Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Je, tunaweza kujua hesabu kamili ya unabii mbalimbali kumhusu Masihi ulio katika Maandiko ya Kiebrania?

Kuchunguza Maandiko ya Kiebrania kwa makini kunatusaidia kutambua unabii mwingi ambao ulitimizwa na Yesu Kristo. Unabii huo mbalimbali ulitabiri kuhusu malezi ya Masihi, wakati ambapo angetokea, mambo ambayo angefanya, jinsi ambavyo angetendewa, na mahali pake katika mpango wa Yehova Mungu. Unabii huo unapatana ili kutokeza picha moja kubwa ambayo inatusaidia kumtambua Yesu kuwa Masihi. Hata hivyo, tunahitaji kuwa waangalifu tunapojaribu kujua hesabu kamili ya unabii mbalimbali kumhusu Masihi unaopatikana katika Maandiko ya Kiebrania.

Si kila mtu anayekubali kwamba unabii fulani unamhusu au haumhusu Masihi. Katika kitabu chake (The Life and Times of Jesus the Messiah), Alfred Edersheim alisema kwamba maandishi ya marabi yaliorodhesha masimulizi 456 kutoka katika Maandiko ya Kiebrania kuwa yanamhusu Masihi hata ingawa masimulizi mengi kati ya hayo hayamtaji Masihi moja kwa moja. Kuchunguza kwa makini masimulizi hayo 456 kunatokeza maswali ikiwa masimulizi fulani kati ya hayo ni unabii unaomhusu Yesu Kristo. Kwa mfano, Edersheim alisema kwamba Wayahudi waliona kuwa andiko la Mwanzo 8:11 linamhusu Masihi. Waliamini kwamba “jani la mzeituni, ambalo lililetwa na yule njiwa, lilitoka kwenye Mlima wa Masihi.” Mwandishi huyo alitaja pia Kutoka 12:42. Akieleza jinsi Wayahudi walivyoelewa andiko hilo kimakosa, aliandika hivi: “Kama vile Musa alivyotoka jangwani, ndivyo Masihi atakavyotoka Roma.” Bila shaka, wasomi wengi na watu wengine wangeona kwamba ni vigumu kumhusianisha Yesu Kristo na maandiko hayo mawili na maelezo yake yenye makosa.

Hata tukikazia fikira tu unabii ambao hasa ulitimizwa na Yesu Kristo, tunapata matatizo ya kukubaliana kuhusu hesabu kamili ya unabii huo. Kwa mfano, fikiria Isaya sura ya 53, ambayo ina mambo mbalimbali ya kinabii kumhusu Masihi. Andiko la Isaya 53:2-7 linatabiri hivi: “Yeye hana umbo la fahari . . . Alidharauliwa na kuepukwa na wanadamu . . . Yeye mwenyewe aliyachukua magonjwa yetu . . . Alikuwa akichomwa kwa silaha kwa ajili ya ukosaji wetu . . . Alikuwa akiletwa kama kondoo machinjioni.” Je, mambo yanayotajwa katika Isaya 53 yanapaswa kuonwa kuwa unabii mmoja kumhusu Masihi, au je, mambo hayo yanapaswa kuonwa kuwa unabii mbalimbali?

Fikiria pia andiko la Isaya 11:1, ambalo linasema hivi: “Tawi litatoka katika kisiki cha Yese; na kutoka katika mizizi yake chipukizi litazaa.” Katika mstari wa 10, unabii huo unarudiwa tena, kwa maneno yanayofanana na hayo. Je, tunapaswa kuhesabu mistari hiyo miwili kuwa maelezo mawili tofauti ya kinabii au kama unabii mmoja unaorudiwa? Ni wazi kwamba uamuzi unaofikiwa kuhusu Isaya sura ya 53 na Isaya sura ya 11 unaweza kuongeza au kupunguza hesabu kamili ya unabii kuhusu Masihi.

Hivyo, ni vizuri tuepuke kutafuta hesabu kamili ya unabii unaomhusu Masihi katika Maandiko ya Kiebrania. Tengenezo la Yehova limechapisha orodha zinazoonyesha unabii mwingi kumhusu Yesu na jinsi ulivyotimizwa. * Orodha hizo zinaweza kutusaidia na kututia moyo katika funzo letu la kibinafsi, la familia, na katika huduma yetu ya hadharani. Zaidi ya hayo, unabii mbalimbali kumhusu Masihi, bila kujali hesabu kamili, unatupatia uthibitisho wenye nguvu kwamba Yesu ndiye Kristo, au Masihi.

[Maelezo ya Chini]

^ Insight on the Scriptures, Buku la 1, ukurasa wa 1223; Buku la 2, ukurasa wa 387; (Étude perspicace des Écritures, Buku la 1, ukurasa wa 1210; Buku la 2, ukurasa wa 272), “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa,” ukurasa wa 343-344; Biblia Inafundisha Nini Hasa? ukurasa wa 200.