Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Kusoma Biblia Kumenitia Nguvu Katika Maisha Yangu Yote

Kusoma Biblia Kumenitia Nguvu Katika Maisha Yangu Yote

Kusoma Biblia Kumenitia Nguvu Katika Maisha Yangu Yote

Limesimuliwa na Marceau Leroy

“HAPO mwanzo Mungu aliumba mbingu na dunia.” Nilianza kusoma maneno hayo ya Biblia nikiwa katika chumba changu. Kwa nini nilisoma kisiri? Bila shaka baba yangu, ambaye alikuwa ametangaza waziwazi kwamba haamini kuna Mungu, hangekubali kitabu nilichokuwa nacho, yaani, Biblia.

Sikuwahi kamwe kusoma Biblia kabla ya hapo, na maneno hayo ya utangulizi katika kitabu cha Mwanzo yalinigusa moyo sana. Nilifikiria hivi: ‘Maneno haya yanaeleza kwa nini kuna upatano katika sheria za asili, jambo ambalo limenishangaza sikuzote!’ Nikiwa nimesisimuka, nilisoma kuanzia saa mbili usiku mpaka saa kumi asubuhi. Hivyo ndivyo nilivyoanza zoea la kusoma Neno la Mungu katika maisha yangu. Acheni nieleze jinsi ambavyo kusoma Biblia kumenitia nguvu katika maisha yangu yote.

“Utalazimika Kukisoma Kila Siku”

Nilizaliwa mwaka wa 1926, huko Vermelles, kaskazini mwa Ufaransa, katika kijiji chenye migodi ya makaa ya mawe. Wakati wa vita vya pili vya ulimwengu, makaa ya mawe yalikuwa ya maana sana katika taifa lote. Hivyo, kwa kuwa nilifanya kazi ya kuchimba makaa ya mawe, niliruhusiwa kutojiunga na jeshi. Lakini ili niboreshe maisha yangu, nilianza kujifunza kuwa fundi wa umeme na kurekebisha redio, na hilo liliniwezesha kuona upatano wa nguvu za asili. Nilipokuwa na umri wa miaka 21, mwanafunzi mwenzangu alinipatia Biblia yangu ya kwanza, akaniambia: “Ni kitabu kinachostahili kusomwa.” Nilipomaliza kuisoma, nilikuwa nimesadiki kwamba Biblia ni Neno la Mungu, ujumbe ambao amewafunulia wanadamu.

Kwa sababu nilifikiria kwamba majirani wangu wangesisimka kwa kusoma Biblia, nilinunua nakala nane za Biblia. Nilishangaa walipoanza kunicheka na kunipinga. Watu wa ukoo ambao waliamini ushirikina walinionya hivi: “Mara tu utakapoanza kusoma kitabu hiki, utalazimika kukisoma kila siku!” Kwa kweli nilikisoma, na sijawahi kamwe kujuta kwa kufanya hivyo. Nikawa na zoea la kuisoma maishani.

Baada ya kuona kwamba nilipendezwa na Biblia, majirani fulani walinipa vitabu vya Mashahidi wa Yehova ambavyo walikuwa wamepokea. Vijitabu kama vile Ulimwengu Mmoja, Serikali Moja * (nakala ya Kifaransa imeonyeshwa) vilieleza kwa nini Biblia inasema kwamba Ufalme wa Mungu ndio tumaini pekee la wanadamu. (Mt. 6:10) Nilikuwa nimeazimia kabisa kuwaeleza wengine kuhusu tumaini hilo.

Noël, ambaye alikuwa rafiki yangu tangu utotoni, alikuwa kati ya watu wa kwanza ambao niliwapa Biblia. Kwa sababu alikuwa Mkatoliki mwenye bidii, alifanya mpango ili tukutane na mwanamume aliyekuwa akijifunza ukasisi. Nilikuwa na wasiwasi, hata hivyo, kwa sababu nilikuwa nimesoma Zaburi 115:4-8 na Mathayo 23:9, 10, nilijua kwamba Mungu hataki watu watumie sanamu katika ibada wala hataki viongozi wa kidini wapewe majina ya cheo. Hilo lilinipa ujasiri wa kutetea imani yangu mpya. Matokeo ni kwamba Noël alikubali kweli, na mpaka leo bado ni Shahidi mwaminifu.

