Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Pumziko la Mungu Ni Nini?

Pumziko la Mungu Ni Nini?

Pumziko la Mungu Ni Nini?

“Bado limebaki pumziko la sabato kwa ajili ya watu wa Mungu.”—EBR. 4:9.

1, 2. Tunaweza kujifunza nini kutokana na tafsiri sahihi ya andiko la Mwanzo 2:3, na ni maswali gani yanayotokea?

 KUANZIA sura ya kwanza ya kitabu cha Mwanzo, tunajifunza kwamba kwa muda wa siku sita, Mungu aliitayarisha dunia ili iwe makao ya wanadamu. Hizo hazikuwa siku za saa 24 kila moja, vilikuwa vipindi virefu zaidi vya wakati. Biblia inasema hivi kuhusu mwisho wa kila kipindi: “Ikawa jioni, ikawa asubuhi.” (Mwa. 1:5, 8, 13, 19, 23, 31) Hata hivyo, kuhusu siku ya saba, Biblia inasema: “Mungu akaibariki siku ya saba na kuifanya takatifu, kwa kuwa katika siku hiyo amekuwa akipumzika kutokana na kazi yake yote ya kuumba.”—Mwa. 2:3.

2 Kitabu cha Mwanzo kiliposema kwamba Mungu “amekuwa akipumzika,” kilimaanisha kwamba Mungu alikuwa bado anapumzika wakati huo. Hilo linaonyesha kwamba Musa alipoandika kitabu cha Mwanzo mwaka wa 1513 K.W.K. “siku” hiyo ya saba ya Mungu ya kupumzika ilikuwa bado inaendelea. Je, siku ya pumziko la Mungu bado inaendelea? Ikiwa ndivyo, je, tunaweza kuingia katika pumziko hilo leo? Majibu ya maswali au maulizo hayo ni ya maana sana kwetu.

Je, Yehova Bado Anaendelea ‘Kupumzika’?

3. Maneno ya Yesu katika Yohana 5:16, 17 yanaonyesha jinsi gani kwamba siku ya saba ilikuwa bado inaendelea katika karne ya kwanza?

3 Kuna sababu mbili zinazoonyesha kwamba siku ya saba ilikuwa bado inaendelea katika karne ya kwanza W.K. Kwanza, fikiria maneno ambayo Yesu aliwaambia wapinzani wake ambao walikasirika kwa sababu aliponya wagonjwa siku ya Sabato, jambo ambalo waliona kuwa ni kazi. Bwana aliwaambia hivi: “Baba yangu anaendelea kufanya kazi mpaka sasa, na mimi ninaendelea kufanya kazi.” (Yoh. 5:16, 17) Alimaanisha nini? Yesu alishtakiwa kuwa alifanya kazi siku ya Sabato. Aliwajibu hivi: “Baba yangu anaendelea kufanya kazi.” Kwa kweli, Yesu alikuwa akiwaambia hivi wapinzani wake: ‘Mimi na Baba yangu tunafanya kazi ileile. Kwa kuwa Baba yangu anaendelea kufanya kazi wakati wa Sabato yake ya maelfu ya miaka, ninaruhusiwa pia kuendelea kufanya kazi hata siku ya Sabato.’ Hivyo, Yesu alimaanisha kwamba kuhusiana na dunia, siku ya Sabato kuu ya Mungu ya kupumzika, yaani, siku ya saba, ilikuwa bado inaendelea katika siku za Yesu. *

4. Ni sababu gani nyingine ambayo Paulo anatoa inayoonyesha kwamba siku ya saba ilikuwa inaendelea katika siku zake?

4 Mtume Paulo anatupatia sababu ya pili inayoonyesha kwamba siku ya saba ilikuwa inaendelea katika karne ya kwanza. Alipotaja andiko la Mwanzo 2:2 kuhusu pumziko la Mungu, Paulo aliandika hivi chini ya mwongozo wa roho ya Mungu: “Sisi ambao tumeonyesha imani tunaingia katika pumziko.” (Ebr. 4:3, 4, 6, 9) Kwa hiyo, siku ya saba ilikuwa bado inaendelea katika siku za Paulo. Siku hiyo ya pumziko ingeendelea kwa muda mrefu kadiri gani?

