Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

“Sitabaki Kilema Milele!”

“Sitabaki Kilema Milele!”

“Sitabaki Kilema Milele!”

Sara van der Monde anaeleza maisha yake

Mara nyingi watu wananiambia, “Sara, kwa nini una sura yenye furaha sikuzote?” Ninawaambia kwamba nina tumaini la pekee. Kwa kifupi tumaini langu ni hili: “Sitabaki kilema milele!”

NILIZALIWA mwaka wa 1974 katika Paris, Ufaransa. Kuzaliwa kwangu kulikuwa kwa shida sana, na baadaye waganga waligundua kwamba nina ugonjwa wa kupooza ubongo. Miguu na mikono ilikuwa yenye kupooza, na ilikuwa vigumu kuelewa mambo ninayosema. Pia niligonjwa kifafa na mwili wangu ungeweza kuambukizwa kwa uharaka.

Nilipokuwa na miaka miwili, familia yetu ilihamia Melbourne, Australia. Miaka miwili baadaye, Baba alimukataa Mama na aliniacha mimi pia. Ninakumbuka kwamba ilikuwa mara ya kwanza nijisikie karibu sana na Mungu. Mama, aliyekuwa Shahidi wa Yehova, alinipeleka kwenye mikutano ya Kikristo kwa ukawaida, na huko nilijifunza kwamba Mungu ananipenda na ananihangaikia. Kujua hivyo, na upendo wa mama yangu na jinsi alivyonitegemeza, vilinisaidia nijisikie salama hata ikiwa hali zetu zilibadilika.

Pia, mama alinifundisha jinsi ya kusali kwa Yehova. Kwa kweli, nimeona kwamba kusali ni rahisi kuliko kuzungumuza. Ninaposali, sitafute maneno ya kutumia, lakini “ninasikia” maneno yakija kwa urahisi katika akili. Hata ikiwa watu hawaelewe ninayosema, ni jambo lenye kufariji kujua kwamba Yehova anaelewa yote, iwe kwa ukimya ao ikiwa sitamuke maneno vizuri.—Zab. 65:2.

Maisha Yenye Vizuizi

Nilipokuwa na miaka mitano, hali yangu ilizidi kuwa mbaya zaidi, ilihitaji wanifunge vyuma ili kukaza miguu yangu. Hata hivyo sikuweza kutembea vizuri! Nilipokuwa na miaka 11, sikuweza hata kutembea. Baadaye, sikuweza kupanda ao kushuka kitandani bila mashini ya kunitia kwenye kinga ya vilema iliyokuwa na motere; niliiongoza kwa kutumia kishikilio.

Wakati fulani hali yangu ilikuwa yenye kunihuzunisha sana. Lakini nakumbuka kanuni ya familia yetu: “Usijihangaishe kuhusu yale hauwezi kufanya. Hangaikia tu yale unayoweza kufanya.” Hilo lilinisaidia niweze kufanya muchezo wa kupanda farasi, wa kuendesha mashua, mutumbwi, na hata kutembeza gari mahali pasipo na gari nyingi! Nina ufundi mbalimbali, ninafurahia kupakaa rangi, kushona, kuchora, na kufanya vyombo vya udongo.

Kwa kuwa hali yangu ilikuwa mbaya sana, watu fulani walisema kwamba sina uwezo wa kutosha ili kuchukua uamuzi wa kumwabudu Mungu. Nilipokuwa na miaka 18, mwalimu mumoja aliniomba nitoke kwetu “niache” dini ya mama yangu. Aliniahidia kwamba atanitolea makao. Lakini nilimwambia kwamba siwezi hata kidogo kuacha imani yangu na kwamba nitaondoka nitakapoweza kujitegemea.

Siku chache kisha kuzungumuza na mwalimu huyo, nilibatizwa Shahidi wa Yehova. Miaka miwili baadaye, nikahamia katika nyumba ndogo. Nilikuwa mwenye furaha kwa kuwa nilipata musaada niliohitaji na uhuru.

Ombi Lisilotazamiwa

Miaka iliyofuata nilipambana na majaribu mengine. Siku moja nilishangaa kabisa wakati mwanafunzi mwenzangu, kilema pia, aliniuliza ikiwa tunaweza kuoana. Mwanzoni nilipendezwa. Kama wanawake wengi, mimi pia nilitazamia siku fulani kuwa na mume. Lakini, kuwa sisi wote vilema kungetokeza magumu katika ndoa yetu. Pia, kijana huyo hakuwa Shahidi wa Yehova. Mambo tuliyoamini, utendaji wetu, na miradi yetu vilitofautiana kabisa. Basi, namna gani tungeweza kuishi pamoja? Pia, niliazimia kutii uongozi wa Mungu ulio wazi wa kuoana tu na Shahidi. (1 Kor. 7:39) Kwa hiyo, nilimwambia kwa upole kwamba siwezi kukubali ombi lake.

Niko hakika kwamba nilifanya uamuzi muzuri, na kwamba nitakuwa mwenye furaha katika dunia mupya ya Mungu. (Zab. 145:16; 2 Pet. 3:13) Ninapongojea dunia mupya, ninaazimia kubaki mwaminifu kwa Yehova na kuelewa hali zangu za sasa.

Ninatazamia sana siku ile nitaacha kinga yangu na kuruka-ruka. Nitapaaza sauti: “Nilikuwa kilema, lakini sasa nina afya nzuri milele!”