, lakini pia anatuonya kuhusu hatari ambazo zinaweza kutuelekeza kwenye njia mbaya.—Kum. 5:32; Isa. 30:21.

2 Katika habari hii na habari inayofuata, tutazungumzia hatari fulani ambazo Rafiki yetu, Yehova Mungu, anatuonya kuzihusu. Tunapaswa kukumbuka sikuzote kwamba Yehova anatupatia maonyo hayo kwa sababu anatujali na anatupenda. Anataka tufike mahali tunapoelekea. Anaumia moyoni watu wanapofuata njia iliyo hatari na kupotea. (Eze. 33:11) Katika habari hii, tutazungumzia hatari tatu. Hatari ya kwanza inatoka nje, ya pili iko ndani yetu. Hatari ya tatu inasababishwa na kitu ambacho si halisi; hata hivyo, ni mbaya sana. Tunahitaji kujua hatari hizo na jinsi Baba yetu wa mbinguni anavyotufundisha kuziepuka. Mtunga-zaburi mmoja aliyeongozwa na roho takatifu alimwambia Yehova hivi: “Nimechukia kila njia ya uwongo.” (Zab. 119:128) Je, unahisi vivyo hivyo? Acheni tuone jinsi tunavyoweza kuazimia kuchukia “kila njia ya uwongo.”

“Usiufuate Umati”

3. (a) Kwa nini inaweza kuwa hatari kufuata wasafiri wengine tunapokuwa na shaka kuhusu njia tunayopaswa kufuata? (b) Ni kanuni gani ya maana ambayo tunapata katika Kutoka 23:2?

3 Ikiwa ungekuwa unasafiri kwenda mbali, ungefanya nini ikiwa ungekuwa na shaka kuhusu njia unayopaswa kufuata? Huenda ungeshawishiwa kufuata wasafiri wengine, hasa ikiwa ungeona wengi wao wakifanya uamuzi uleule. Ni hatari kufanya hivyo. Kwa kweli, huenda wasafiri hao hawaendi mahali unapoenda, au huenda wao pia wamepotea njia. Kuhusiana na jambo hilo, fikiria kanuni ambayo iliongoza sheria fulani ambayo Waisraeli wa kale walipewa. Wale waliotumika wakiwa waamuzi au mashahidi katika mambo ya kihukumu walionywa kuhusu hatari ya ‘kufuata umati.’ (Soma Kutoka 23:2.) Bila shaka, ni rahisi sana kwa wanadamu wasio wakamilifu kufuata umati, na kupotosha haki. Hata hivyo, je, kanuni kuhusu kutofuata umati inahusu tu mambo ya kihukumu? Hapana.

4, 5. Yoshua na Kalebu walipata mkazo gani wa kufuata umati, lakini ni nini kilichowawezesha kuushinda?

4 Ni kweli kwamba wakati wowote tunaweza kupata mkazo wa ‘kufuata umati.’ Mkazo huo unaweza kutokea kwa ghafula, na inaweza kuwa vigumu sana kuushinda. Kwa mfano, fikiria jinsi Yoshua na Kalebu walivyopata mkazo kutoka kwa Waisraeli wenzao. Walikuwa kati ya wanaume 12 ambao walienda kupeleleza ile Nchi ya Ahadi. Waliporudi, kumi kati ya wanaume hao walileta habari mbaya na yenye kuvunja moyo. Hata walidai kwamba wakaaji fulani wa nchi hiyo walikuwa majitu ambayo yalitokana na Wanefili, wazao wa malaika waasi na wanawake. (Mwa. 6:4) Kwa kweli, dai hilo lilikuwa la uwongo. Wazao hao waovu walikuwa wameangamizwa katika Gharika karne nyingi mapema, na hawakuacha mzao hata mmoja. Lakini hata madai yasiyo na msingi yanaweza kuwashawishi sana wale walio na imani dhaifu. Habari hiyo mbaya kutoka kwa wale wapelelezi kumi ilieneza kwa haraka woga na wasiwasi kati ya watu. Baada ya muda mfupi, wengi wao walikuwa na hakika kwamba lingekuwa kosa kuingia katika ile Nchi ya Ahadi kama walivyokuwa wameagizwa na Yehova. Yoshua na Kalebu walifanya nini katika hali hiyo ngumu?—Hes. 13:25-33.