5. Ni nini lililokuwa kusudi la siku ya saba, na kusudi hilo litatimia kabisa wakati gani?

5 Ili kujibu swali hilo, ni lazima tukumbuke kusudi la siku ya saba. Andiko la Mwanzo 2:3 linaeleza hivi: “Mungu akaibariki siku ya saba na kuifanya takatifu.” Siku hiyo ‘ilifanywa kuwa takatifu,’ yaani, ilitakaswa, au iliwekwa kando na Yehova ili kukamilisha kusudi lake. Kusudi hilo ni kwamba dunia ikaliwe na wanaume na wanawake watiifu ambao wataitunza na kutunza viumbe wote walio hai. (Mwa. 1:28) Yehova Mungu na Yesu Kristo, ambaye ni “Bwana wa Sabato,” ‘wameendelea kufanya kazi mpaka sasa’ ili watimize kusudi hilo. (Mt. 12:8) Siku ya pumziko la Mungu itaendelea mpaka kusudi lake kuhusiana na siku hiyo litimie kabisa mwishoni mwa Utawala wa Miaka Elfu Moja wa Kristo.

‘Usianguke Katika Kielelezo Kilekile cha Kutotii’

6. Ni mifano gani inayotuonya sisi, na tunaweza kujifunza nini kutokana nayo?

6 Mungu aliwaeleza waziwazi Adamu na Hawa kusudi lake kwa ajili ya dunia, lakini walitenda kinyume na kusudi hilo. Bila shaka, Adamu na Hawa ndio wanadamu wa kwanza ambao hawakumtii Mungu. Tangu wakati huo kumekuwa na mamilioni ya watu wengine ambao wametenda vivyo hivyo. Hata watu wa Mungu waliochaguliwa, taifa la Israeli, walikosa tena na tena kumtii Mungu. Na jambo la maana zaidi ni kwamba Paulo aliwaonya Wakristo wa karne ya kwanza kuwa hata wengine kati yao wangeanguka katika mtego huohuo wa Waisraeli wa kale. Aliandika hivi: “Kwa hiyo acheni sisi tufanye yote tunayoweza ili kuingia katika pumziko hilo, yeyote asije akaanguka katika kielelezo kilekile cha kutotii.” (Ebr. 4:11) Maneno ya Paulo yanaonyesha kwamba watu wasiotii hawawezi kuingia katika pumziko la Mungu. Hilo linamaanisha nini kwetu? Je, linamaanisha kwamba tukiasi na kutenda kwa njia fulani kinyume na kusudi la Mungu, hatutaingia katika pumziko la Mungu? Ni wazi kwamba jibu la swali hilo ni la maana sana, na tutalichunguza kwa undani zaidi. Hata hivyo, acheni sasa tuone jambo lingine tunaloweza kujifunza kuhusu kuingia katika pumziko la Mungu kwa kuchunguza mfano mbaya wa Waisraeli.

“Hawataingia Katika Pumziko Langu”

7. Yehova alikuwa na kusudi gani alipowakomboa Waisraeli kutoka utumwani huko Misri, na aliwatazamia wafanye nini?

7 Katika mwaka wa 1513 K.W.K., Yehova alimfunulia Musa mtumishi wake kusudi lake kuhusu Waisraeli. Mungu alisema hivi: “Ninashuka ili kuwakomboa kutoka katika mkono wa Wamisri na kuwatoa katika nchi hiyo [ya Misri] mpaka kwenye nchi nzuri na kubwa, nchi inayotiririka maziwa na asali.” (Kut. 3:8) Kama vile tu Yehova alivyomwahidi babu yao, Abrahamu, kusudi la Mungu la kuwakomboa Waisraeli “kutoka katika mkono wa Wamisri” lilikuwa kuwafanya wawe watu wake. (Mwa. 22:17) Mungu aliwapa Waisraeli sheria ambazo zingewasaidia kuwa na uhusiano wenye amani pamoja naye. (Isa. 48:17, 18) Aliwaambia Waisraeli hivi: “Ikiwa mtaitii sauti yangu kabisa na kulishika kwa kweli agano langu [kama ilivyoonyeshwa katika ile Sheria iliyoandikwa], ndipo hakika mtakapokuwa mali yangu ya pekee kutoka kati ya vikundi vingine vyote vya watu, kwa sababu dunia nzima ni yangu.” (Kut. 19:5, 6) Kwa hiyo, Waisraeli wangeendelea kufurahia pendeleo la kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Mungu ikiwa tu wangetii sauti yake.

