Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Yehova—“Mungu Anayetoa Amani”

Yehova—“Mungu Anayetoa Amani”

Yehova—“Mungu Anayetoa Amani”

“Mungu anayetoa amani na awe pamoja nanyi nyote.”—ROM. 15:33.

1, 2. Andiko la Mwanzo sura ya 32 na 33 linaeleza kuhusu hali gani yenye kuogopesha, na matokeo yalikuwa nini?

 NDUGU wawili wako karibu kukutana huko Penueli, karibu na bonde la Yaboki upande wa mashariki wa mto Yordani. Esau amesikia kwamba ndugu yake pacha, Yakobo, anarudi nyumbani. Hata ingawa miaka 20 imepita tangu Esau alipomuuzia ndugu yake haki yake ya kuwa mzaliwa wa kwanza, Yakobo anaogopa kwamba huenda ndugu yake bado amekasirika na anataka kumuua. Esau anaenda na wanaume 400 kumwona ndugu yake ambaye alikosana naye. Akitazamia kwamba ndugu yake atamshambulia, Yakobo anawatuma watumishi wake wampelekee Esau zawadi nyingi sana za wanyama zaidi ya 550 wa kufugwa. Kila mara, watumishi wa Yakobo wanapompa Esau kikundi cha wanyama, wanamwambia kwamba ni zawadi kutoka kwa ndugu yake.

2 Mwishowe ndugu hao wawili wanakutana! Yakobo anapotembea kwa ujasiri kumwelekea Esau, anainama chini, si mara moja tu bali mara saba. Tayari Yakobo amefanya jambo la maana zaidi ili kuutuliza moyo wa ndugu yake. Yakobo amesali kwa Yehova ili amkomboe kutoka katika mkono wa Esau. Je, Yehova anajibu sala hiyo? Ndiyo. Biblia inatuambia hivi: “Esau akaanza kukimbia kwenda kumpokea. Naye akaanza kumkumbatia na kumwangukia shingoni, akambusu.”—Mwa. 32:11-20; 33:1-4.

3. Tunajifunza nini kutokana na simulizi kuhusu Yakobo na Esau?

3 Simulizi hilo kuhusu Yakobo na Esau linaonyesha kwamba tunapaswa kujikaza kabisa na kuchukua hatua zinazofaa ili kutatua matatizo ambayo yanaweza kuharibu amani tunayofurahia katika kutaniko la Kikristo. Yakobo alijitahidi kufanya amani pamoja na Esau, lakini si kwa sababu Yakobo alikuwa amemkosea ndugu yake na alihitaji kumwomba msamaha. Hapana, Esau alikuwa amedharau haki yake ya kuwa mzaliwa wa kwanza na akamuuzia Yakobo haki hiyo kwa bakuli la mchuzi. (Mwa. 25:31-34; Ebr. 12:16) Hata hivyo, njia ambayo Yakobo alitumia kumfikia Esau inaonyesha jinsi tunavyopaswa kujitahidi sana ili kudumisha amani pamoja na ndugu zetu Wakristo. Inaonyesha pia kwamba Mungu wa kweli anabariki sala na jitihada zetu za kufanya amani. Biblia ina mifano mingine mingi sana ambayo inatufundisha kuwa watu wenye kufanya amani.

Mfano Bora Kabisa wa Kuiga

4. Mungu alifanya nini ili awaokoe wanadamu kutoka katika dhambi na kifo?

4 Yehova ambaye ni “Mungu anayetoa amani” ameweka mfano bora kabisa katika kufanya amani. (Rom. 15:33) Fikiria mambo yote ambayo Yehova alifanya ili tuweze kuwa na uhusiano wenye amani pamoja naye. Tukiwa wazao wenye dhambi wa Adamu na Hawa, tunastahili “mshahara ambao dhambi hulipa.” (Rom. 6:23) Hata hivyo, kwa sababu anatupenda sana, Yehova alifanya mpango wa kutuokoa kwa kumtuma Mwana wake mpendwa kutoka mbinguni ili azaliwe akiwa mwanadamu mkamilifu. Na Mwana wake alikubali kwa kupenda. Yeye mwenyewe alikubali maadui wa Mungu wamuue. (Yoh. 10:17, 18) Mungu wa kweli alimfufua Mwana wake mpendwa, ambaye baada ya kufufuliwa alimtolea Baba yake thamani ya damu yake iliyomwagwa, ambayo ingekuwa fidia au dhabihu ya ukombozi ya kuwaokoa watenda-dhambi wanaotubu ili wasife milele.—Soma Waebrania 9:14, 24.

