Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Kutembea Kupatana na Roho, Kunamaanisha Uzima na Amani

Kutembea Kupatana na Roho, Kunamaanisha Uzima na Amani

Kutembea Kupatana na Roho, Kunamaanisha Uzima na Amani

‘Tutembee, si kupatana na mwili, bali kupatana na roho.’—ROM. 8:4.

1, 2. (a) Kukengeushwa na mambo mengine wakati mutu anapotembeza gari kunaweza kutokeza hatari gani? (b) Kukengeushwa kiroho kunaweza kutokeza hatari gani?

 KIONGOZI anayesimamia mambo ya usafirishaji katika serikali ya Amerika alisema kwamba misiba inayotokea kwa sababu wale wanaotembeza magari ni wenye kukengeushwa, inazidi kuongezeka sana kila mwaka. Kwa mufano, mutu akitumia telefone ya mukononi anapotembeza gari, jambo hilo linaweza kumukengeusha. Watu wengi walioulizwa walisema kwamba waligongwa ao walikaribia kugongwa na gari lililotembezwa na mutu aliyekuwa akizungumuza kwenye telefone. Mutu kuzungumuza kwenye telefone akiwa mwenye kutembeza gari labda kunaweza kumusaidia amalize tatizo fulani, lakini jambo hilo linaweza pia kutokeza musiba.

2 Inaweza pia kuwa hivyo kuhusu hali yetu ya kiroho. Mutu akikengeushwa anapotembeza gari hawezi kuona hatari iliyo mbele yake, vivyo hivyo yule anayekengeushwa kiroho anaweza kuangukia kwa urahisi katika hatari ya kiroho. Ikiwa tunakengeushwa na mambo mbalimbali, hilo linaweza kuhatarisha maisha yetu ya Kikristo na kutufanya tusitimize utendaji wetu mbalimbali wa Kiteokrasi. Imani yetu inaweza kuharibika kama mashua inayovunjika. (1 Tim. 1:18, 19) Kuhusu hatari hiyo, mutume Paulo aliwaonya Wakristo wenzake katika Roma kwa maneno haya: “Kukaza akili juu ya mwili humaanisha kifo, bali kukaza akili juu ya roho humaanisha uzima na amani.” (Rom. 8:6) Paulo alimaanisha nini? Namna gani tunaweza kuepuka “kukaza akili juu ya mwili” na kuendelea “kukaza akili juu ya roho”?

“Hawana Hukumu ya Hatia”

3, 4. (a) Mutume Paulo aliandika kuhusu pigano gani alilokuwa nalo? (b) Kwa nini tunapaswa kufikiria hali ya mutume Paulo?

3 Katika barua yake kwa Waroma, Paulo aliandika kuhusu pigano lililokuwa kati ya mwili wake na akili yake. (Soma Waroma 7:21-23.) Paulo hakusema hivyo ili kujitetea ao kujisikitikia, wala hakusema hivyo ili kuonyesha kwamba alilemewa sana na zambi na kwamba haingewezekana afanye yaliyo haki. Tukumbuke kwamba, Paulo alikuwa Mukristo mutiwa-mafuta mwenye kukomaa, aliyechaguliwa kuwa ‘mutume kwa mataifa.’ (Rom. 1:1; 11:13) Hivyo basi, kwa nini Paulo aliandika kuhusu pigano hilo?

4 Paulo alionyesha bila kuficha kwamba hangeweza kufanya mapenzi ya Mungu kama anavyotaka kwa uwezo wake mwenyewe. Kwa nini? Anaonyesha sababu anaposema: ‘Wote wamefanya zambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu.’ (Rom. 3:23) Kwa kuwa yeye pia ni muzao wa Adamu, Paulo hangeepuka matokeo ya zambi juu ya mwili wake usiokamilika. Kwa kuwa sisi wote hatukamilike na tunafanya pigano kama lake kila siku, tunaweza kuelewa hali yake. Zaidi ya hilo, kuna mambo mengi yanayoweza kutukengeusha na kutuondoa kwenye ‘barabara inayosonga inayoongoza kwenye uzima.’ (Mt. 7:14) Lakini Paulo hakuvunjika moyo, nasi pia.

