Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Sisi Ni “Wakaaji wa muda” Katika Ulimwengu Huu Mwovu

Sisi Ni “Wakaaji wa muda” Katika Ulimwengu Huu Mwovu

Sisi Ni “Wakaaji wa muda” Katika Ulimwengu Huu Mwovu

‘Katika imani hawa wote . . . walitangaza hazarani kwamba wao ni wageni na wakaaji wa muda katika inchi.’—EBR. 11:13.

1. Yesu alisema nini kuhusu musimamo wa wanafunzi wake kuhusiana na ulimwengu huu?

 KUHUSU wanafunzi wake, Yesu alisema hivi: “Wao wamo ulimwenguni.” Akaongeza: “Wao si sehemu ya ulimwengu, kama vile ambavyo mimi si sehemu ya ulimwengu.” (Yoh. 17:11, 14) Hivyo, Yesu alionyesha wazi musimamo wa wanafunzi wake wa kweli kuhusiana na ‘mufumo huu wa mambo’ unaotawaliwa na Shetani. (2 Kor. 4:4) Hata ikiwa wanaishi katika ulimwengu huu mwovu, hawapaswi kuwa sehemu yake. Hali yao inafanana na ile ya “wageni na wakaaji wa muda.”—1 Pet. 2:11.

Wanaishi Kama “Wakaaji wa Muda”

2, 3. Kwa nini tunaweza kusema kwamba Enoko, Noa, Abrahamu na Sara waliishi kama “wageni na wakaaji wa muda”?

2 Tangu zamani, watumishi waaminifu wa Yehova walikuwa tofauti na watu wa ulimwengu wasiomwogopa Mungu. Kwa mufano, mbele ya Garika, Enoko na Noa ‘walitembea pamoja na Mungu wa kweli.’ (Mwa. 5:22-24; 6:9) Wote wawili walihubiri kwa ujasiri hukumu ya Mungu juu ya ulimwengu mwovu wa Shetani. (Soma 2 Petro 2:5; Yuda 14, 15.) Kwa kuwa walitembea pamoja na Mungu katika ulimwengu wa watu wasiomuogopa Mungu, Enoko ‘alimupendeza Mungu vema’ na Noa ‘alionekana kuwa mutu asiye na kosa kati ya watu wa siku zake.’—Ebr. 11:5; Mwa. 6:9.

3 Mufano mwingine ni ule wa Abrahamu na Sara. Mungu alipowaomba waondoke katika Uru ya Wakaldayo, walikubali kuacha maisha mazuri waliyokuwa nayo na kwenda kuishi maisha ya kuhama-hama katika inchi ya kigeni. (Mwa. 11:27, 28; 12:1) Paulo aliandika hivi: ‘Kwa imani Abrahamu, alipoitwa, alitii kwa kutoka akaenda na kuingia mahali alipokusudiwa kupokea kuwa uriti; naye akatoka, ijapokuwa hakujua mahali alipokuwa akienda. Kwa imani alikaa kama mugeni katika inchi ya ahadi kama katika inchi ya ugenini, akakaa katika mahema pamoja na Isaka na Yakobo, wariti pamoja naye wa ahadi ileile.’ (Ebr. 11:8, 9) Kuhusu watumishi hao waaminifu, Paulo alisema: ‘Katika imani hawa wote walikufa, ijapokuwa hawakupata utimizo wa zile ahadi, bali waliziona kwa mbali na kuzikaribisha na kutangaza hazarani kwamba wao ni wageni na wakaaji wa muda katika inchi.’—Ebr. 11:13.