Nilimtembelea pia dada yangu. Mume wake alikuwa na vitabu vilivyozungumzia mazoea ya kuwasiliana na pepo na alikuwa akisumbuliwa na roho waovu. Ingawa mwanzoni nilihisi kwamba sikuwa na nguvu, Maandiko ya Biblia kama vile Waebrania 1:14 yalinisadikisha kwamba malaika wa Yehova walikuwa wakinitegemeza. Mume wa dada yangu alipofuata kanuni za Biblia na kutupa kila kitu kilichohusiana na roho waovu, aliacha kusumbuliwa na roho waovu. Yeye na dada yangu wakawa Mashahidi wenye bidii.

Mwaka wa 1947, Arthur Emiot, Shahidi kutoka Marekani, alikuja nyumbani kwangu. Kwa msisimko, nilimuuliza mahali ambapo Mashahidi walikuwa wakikutana. Akaniambia kwamba kulikuwa na kikundi huko Liévin, umbali wa kilomita 10 hivi. Ilikuwa vigumu kupata baiskeli siku hizo, hivyo kwa miezi fulani nilitembea kwenda na kurudi kutoka kwenye mikutano. Kazi ya Mashahidi wa Yehova ilikuwa imepigwa marufuku nchini Ufaransa kwa miaka minane. Kulikuwa na Mashahidi 2,380 tu katika nchi yote, wengi wao wakiwa wahamiaji kutoka Poland. Lakini mnamo Septemba 1, 1947 (1/9/1947), kazi yetu nchini Ufaransa ilitambuliwa tena kisheria. Ofisi ya tawi ilifunguliwa tena huko Villa Guibert, katika mji wa Paris. Kwa vile hakukuwa na painia hata mmoja nchini Ufaransa, toleo la Desemba (Mwezi wa 12) 1947 la Informant (sasa ni Huduma Yetu ya Ufalme) liliwatia moyo wahubiri wawe mapainia wa kawaida na kuhubiri saa 150 kila mwezi. (Mwaka wa 1949, saa hizo zilipunguzwa mpaka saa 100.) Nilikubali kabisa maneno ya Yesu katika Yohana 17:17, “Neno [la Mungu] ni kweli,” na hivyo nikabatizwa mwaka wa 1948, na nikawa painia Desemba 1949.

Kutoka Gerezani na Kurudi Dunkerque

Mgawo wangu wa kwanza ulikuwa wa muda mfupi, na ulikuwa huko Agen, kusini mwa Ufaransa. Kwa sababu nilikuwa nimeacha kazi ya kuchimba makaa ya mawe, kulingana na sheria nilipaswa kujiunga na jeshi. Nilikataa kujiunga na jeshi, hivyo nikafungwa gerezani. Ingawa sikuruhusiwa kuwa na Biblia, nilifanikiwa kupata kurasa chache za kitabu cha Zaburi. Nilitiwa moyo nilipozisoma. Nilipoachiliwa nililazimika kufanya uamuzi: Je, niache utumishi wa wakati wote ili nianze maisha ya kawaida? Wakati huo, jambo fulani nililosoma katika Biblia lilinisaidia. Nilitafakari maneno ya Paulo katika Wafilipi 4:11-13: “Kwa mambo yote nina nguvu kupitia yeye anayenipa nguvu.” Niliamua kuendelea na upainia. Mwaka wa 1950, nilipewa mgawo mpya katika mji wa Dunkerque, ambako nilihubiri zamani.

Nilipofika huko, sikuwa na kitu chochote. Mji huo ulikuwa umeharibiwa sana wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu, na ilikuwa vigumu kupata mahali pa kulala. Niliamua kutembelea familia moja ambayo nilikuwa nikiitembelea zamani, na mwanamke mwenye nyumba alifurahi sana na kusema: “Ah, Bwana Leroy, umeachiliwa! Mume wangu anasema kwamba kama kungekuwa na wanaume wengi kama wewe, hakungekuwa na vita kamwe.” Walikuwa na nyumba ya wageni, hivyo, wakanipa mahali pa kuishi mpaka kipindi cha watalii kilipofika. Siku hiyohiyo, Evans, ndugu ya Arthur Emiot, alinipa kazi. * Alikuwa mtafsiri katika bandari na alikuwa akitafuta mlinzi wa usiku ili alinde meli fulani. Alinitambulisha kwa mmoja wa maofisa wasimamizi wa meli hiyo. Baada ya kuishi gerezani, nilikuwa mwembamba kama sindano. Evans alipomweleza kwa nini nilikuwa mwembamba, ofisa huyo aliniambia nichukue chakula kilichokuwa ndani ya friji. Siku hiyohiyo, nilipata mahali pa kuishi, kazi, na chakula! Uhakika wangu katika maneno ya Yesu kwenye Mathayo 6:25-33 ulitiwa nguvu kwelikweli.