5, 6. Damu ya Yesu iliyomwagwa inawasaidia jinsi gani wanadamu wenye dhambi kuwa tena na uhusiano wenye amani pamoja na Mungu?

5 Kwa sababu ya dhambi, uhusiano kati ya Mungu na wanadamu uliharibika. Dhabihu ya ukombozi ya Mwana wa Mungu inawasaidia wanadamu jinsi gani? Andiko la Isaya 53:5 linasema: ‘Alikuwa akipondwa kwa ajili ya makosa yetu. Na kwa sababu ya majeraha yake sisi tumeponywa.’ Badala ya kuonwa kuwa maadui wa Mungu, wanadamu watiifu wanaweza sasa kuwa na uhusiano wenye amani pamoja na Mungu. “Kwa njia [ya Yesu] tuna kuachiliwa huru kwa njia ya fidia kupitia damu ya huyo, ndiyo, msamaha wa makosa yetu.”—Efe. 1:7.

6 Biblia inasema hivi: “Mungu aliona ni vema ujazo wote ukae katika [Kristo].” Alifanya hivyo kwa sababu Kristo ndiye mtu wa maana zaidi katika kutimizwa kwa kusudi la Mungu. Na Yehova ana kusudi gani? Kusudi lake ni ‘kupatanisha tena kwake mwenyewe vitu vingine vyote kwa kufanya amani kupitia damu iliyomwagwa’ ya Yesu Kristo. “Vitu vingine vyote” ambavyo Mungu analeta katika uhusiano wenye amani pamoja naye ni “vitu vilivyo mbinguni” na “vitu vilivyo duniani.” Ni vitu gani hivyo?—Soma Wakolosai 1:19, 20.

7. Ni nini “vitu vilivyo mbinguni” na “vitu vilivyo duniani” ambavyo vinakuwa na uhusiano wenye amani pamoja na Mungu?

7 Kwa sababu ya dhabihu ya ukombozi ya Yesu, Wakristo watiwa-mafuta ‘wametangazwa kuwa waadilifu’ wakiwa wana wa Mungu, ili ‘wafurahie amani pamoja na Mungu.’ (Soma Waroma 5:1.) Wanaitwa “vitu vilivyo mbinguni” kwa sababu wana tumaini la kwenda mbinguni na “watatawala wakiwa wafalme juu ya dunia” na kumtumikia Mungu wakiwa makuhani. (Ufu. 5:10) Kwa upande mwingine, “vitu vilivyo duniani” ni wanadamu wenye kutubu, ambao mwishowe watapata uzima wa milele duniani.—Zab. 37:29.

8. Mfano wa Yehova unakusaidia jinsi gani matatizo yanapotokea katika kutaniko?

8 Paulo aliwaandikia Wakristo watiwa-mafuta huko Efeso akieleza uthamini wake wa kutoka moyoni kwa ajili ya uandalizi huo kutoka kwa Yehova: “Mungu, aliye tajiri katika rehema, . . . alitufanya hai pamoja na Kristo, tulipokuwa wafu katika makosa—kwa fadhili zisizostahiliwa ninyi mmeokolewa.” (Efe. 2:4, 5) Iwe tuna tumaini la kwenda mbinguni au la kuishi duniani, tuna deni kubwa sana kwa Mungu kwa sababu ya rehema na fadhili zake zisizostahiliwa. Tunapofikiria mambo yote ambayo Yehova alifanya ili kuwawezesha wanadamu kufurahia tena uhusiano wenye amani pamoja naye mioyo yetu inajaa shukrani. Wakati matatizo yanapotokea ambayo yanahatarisha umoja na amani ya kutaniko, je, hatupaswi kufikiria mfano wa Mungu na kuchochewa kufanya amani?