Onyo kwa Waisraeli

4. Waisraeli walipewa onyo gani mbele ya kuingia katika inchi waliyopewa?

4 Wazao wa Abrahamu, yaani, Waisraeli, wakawa wengi na mwishowe Mungu akawafanya kuwa taifa, akawapatia sheria na inchi. (Mwa. 48:4; Kum. 6:1) Waisraeli hawangesahau hata kidogo kwamba inchi hiyo haikuwa yao lakini ya Yehova. (Law. 25:23) Walikuwa kama wapangaji tu, kwa hiyo walipaswa kutii kanuni zake. Pia, walipaswa kukumbuka kwamba ‘mwanadamu haishi kwa mukate tu’; kwa hiyo hawangepaswa kuruhusu vitu vya kimwili viwafanye wamusahau Yehova. (Kum. 8:1-3) Mbele ya kuingia katika inchi yao, Waisraeli walionywa hivi: ‘Na itatukia kwamba Yehova Mungu wako atakapokuleta katika inchi ambayo aliwaapia mababu zako Abrahamu, Isaka na Yakobo, kwamba atakupa, majiji makubwa na yenye kupendeza ambayo wewe hukuyajenga, na nyumba zilizojaa vitu vyote vizuri na ambazo hukuzijaza, na mashimo ya maji yaliyochimbwa ambayo hukuyachimba, mashamba ya mizabibu na mizeituni ambayo hukuipanda, nawe utakapokuwa umekula na kushiba, jiangalie usije ukamusahau Yehova, aliyekutoa katika inchi ya Misri, kutoka katika nyumba ya watumwa.’—Kum. 6:10-12.

5. Kwa nini Yehova aliacha Israeli na ni taifa gani jipya ambalo alichagua?

5 Yehova alijua kile alichokuwa akisema. Katika siku za Nehemia, kikundi cha Walawi walikumbuka kwa haya mambo yaliyotukia wakati Waisraeli walichukua Inchi ya Ahadi. Waisraeli walipokaa katika nyumba nzuri na kuwa na vyakula kwa uwingi na divai, “wakaanza kula na kushiba na kunenepa.” Wakamuasi Mungu, na hata wakawaua manabii ambao walitumwa ili kuwaonya. Basi, Yehova akawaacha katika mikono ya maadui wao. (Soma Nehemia 9:25-27; Hos. 13:6-9) Baadaye, wakati wa utawala wa Waroma, Wayahudi wasio na imani walimuua Masihi aliyeahidiwa! Yehova akawaacha na akachagua taifa jipya, yaani Israeli la kiroho.—Mt. 21:43; Mdo. 7:51, 52; Gal. 6:16.

“Si Sehemu ya Ulimwengu”

6, 7. (a) Yesu alisema nini kuhusu musimamo wa wanafunzi wake kuhusiana na ulimwengu? (b) Kwa nini Wakristo wa kweli wanapaswa kuendelea kutokuwa sehemu ya ulimwengu wa Shetani?

6 Mwanzoni mwa habari hii tulijifunza kwamba Yesu Kristo aliye kichwa cha kutaniko la Kikristo, alisema kwamba wanafunzi wake hawapaswi kuwa sehemu ya ulimwengu huu mwovu. Muda kidogo mbele ya kufa kwake, Yesu aliwaambia wanafunzi wake: ‘Kama mungekuwa sehemu ya ulimwengu, ulimwengu ungependa kilicho chake. Sasa kwa sababu ninyi si sehemu ya ulimwengu, bali nimewachagua ninyi kutoka ulimwenguni, kwa sababu hiyo ulimwengu unawachukia ninyi.’—Yoh. 15:19.

7 Kwa kuwa Ukristo ulienea, je, Wakristo wangebadili sasa musimamo wao? Je, wangeanza sasa kutenda kama watu wa ulimwengu na kuwa sehemu yake? Hapana. Popote walipoishi, walikuwa tofauti na ulimwengu wa Shetani. Miaka 30 hivi kisha kifo cha Kristo, mutume Petro aliwaandikia Wakristo walioishi katika sehemu mbalimbali zilizotawaliwa na Roma: ‘Wapendwa, nawahimiza ninyi kama wageni na wakaaji wa muda kwamba mwendelee kujiepusha na tamaa za kimwili, ambazo ndizo huendelea kupambana na nafsi. Dumisheni mwenendo wenu ukiwa muzuri katikati ya mataifa.’—1 Pet. 1:1; 2:11, 12.

