Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Ushindi wa Kisheria Baada ya Kupambana kwa Muda Mrefu!

Ushindi wa Kisheria Baada ya Kupambana kwa Muda Mrefu!

Ushindi wa Kisheria Baada ya Kupambana kwa Muda Mrefu!

VITA hivyo vya kisheria vilianza mwaka wa 1995 na vilidumu kwa miaka 15. Wakati huo wote, Wakristo wa kweli katika nchi ya Urusi walishambuliwa na watu waliopinga uhuru wa kidini. Wapinzani hao waliazimia kuhakikisha kwamba Mashahidi wa Yehova wamepigwa marufuku huko Moscow na katika sehemu nyingine. Hata hivyo, Yehova aliona kwamba inafaa kuwathawabisha ndugu na dada zetu wapendwa wanaoshika utimilifu huko Urusi kwa kuwapa ushindi wa kisheria. Lakini, ni nini kilichosababisha mapambano hayo?

MWISHOWE WANAPATA UHURU!

Mwanzoni mwa miaka ya 1990, ndugu zetu huko Urusi walipata tena uhuru wa kidini ambao walipoteza mwaka wa 1917. Mwaka wa 1991, waliandikishwa na serikali ya Muungano wa Sovieti kuwa dini inayotambuliwa kisheria. Baada ya Muungano wa Sovieti kuvunjika, Mashahidi wa Yehova waliandikishwa katika Shirikisho la Urusi. Zaidi ya hayo, Mashahidi ambao walikuwa wamepata mateso ya kidini makumi ya miaka kabla ya hapo walitambuliwa kisheria na Serikali kuwa watu waliokandamizwa kwa sababu za kisiasa. Mwaka wa 1993, Idara ya Haki ya Moscow iliandikisha kirasmi Shirika la Mashahidi wa Yehova la Moscow, kama tunavyojulikana kisheria huko. Mwaka huohuo pia, katiba au sheria mpya za Urusi ambazo zinawahakikishia watu uhuru wa kidini, zilianza kufuatwa. Haishangazi kwamba ndugu mmoja alisema hivi kwa mshangao, “Hata hatukufikiria kamwe kwamba tunaweza kupata uhuru huo!” Kisha akaendelea kusema hivi: “Kwa miaka 50 tulikuwa tukingoja kupata uhuru huu!”

Akina ndugu na dada huko Urusi walitumia vizuri ‘majira hayo yanayofaa’ kwa kuongeza haraka kazi yao ya kuhubiri, na watu wengi walikubali ujumbe wao. (2 Tim. 4:2) Mtu mmoja alisema hivi: “Watu walipendezwa sana na dini.” Baada ya muda mfupi, hesabu ya wahubiri, mapainia, na makutaniko iliongezeka sana. Kwa kweli, kuanzia mwaka wa 1990 mpaka 1995, hesabu ya Mashahidi huko Moscow iliongezeka kutoka 300 mpaka zaidi ya 5,000! Kadiri hesabu ya watumishi wapya wa Yehova ilivyozidi kuongezeka huko Moscow, ndivyo watu waliopinga uhuru wa kidini walivyokasirika. Katikati ya miaka ya 1990, watu hao walishambulia kwa kuchochea vita vya kisheria. Mapambano hayo yalitukia katika hatua nne ndefu kabla ya kutatuliwa mwishowe.