5. Paulo alipata musaada na kitulizo wapi?

5 Paulo alijiuliza ikiwa ni nani atakayemuokoa na pigano hilo, na kisha akasema: “Shukrani kwa Mungu kupitia Yesu Kristo Bwana wetu!” (Rom. 7:24, 25) Kisha akawaandikia wale Wakristo watiwa-mafuta “walio katika muungano na Kristo Yesu.” (Soma Waroma 8:1, 2.) Kupitia roho yake takatifu, Yehova anawafanya kuwa wana wake, na anawaita ili wawe ‘wariti pamoja na Kristo.’ (Rom. 8:14-17) Roho hiyo na imani yao katika zabihu ya ukombozi ya Kristo, vinawasaidia ili washinde katika pigano ambalo Paulo alizungumuzia, na hivyo “hawana hukumu ya hatia.” Wamewekwa huru ‘kutoka katika sheria ya zambi na kifo.’

6. Kwa nini watumishi wote wa Mungu wanapaswa kufikiria maneno ya mutume Paulo?

6 Ingawa Paulo aliandikia Wakristo watiwa-mafuta, yale aliyosema kuhusu roho ya Mungu na zabihu ya ukombozi ya Kristo yanaweza kusaidia watumishi wote wa Yehova iwe wana tumaini la kuishi mbinguni ao duniani. Ijapokuwa Paulo aliongozwa na roho ya Mungu ili kutolea Wakristo watiwa-mafuta shauri hilo, ni lazima watumishi wote wa Mungu waelewe mambo aliyoandika na kujikaza kufaidika nayo.

Jinsi Mungu ‘Alivyoihukumu Zambi Katika Mwili’

7, 8. (a) Ni katika maana gani Sheria ilikuwa ‘zaifu kupitia mwili’? (b) Mungu ametimiza nini kupitia roho yake na zabihu ya ukombozi?

7 Katika sura ya 7 ya Waroma, Paulo alitambua uwezo wa zambi juu ya mwili usiokamilika. Katika sura ya 8, alizungumuzia uwezo wa roho takatifu. Mutume Paulo alieleza jinsi roho hiyo inavyoweza kusaidia Wakristo wanapopigana na nguvu ya zambi ili waishi kulingana na mapenzi ya Yehova na kukubaliwa naye. Paulo alionyesha kwamba Mungu anatumia roho yake takatifu na pia zabihu ya ukombozi ya Mwana wake, ili kutimiza kile Sheria ya Musa haikutimiza.

8 Sheria hiyo, pamoja na amri zake nyingi, iliwahukumu watenda zambi. Zaidi ya hilo, makuhani wakuu wa Israeli waliotumika chini ya Sheria hawakuwa wakamilifu, kwa hiyo hawangeweza kutoa zabihu ambayo ingeondoa zambi kabisa. Katika maana hiyo Sheria ilikuwa ‘zaifu kupitia mwili.’ Lakini ‘kwa kumutuma Mwana wake mwenyewe akiwa katika mufano wa mwili wenye zambi’ na kumutoa awe zabihu ya ukombozi, Mungu ‘aliihukumu zambi katika mwili,’ na hivyo kupitia zabihu hiyo ushindi juu ya ‘sheria isiyo na uwezo’ ulipatikana. Kwa hiyo, kwa kuwa Wakristo watiwa-mafuta wana imani katika zabihu ya ukombozi ya Yesu, Yehova anawaona kuwa wenye haki. Paulo anawatia moyo ‘kutembea, si kupatana na mwili, bali kupatana na roho.’ (Soma Waroma 8:3, 4.) Wanapaswa kufanya hivyo kwa uaminifu mupaka mwisho wa maisha yao duniani ili wapewe “taji la uzima.”—Ufu. 2:10.

9. Neno “sheria” linalotumiwa kwenye Waroma 8:2 linamaanisha nini?

9 Paulo alizungumuzia pia “sheria ya ile roho” na ‘sheria ya zambi na kifo.’ (Rom. 8:2) Hizo ni sheria gani? Neno “sheria” linalotumiwa hapa halimaanishe kanuni fulani, kama zile zinazopatikana katika Sheria ya Musa. Kitabu kimoja kinasema hivi: “Neno la Kigiriki linalotafsiriwa sheria katika andiko hili linamaanisha kanuni ambayo mutu anayo ndani yake inayomuchochea kutenda mazuri ao mabaya na inayomutawala kama sheria. Neno hilo linaweza pia kumaanisha kanuni za maisha ambazo mutu anajichagulia.”