8. Ni maisha ya aina gani ambayo Waisraeli wangekuwa nayo ikiwa wangemtii Mungu?

8 Fikiria maisha ambayo Waisraeli wangekuwa nayo ikiwa tu wangetii sauti ya Mungu! Yehova angebariki mashamba yao, mizabibu yao, na wanyama wao. Aliahidi pia kwamba angewalinda kutokana na maadui wao. (Soma 1 Wafalme 10:23-27.) Wakati Masihi angetokea, inaelekea kwamba angewakuta Waisraeli wakijitawala wenyewe kama taifa huru, na si chini ya ukandamizaji wa Waroma. Yehova alitaka taifa la Israeli liwe mfano mzuri kwa mataifa mengine. Alitaka kila mtu aelewe waziwazi kwamba wale wanaomtii yeye akiwa Mungu wa kweli, wanapata baraka nyingi kutoka kwake.

9, 10. (a) Kwa nini lilikuwa kosa zito kwa Waisraeli kutamani kurudi Misri? (b) Je, Waisraeli wangemwabudu Yehova kwa njia aliyotaka ikiwa wangerudi Misri?

9 Waisraeli walikuwa na pendeleo la pekee kama nini la kumruhusu Yehova awatumie ili kutimiza kusudi lake! Wangepokea baraka za Yehova na pia wangeziletea familia zote za dunia baraka nyingi. (Mwa. 22:18) Hata hivyo, Waisraeli wengi hawakuchukua kwa uzito pendeleo la kuwa taifa la Mungu na kuwa mfano mzuri kwa mataifa mengine. Hata walisema kwamba walitaka kurudi Misri! (Soma Hesabu 14:2-4.) Sasa, ikiwa wangerudi Misri wangetimiza jinsi gani kusudi la Mungu la kufanya ufalme wa Israeli uwe mfano mzuri kwa mataifa mengine? Hilo halingewezekana. Kwa kweli, ikiwa Waisraeli wangerudi kuwa tena watumwa huko Misri, hawangeweza kamwe kufuata Sheria ya Musa na kufaidika na mpango wa Yehova wa kuwasamehe dhambi zao. Walikuwa wakijifikiria wenyewe tu bila kufikiria kusudi la Mungu! Haishangazi kwamba Yehova aliwaambia hivi waasi hao: “Nikachukizwa na kizazi hiki, nikasema, ‘Wao hupotea sikuzote katika mioyo yao, nao wenyewe hawajapata kuzijua njia zangu.’ Kwa hiyo niliapa kwa hasira yangu, ‘Hawataingia katika pumziko langu.’”—Ebr. 3:10, 11; Zab. 95:10, 11.

10 Kwa kutamani kurudi Misri, taifa hilo lililopotea lilionyesha kwamba halikuthamini baraka za kiroho ambazo lilipokea, na badala yake likapendelea vitunguu vya majani, vitunguu, na vitunguu saumu ambavyo vilikuwa Misri. (Hes. 11:5) Kama Esau asiye na shukrani, waasi hao walikuwa tayari kupoteza urithi wa kiroho wenye thamani kwa kubadilishana na chakula kitamu.—Mwa. 25:30-32; Ebr. 12:16.

11. Kwa kuwa Waisraeli wa siku za Musa hawakuwa waaminifu, je, hilo lilibadili kusudi la Mungu?

11 Ingawa Waisraeli hao waliotoka Misri hawakuwa waaminifu, Yehova ‘aliendelea kufanya kazi’ kwa subira ili kutimiza kusudi lake kuelekea taifa hilo, akikazia uangalifu wake kizazi kilichofuata. Washiriki wa kizazi hicho kipya walikuwa watiifu zaidi kuliko baba zao. Kulingana na amri ya Yehova, waliingia katika Nchi ya Ahadi na wakaanza kuimiliki. Tunasoma hivi katika Yoshua 24:31: “Israeli wakaendelea kumtumikia Yehova siku zote za Yoshua na siku zote za wale wanaume wazee walioendelea kuishi baada ya Yoshua, waliokuwa wamejua kazi yote ya Yehova ambayo alifanya kwa ajili ya Israeli.”