UCHUNGUZI WA UHALIFU ULIFIKIA MWISHO KWA NJIA YA AJABU

Hatua ya kwanza ya mapambano ilianza Juni (Mwezi wa 6) 1995. Kikundi cha watu huko Moscow ambao wanaunga mkono Kanisa Othodoksi la Urusi waliwashtaki ndugu zetu mahakamani kwamba wanashiriki katika mambo ya uhalifu. Kikundi hicho kilidai kwamba kilikuwa kikiwatetea washiriki wa familia ambao hawakutaka wenzi wao wa ndoa au watoto wao wawe Mashahidi. Mwezi wa Juni 1996, wachunguzi walianza kutafuta ushahidi wa makosa, lakini hawakupata uthibitisho au ushahidi wowote. Hata hivyo, kikundi hicho cha Moscow kiliwashtaki tena ndugu zetu kwamba walishiriki katika mambo ya uhalifu. Wachunguzi walifanya uchunguzi mwingine, lakini mashtaka yote yalikataliwa. Hata hivyo, wapinzani waliwashtaki kwa mara ya tatu, wakitoa madai yaleyale. Kwa mara nyingine tena, Mashahidi wa Yehova huko Moscow walichunguzwa, lakini yule kiongozi wa mashtaka alifanya uamuzi uleule, kwamba hakukuwa na msingi wa kuwashtaki Mashahidi kuwa wahalifu. Kisha, wapinzani hao waliwashtaki tena Mashahidi kwa mara ya nne wakiwa na madai yaleyale, na kwa mara nyingine tena, yule ofisa wa mashtaka hakupata ushahidi. Jambo la kushangaza ni kwamba kikundi hichohicho kiliomba uchunguzi mwingine ufanywe. Mwishowe, ofisa mpya wa uchunguzi alitupilia mbali kesi hiyo Aprili 13, 1998 (13/4/1998).

Mwanasheria ambaye alihusika katika kesi hiyo anasema hivi: “Lakini jambo fulani la ajabu lilitokea.” Ingawa mwanamke ambaye alikuwa mwakilishi wa ofisi ya kiongozi wa mashtaka na ambaye alikuwa ameongoza uchunguzi huo wa tano alikubali kwamba hakukuwa na ushahidi wa kuonyesha kuwa Mashahidi walishiriki katika uhalifu, bado alishauri kwamba ndugu zetu wafunguliwe kesi ya kiraia. Mwakilishi huyo alidai kwamba Shirika la Mashahidi wa Yehova la Moscow lilivunja sheria ya taifa na ya kimataifa. Kiongozi wa mashtaka wa Eneo la Kaskazini la jiji la Moscow alikubali na kuwafungulia kesi hiyo. * Mnamo Septemba 29, 1998, kesi hiyo ilianza kusikilizwa katika Mahakama ya Wilaya ya Golovinsky huko Moscow. Hatua ya pili ya mapambano ilikuwa imeanza.

BIBLIA KATIKA MAHAKAMA

Katika chumba cha mahakama kilichojaa watu kaskazini mwa Moscow, Kiongozi wa Mashtaka anayeitwa Tatyana Kondratyeva alianza kuwashambulia Mashahidi wa Yehova akitumia sheria ya serikali iliyotiwa sahihi mwaka wa 1997 ambayo inasema kwamba kanisa la Othodoksi la Kikristo, Uislamu, Dini ya Kiyahudi, na Ubudha ni dini za zamani. * Kwa kweli, sheria hiyohiyo imefanya iwe vigumu kwa dini nyingine kutambuliwa kisheria. Pia, inaruhusu mahakama zipige marufuku dini ambazo zinaeneza chuki. Akitumia sheria hiyo, kiongozi wa mashtaka alitoa mashtaka ya uwongo ya kwamba Mashahidi wa Yehova wanaeneza chuki na kuharibu familia na hivyo wanapaswa kupigwa marufuku.

Mwanasheria aliyewatetea ndugu zetu aliuliza hivi: “Ni watu gani katika Kutaniko la Moscow ambao wana hatia ya kuvunja sheria?” Kiongozi wa mashtaka hakutaja jina hata moja. Hata hivyo, alidai kwamba vichapo vya Mashahidi wa Yehova vinachochea uadui wa kidini. Ili kuthibitisha jambo hilo, alisoma magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! na vichapo vingine (ona picha iliyo hapo juu). Alipoulizwa vichapo hivyo vinasababisha uadui katika njia gani, alisema hivi: “Mashahidi wa Yehova wanafundisha kwamba dini yao ndiyo ya kweli.”