Kujifunza Kutokana na Mfano wa Abrahamu na Isaka

9, 10. Abrahamu alionyesha jinsi gani kwamba alitaka kufanya amani na wengine?

9 Biblia inasema hivi kuhusu mzee wa ukoo Abrahamu: “‘Abrahamu alikuwa na imani katika Yehova, na ikahesabiwa kwake kuwa ni uadilifu,’ naye akaitwa ‘rafiki ya Yehova.’” (Yak. 2:23) Abrahamu alionyesha imani yake kwa kuchukua hatua zilizoonyesha kwamba alipenda amani. Kwa mfano, makundi ya wanyama wa Abrahamu yalipoongezeka, ugomvi ulitokea kati ya wachungaji wake na wachungaji wa Loti, mwana wa ndugu yake. (Mwa. 12:5; 13:7) Abrahamu na Loti waliamua kwamba njia nzuri ya kutatua tatizo hilo ni kutengana. Abrahamu angeshughulikia jinsi gani tatizo hilo gumu? Badala ya kutumia umri wake na uhusiano wake wa pekee pamoja na Mungu kumwambia mwana wa ndugu yake jambo la kufanya, Abrahamu alionyesha wazi kwamba alikuwa mfanya-amani wa kweli.

10 Abrahamu alimwambia hivi mwana wa ndugu yake: “Tafadhali, usiruhusu ugomvi wowote uendelee kuwa kati yangu na wewe na kati ya wachungaji wangu na wachungaji wako, kwa kuwa sisi ni ndugu.” Kisha mzee huyo wa ukoo akaendelea kusema hivi: “Je, nchi yote haiko mbele yako? Tafadhali, jitenge nami. Ukienda kushoto, mimi nitakwenda kuume; lakini ukienda kuume, mimi nitakwenda kushoto.” Loti alichagua sehemu nzuri zaidi ya nchi, lakini Abrahamu hakumkasirikia moyoni. (Mwa. 13:8-11) Baadaye Loti alipochukuliwa mateka na majeshi yaliyovamia, Abrahamu hakusita kumwokoa mwana wa ndugu yake.—Mwa. 14:14-16.

11. Abrahamu alifuatilia amani jinsi gani pamoja na majirani wake Wafilisti?

11 Fikiria pia jinsi Abrahamu alivyofuatilia amani pamoja na majirani wake Wafilisti katika nchi ya Kanaani. Wafilisti walikuwa “wamechukua kwa jeuri” kisima cha maji kilichochimbwa na watumishi wa Abrahamu huko Beer-sheba. Mwanamume ambaye alimwokoa mwana wa ndugu yake kwa kuwashinda wafalme wanne waliokuwa wamemteka angeshughulikia jinsi gani hali hiyo? Badala ya kupigana nao na kuchukua kisima chake, Abrahamu aliamua kutosema jambo lolote. Baadaye, mfalme wa Wafilisti alimtembelea Abrahamu ili afanye agano la amani pamoja naye. Abrahamu alizungumza kuhusu kisima hicho kilichoibiwa baada tu ya mfalme huyo kumsihi Abrahamu aape kwamba angewatendea kwa fadhili wazao wa mfalme huyo. Mfalme huyo alishtuka aliposikia jambo hilo hivi kwamba akamrudishia Abrahamu kisima hicho. Abrahamu aliendelea kuishi kwa amani akiwa mkaaji mgeni katika nchi hiyo.—Mwa. 21:22-31, 34.

12, 13. (a) Isaka aliiga jinsi gani mfano wa baba yake? (b) Yehova alibariki jinsi gani jitihada za Isaka za kufanya amani?