8. Mwanahistoria mumoja alisema nini ili kuonyesha kwamba Wakristo wa kwanza hawakuwa sehemu ya ulimwengu?

8 Ili kuonyesha kwamba Wakristo wa wakati huo walijiendesha kama “wageni na wakaaji wa muda” katika sehemu mbalimbali zilizotawaliwa na Roma, mwanahistoria Kenneth Scott Latourette aliandika hivi: ‘Imejulikana vizuri kwamba katika kipindi cha miaka 300 ya kwanza, Wakristo waliteswa vikali na hilo lilifanyika kwa ukawaida. Walishitakiwa mambo tofauti. Walishitakiwa kuwa watu wasiomwamini Mungu kwa sababu walikataa kushiriki katika sherehe za kidini za kipagani. Walishitakiwa kuwa watu wanaowachukia wanadamu wenzao kwa kuwa walikataa kushirikiana na wengine katika mambo mengi waliyokuwa wakifanya. Mambo kama vile karamu za kipagani na viburudisho vilivyohuzuriwa na watu wengi; mambo ambayo Wakristo waliona kuwa yamejaa imani za kipagani, matendo maovu, na kila aina ya uasherati.’

Tusiutumie Ulimwengu kwa Ukamili

9. Namna gani sisi Wakristo wa kweli tunaonyesha kwamba ‘hatuwachukie wanadamu wenzetu’?

9 Hali iko namna gani leo? Sisi pia tunaendelea kuwa na musimamo kama ule wa Wakristo wa kwanza. (Gal. 1:4) Kwa sababu hiyo, watu wengi hawatuelewi na wengine hata wanatuchukia. Hata hivyo, sisi ‘hatuwachukie wanadamu wenzetu.’ Kwa kuwa tunawapenda wanadamu wenzetu, tunaenda nyumba kwa nyumba, tunajikaza kuhubiria kila mukaaji “habari njema ya Ufalme.” (Mt. 22:39; 24:14) Tunafanya hivyo kwa kuwa tunasadiki kwamba hivi karibuni Ufalme wa Mungu utakaosimamiwa na Kristo utaondoa utawala wa wanadamu wasiokamilika na kuweka ulimwengu mupya wenye haki.—Dan. 2:44; 2 Pet. 3:13.

10, 11. (a) Namna gani Wakristo wanautumia ulimwengu leo? (b) Ni katika njia gani fulani Wakristo wanakuwa waangalifu ili wasiutumie ulimwengu kwa ukamili?

10 Kwa kuwa mwisho unakaribia, sisi watumishi wa Yehova tunaelewa kwamba huu sio wakati wa kutafuta kuwa na maisha ya raha. Tunatii maneno haya ya mutume Paulo: “Nasema hili, akina ndugu, wakati uliobaki umepungua. Tangu sasa wale . . . wanaonunua wawe kama wale wasio na kitu, na wale wanaoutumia ulimwengu wawe kama wale wasioutumia kwa ukamili; kwa maana tamasha ya ulimwengu huu inabadilika.” (1 Kor. 7:29-31) Lakini namna gani Wakristo wa leo wanautumia ulimwengu? Wanafanya hivyo kwa kutumia teknolojia ya sasa na vifaa vya kupashana habari ili kueneza ujuzi wa Biblia ulimwenguni pote katika luga nyingi. Wanafanya kazi ili kupata feza wanazohitaji ili kuishi. Wananunua na kutumia vitu mbalimbali vya lazima ambavyo ulimwengu unawatolea. Lakini hawautumie ulimwengu kwa ukamili, yaani hawafanye vitu walivyo navyo ao kazi yao vichukue mahali pa kwanza katika maisha yao.—Soma 1 Timotheo 6:9, 10.