Mwanasheria mmoja ambaye ni ndugu yetu, alimpa mwamuzi au hakimu nakala moja ya Biblia na nakala nyingine akampa yule kiongozi wa mashtaka kisha akasoma andiko la Waefeso 4:5: “Bwana mmoja, imani moja, ubatizo mmoja.” Muda si muda, hakimu, kiongozi wa mashtaka, na yule mwanasheria, wote wakiwa wameshika Biblia mkononi, walikuwa wakizungumzia maandiko kama vile Yohana 17:18 na Yakobo 1:27. Hakimu akauliza hivi: “Je, maandiko hayo yanachochea uadui wa kidini?” Yule kiongozi wa mashtaka akajibu kwamba hana ujuzi wa kutosha wa kutoa maelezo kuhusu Biblia. Mwanasheria huyo aliwaonyesha vichapo vya Kanisa Othodoksi la Urusi ambavyo vinawachambua vikali Mashahidi wa Yehova, akawauliza hivi: “Je, maneno haya yanavunja sheria?” Yule kiongozi wa mashtaka akajibu hivi: “Sina ujuzi wa kutosha kutoa maelezo kuhusu ubishi wa makasisi.”

MASHTAKA YAKOSA USHAHIDI

Kiongozi wa mashtaka alidai kwamba Mashahidi wanaharibu familia, kwa sababu hawasherehekei sikukuu kama vile Krismasi. Hata hivyo, baadaye alikubali kwamba sheria ya Urusi haiwataki raia washerehekee Krismasi. Warusi, kutia ndani Mashahidi wa Yehova Warusi, wana haki ya kuchagua jambo la kufanya. Kiongozi wa mashtaka alidai pia kwamba tengenezo letu ‘linawanyima watoto pumziko la kawaida na nafasi za kupata shangwe.’ Hata hivyo, alipoulizwa maswali, alikubali kwamba hajawahi kamwe kuzungumza na kijana yeyote aliyelelewa na wazazi ambao ni Mashahidi. Mwanasheria mmoja alipomuuliza kiongozi wa mashtaka ikiwa amewahi kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova, alijibu hivi: “Hakuna haja.”

Kiongozi wa mashtaka alimwita profesa wa magonjwa ya akili ili atoe ushahidi akiwa shahidi mwenye ujuzi. Alidai kwamba kusoma vitabu vyetu kunasababisha matatizo ya kiakili. Mwanasheria aliyetetea Mashahidi aliposema kwamba maandishi ambayo profesa huyo alitoa mahakamani yanafanana na maandishi ya kitabu fulani ambacho kiliandikwa na Viongozi wa Kidini wa Moscow, profesa huyo alikubali kwamba sehemu fulani zilifanana, neno kwa neno. Alisema hivi: “Tunafanya kazi kwa kutumia kompyuta moja.” Alipoulizwa maswali zaidi alifunua kwamba hajawahi kamwe kumtibu Shahidi wa Yehova. Kwa upande mwingine, profesa mwingine wa magonjwa ya akili alitoa ushahidi mahakamani kwamba alikuwa amewachunguza Mashahidi zaidi ya 100 huko Moscow. Alipata kwamba kikundi hicho kina afya ya kawaida ya akili, naye akaongeza kwamba washiriki wa kikundi hicho wanajitahidi zaidi kuvumilia dini nyingine wanapogeuka na kuwa Mashahidi.

USHINDI—LAKINI SI WA MWISHO

Mnamo Machi 12, 1999 (12/3/1999), hakimu aliwachagua watu watano wenye elimu ya juu ili wachunguze vitabu vya Mashahidi wa Yehova, na akasimamisha kesi kwa muda. Katika hali nyingine isiyohusiana na kesi ya Moscow, Wizara ya Masuala ya Haki katika serikali ya shirikisho la Urusi ilikuwa tayari imeagiza kikundi cha wasomi kichunguze vitabu vyetu. Kikundi hicho ambacho kilipewa kazi na Wizara hiyo kilitoa ripoti yake Aprili 15, 1999, kwamba hawakupata jambo lolote baya katika vichapo vyetu. Kwa hiyo, Aprili 29, 1999, Wizara ya Masuala ya Haki iliwaandikisha kirasmi tena Mashahidi wa Yehova. Hata kukiwa na ripoti hiyo nzuri ya uchunguzi huo mpya, mahakama ya Moscow ilisisitiza kwamba kikundi kipya kichunguze vichapo vyetu. Jambo hilo lilisababisha hali fulani ya ajabu, Mashahidi wa Yehova walitambuliwa katika taifa hilo na Wizara ya Urusi ya Masuala ya Haki kuwa dini inayokubaliwa ambayo inafuata sheria, lakini wakati huohuo, walikuwa wakichunguzwa na Idara ya Haki ya Moscow kwa madai ya kwamba wanavunja sheria!