5 Yoshua na Kalebu hawakufuata umati. Ingawa umati huo wa Waisraeli haukutaka kusikia, wanaume hao wawili walisema ukweli na wakashikamana nao, hata walipotishwa kwamba wangepigwa mawe mpaka kufa! Walipata wapi ujasiri huo? Bila shaka, walipata ujasiri mwingi kutokana na imani yao. Watu wenye imani wanaona waziwazi tofauti kati ya ahadi takatifu za Yehova Mungu na madai ya watu yasiyo na msingi. Baadaye, wanaume hao wawili walieleza namna walivyohisi kuhusu jinsi Yehova alivyotimiza kila moja ya ahadi zake wakati uliopita. (Soma Yoshua 14:6, 8; 23:2, 14.) Yoshua na Kalebu walishikamana na Mungu wao mwaminifu, na hawangeweza hata kuwazia kumuumiza moyoni kwa kufuata umati usio na imani. Kwa hiyo, walisimama imara, na wakatuwekea mfano mzuri sana leo.—Hes. 14:1-10.

6. Ni katika mambo gani tunaweza kusukumwa kufuata umati?

6 Je, nyakati nyingine unasukumwa kufuata umati? Bila shaka, watu ambao wametengwa mbali na Yehova na ambao wanadharau viwango vyake vya maadili ni wengi sana leo. Mara nyingi umati huo unaeneza mawazo yasiyo na msingi kuhusu vitumbuizo na tafrija. Huenda wakasisitiza kwamba hakuna madhara yoyote kutazama upotovu wa maadili, jeuri, na mazoea ya kupashana habari na roho waovu, mambo ambayo yameenea sana katika programu za televisheni, sinema, na katika michezo ya video. (2 Tim. 3:1-5) Unapochagua vitumbuizo kwa ajili yako na familia yako, je, unaruhusu dhamiri dhaifu za watu wengine ziongoze dhamiri yako na kukuchochea kufanya maamuzi? Ikiwa hivyo ndivyo unavyofanya maamuzi, basi unafuata umati.

7, 8. (a) ‘Nguvu zetu za ufahamu’ zinazoezwa jinsi gani, na kwa nini mazoezi hayo ni ya maana kuliko kufuata orodha ya sheria kali? (b) Kwa nini unatiwa moyo na mfano wa vijana wengi Wakristo?

7 Yehova ametupatia zawadi yenye thamani ili kutusaidia kufanya maamuzi, yaani, ‘nguvu zetu za ufahamu.’ Hata hivyo, nguvu hizo zinahitaji kuzoezwa ‘kwa kutumiwa.’ (Ebr. 5:14) Kuufuata umati hakuwezi kuzoeza nguvu zetu za ufahamu wala sheria kali za mambo yanayohusu dhamiri. Hiyo ndiyo sababu watu wa Yehova hawapewi orodha ya sinema, vitabu, na vituo vya Intaneti ambavyo wanapaswa kuepuka. Kwa kuwa ulimwengu huu unabadilika haraka sana, orodha kama hiyo ingehitaji kubadilishwa kila wakati. (1 Kor. 7:31) Lakini jambo baya zaidi ni kwamba orodha kama hiyo ingetuzuia kufanya kazi ya maana zaidi ya kuchunguza kwa makini kanuni za Biblia na kusali na kisha kufanya maamuzi kwa msingi wa kanuni hizo.—Efe. 5:10.

8 Bila shaka, nyakati nyingine huenda maamuzi yetu yanayotegemea Biblia yasiwapendeze watu wengi. Vijana Wakristo wanaweza kusukumwa sana na wanafunzi wenzao shuleni ili waone na kufanya mambo ambayo kila mtu anaona na kufanya. (1 Pet. 4:4) Kwa hiyo, inapendeza kuona Wakristo vijana na waliozeeka wakiiga imani ya Yoshua na Kalebu kwa kukataa kuufuata umati.