12. Tunajua jinsi gani kwamba inawezekana leo kuingia katika pumziko la Mungu?

12 Hata hivyo, kizazi hicho kilichotii kilikufa hatua kwa hatua na kizazi kingine ambacho “hakikumjua Yehova wala ile kazi ambayo alikuwa amewafanyia Israeli” kikachukua mahali pake. Kwa hiyo, “wana wa Israeli wakaanza kufanya yaliyo mabaya machoni pa Yehova, wakatumikia Mabaali.” (Amu. 2:10, 11) Kwa kweli, Nchi hiyo ya Ahadi haikuwa “mahali pa pumziko” kwao. Kwa sababu ya kutotii kwao, hawakufurahia amani yenye kudumu pamoja na Mungu. Baadaye, Paulo aliandika hivi kuhusu Waisraeli hao: “Kama Yoshua angekuwa amewaingiza [Waisraeli] katika mahali pa pumziko, Mungu hangesema baadaye juu ya siku nyingine. Kwa hiyo bado limebaki pumziko la sabato kwa ajili ya watu wa Mungu.” (Ebr. 4:8, 9) “Watu wa Mungu” ambao Paulo alikuwa akizungumzia walikuwa Wakristo. Je, hilo linamaanisha kwamba Wakristo wangeweza kuingia katika pumziko la Mungu? Bila shaka, hilo lilitia ndani Wakristo Wayahudi na Wakristo wasio Wayahudi!

Wakristo Wengine Hawakuingia Katika Pumziko la Mungu

13, 14. Kulikuwa na uhusiano gani kati ya kufuata Sheria ya Musa na kuingia katika pumziko la Mungu (a) katika siku za Musa? (b) katika karne ya kwanza?

13 Paulo aliwaandikia Wakristo Waebrania kwa sababu wengine wao walikuwa wakitenda kinyume na kusudi la Mungu. (Soma Waebrania 4:1.) Katika maana gani? Jambo la kushangaza ni kwamba bado walikuwa wakifuata Sheria ya Musa. Ni kweli kwamba kwa miaka 1,500 hivi, Mwisraeli yeyote ambaye alitaka kuishi kulingana na kusudi la Mungu alipaswa kufuata Sheria ya Musa. Hata hivyo, baada ya kifo cha Yesu, Sheria hiyo iliondolewa. Wakristo fulani walikosa kutambua jambo hilo, na walisisitiza kuendelea kufuata mambo fulani katika Sheria ya Musa. *

14 Paulo aliwaeleza Wakristo waliokuwa na mwelekeo wa kufuata Sheria ya Musa kwamba ukuhani mkuu wa Yesu, agano jipya, na hekalu la kiroho, vyote hivyo vilikuwa bora zaidi kuliko agano la Mungu pamoja na Waisraeli. (Ebr. 7:26-28; 8:7-10; 9:11, 12) Kwa hiyo, inaelekea kwamba akifikiria wale walioshika Sabato ya kila juma chini ya Sheria, Paulo aliandika kuhusu pendeleo la kuingia katika siku ya pumziko la Yehova: “Bado limebaki pumziko la sabato kwa ajili ya watu wa Mungu. Kwa maana mtu ambaye ameingia katika pumziko la Mungu yeye mwenyewe pia amepumzika kutokana na kazi zake mwenyewe, kama Mungu alivyopumzika kutokana na kazi zake mwenyewe.” (Ebr. 4:8-10) Wakristo hao Waebrania walipaswa kuacha kufikiri kwamba wangeweza kukubaliwa na Yehova kwa kufuata matendo yaliyotegemea Sheria ya Musa. Tangu Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K., ni wale tu ambao wanamwamini Yesu Kristo ndio wanaopata kwa rehema kibali cha Mungu.