Karibu miaka miwili ilipita kabla ya kesi hiyo kuanza tena, na mnamo Februari 23, 2001, Hakimu Yelena Prokhorycheva alifanya uamuzi. Baada ya kuchunguza matokeo ya uchunguzi wa kikundi ambacho alichagua, aliamua hivi: “Hakuna msingi wa kusimamisha na kupiga marufuku kazi ya shirika la kidini la Mashahidi wa Yehova katika Moscow.” Mwishowe, ilithibitishwa kisheria kwamba ndugu zetu hawakuwa na hatia kuhusu mashtaka yote ambayo yaliletwa juu yao! Hata hivyo, kiongozi wa mashtaka alikataa uamuzi huo na kukata rufani katika Mahakama ya Jiji la Moscow. Miezi mitatu baadaye, mnamo Mei 30, 2001, mahakama hiyo ilifutilia mbali uamuzi wa Hakimu Prokhorycheva. Iliagiza kesi hiyo isikilizwe upya na ishughulikiwe na yuleyule kiongozi wa mashtaka lakini isimamiwe na hakimu tofauti. Hatua ya tatu ya mapambano ilikuwa karibu kuanza.

TULISHINDWA—LAKINI HAUKUWA MWISHO

Mnamo Oktoba 30, 2001 (30/10/2001), Hakimu Vera Dubinskaya alianza kusikiliza upya kesi hiyo. * Kiongozi wa mashtaka, Kondratyeva, alirudia tena shtaka la kwamba Mashahidi wa Yehova wanaeneza chuki, lakini aliongezea kwamba kupiga marufuku shirika la kisheria la Mashahidi wa Yehova ilikuwa njia ya kulinda haki za Mashahidi huko Moscow! Ili kupinga dai hilo la kushangaza, Mashahidi wote 10,000 katika Moscow walitia sahihi mara moja ombi la kuitaka mahakama ifutilie mbali dai la kiongozi huyo wa mashtaka kwamba “analinda,” haki zao.

Kiongozi wa mashtaka alisema kwamba hakukuwa na uhitaji wa yeye kutoa ushahidi wa kuthibitisha kwamba Mashahidi walikuwa na hatia ya kufanya makosa. Alisema kwamba kesi hiyo ilihusu vichapo na mafundisho ya Mashahidi wa Yehova, bali si utendaji wao mbalimbali. Alitangaza kwamba angemtumia msemaji wa Kanisa Othodoksi la Urusi kama shahidi mwenye ujuzi. Bila shaka, tangazo hilo lilionyesha wazi kwamba kwa kweli viongozi wa kidini walichochea sana ili Mashahidi wapigwe marufuku. Mnamo Mei 22, 2003, hakimu aliagiza kwamba kikundi cha watu wenye elimu ya juu kichunguze tena vichapo vya Mashahidi wa Yehova.

Mnamo Februari 17, 2004, kesi hiyo ilianza tena kuchunguza matokeo ya uchunguzi wa kile kikundi cha wasomi. Wasomi hao waligundua kwamba vichapo vyetu vinawatia moyo wasomaji “walinde familia na mpango wa ndoa” na dai la kwamba vichapo vyetu vinaeneza chuki “halikuwa na msingi.” Wasomi wengine walikubaliana na jambo hilo. Profesa wa historia ya kidini aliulizwa hivi: “Kwa nini Mashahidi wa Yehova wanahubiri?” Akajibu mahakama hivi: “Kazi ya kuhubiri ni ya lazima kwa Mkristo. Hivyo ndivyo Injili inavyosema na hiyo ndiyo kazi ambayo Kristo aliwapa wanafunzi wake wafanye, ‘waende na kuhubiri katika nchi zote.’” Hata hivyo, Machi 26, 2004, hakimu alipiga marufuku utendaji mbalimbali wa Mashahidi wa Yehova huko Moscow. Mnamo Juni 16, 2004, Mahakama ya Jiji la Moscow iliunga mkono uamuzi huo. * Akizungumza kuhusu uamuzi huo, Shahidi mmoja wa muda mrefu alisema hivi: “Katika nyakati za Sovieti, Mrusi hakupaswa kuamini kwamba kuna Mungu. Leo, ni lazima Mrusi awe Mwothodoksi.”