11 Wakristo waangalifu hawatumie ulimwengu kwa ukamili kuhusiana na elimu ya juu. Watu wengi wanafikiri kwamba elimu ya juu ndio njia inayomusaidia mutu kujulikana sana na kupata feza nyingi. Lakini sisi Wakristo tunaishi kama wakaaji wa muda na tuna miradi tofauti. ‘Hatukaze akili juu ya mambo makuu.’ (Rom. 12:16; Yer. 45:5) Sisi wafuasi wa Yesu, tunatii onyo hili: ‘Endeleeni kufungua macho yenu na mujilinde na kila namna ya tamaa, kwa sababu hata wakati mutu ana vitu vingi uzima wake hautokani na vitu alivyo navyo.’ (Luka 12:15) Kwa hiyo, vijana Wakristo wanatiwa moyo kufuatia miradi ya kiroho, hivyo wanahitaji kupata elimu itakayowasaidia kutosheleza mahitaji yao ya lazima. Wanapaswa kujua kwamba elimu wanayopata ina kusudi la kuwatayarisha ili wamutumikie Yehova ‘kwa moyo wao wote na kwa nafsi yao yote na kwa nguvu zao zote na kwa akili yao yote.’ (Luka 10:27) Kwa kufanya hivyo, wanaweza kuwa ‘matajiri kwa Mungu.’—Luka 12:21; soma Mathayo 6:19-21.

Usilemewe na Mahangaiko ya Maisha

12, 13. Namna gani kutii maneno ya Yesu yaliyo kwenye Mathayo 6:31-33 kunatufanya tuwe tofauti na watu wa ulimwengu?

12 Watumishi wa Yehova wanatofautiana na watu wa ulimwengu kuhusiana na jinsi wanavyoona vitu vya kimwili. Kuhusu jambo hilo, Yesu aliwaambia wafuasi wake: “Musihangaike kamwe na kusema, ‘Tutakula nini?’ ao, ‘Tutakunywa nini?’ ao, ‘Tutavaa nini?’ Kwa maana vyote hivi ndivyo vitu ambavyo mataifa yanafuatilia kwa tamaa. Kwa maana Baba yenu wa mbinguni anajua munahitaji vitu hivi vyote. Endeleeni kuutafuta kwanza ufalme na uadilifu wake, nanyi mutaongezewa hivi vitu vingine vyote.” (Mt. 6:31-33) Watumishi wengi wa Yehova wamejionea wenyewe katika maisha yao utimizo wa maneno hayo. Baba yetu wa mbinguni anawatolea vitu wanavyohitaji.

13 “Utawa pamoja na kuridhika ni faida kubwa.” (1 Tim. 6:6, The Holy Bible in Swahili Union Version) Watu wa ulimwengu hawafikiri hivyo. Kwa mufano, vijana wengi wanapofunga ndoa wanatamani mara moja kupata kila kitu, yaani, nyumba yenye kuwa na kila kitu, gari nzuri, na vifaa vingine vingi vya bei kali. Lakini, Wakristo wanaoishi kama wakaaji wa muda hawatamani kununua vitu kwa sababu ya kununua tu ao kutamani kuwa na vitu ambavyo hawana uwezo wa kupata. Ni jambo lenye kupendeza kabisa kuona kwamba ndugu na dada wengine wanajinyima mambo ya kimwili ili kupata wakati mwingi na nguvu ya kuhubiri Ufalme kwa bidii. Wengine wanatumika kama mapainia, wanabetheli, waangalizi wenye kusafiri, ao misionari. Bila shaka sisi wote tunapendezwa kabisa na utumishi wao.

14. Tunaweza kujifunza nini kutokana na mufano wa Yesu wa mupandaji?

14 Katika mufano wake wa mupandaji, Yesu alisema kwamba ‘mahangaiko ya mufumo huu wa mambo na nguvu za udanganyifu wa utajiri’ vinaweza kulisonga neno la Mungu katika mioyo yetu na kutufanya tusizae matunda. (Mt. 13:22) Tukiwa wakaaji wa muda katika ulimwengu huu, kutosheka kunaweza kutusaidia tusiangukie katika mutego. Pia, kunatusaidia kuendelea kuwa na jicho “rahisi” na kutia faida za Ufalme pa nafasi ya kwanza maishani.—Mt. 6:22.