Msifuate “Mioyo Yenu na Macho Yenu”

9. (a) Kwa nini inaweza kuwa hatari kufuata maoni na hisia zetu tunapokuwa katika safari? (b) Kwa nini sheria iliyo katika Hesabu 15:37-39 ilikuwa na faida kwa watu wa kale wa Mungu?

9 Hatari ya pili ambayo tutazungumzia iko ndani yetu. Tunaweza kuilinganisha na mfano huu: Kama ungekuwa safarini kuelekea mahali fulani, je, unaweza kuamua kutupa ramani ya njia na kufuata hisia zako, labda kwa kufuata njia yoyote ambayo inaonekana kuwa na maeneo yenye kupendeza? Bila shaka, huwezi kufika mahali unapoenda ukifuata maoni kama hayo. Kuhusiana na jambo hilo, fikiria sheria nyingine ambayo Yehova aliwapa Waisraeli wa kale. Inaweza kuwa vigumu kwa watu wengi leo kuelewa sheria ambayo inawataka watu kuweka pindo na nyuzi za bluu kwenye mavazi yao. (Soma Hesabu 15:37-39.) Hata hivyo, je, unaona faida ya kufanya hivyo? Kutii sheria kama hiyo kuliwasaidia watu wa Mungu kuwa tofauti na kujitenga na mataifa ya kipagani yaliyowazunguka. Walipaswa kufanya hivyo ili waendelee kukubaliwa na Yehova. (Law. 18:24, 25) Hata hivyo, sheria hiyo inafunua hatari nyingine iliyo ndani yetu ambayo inaweza kutukengeusha tusipate uzima wa milele. Jinsi gani?

10. Yehova ameonyesha jinsi gani kwamba anaelewa utu wa mwanadamu?

10 Ona jinsi Yehova alivyoeleza sababu ya kuwapa watu wake sheria hiyo: “Wala hamtaifuata mioyo yenu na macho yenu, ambayo mnayafuata katika uasherati.” Yehova anaelewa vizuri sana utu wa mwanadamu. Anajua jinsi ilivyo rahisi sana kwa moyo wetu, au mtu wetu wa ndani, kudanganywa na mambo tunayotazama kwa macho yetu. Hivyo, Biblia inatuonya hivi: “Moyo ni wenye hila kuliko kitu kingine chochote nao ni hatari. Ni nani anayeweza kuujua?” (Yer. 17:9) Hivyo basi, je, unaona jinsi onyo la Yehova kwa Waisraeli lilivyokuwa lenye kufaa? Alijua vizuri kwamba wangekuwa na mwelekeo wa kuangalia wapagani waliowazunguka na kushawishiwa kufanya mambo waliyoona. Huenda wangeshawishiwa kuwa kama watu hao wasio waamini na kisha kufikiri, kuhisi, na kutenda kama wao.—Met. 13:20.

11. Tunaweza kushawishiwa kwa njia gani na hisia zetu za kimwili?

11 Leo, ni rahisi hata zaidi kwa moyo wetu wenye hila kuongozwa vibaya na hisia zetu za kimwili. Tunaishi katika ulimwengu ambao unachochea watu wafuate tamaa za kimwili. Kwa hiyo, tunaweza kutumia jinsi gani kanuni iliyo katika Hesabu 15:39? Fikiria jambo hili: Ikiwa watu wanaokuzunguka shuleni, kazini, au katika ujirani wenu wanavalia kwa njia yenye kuvutia kingono, je, unaweza kushawishiwa kuvalia hivyo? Je, unaweza kushawishiwa ‘kufuata moyo na macho yako’ na kuchochewa kufanya mambo unayoona? Na je, unaweza kushawishiwa kulegeza viwango vyako mwenyewe na kuvalia kwa njia kama hiyo?—Rom. 12:1, 2.

