Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Intaneti Kutumia kwa Hekima Kifaa cha Ulimwenguni Pote

Intaneti Kutumia kwa Hekima Kifaa cha Ulimwenguni Pote

Intaneti Kutumia kwa Hekima Kifaa cha Ulimwenguni Pote

MASHINI za kupiga chapa zilipoanza kutumiwa karne nyingi zilizopita, njia ya watu ya kupashana habari ilibadilika. Katika nyakati zetu, kuanzishwa kwa Intaneti kumelinganishwa na mabadiliko hayo. Kifaa hicho chenye faida kimeitwa kifaa cha ulimwenguni pote cha kupashana habari, na ndivyo ilivyo. Unapotumia “mtandao huo bora wa habari,” unaweza kupata habari za hakika, hesabu au idadi za vitu mbalimbali, na maoni kuhusu mambo mengi mbalimbali.

Uwezo wa kupashana habari ni zawadi nzuri ajabu kutoka kwa Muumba wetu. Uwezo huo unatuwezesha kuzungumza kuhusu mawazo mbalimbali na kupashana habari na wengine. Yehova ndiye aliyekuwa wa kwanza kupashana habari na familia yake ya kibinadamu. Alitoa habari iliyo wazi na inayoeleweka kuhusu jinsi ya kuwa na maisha yenye kusudi. (Mwa. 1:28-30) Hata hivyo, kama mambo yaliyotokea mwanzoni mwa historia ya wanadamu yanavyoonyesha, zawadi ya kupashana habari inaweza kutumiwa vibaya. Shetani alimwambia Hawa habari ya uwongo kabisa. Hawa alikubali mambo ambayo Shetani alimwambia naye akamjulisha Adamu, ambaye aliwaongoza wanadamu kuingia katika msiba.—Mwa. 3:1-6; Rom. 5:12.

Tunaweza kusema nini kuhusu kutumia Intaneti? Ingawa Intaneti inaweza kuwa na habari zenye thamani, inaweza kuokoa wakati wetu, na kutuletea faida, inaweza pia kutupotosha, kutumia wakati wetu mwingi, na kuchafua maadili yetu. Acheni tuone jinsi tunavyoweza kutumia kifaa hiki cha ulimwenguni pote kwa faida yetu.

Je, Ni Habari za Kutegemeka au za Uwongo?

Usifikiri kamwe kwamba habari zote zinazopatikana katika Intaneti ni nzuri na ni zenye faida. Vituo vya kutafuta habari katika Intaneti vinaweza kulinganishwa na kikundi kikubwa cha watu wanaovuna kwa bidii uyoga wa kila aina, wanavuna uyoga unaoweza kuliwa na uyoga wenye sumu, na kukusanya uyoga wote katika kikapu kimoja na kutugawia ili tule. Je, ungeanza kula bila kuchunguza kila uyoga kwa uangalifu? Bila shaka huwezi kufanya hivyo! Vituo vya kutafuta habari katika Intaneti vinatumia kompyuta nyingi kuchagua au kukusanya habari kutoka katika mabilioni ya vituo vyenye habari za kila aina, kuanzia habari nzuri sana mpaka habari mbaya zaidi. Tunahitaji utambuzi ili kutenganisha kwa njia ya mfano ngano kutoka katika makapi, ili akili zetu zisitiwe sumu na habari zenye kupotosha.

Mwaka wa 1993, gazeti moja linalojulikana sana lilikuwa na mchoro ambao ulionyesha mbwa wawili wakiwa mbele ya kompyuta. Mbwa mmoja anamwambia hivi yule mwingine: “Katika Intaneti, hakuna mtu anayejua kwamba wewe ni mbwa.” Zamani za kale, Shetani alijificha kwa kumtumia nyoka kuanzisha mazungumzo na Hawa na kumwambia kwamba angekuwa kama Mungu. Leo, mtu yeyote ambaye anaweza kutumia Intaneti anaweza kujifanya kuwa profesa, kana kwamba anajua kila jambo, bila hata kufunua jina lake. Na hakuna sheria zinazomzuia mtu yeyote kuweka mawazo, habari, picha, na mapendekezo katika Intaneti.