Akina ndugu walitenda jinsi gani walipopigwa marufuku? Walitenda kama Nehemia wa kale. Katika siku zake, wakati maadui wa watu wa Mungu walipopinga jitihada zake za kujenga upya ukuta wa Yerusalemu, Nehemia na watu wake hawakujiacha wakengeushwe na upinzani wa aina yoyote. Badala yake, ‘waliendelea kujenga’ na “wakaendelea kuwa na moyo wa kufanya kazi.” (Neh. 4:1-6) Vivyo hivyo, ndugu zetu huko Moscow hawakuacha wapinzani wawakengeushe kutoka katika kazi inayopaswa kufanywa leo, kazi ya kuhubiri habari njema. (1 Pet. 4:12, 16) Walikuwa na uhakika kwamba Yehova angewatunza, na walikuwa tayari kuingia katika hatua ya nne ya mapambano hayo ya muda mrefu.

UPINZANI UNAONGEZEKA

Mnamo Agosti 25, 2004, ndugu zetu walituma ombi lao huko Kremlin ambalo walimwandikia Vladimir Putin, aliyekuwa rais wa Urusi wakati huo. Ombi hilo, ambalo lilieleza jinsi walivyohangaishwa sana na yale marufuku, lilikuwa limeandikwa katika mabuku 76 na lilikuwa limetiwa sahihi zaidi ya 315,000. Wakati huo, viongozi wa kanisa Othodoksi la Urusi walionyesha jinsi walivyo kikweli. Msemaji wa Kiongozi wa Dini wa Moscow alitangaza hivi: “Tunapinga kabisa kazi ya Mashahidi wa Yehova.” Kiongozi mmoja Mwislamu alisema kwamba uamuzi huo wa kupiga marufuku “ulikuwa wa maana sana na wa kihistoria.”

Haishangazi kwamba watu waliopotoshwa katika nchi ya Urusi walipata ujasiri wa kuwashambulia Mashahidi wa Yehova. Mashahidi fulani ambao walikuwa wakishiriki katika kazi ya kuhubiri huko Moscow walipigwa ngumi na mateke na wapinzani. Mwanamume aliyekasirika sana alimkimbiza dada mmoja kutoka katika nyumba fulani na kumpiga teke kwa nguvu sana kwenye uti wa mgongo hivi kwamba dada huyo akaanguka chini kwa kichwa na kuumia. Alihitaji kupata matibabu; lakini polisi hawakumchukulia hatua yoyote mtu aliyemshambulia. Mashahidi wengine walikamatwa na polisi, alama za vidole vyao zikachukuliwa, wakapigwa picha, na kufungwa gerezani usiku kucha. Wasimamizi wa mahali pa kufanyia mikutano huko Moscow walitishwa kwamba wangefutwa kazi ikiwa wangeendelea kuwaruhusu Mashahidi kukodi majengo yao. Muda si muda, makutaniko mengi yalifukuzwa katika majengo waliyokodi. Makutaniko 40 yamelazimika kutumia jengo lenye Majumba manne ya Ufalme. Kutaniko moja linalotumia jengo hilo lililazimika kufanya Mkutano wa Watu Wote saa moja na nusu asubuhi. Mwangalizi mmoja anayesafiri alisema hivi: “Ili kuhudhuria mkutano, wahubiri walihitaji kuamka saa 11 asubuhi, lakini walifanya hivyo kwa kupenda kwa zaidi ya mwaka mmoja.”

“ILI KUWA USHAHIDI”

Ili kuthibitisha kwamba marufuku ya Moscow yalivunja sheria, katika Desemba (Mwezi wa 12) 2004 wanasheria wetu walitafuta msaada katika Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu. (Ona sanduku “Kwa Nini Uamuzi wa Urusi Ulichunguzwa Tena Huko Ufaransa?” kwenye ukurasa wa 6.) Miaka sita baadaye, katika Juni 10, 2010, Mahakama ilifanya uamuzi wa pamoja ambao ulionyesha kwamba Mashahidi wa Yehova hawana hatia hata kidogo! * Mahakama hiyo ilichunguza mashtaka yote ambayo yalitolewa juu yetu na ikapata kwamba hayakuwa na msingi wowote. Ilisema pia kwamba Urusi ilikuwa na daraka la kisheria la “kuzuia uvunjaji wa sheria ambao Mahakama hiyo ilipata na kurekebisha mambo kadiri iwezekanavyo.”—Ona sanduku “Uamuzi wa Mahakama,” kwenye ukurasa wa 8.