“Ulimwengu Unapitilia Mbali”

15. Ni maneno gani ya mutume Yohana yanayoonyesha jinsi Wakristo wa kweli wanapaswa kuuona ulimwengu wa leo na jinsi wanapaswa kujiendesha?

15 Sisi Wakristo wa kweli tunajiona kuwa “wageni na wakaaji wa muda” kwa sababu tunaamini kabisa kwamba ulimwengu huu utaharibiwa hivi karibuni. (1 Pet. 2:11; 2 Pet. 3:7) Maamuzi yetu, mambo tunayopenda katika maisha na miradi tuliyo nayo ndivyo vinavyoonyesha ikiwa kweli tunaamini jambo hilo. Mutume Yohana aliwashauria waamini wenzake wasipende ulimwengu na vitu vilivyo katika ulimwengu kwa kuwa “ulimwengu unapitilia mbali na pia tamaa yake, lakini yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele.”—1 Yoh. 2:15-17.

16. Namna gani tunaweza kuonyesha kwamba tumechaguliwa kuwa watu tofauti?

16 Yehova aliwaambia Waisraeli kwamba wakimutii, watakuwa ‘mali yake ya pekee kutoka kati ya vikundi vingine vyote vya watu.’ (Kut. 19:5) Walipomutii Mungu, ibada na maisha yao vilikuwa tofauti na mataifa mengine. Leo pia, Yehova amejichagulia watu walio tofauti kabisa na ulimwengu wa Shetani. Kwa hiyo tunaonywa kwamba, ‘Tukatae kabisa kutomwogopa Mungu na tamaa za kilimwengu na tuishi kwa utimamu wa akili na uadilifu na ujitoaji-kimungu katikati ya mufumo wa mambo wa sasa, huku tukilingojea tumaini la furaha na kufunuliwa kwenye utukufu kwa Mungu mukuu na kwa Mwokozi wetu, Kristo Yesu, aliyejitoa mwenyewe kwa ajili yetu ili atukomboe sisi kutoka katika kila namna ya uasi-sheria na kujisafishia mwenyewe watu walio wake kwa njia ya pekee, walio na bidii kwa ajili ya kazi njema.’ (Tito 2:11-14) “Watu” hao ni Wakristo watiwa-mafuta na mamilioni ya “kondoo wengine” wa Yesu, wanaosaidia na kutegemeza Wakristo watiwa-mafuta.—Yoh. 10:16.

17. Kwa nini watiwa-mafuta na kondoo wengine hawatasikitika hata kidogo kwamba waliishi kama wakaaji wageni katika ulimwengu huu mwovu?

17 “Tumaini la furaha” la watiwa-mafuta ni kutawala na Kristo mbinguni. (Ufu. 5:10) Tumaini la kondoo wengine la kuishi milele duniani litakapotimia, wao hawatakuwa tena wakaaji wa muda katika ulimwengu huu mwovu. Watakuwa na nyumba nzuri na chakula na kinywaji kwa uwingi. (Zab. 37:10, 11; Isa. 25:6; 65:21, 22) Tofauti na Waisraeli, hawatasahau hata kidogo kwamba vitu vyote hivyo vinatoka kwa Yehova, “Mungu wa dunia yote.” (Isa. 54:5) Watiwa-mafuta na kondoo wengine hawatasikitika kwamba waliishi kama wakaaji wa muda katika ulimwengu huu mwovu.

Unaweza Kujibu Namna Gani?

• Namna gani waaminifu wa zamani waliishi kama wakaaji wa muda?

• Namna gani Wakristo wa kwanza walijiendesha katika ulimwengu wa wakati wao?

• Namna gani Wakristo wa kweli hawatumie ulimwengu kwa ukamili?

• Kwa nini hatutasikitika hata kidogo kwamba tuliishi kama wakaaji wageni katika ulimwengu huu mwovu?

[Maulizo ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 18]

Wakristo wa kwanza walijiepusha na viburudisho vyenye jeuri na mwenendo muchafu