Unapotumia Intaneti usiwe mpumbavu kama Hawa. Uwe mwangalifu sana kabla ya kuamini habari unayopata katika Intaneti. Kabla ya kuamini habari, jiulize hivi: (1) Ni nani aliyeandika habari hiyo? Mwandishi huyo ana sifa au mamlaka gani kuhusu habari ambazo anaandika? (2) Kwa nini aliandika habari hiyo? Ni nini kilichomchochea mwandishi huyo kuandika habari hiyo? Je, anapendelea upande fulani? (3) Mwandishi huyo alipata wapi habari hiyo? Je, anataja vyanzo vya habari ambavyo vinaweza kuchunguzwa? (4) Je, habari hiyo ni ya karibuni? Katika karne ya kwanza, mtume Paulo alimpa Timotheo mashauri ambayo yanafaa kabisa leo. Paulo aliandika hivi: “Linda lililowekwa amana kwako, ukigeuka mbali kutoka kwenye maneno matupu ambayo huchafua mambo matakatifu na kutoka kwenye maneno yanayopingana ya ule unaoitwa kwa uwongo ‘ujuzi.’”—1 Tim. 6:20.

Je, Inaokoa Wakati au Inapoteza Wakati?

Bila shaka, Intaneti ikitumiwa kwa hekima inaweza kutusaidia kuokoa wakati, nguvu, na pesa. Tunaweza kununua kwa urahisi kitu fulani bila kuondoka nyumbani. Kulinganisha bei za vitu kunaweza kutusaidia kuokoa pesa. Kutumia Intaneti kushughulikia mambo ya benki kumefanya maisha ya watu wengi yawe rahisi zaidi; mtu anaweza kushughulikia mambo ya kifedha wakati wowote akiwa amestarehe nyumbani. Intaneti ina vifaa muhimu vya kupanga safari kwa njia inayofaa na inayookoa pesa na inatusaidia kushika nafasi mapema au kulipia mapema huduma tunazohitaji. Tunaweza kutafuta haraka nambari za simu, anwani, na njia mbalimbali za kufika mahali tunapotaka kwenda. Ulimwenguni pote, ofisi za tawi za Mashahidi wa Yehova zinatumia huduma nyingi za Intaneti ili kuokoa wakati, pesa, na kutumia wafanyakazi wachache.

Hata hivyo, tunapaswa pia kuchunguza hatari ya kutumia Intaneti. Hatari hiyo inahusu kiasi cha wakati ambacho tunaweza kutumia katika Intaneti. Kwa watu fulani, Intaneti imekuwa kifaa cha kuchezea chenye kuvutia badala ya kuwa kifaa chenye faida. Wanatumia wakati mwingi kupita kiasi kucheza, kununua vitu, kuzungumza na wengine, kutuma barua, kutafuta-tafuta habari, na kuchunguza mambo mbalimbali. Mwishowe, huenda wakaanza kupuuza mambo yaliyo ya maana zaidi yanayohusu familia, marafiki, na kutaniko. Hata mtu anaweza kuwa na zoea la kutumia Intaneti kupita kiasi. Kwa mfano, uchunguzi ambao ulichapishwa katika mwaka wa 2010 ulionyesha kwamba asilimia 18.4 ya vijana nchini Korea wana zoea la kutumia Intaneti kupita kiasi. Huko Ujerumani, watafiti walisema kwamba “wanawake wengi zaidi wanalalamika kwamba wenzi wao wa ndoa wana zoea la kutumia Intaneti kupita kiasi.” Mwanamke mmoja alilalamika kwamba zoea la kutumia Intaneti kupita kiasi limemfanya mume wake abadilike kabisa hivi kwamba ndoa yao imeharibika.

Ofisi fulani ya tawi ya Mashahidi wa Yehova ilipokea barua kutoka kwa mtu ambaye alijiita mlevi wa Intaneti. Nyakati nyingine alitumia Intaneti kwa muda wa karibu saa 10 kwa siku. Baada ya kusema kwamba “mwanzoni jambo hilo halikuonekana kuwa hatari,” aliongeza hivi: “Baada ya muda, sikuhudhuria mikutano kwa ukawaida na nikaacha kusali.” Alipohudhuria mikutano, hakuwa amejitayarisha na katika akili yake alitamani kurudi nyumbani ili atumie Intaneti tena. Inafurahisha kwamba alitambua uzito wa tatizo hilo na kuchukua hatua za kurekebisha mambo. Tusifikie kamwe hatua ya kutumia Intaneti kupita kiasi.