Maamuzi ya Mahakama hiyo ambayo yanaeleza waziwazi jinsi Makubaliano au Mkataba wa Ulaya unavyolinda kazi ya Mashahidi wa Yehova hayahusu tu Urusi bali pia mataifa mengine 46 ambayo ni sehemu ya Baraza la Ulaya. Zaidi ya hayo, kwa sababu ya maelezo yake ya ndani sana kuhusu uchunguzi wa kisheria na mambo ya hakika, mambo hayo yatasomwa kwa makini na wasomi wa mambo ya sheria, mahakimu, wale wanaotunga sheria, na wataalamu wa haki za kibinadamu ulimwenguni pote. Kwa nini? Ili kufikia uamuzi wake, Mahakama hiyo haikutaja tu maamuzi manane ambayo ilifanya zamani ambayo yanawaunga mkono Mashahidi wa Yehova bali pia ilitaja kesi tisa ambazo Mashahidi wa Yehova walishinda kabla ya hapo katika mahakama kuu zaidi huko Afrika Kusini, Argentina, Hispania, Japani, Kanada, Marekani, Uingereza, na Urusi. Maamuzi hayo pamoja na hatua ya Mahakama hiyo ya kupinga vikali sana mashtaka yaliyotolewa na kiongozi wa mashtaka wa Moscow yanawapa Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote kifaa chenye nguvu sana cha kutumia ili kutetea imani na kazi yao.

Yesu aliwaambia wafuasi wake hivi: “Mtakokotwa na kupelekwa mbele ya magavana na wafalme kwa ajili yangu, ili kuwa ushahidi kwao na kwa mataifa.” (Mt. 10:18) Mapambano ya kisheria ambayo yalitokea katika miaka 15 iliyopita yaliwapa ndugu zetu nafasi ya kutangaza jina la Yehova kuliko wakati mwingine wowote huko Moscow na sehemu nyingine. Kwa kweli, uchunguzi, kesi za mahakama, na uamuzi wa mahakama ya kimataifa ambao umewakazia uangalifu Mashahidi ‘umekuwa ushahidi’ na umesaidia “kuendeleza mbele habari njema.” (Flp. 1:12) Kwa hakika, Mashahidi huko Moscow wanaposhiriki katika kazi ya kuhubiri leo, wenye nyumba wengi wanauliza hivi: “Ninyi watu si mlipigwa marufuku?” Mara nyingi swali au ulizo hilo linawapa ndugu zetu nafasi ya kuwaeleza wenye nyumba habari zaidi kuhusu mafundisho yetu. Ni wazi kwamba hakuna upinzani wowote unaoweza kutuzuia tusihubiri habari njema ya Ufalme. Tunasali ili Yehova aendelee kuwabariki na kuwatunza ndugu na dada zetu wapendwa na wenye ujasiri huko Urusi.

[Maelezo ya Chini]

^ Kesi hiyo ilifunguliwa mnamo Aprili 20, 1998. Baada ya majuma mawili, tarehe 5 Mei (Mwezi wa 5), nchi ya Urusi ilitia sahihi Makubaliano au Mkataba wa Ulaya Unaohusu Haki za Kibinadamu.

^ “Sheria hiyo ilifuatwa kwa sababu ya uchochezi mkubwa wa Kanisa Othodoksi la Urusi, ambalo linalinda kwa wivu cheo chake nchini Urusi na linatamani kuona Mashahidi wa Yehova wakipigwa marufuku.”​—Associated Press, Juni 25, 1999.

^ Inashangaza kwamba tarehe hiyohiyo ilikuwa pia tarehe ya kusherehekea miaka kumi tangu Urusi ilipopitisha sheria inayowatambua Mashahidi wa Yehova kuwa watu walioteswa kwa msingi wa dini wakati wa utawala wa Sovieti.