15. Kwa nini kutii ni jambo la maana ikiwa tunataka kuingia katika pumziko la Mungu?

15 Ni nini kilichowazuia Waisraeli wa siku za Musa kuingia katika ile Nchi ya Ahadi? Ni kutotii. Ni nini kilichokuwa kikiwazuia Wakristo fulani katika siku za Paulo kuingia katika pumziko la Mungu? Ni jambo lilelile, kutotii. Walishindwa kutambua kwamba Sheria ilitimiza kusudi lake na kwamba Yehova alikuwa akiwaongoza watu wake katika njia tofauti.

Kuingia Katika Pumziko la Mungu Leo

16, 17. (a) Inamaanisha nini kuingia katika pumziko la Mungu leo? (b) Tutazungumzia nini katika habari inayofuata?

16 Ni Wakristo wachache leo ambao wanaweza kusisitiza kufuata sehemu fulani za Sheria ya Musa ili kupata wokovu. Maneno ya Paulo yaliyoongozwa na roho ya Mungu ambayo aliwaandikia Waefeso yako wazi kabisa: “Kwa fadhili hizi zisizostahiliwa, kwa kweli, ninyi mmeokolewa kupitia imani; na hiyo si kutokana na ninyi, ni zawadi ya Mungu. Hapana, si kutokana na matendo, ili mtu yeyote asiwe na sababu ya kujisifu.” (Efe. 2:8, 9) Hivyo basi, inamaanisha nini kwa Wakristo kuingia katika pumziko la Mungu? Kumbuka kwamba Yehova alichagua siku ya saba kuwa siku yake ya pumziko ili kutimiza kusudi lake kwa ajili ya dunia kwa njia yenye utukufu. Tunaweza kuingia katika pumziko la Yehova au kujiunga naye katika pumziko lake, kwa kutii na kufanya kazi kulingana na kusudi lake linalosonga mbele kama linavyofunuliwa kwetu kupitia tengenezo lake.

17 Kwa upande mwingine, tukipuuza mashauri yanayotegemea Biblia ambayo tunapata kupitia jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara, huku tukichagua kujitegemea wenyewe, tutakuwa tunapinga kusudi la Mungu ambalo linatimizwa hatua kwa hatua. Jambo hilo lingehatarisha uhusiano wetu wenye amani pamoja na Yehova. Katika habari inayofuata, tutazungumza kuhusu hali fulani za kawaida ambazo zinatupatia nafasi ya kuonyesha kwamba sisi ni watiifu. Maamuzi tunayofanya katika hali hizo yanaweza kuonyesha ikiwa kwa kweli tumeingia katika pumziko la Mungu.

[Maelezo ya Chini]

^ Makuhani na Walawi walifanya kazi za hekalu siku ya Sabato, hata hivyo ‘walibaki bila hatia.’ Akiwa kuhani mkuu wa hekalu kuu la kiroho la Mungu, Yesu angeweza pia kutimiza mgawo wake wa kiroho bila kuogopa kuvunja Sabato.—Mt. 12:5, 6.

^ Hatujui ikiwa Mkristo yeyote Myahudi alitoa dhabihu Siku ya Upatanisho baada ya siku ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K. Bila shaka, Mkristo ambaye angefanya hivyo angeonyesha kwamba haheshimu dhabihu ya Yesu. Lakini, Wakristo fulani Wayahudi walishikilia mapokeo mengine yaliyohusiana na Sheria.—Gal. 4:9-11.

Maswali ya Kutafakari

• Ni nini lililokuwa kusudi la siku ya saba ya pumziko la Mungu?

• Tunajua jinsi gani kwamba siku ya saba bado inaendelea leo?

• Ni nini kilichowazuia Waisraeli katika siku za Musa na pia Wakristo fulani katika karne ya kwanza kuingia katika pumziko la Mungu?

• Inamaanisha nini kuingia katika pumziko la Mungu leo?

[Maswali ya Funzo]

[Blabu katika ukurasa wa 27]

Tunaweza kuingia katika pumziko la Yehova leo kwa kutii na kufanya kazi kulingana na kusudi lake linalosonga mbele kama linavyofunuliwa kwetu kupitia tengenezo lake

[Picha katika ukurasa wa 26, 27]

Ni jambo gani ambalo bado ni la maana kwa watu wa Mungu ili kuingia katika pumziko lake?