Je, Ni Habari Zinazofaa au Zisizofaa?

Katika andiko la 1 Wathesalonike 5:21, 22, tunasoma hivi: “Hakikisheni mambo yote; shikeni sana yaliyo mazuri. Jiepusheni na kila namna ya uovu.” Tunahitaji kujua ikiwa habari tunazopata katika Intaneti zinampendeza Mungu, na zinapatana na viwango vyake vya juu. Zinapaswa kuwa habari zenye maadili yanayofaa na zinazomfaa Mkristo. Ponografia (picha au habari za ngono) zimeenea sana hasa katika Intaneti, na tusipokuwa waangalifu, zinaweza kwa urahisi kutushawishi tuanguke katika mtego huo.

Ni jambo la hekima kwetu kujiuliza, ‘Je, ninatazama mambo ambayo nitaficha haraka ikiwa mwenzi wangu wa ndoa, wazazi wangu, au ndugu zangu Wakristo wataingia chumbani?’ Ikiwa jibu ni ndiyo, itakuwa vizuri kutumia Intaneti wakati tu ambapo kuna watu wengine. Kwa kweli, Intaneti imebadili jinsi tunavyopashana habari na kununua vitu. Zaidi ya hayo, imefungua njia mpya kabisa ya ‘kufanya uzinzi moyoni mwetu.’—Mt. 5:27, 28.

Tuwatumie au Tusiwatumie Wengine Habari Kupitia Intaneti?

Kutumia Intaneti kunatia ndani kupata habari na pia kuzieneza. Ingawa tuna uhuru wa kupokea na kuwatumia wengine habari, pia tuna daraka la kuhakikisha kwamba habari hizo ni za kweli na ni safi kiadili. Je, tunaweza kuthibitisha kwamba habari tunazoandika au kuwatumia wengine ni sahihi? Je, tuna ruhusa ya kueneza habari hizo? * Je, ni habari zinazofaa na zenye kujenga? Tuna nia gani tunapoeneza habari hizo? Je, tunataka kufanya hivyo ili wengine watusifu?

Barua zinazotumwa kupitia Intaneti zinaweza kuwa na faida sana zinapotumiwa kwa njia inayofaa. Tunaweza kupata pia habari nyingi sana kupitia barua hizo. Je, tunawalemea wengine kwa kueneza habari mpya au mambo yasiyofaa kwa marafiki wengi, labda tukitumia wakati wao wenye thamani? Je, hatupaswi kuchunguza nia yetu kabla ya kueneza habari kupitia Intaneti? Kwa kweli tuna kusudi gani? Zamani watu waliandika barua ili kueleza mambo yanayowahusu wao pamoja na familia na marafiki wao, wakiwajulisha wengine hali yao. Je, hatupaswi kuandika barua-pepe tukiwa na kusudi hilo? Kwa nini tuwatumie wengine habari ambazo hatuwezi kuzithibitisha?

Hivyo basi, tunapaswa kufanya nini kuhusiana na Intaneti? Je, tuiepuke kabisa? Nyakati nyingine huenda tukahitaji kufanya hivyo. Yule mlevi wa Intaneti ambaye alitajwa mapema alifanya hivyo ili aache uzoefu wake wa miaka mingi. Kwa upande mwingine, Intaneti inaweza kutufaidi, ikiwa tutaacha ‘uwezo wa kufikiri ututunze na utambuzi utulinde.’—Met. 2:10, 11.

[Maelezo ya Chini]

^ Habari hii inahusu pia picha. Ingawa tunaweza kupiga picha zetu binafsi, huenda hatuna ruhusa ya kuzieneza, wala hata kusambaza majina ya watu ambao wako katika picha hizo na kutaja mahali wanapoishi.

[Picha katika ukurasa wa 4]

Unaweza kuepuka jinsi gani habari zenye kupotosha?

[Picha katika ukurasa wa 5]

Unapaswa kufikiria nini kabla ya kueneza habari kupitia Intaneti?