^ Marufuku hayo yalisababisha kufungwa kwa shirika lililoandikishwa kisheria ambalo lilikuwa likitumiwa na makutaniko huko Moscow. Wapinzani walitumaini kwamba kufungwa kwa shirika hilo kungewazuia ndugu zetu kuendelea na huduma yao.

^ Mnamo Novemba 22, 2010 (22/11/2010), kikundi cha mahakimu watano wa Baraza Kuu la Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu kilikataa ombi la Urusi la kutaka kesi hiyo ipelekwe katika Baraza Kuu la Mahakama hiyo. Walipokataa ombi hilo, walionyesha kwamba uamuzi wa Juni 10, 2010, ulikuwa wa mwisho na hivyo unapaswa kutekelezwa.

[Sanduku/​Picha katika ukurasa wa 6]

Kwa Nini Uamuzi wa Urusi Ulichunguzwa Tena Huko Ufaransa?

Mnamo Februari 28, 1996 (28/2/1996), Urusi ilitia sahihi Mkataba wa Ulaya wa Haki za Kibinadamu. (Mnamo Mei 5, 1998, Urusi ilikubali rasmi Mkataba huo.) Serikali ya Urusi ilipotia sahihi mkataba huo, ilitangaza kwamba raia wake wana

‘haki ya uhuru wa kidini na haki ya kufuata dini yao wakiwa nyumbani au mbele ya watu na kubadili dini yao ikiwa wanataka kufanya hivyo.’​—Kifungu cha 9.

‘haki ya kusema na kuandika kwa njia inayofaa mambo wanayofikiri na kuwapa wengine habari.’​—Kifungu cha 10.

‘haki ya kuhudhuria mikutano inayofanywa kwa amani.’​—Kifungu cha 11.

Mashirika au mtu mmoja-mmoja ambaye anatendewa vibaya kwa sababu ya mkataba huo kutofuatwa na ambao wameshindwa kupata haki kwa njia yoyote ya kisheria katika nchi zao wanaweza kupeleka kesi kwenye Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu huko Strasbourg, Ufaransa (iliyoonyeshwa hapo juu). Mahakama hiyo ina mahakimu au waamuzi 47, idadi hiyo inalingana na idadi ya nchi ambazo zilitia sahihi Mkataba wa Ulaya wa Haki za Kibinadamu. Ni lazima maamuzi ya Mahakama hiyo yafuatwe. Nchi ambazo zilitia sahihi mkataba huo ni lazima zikubali maamuzi yake.

[Sanduku katika ukurasa wa 8]

Uamuzi wa Mahakama

Hapa chini pana mafungu matatu mafupi yanayoonyesha uamuzi uliofanywa na Mahakama.

Shtaka moja lilisema kwamba Mashahidi wa Yehova wanavunja familia. Mahakama ilifanya uamuzi uliopinga shtaka hilo. Ilisema hivi:

“Matatizo yanasababishwa na washiriki wa familia ambao si wanadini ambao wanapinga na hawako tayari kukubali na kuheshimu uhuru wa kidini wa watu wao wa ukoo na haki yao ya kufuata dini yao.”​—Fungu la 111.

Mahakama hiyo pia haikupata ushahidi wa kuunga mkono shtaka la kwamba Mashahidi “wanawapofusha watu akili.” Ilisema hivi:

“Mahakama hii inashangaa kwamba mahakama za [Urusi] hazikutaja jina la mtu hata mmoja ambaye inasemekana kwamba haki yake ya kuwa na uhuru wa dhamiri ilipuuzwa kupitia mbinu hizo.”​—Fungu la 129.

Shtaka lingine lilisema kwamba Mashahidi wa Yehova wanaharibu afya ya waamini kwa kutokubali kutiwa damu mishipani. Mahakama hiyo ilitoa uamuzi ambao ni kinyume. Ilisema hivi:

“Uhuru wa kukubali au kukataa matibabu fulani, au kuchagua aina nyingine ya matibabu, ni wa maana katika kanuni za uhuru wa kibinafsi na wa mtu kujiamulia mambo yake mwenyewe. Kwa mfano, mtu mzima ambaye ni mgonjwa ana uhuru wa kuamua ikiwa atakubali au hatakubali matibabu au kufanyiwa upasuaji au, kwa msingi huohuo, ana uhuru wa kuamua kama atatiwa damu mishipani.”​—Fungu la 136.