Kipindi cha watalii kilipofika, mimi na painia mwenzangu, Simon Apolinarski, tulilazimika kutafuta mahali pengine pa kuishi, lakini tulikuwa tumeazimia kubaki katika mgawo wetu. Tuliruhusiwa kuishi katika nyumba iliyozeeka ya farasi, ambamo tulilala kwenye magodoro yaliyotengenezwa kwa nyasi zilizokaushwa. Tulihubiri wakati wa mchana. Tulimhubiria mwenye ile nyumba ya farasi, akawa mmoja kati ya watu wengi waliokubali kweli. Baada ya muda mfupi, gazeti la eneo hilo lilichapisha habari ambayo iliwaonya wakaaji wa Dunkerque kuhusu “kuenea kwa kazi ya Mashahidi wa Yehova katika eneo hilo.” Hata hivyo, mimi, Simon, na wahubiri wachache tu ndio tuliokuwa Mashahidi katika eneo hilo! Tulipopata magumu, tulitiwa moyo kwa kutafakari kuhusu tumaini letu la Kikristo na kufikiria jinsi Yehova alivyokuwa ametutunza. Kulikuwa na wahubiri 30 wa kawaida huko Dunkerque nilipopokea mgawo mwingine mwaka wa 1952.

Kutiwa Nguvu kwa Ajili ya Madaraka Mengine

Baada ya kukaa kwa muda mfupi katika mji wa Amiens, niliwekwa rasmi kuwa painia wa pekee huko Boulogne-Billancourt, eneo lililo kando-kando mwa mji wa Paris. Nilipata mafunzo mengi ya Biblia, na baadaye wengine wao wakaanza utumishi wa wakati wote au kazi ya umishonari. Kijana mmoja, Guy Mabilat, alikubali kweli na akaanza kutumika akiwa mwangalizi wa mzunguko na kisha akawa mwangalizi wa wilaya. Baadaye, alisimamia kazi ya ujenzi wa kiwanda cha kuchapisha kwenye eneo ambalo sasa ni Betheli huko Louviers, mji ulio mbali kutoka Paris. Kwa kuzungumza kwa ukawaida kuhusu Biblia katika huduma, Neno la Mungu lilitia mizizi zaidi katika akili yangu na kuniletea shangwe na hilo likaniwezesha kuboresha uwezo wangu wa kufundisha.

Kisha mwaka wa 1953, bila kutazamia, niliwekwa rasmi kuwa mwangalizi wa mzunguko huko Alsace-Lorraine, eneo ambalo lilikuwa chini ya utawala wa Ujerumani mara mbili kati ya mwaka wa 1871 na 1945. Hivyo, nililazimika kujifunza kuzungumza Kijerumani. Wakati nilipoanza kazi ya kuzunguka, kulikuwa na magari machache, televisheni chache, na mashini chache za kupiga chapa katika eneo hilo na hakukuwa na redio wala kompyuta za kibinafsi. Lakini sikuishi maisha ya huzuni na kujinyima raha. Kwa kweli, kilikuwa kipindi chenye shangwe zaidi. Kufuata shauri la Biblia la kuwa na ‘jicho rahisi’ kulimaanisha kwamba kulikuwa na vikengeusha-fikira vichache katika utumishi wa Yehova kuliko ilivyo leo.—Mt. 6:19-22.

Siwezi kusahau kusanyiko la “Ufalme Wenye Ushindi” ambalo lilifanywa huko Paris, mwaka wa 1955. Katika kusanyiko hilo, nilikutana na Irène Kolanski ambaye alikuja kuwa mke wangu, na ambaye alianza utumishi wa wakati wote mwaka mmoja kabla yangu. Wazazi wake ambao walikuwa Wapolandi, walikuwa Mashahidi wa muda mrefu wenye bidii. Wakiwa Ufaransa walitembelewa na Adolf Weber. Alikuwa akitunza bustani ya Ndugu Russell na alikuja Ulaya kuhubiri habari njema. Mimi na Irène tulioana mwaka wa 1956, na akajiunga nami katika kazi ya mzunguko. Amekuwa msaada mkubwa kama nini kwangu kwa miaka mingi!