12, 13. (a) Tunapaswa kufanya nini ikiwa macho yetu yanatanga-tanga na kutazama mambo yasiyofaa? (b) Ni nini kinachoweza kutuchochea kuepuka kuwa chanzo cha kuwashawishi wengine?

12 Tunahitaji kusitawisha kwa haraka sifa ya kujizuia. Ikiwa macho yetu yanatanga-tanga na kutazama mambo yasiyofaa, acheni tukumbuke azimio la Ayubu aliyekuwa mwaminifu, ambaye alifanya agano na macho yake, alikuwa ameazimia kabisa kutomtazama kimapenzi mwanamke ambaye si mke wake. (Ayu. 31:1) Vivyo hivyo, Mfalme Daudi aliazimia hivi: “Sitaweka mbele ya macho yangu kitu chochote kisichofaa.” (Zab. 101:3) Kitu chochote ambacho kinaweza kuchafua dhamiri zetu safi na kuharibu uhusiano wetu pamoja na Yehova ni ‘kitu kisichofaa.’ Kitu kisichofaa kinaweza kuwa kishawishi chochote ambacho kinavutia macho yetu na kujaribu kushawishi moyo wetu ufanye dhambi.

13 Kwa upande mwingine, bila shaka, hatungependa kuwa ‘kitu kisichofaa’ kwa wengine kwa kujaribu kuwashawishi kufanya mambo yasiyofaa. Kwa hiyo, tunachukua kwa uzito shauri la Biblia lililoongozwa na roho ya Mungu kuhusu kuvalia mavazi yenye mpangilio mzuri na yenye kiasi. (1 Tim. 2:9) Kuvalia mavazi yenye kiasi hakumaanishi kuvalia jinsi tunavyopenda. Tunahitaji kujali dhamiri na hisia za watu wanaotuzunguka, na kufikiria kwanza amani yao ya akili na hali yao nzuri badala ya mapendezi yetu wenyewe. (Rom. 15:1, 2) Kutaniko la Kikristo limebarikiwa kwa kuwa na maelfu ya vijana ambao wanaweka mfano mzuri katika jambo hilo. Tunafurahi tunapoona kwamba wanakataa ‘kufuata mioyo yao na macho yao,’ na badala yake wanaamua kumpendeza Yehova katika kila jambo wanalofanya, hata katika njia wanayovalia!

Usifuate “Vitu Visivyo vya Kweli”

14. Samweli alitangaza onyo gani kuhusu kufuatia “vitu visivyo vya kweli”?

14 Wazia kwamba ukiwa safarini unapita katika jangwa kubwa, na kwa mbali unaona kitu kinachofanana na maji, lakini si maji. Ni nini kingetokea ikiwa ungeacha barabara ili kwenda kuona kitu hicho kinachoonekana kama maji? Unaweza kupoteza uhai wako ukifuata kitu hicho ambacho si cha kweli! Yehova anajua vizuri hatari hiyo. Fikiria mfano fulani. Waisraeli walitaka kuwa kama mataifa yaliyowazunguka, ambayo yalitawaliwa na wafalme wa kibinadamu. Kwa kweli, tamaa hiyo ilikuwa dhambi kubwa kwa sababu ilikuwa sawa na kumkataa Yehova kuwa Mfalme wao. Ingawa Yehova aliwaruhusu kuwa na mfalme wa kibinadamu, alimwongoza nabii wake Samweli kutangaza onyo kuhusu kufuata “vitu visivyo vya kweli.”—Soma 1 Samweli 12:21.