12 Isaka, mwana wa Abrahamu, alimwiga baba yake katika kupenda amani. Hilo linaonekana wazi kutokana na jinsi Isaka alivyowatendea Wafilisti. Kwa sababu ya njaa katika nchi, Isaka alihamisha familia yake kutoka katika eneo lenye ukame la Beer-lahai-roi huko Negebu na kwenda Gerari, upande wa kaskazini katika eneo la Wafilisti lenye udongo mzuri zaidi. Akiwa huko, Yehova alimbariki Isaka kwa kumpa mazao mengi na kuongeza mifugo yake. Wafilisti wakaanza kumwonea wivu. Kwa kuwa Wafilisti hawakutaka Isaka afanikiwe kama baba yake, walifunika visima ambavyo watumishi wa Abrahamu walichimba katika eneo hilo. Mwishowe, mfalme wa Wafilisti alimwambia Isaka ‘aondoke katika ujirani wake.’ Isaka, mwanamume aliyependa amani alitii.—Mwa. 24:62; 26:1, 12-17.

13 Baada ya Isaka kuhamia na familia yake mbali zaidi, wachungaji wake walichimba kisima kingine. Wachungaji Wafilisti walidai kwamba maji hayo yalikuwa yao. Kama Abrahamu, baba yake, Isaka hakupigana nao kwa sababu ya kisima. Badala yake, Isaka aliwaambia tena wanaume wake wachimbe kisima. Kwa mara nyingine tena Wafilisti walidai kwamba kisima hicho ni chao. Ili kudumisha amani, Isaka alihamisha familia yake kubwa mpaka eneo lingine. Katika eneo hilo watumishi wake walichimba kisima ambacho Isaka alikiita Rehobothi. Baada ya muda, alihamia eneo lenye rutuba zaidi la Beer-sheba, ambako Yehova alimbariki na kumwambia hivi: “Usiogope, kwa sababu mimi nipo pamoja nawe, nami nitakubariki wewe na kuuzidisha uzao wako kwa sababu ya Abrahamu mtumishi wangu.”—Mwa. 26:17-25.

14. Isaka alionyesha jinsi gani kwamba alikuwa mtu anayefanya amani wakati mfalme wa Wafilisti alipotaka kufanya agano la amani pamoja naye?

14 Bila shaka, Isaka angeweza kupigania haki yake ya kutumia visima vyote ambavyo watumishi wake walichimba. Kwa kweli, mfalme wa Wafilisti na maofisa wake walienda kumtembelea huko Beer-sheba ili wafanye agano la amani pamoja naye, wakisema hivi: “Bila shaka sisi tumeona kwamba Yehova amekuwa pamoja nawe.” Hata hivyo, ili kuwe na amani, Isaka aliamua kuhama mara nyingi badala ya kupigana. Wakati huo pia Isaka alionyesha wazi kwamba yeye ni mtu anayefanya amani. Rekodi ya masimulizi hayo inasema hivi: “Akawafanyia karamu [wageni wake] nao wakala na kunywa. Asubuhi iliyofuata waliamka mapema nao wakatoleana ahadi zenye kiapo. Baada ya hayo Isaka akawaacha waende zao . . . kwa amani.”—Mwa. 26:26-31.

Kujifunza Kutoka kwa Mwana Ambaye Yakobo Alimpenda Zaidi

15. Kwa nini ndugu za Yosefu hawakuzungumza naye kwa amani?

15 Yakobo, mwana wa Isaka alikomaa na kuwa “mwanamume asiye na lawama.” (Mwa. 25:27) Kama tulivyozungumzia mwanzoni, Yakobo alijitahidi kufanya amani pamoja na Esau, ndugu yake. Bila shaka, Yakobo alikuwa amefaidika kutokana na mfano wa Isaka, baba yake ambaye alikuwa mfanya-amani. Tunaweza kusema nini kuhusu wana wa Yakobo? Yakobo alimpenda zaidi Yosefu kati ya wana 12 aliokuwa nao. Yosefu alikuwa mwana mtiifu na mwenye heshima ambaye alimsaidia sana baba yake. (Mwa. 37:2, 14) Hata hivyo, ndugu wakubwa wa Yosefu walimwonea wivu hivi kwamba hawakuzungumza naye kwa njia ya amani. Kwa jeuri, walimuuza Yosefu utumwani na kumdanganya baba yao kwa kumfanya aamini kwamba mnyama-mwitu alikuwa amemuua Yosefu.—Mwa. 37:4, 28, 31-33.