10. Namna gani sheria ya zambi na kifo inatutawala?

10 Mutume Paulo aliandika hivi: ‘Kupitia mutu mumoja zambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia zambi, na hivyo kifo kikaenea kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya zambi.’ (Rom. 5:12) Kwa kuwa sisi wote ni watoto wa Adamu, tunatawaliwa na sheria ya zambi na kifo. Mwili wetu wenye zambi unatuchochea kila mara kufanya mambo yanayomuchukiza Mungu, mambo hayo yanatuongoza kwenye kifo. Katika barua yake kwa Wagalatia, Paulo alitaja matendo hayo na tabia hizo kuwa “matendo ya mwili.” Kisha akaongeza: ‘Wale walio na mazoea ya kufanya mambo ya namna hiyo hawatauriti ufalme wa Mungu.’ (Gal. 5:19-21) Watu hao si tofauti na wale wanaotembea kupatana na mwili. (Rom. 8:4) ‘Kanuni iliyo ndani yao inayowachochea kutenda’ na ‘kanuni za maisha ambazo wamejichagulia’ ni za tamaa ya kimwili kabisa. Lakini je, wale wanaofanya uasherati, wanaoabudu sanamu, wanaopashana habari na roho waovu, ao wanaofanya zambi zingine nzito ndiyo tu wanaotembea kupatana na mwili? Hapana, kwa kuwa matendo ya mwili yanatia ndani pia mambo ambayo watu fulani wanawazia kuwa tu uzaifu wa mutu, kama vile wivu, hasira, na magomvi. Ni nani anayeweza kusema kwamba yeye amekwisha kujikomboa kabisa na hatembei tena kupatana na mwili?

11, 12. Yehova amefanya nini ili kutusaidia kushinda sheria ya zambi na kifo, na tunapaswa kufanya nini ili kukubaliwa na Mungu?

11 Sisi ni wenye furaha kabisa kwa kuwa Yehova amefanya iwezekane tushinde sheria ya zambi na kifo. Yesu alisema: ‘Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamutoa Mwana wake muzaliwa-pekee, ili kila mutu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.’ Kwa kukubali upendo wa Mungu na kuwa na imani katika zabihu ya ukombozi ya Yesu Kristo, tunaweza kukombolewa na hukumu inayoletwa na zambi tuliyoriti. (Yoh. 3:16-18) Kwa hiyo, tunaweza kusema kama mutume Paulo: “Shukrani kwa Mungu kupitia Yesu Kristo Bwana wetu!”

12 Hali yetu ni kama mutu anayetunzwa ugonjwa mukali. Ikiwa tunataka kupona kabisa, tunapaswa kufanya yale muganga anatuambia tufanye. Hata ikiwa kuamini zabihu ya ukombozi kunaweza kutukomboa kutoka katika sheria ya zambi na kifo, tungali watu wasiokamilika na wenye zambi. Ili kuendelea kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Mungu, kukubaliwa naye, na kupata baraka zake, bado kuna jambo lingine tunalopaswa kufanya. Mutume Paulo alizungumuzia pia jambo la kutembea kupatana na roho ili kutimiza “takwa la uadilifu la Sheria.”

Kutembea Kupatana na Roho

13. Kutembea kupatana na roho kunamaanisha nini?

13 Tunapotembea, tunaelekea hatua kwa hatua mahali fulani. Kwa hiyo, ili kutembea kupatana na roho ni lazima tuendelee kufanya maendeleo ya kiroho, lakini hilo halimaanishi kwamba hatutafanya tena makosa. (1 Tim. 4:15) Siku baada ya siku na kulingana na uwezo wetu, tunapaswa kujikaza kutembea, ao kuishi, kupatana na uongozi wa roho. “Kutembea kwa roho” kutafanya tukubaliwe na Mungu.—Gal. 5:16.

14. Wale wanaotembea ‘kupatana na mwili’ wanafikiria nini?

14 Katika barua yake kwa Waroma, Paulo alizungumuzia aina mbili ya watu wanaokaza akili zao juu ya mambo mawili tofauti. (Soma Waroma 8:5.) Neno mwili unaozungumuziwa hapa haumaanishi tu mwili wetu wa kawaida. Wakati fulani katika Biblia, neno “mwili” linatumiwa pia ili kumaanisha kutokamilika kwa mwili wetu wenye zambi. Kutokamilika ndiko kunafanya vita iwe kati ya mwili na akili, vita ambayo mutume Paulo alizungumuzia hapo juu. Paulo alipigana na mwili ao kutokamilika, lakini wale “wanaopatana na mwili” hawajaribu hata kupiganisha tamaa zao mbaya. Kuliko kufikiria mambo ambayo Mungu anataka wafanye na kukubali musaada ambao anawatolea, ‘wanakaza akili zao juu ya mambo ya mwili.’ Mara nyingi wanafikiria tu mambo ya kufurahisha mwili wao na kutosheleza tamaa zao. Lakini, wale ‘wanaopatana na roho’ wanakaza akili zao juu ya “mambo ya roho,” wanafikiria sana uhusiano wao pamoja na Mungu na utendaji mbalimbali wa kiroho.