15. Waisraeli walifuata jinsi gani vitu visivyo vya kweli?

15 Je, watu hao walifikiria kwamba kwa njia fulani mfalme wa kibinadamu angekuwa halisi zaidi, mwenye kutegemeka zaidi, kuliko Yehova? Ikiwa ndivyo, kwa kweli walikuwa wakifuatia vitu visivyo vya kweli! Na walikuwa katika hatari ya kufuatia vitu vingine vingi vya kishetani visivyo vya kweli. Wafalme wa kibinadamu wangewaongoza kwa urahisi kuabudu sanamu. Watu wanaoabudu sanamu wanakosea kwa kufikiria kwamba vitu vinavyoonekana, yaani, miungu iliyotengenezwa kwa mbao au mawe, kwa njia fulani ni halisi zaidi, ni yenye kutegemeka zaidi kuliko Yehova, Mungu asiyeonekana ambaye aliumba vitu vyote. Lakini kama mtume Paulo alivyosema, sanamu “si kitu.” (1 Kor. 8:4) Haziwezi kuona, kusikia, kuzungumza, au kutenda. Unaweza kuziona na kuzigusa, lakini ikiwa ungeabudu sanamu, kwa kweli ungekuwa ukifuatia kitu kisicho cha kweli, jambo lisilo halisi ambalo lingeleta msiba tu.—Zab. 115:4-8.

16. (a) Shetani anawashawishi jinsi gani watu wengi wafuatie vitu visivyo vya kweli? (b) Kwa nini tunaweza kusema kwamba vitu vya kimwili ni vitu visivyo vya kweli, hasa vikilinganishwa na Yehova Mungu?

16 Bado Shetani ni fundi katika kuwasadikisha watu wafuatie vitu ambavyo si vya kweli. Kwa mfano, amewashawishi watu wengi sana wafuatie vitu vya kimwili ili kupata usalama. Inaweza kuonekana kwamba pesa, mali, na kazi zenye mishahara mikubwa zinaleta faida. Hata hivyo, vitu vya kimwili vina faida gani wakati afya ya mtu inapodhoofika, wakati mfumo wa kiuchumi unapoporomoka, au wakati msiba wa kiasili unapotokea? Vitu vya kimwili vina faida gani watu wanapoona kwamba hawafai chochote, wanapokosa kusudi, mwongozo, na majibu ya maswali au maulizo ya maana zaidi maishani? Vinaweza kuwa na faida gani mtu anapokaribia kufa? Tukitazamia kwamba vitu vya kimwili vitatimiza uhitaji wetu wa kiroho, tutavunjika moyo. Vitu vya kimwili haviwezi kuleta furaha wala kuondoa matatizo yote; ni vitu visivyo vya kweli. Mwishowe, haviwezi kuleta usalama wa kimwili, kwa kuwa haviwezi kuongeza urefu wa maisha ya mwanadamu, au kuondoa magonjwa na kifo. (Met. 23:4, 5) Lakini Mungu wetu Yehova ni halisi kabisa! Tunaweza tu kupata usalama wa kweli tukiwa na uhusiano wa karibu zaidi pamoja naye. Hiyo ni baraka yenye thamani kama nini! Na tusimwache kamwe kwa kufuatia vitu visivyo vya kweli.

17. Umeazimia kufanya nini kuhusiana na hatari ambazo tumezungumzia?

17 Je, si ni kweli kwamba tumebarikiwa kwa sababu Yehova ni Rafiki yetu na Kiongozi wetu katika safari ya kupata uzima? Tukiendelea kutii maonyo yake kuhusu hatari tatu, yaani, umati, mioyo yetu, na vitu visivyo vya kweli, inaelekea kwamba tutafanikiwa kufika mwisho wa safari yetu, yaani, kupata uzima wa milele. Katika habari inayofuata tutazungumzia maonyo mengine matatu ambayo Yehova anatupatia ili kutusaidia kuchukia na kuepuka njia za uwongo ambazo zinawapoteza watu wengi sana.—Zab. 119:128.

Una Maoni Gani?

Wewe binafsi unaweza kutumia jinsi gani kanuni zinazopatikana katika Maandiko yafuatayo?

Kutoka 23:2

Hesabu 15:37-39

1 Samweli 12:21

Zaburi 119:128

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 11]

Je, nyakati nyingine unashawishiwa kufuata umati?

[Picha katika ukurasa wa 13]

Kwa nini ni hatari kufuata maoni na hisia zako?

[Picha katika ukurasa wa 14]

Je, kwa njia fulani unafuatia vitu visivyo vya kweli?