16, 17. Yosefu alionyesha jinsi gani kwamba alipenda amani aliposhughulika na ndugu zake?

16 Yehova alikuwa pamoja na Yosefu. Baada ya muda, Yosefu akawa waziri mkuu wa Misri, mtu wa pili mwenye mamlaka zaidi baada ya Farao. Ndugu za Yosefu walipokuja Misri kununua chakula kwa sababu ya njaa kali, hata hawakumtambua kwa kuwa alikuwa amevaa mavazi ya kifalme ya Misri. (Mwa. 42:5-7) Ingekuwa rahisi kama nini kwa Yosefu kulipiza kisasi kwa ndugu zake kwa sababu ya kumtendea yeye na baba yake kwa jeuri! Hata hivyo, badala ya kulipiza kisasi, Yosefu alijitahidi kufanya amani pamoja nao. Alipoona wazi kwamba ndugu zake walikuwa wametubu, alijitambulisha kwao, akisema: “Msihuzunike wala msijikasirikie kwa sababu mliniuza huku; kwa sababu Mungu alinituma mbele yenu ili kuhifadhi uhai.” Kisha akawabusu ndugu zake wote akawalilia.—Mwa. 45:1, 5, 15.

17 Baada ya kifo cha baba yao Yakobo, ndugu za Yosefu walifikiri kwamba huenda Yosefu angelipiza kisasi juu yao. Walipomweleza kuhusu woga wao, Yosefu ‘alilia’ na kuwajibu hivi: “Msiogope. Mimi nitaendelea kuwapa chakula ninyi na watoto wenu wadogo.” Yosefu ambaye alipenda amani ‘aliwafariji na kusema nao kwa kuwatuliza.’—Mwa. 50:15-21.

“Yaliandikwa ili Kutufundisha”

18, 19. (a) Umefaidika jinsi gani kwa kuchunguza mifano ya watu waliofanya amani ambao wamezungumziwa katika habari hii? (b) Tutazungumzia nini katika habari inayofuata?

18 Paulo aliandika hivi: “Mambo yote yaliyoandikwa zamani yaliandikwa ili kutufundisha sisi, ili kupitia uvumilivu wetu na kupitia faraja kutokana na Maandiko tuwe na tumaini.” (Rom. 15:4) Tumefaidika jinsi gani kwa kuchunguza mfano bora kabisa wa Yehova na pia masimulizi ya Kimaandiko kuhusu Abrahamu, Isaka, Yakobo, na Yosefu?

19 Je, hatuchochewi kufanya yote tunayoweza ili kufuatilia amani pamoja na wengine tunapotafakari na kuthamini mambo ambayo Yehova amefanya ili kurekebisha uhusiano ulioharibika kati yake na wanadamu wenye dhambi? Mifano ya Abrahamu, Isaka, Yakobo, na Yosefu inaonyesha kwamba wazazi wanaweza kuwachochea watoto wao kuiga mfano wao mzuri. Pia, masimulizi hayo yanaonyesha kwamba Yehova anabariki jitihada za wale wanaojitahidi kufanya amani. Haishangazi kwamba Paulo anamwita Yehova, “Mungu anayetoa amani”! (Soma Waroma 15:33; 16:20.) Habari inayofuata itaonyesha kwa nini Paulo alikazia kwamba tunahitaji kufuatilia amani na jinsi tunavyoweza kuwa watu wanaofanya amani.

Umejifunza Nini?

• Yakobo alijitahidi jinsi gani kufanya amani alipokuwa karibu kukutana na Esau?

• Umechochewa jinsi gani na mambo ambayo Yehova alifanya ili kuwawezesha wanadamu kuwa na amani pamoja naye?

• Umejifunza nini kutokana na mfano wa Abrahamu, Isaka, Yakobo, na Yosefu ambao walifanya amani?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 23]

Yakobo alichukua hatua gani ya maana zaidi ili kufanya amani pamoja na Esau?