15, 16. (a) Namna gani kukaza akili juu ya jambo fulani kunaweza kuharibu mwelekeo wa akili wa mutu? (b) Watu wengi leo wanakazia akili zao juu ya mambo gani?

15 Soma Waroma 8:6. Ili mutu afikie kufanya jambo fulani—nzuri ao mbaya—ni lazima kwanza akazie akili yake juu ya jambo hilo. Watu wanaoendelea kukaza akili zao juu ya mambo ya mwili wanakuwa na mutazamo wa akili ao mwelekeo wa kupenda ao kufanya mambo hayo ya mwili. Mara nyingi wanawaza, wanapendezwa, na wanahangaikia tu mambo hayo.

16 Ni mambo gani ambayo watu wengi wanahangaikia sana leo? Mutume Yohana aliandika hivi: ‘Kila kitu kilicho katika ulimwengu—tamaa ya mwili na tamaa ya macho na mutu kujionyesha mali yake maishani—hakitokani na Baba, bali hutokana na ulimwengu.’ (1 Yoh. 2:16) Tamaa hizo zinatia ndani mambo kama vile uasherati, kutafuta kujulikana, na kutafuta vitu vingi. Vitabu, magazeti, sinema, televizyo, na Internet vinajaa habari za namna hiyo, kwanza kwa sababu watu wengi wanakaza akili zao juu ya mambo hayo na wanayapenda kabisa. Hata hivyo, kumbuka kwamba, “kukaza akili juu ya mwili kunamaanisha kifo,” yaani kuharibu uhusiano wetu na Mungu sasa na kupoteza kabisa uzima wakati ujao. Kwa nini? ‘kwa sababu kukaza akili juu ya mwili kunamaanisha uadui na Mungu, kwa maana mwili haujitiishi chini ya sheria ya Mungu, nao kwa kweli hauwezi kujitiisha. Kwa hiyo wale wanaopatana na mwili hawawezi kumupendeza Mungu.’—Rom. 8:7, 8.

17, 18. Namna gani tunaweza kuendelea kukaza akili juu ya mambo ya roho, na matokeo yatakuwa nini tukifanya hivyo?

17 Pia, “kukaza akili juu ya roho kunamaanisha uzima na amani,” yaani uzima wa milele wakati ujao na kuwa na amani ya moyoni, ya akilini, na pia kuwa na amani pamoja na Mungu sasa. Namna gani tunaweza kuendelea “kukaza akili juu ya roho”? Kwa kukaza kwa ukawaida akili zetu juu ya mambo ya roho na kuacha mawazo na mutazamo wa kiroho vitutawale. Tunapofanya hivyo, akili yetu ‘itajitiisha chini ya sheria ya Mungu’ na ‘itapatana’ na mawazo yake. Tunaposhawishiwa, tutajua kwa uhakika jambo tunalopaswa kufuata. Tutachochewa kufanya uamuzi unaofaa, yaani uamuzi unaopatana na roho ya Mungu.

18 Kwa hiyo, ni jambo la maana kukaza akili zetu juu ya mambo ya roho. Tunafanya hivyo kwa ‘kukaza akili zetu juu ya utendaji,’ yaani kuwa na programu ya kiroho maishani inayotia ndani kusali kwa ukawaida, kusoma na kujifunza Biblia, kuhuzuria mikutano, na kuhubiri. (1 Pet. 1:13) Kuliko kuruhusu mambo ya mwili yatukengeushe, acheni tukaze akili zetu juu ya mambo ya roho. Tukifanya hivyo tutaendelea kutembea kupatana na roho na tutapata baraka nyingi, kwa kuwa kukaza akili juu ya mambo ya roho kunamaanisha uzima na amani.—Gal. 6:7, 8.

Je, Unaweza Kueleza?

• Ni katika maana gani ‘Sheria haikuwa na uwezo,’ na namna gani Mungu alitatua jambo hilo?

• ‘Sheria ya zambi na kifo’ ni nini, na namna gani tunaweza kukombolewa kutoka sheria hiyo?

• Tunapaswa kufanya nini ili ‘kukaza akili yetu juu ya mambo ya roho’?

[Maulizo ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 12, 13]

Je, wewe unatembea kupatana na mwili ao kupatana na roho?