Miaka miwili baadaye, jambo lingine lenye kusisimua ambalo sikutazamia lilitokea, niliwekwa rasmi kuwa mwangalizi wa wilaya. Hata hivyo, kwa sababu kulikuwa na ndugu wachache waliostahili, niliendelea kutembelea makutaniko fulani nikiwa mwangalizi wa mzunguko. Kilikuwa kipindi chenye shughuli nyingi kama nini! Zaidi ya kuhubiri saa 100 kila mwezi, pia kila juma nilitoa hotuba mbalimbali, nilitembelea vikundi vitatu vya funzo la kitabu, nilikagua rekodi, na kutayarisha ripoti. Ningeweza kununua jinsi gani wakati wa kusoma Neno la Mungu? Nilikuwa na suluhisho moja tu, nilikata kurasa za Biblia iliyozeeka na kubeba kurasa fulani kati ya hizo. Kila nilipolazimika kumngojea mtu fulani, nilitoa kurasa hizo na kuanza kuzisoma. Vipindi hivyo vifupi vya kujiburudisha kiroho vilitia nguvu azimio langu la kuendelea katika mgawo wangu.

Mwaka wa 1967, mimi na Irène tulialikwa kutumika tukiwa washiriki wa kudumu wa familia ya Betheli huko Boulogne-Billancourt. Nilianza kufanya kazi katika Idara ya Utumishi, na sasa baada ya miaka zaidi ya 40 kupita, bado nina pendeleo hilo. Jambo ambalo nimefurahia zaidi katika kazi yangu ni kujibu barua za maswali ya Biblia. Ninafurahia kama nini kuchimba ndani ya Neno la Mungu na ‘kutetea habari njema’! (Flp. 1:7) Pia, ninafurahia kuongoza mazungumzo ya Biblia wakati wa ibada ya asubuhi kabla ya chakula cha asubuhi. Mwaka wa 1976, niliwekwa rasmi kuwa mshiriki wa Halmashauri ya Tawi nchini Ufaransa.

Njia Bora Zaidi ya Maisha

Ingawa nimekabiliana na hali ngumu, wakati mgumu zaidi katika maisha yangu ni sasa ambapo kuzeeka na matatizo ya kiafya yananizuia mimi na Irène kufanya mambo mengi. Lakini, bado kusoma na kujifunza Neno la Mungu pamoja kunatusaidia kuendelea kuwa na tumaini. Tunafurahia kusafiri kwa basi kwenda kwenye eneo la kutaniko letu ili kuzungumza na wengine kuhusu tumaini hilo. Miaka zaidi ya 120 ambayo sote wawili tumekuwa katika utumishi wa wakati wote inatuchochea kuwapendekezea kwa moyo wote wale ambao wangependa kuingia katika utumishi huu wafanye hivyo, kwa kuwa unasisimua, unaleta shangwe, na ndiyo njia nzuri ya kutumia maisha yetu. Mfalme Daudi alipoandika maneno ya Zaburi 37:25, alikuwa ‘amezeeka,’ na kama yeye, mimi pia “sijamwona mtu yeyote mwadilifu akiwa ameachwa kabisa.”

Katika maisha yangu yote, Yehova amenitia nguvu kupitia Neno lake. Watu wangu wa ukoo walitabiri miaka zaidi ya 60 iliyopita kwamba ningekuwa na zoea la kusoma Biblia katika maisha yangu yote. Walisema kweli. Imekuwa hivyo, limekuwa zoea la kila siku ambalo sijajutia kamwe!

[Maelezo ya Chini]

^ Kilichapishwa mwaka wa 1944 lakini sasa hakichapishwi tena.

^ Kwa habari zaidi kuhusu Evans Emiot, ona gazeti la Mnara wa Mlinzi la Januari 1, 1999 (1/1/1999), ukurasa wa 22 na 23.

[Picha katika ukurasa wa 5]

Mimi na Simon

[Picha katika ukurasa wa 5]

Biblia inayofanana na ile niliyopokea mara ya kwanza

[Picha katika ukurasa wa 5]

Nilipokuwa nikitumika nikiwa mwangalizi wa wilaya

[Picha katika ukurasa wa 6]

Siku yetu ya harusi

[Picha katika ukurasa wa 6]

Mimi na Irène tunafurahia kusoma na kujifunza Neno la Mungu