Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Maulizo Kutoka kwa Wasomaji

Maulizo Kutoka kwa Wasomaji

Maulizo Kutoka kwa Wasomaji

Je, tunaweza kujua saa kamili ambayo Yesu Kristo alitundikwa kwenye muti?

Ulizo hilo linaulizwa kwa kuwa inaonekana kwamba kuna tofauti kati ya injili iliyoandikwa na Marko na ile iliyoandikwa na mutume Yohana kuhusu kifo cha Yesu. Marko aliandika hivi: ‘Sasa ilikuwa saa [ya] tatu, nao [maaskari] wakamutundika mutini.’ (Marko 15:25) Yohana aliandika, “karibu saa [ya] sita,” Pilato alimwacha Yesu mikononi mwa wayahudi ili atundikwe mutini. (Yoh. 19:14-16) Wafafanuzi wa Biblia wametoa maelezo mbalimbali ili kuelewa tofauti hiyo. Lakini, Biblia haitoi habari za kutosha ili kutusaidia tuelewe tofauti iliyo kati ya injili mbili hizo. Hata hivyo, tunapofikiria jinsi watu walivyokuwa wakihesabu saa katika siku hizo, hilo linaweza kusaidia.

Wakati wa Yesu Wayahudi waligawanya muchana katika saa 12, kuanzia kuamuka kwa jua. (Yoh. 11:9) Kwa hiyo ‘saa [ya] tatu’ ilikuwa kipindi kati ya saa mbili na saa tatu ya asubuhi na ‘saa [ya] sita’ ilikuwa kipindi kati ya saa tano na saa sita ao midi. Ni wazi kwamba jua liliamuka na lilitua kwa wakati tofauti katika mwaka. Kwa hiyo, urefu wa kipindi cha muchana ulibadilika kulingana na majira. Zaidi ya hilo, watu walijua wakati kwa kutazama mahali ambapo jua lipo. Hivyo, saa iliyokuwa ikitolewa ilikuwa ya kukadiria tu, haikuwa saa kamili. Kwa kawaida, Maandiko ya Kikristo ya Kigiriki yanazungumuzia matukio yaliyotokea saa tatu, saa sita, ao saa kenda—mara nyingi yakimaanisha kwamba tukio fulani lilitokea karibu na wakati huo. (Mt. 20:3, 5; Mdo. 10:3, 9, 30) Mara nyingi saa ilikuwa ikitajwa moja kwa moja, kama vile “saa saba,” ikiwa ilikuwa jambo la lazima kutaja saa hiyo ili kuonyesha jinsi jambo fulani lilivyotukia.—Yoh. 4:52.

Habari zilizo katika Injili zinapatana kuhusiana na wakati wa matukio ya siku za mwisho za maisha ya Yesu. Injili zote ine zinaonyesha kwamba makuhani na wazee walikutana asubuhi mbele ya jua kuamuka kisha wakamupeleka Yesu kwa Gavana Muroma Pontio Pilato. (Mt. 27:1; Marko 15:1; Luka 22:66; Yoh. 18:28) Mathayo, Marko, na Luka wanaripoti kuanzia saa [ya] sita, wakati ambapo Yesu alikuwa tayari kwenye muti wa mateso, giza likawa katika inchi yote ‘mupaka saa [ya] tisa.’—Mt. 27:45, 46; Marko 15:33, 34; Luka 23:44.

Jambo lingine la maana linaloweza kutusaidia tukadirie wakati ambapo Yesu alitundikwa juu ya muti ni hili: Kupigwa mijeledi kulionwa kuwa sehemu ya kwanza ya kipindi kinachoendelea mupaka kutundikwa juu ya muti. Nyakati fulani mutu aliyepigwa mijeledi alipigwa vikali sana hivi kwamba alikufa. Kumuhusu Yesu, lazima alipigwa vikali hivi kwamba alihitaji mutu amusaidie kuubeba muti wake wa mateso aliokuwa ameubeba peke yake kumekwisha kupita kipindi fulani. (Luka 23:26; Yoh. 19:17) Ikiwa kupigwa mijeledi kulionwa kuwa mwanzo wa kutundikwa kwa Yesu, basi kipindi fulani cha wakati kilikuwa kimekwisha kupita walipoanza kumupiga Yesu misumari kwenye muti wa mateso. Ikiwa ni hivyo, basi, kila mutu anaweza kutoa saa tofauti kuhusu kutundikwa kwa Yesu juu ya muti, hilo likitegemea wakati mutu huyo alianza kuhesabu saa, iwe wakati walianza kumupiga mijeledi ao baadaye.

Mutume Yohana alipoandika Injili yake waandikaji wengine wa injili walikuwa wamekwisha kuandika zao miaka mingi mbele. Kwa hiyo, alikuwa na nafasi ya kuchunguza mambo waliyoandika. Ni wazi kwamba Yohana aliandika saa inayoonekana kuwa tofauti na ile ya Marko. Hata hivyo, hilo linaonyesha wazi kwamba Yohana hakuandika kwa kufuata moja kwa moja yale ambayo Marko aliandika. Wote wawili, Yohana na Marko waliongozwa na roho ya Mungu. Hata ikiwa Biblia haitoi habari za kutosha ili kutusaidia kuelewa tofauti hiyo, tunaweza kutumainia habari za Injili.