Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Tuwasaidie Wanaume Wafanye Maendeleo Ya kiroho

Tuwasaidie Wanaume Wafanye Maendeleo Ya kiroho

Tuwasaidie Wanaume Wafanye Maendeleo Ya kiroho

“Tangu sasa na kuendelea utakuwa ukiwavua watu wakiwa hai.”—LUKA 5:10.

1, 2. (a) Wanaume wengi walifanya nini walipomusikiliza Yesu akihubiri? (b) Tutazungumuzia nini katika habari hii?

 WALIPOKUWA Galilaya, Yesu na wanafunzi wake walitembea huku na huku wakihubiri. Siku moja waliingia katika mashua na kuenda mahali pasipo na watu. Lakini kikundi cha watu kiliwafuata kwa miguu. Wale waliowafuata siku hiyo walikuwa “wanaume karibu elfu tano, bila kuhesabu wanawake na watoto wachanga.” (Mt. 14:21) Wakati mwingine, kikundi cha watu kilimukaribia Yesu ili kumusikiliza na kuponywa. Kulikuwa ‘wanaume elfu ine, bila kuhesabu wanawake na watoto wachanga.’ (Mt. 15:38) Ni wazi kwamba, wanaume wengi walikua kati ya watu waliomukaribia Yesu na waliopendezwa na mafundisho yake. Yesu alitazamia kwamba wanaume wengine wengi watamusikiliza, kwa kuwa kisha kufanya muujiza uliowawezesha wanafunzi wake kuvua samaki wengi, Yesu alimwambia Simoni hivi: “Tangu sasa na kuendelea utakuwa ukiwavua watu wakiwa hai.” (Luka 5:10) Wanafunzi wake walipaswa kutupa nyavu zao za mufano na kutazamia ‘kuwavua’ wanaume wengi pia.

2 Leo pia, wanaume wanapendezwa na ujumbe wa Biblia tunaotangaza na wanaukubali. (Mt. 5:3) Lakini, wanaume wengi wanasita na hawafanye maendeleo ya kiroho. Tunaweza kuwasaidia namna gani? Ijapokuwa Yesu hakuwatafuta tu wanaume, yeye alizungumuzia mambo ambayo wanaume walikuwa wakihangaikia katika siku zake. Kwa kufuata mufano wake, acheni tuzungumuzie jinsi tunavyoweza kuwasaidia wanaume wapambane na mambo matatu ambayo kwa kawaida yanawatia wasiwasi leo: (1) kuhangaikia maisha, (2) kuogopa yale ambayo watu watasema, na (3) mutu kujisikia kwamba hastahili.

Kuhangaikia Maisha

3, 4. (a) Wanaume wengi wanahangaikia mambo gani? (b) Kwa nini wanaume fulani wanahangaikia kwanza kutafuta maisha kuliko kufuatia mambo ya kiroho?

3 Mwandishi mumoja alimwambia Yesu: “Mwalimu, mimi nitakufuata mahali popote unapoenda.” Yesu alipomwambia kwamba “Mwana wa binadamu hana mahali popote pa kulaza kichwa chake,” mwandishi huyo akabadili maoni yake. Huenda mwandishi huyo alijiuliza sana ikiwa anamufuata Yesu atakula nini na ataishi wapi, kwa kuwa hakuna andiko linaloonyesha kwamba alimufuata Kristo.—Mt. 8:19, 20.

4 Mara nyingi wanaume wanahangaikia kwanza vitu vya kimwili kuliko mambo ya kiroho. Hangaiko la wanaume wengi ni kusoma kwanza masomo ya juu na kisha kupata kazi yenye mushahara muzuri. Wao wanafikiri kwamba kutafuta feza kunaweza kuwafaidi zaidi kuliko kujifunza Biblia na kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Mungu. Wanaweza kuvutiwa na mafundisho ya Biblia, lakini ‘mahangaiko ya mufumo huu wa mambo na nguvu za udanganyifu za utajiri’ vinaweza kusonga kupendezwa kwao. (Marko 4:18, 19) Tuone jinsi Yesu alivyowasaidia wanafunzi wake wajue mambo ya kutia pa nafasi ya kwanza.

5, 6. Ni nini kilichowasaidia Andrea, Petro, Yakobo, na Yohana wabadilishe maoni yao kuhusu kazi ya kuhubiri na kuhangaikia maisha?

5 Andrea na ndugu yake Simoni Petro walifanya kazi ya kuvua samaki pamoja. Pia, Yakobo, ndugu ya Yohana, na baba yao Zebedayo walifanya pamoja kazi hiyo. Kazi hiyo iliendelea vizuri na kwa hiyo walikuwa na wafanyakazi wa kulipwa mushahara. (Marko 1:16-20) Yohana Mubatizaji alipowajulisha Andrea na Yohana habari kuhusu Yesu, walisadikishwa kwamba walikuwa wamemupata Masihi. Andrea akamujulisha ndugu yake Simoni Petro habari hiyo, na labda Yohana pia alimujulisha ndugu yake Yakobo. (Yoh. 1:29, 35-41) Miezi iliyofuata, wote wane walikuwa pamoja na Yesu alipokuwa akihubiri katika Galilaya, Yudea, na Samaria. Kisha wanafunzi hao wane wakarudilia kazi yao ya kuvua samaki. Walipendezwa na mambo ya kiroho, lakini kazi ya kuhubiri haikuwa hangaiko lao la kwanza.

6 Muda fulani baadaye, Yesu aliwaita Petro na Andrea wamufuate na kuwa “wavuvi wa watu.” Walifanya nini? “Mara moja wakaziacha nyavu, wakamufuata.” Yakobo na Yohana walifanya hivyo pia. ‘Mara moja wakaacha ile mashua na baba yao, wakamufuata.’ (Mt. 4:18-22) Ni nini kilichowasaidia wanaume hao waamue kuanza utumishi wa wakati wote? Je, waliamua hivyo bila kufikiri? Hapana! Miezi iliyotangulia, wanaume hao walisikiliza mafundisho ya Yesu, waliona miujiza aliyofanya, waliona bidii yake katika kufuatia haki na waliona jinsi watu wengi walivyofurahia mafundisho yake. Hivyo, wakawa na imani yenye nguvu na wakamutumainia kabisa Yehova!

7. Namna gani tunaweza kuwasaidia wale tunaojifunza nao Biblia watumainie kwamba Yehova ana uwezo wa kutosheleza mahitaji ya watu wake?

7 Namna gani tunaweza kumwiga Yesu kwa kuwasaidia watu tunaojifunza nao Biblia wamutumainie Yehova? (Met. 3:5, 6) Hilo litategemea namna tunavyowafundisha. Tunapowafundisha, tunaweza kukazia kwamba Yehova atatubariki sana ikiwa tunatia faida za Ufalme pa nafasi ya kwanza. (Soma Malaki 3:10; Mathayo 6:33.) Ijapokuwa tunaweza kutumia maandiko ili kuonyesha jinsi Yehova anavyotosheleza mahitaji ya watu wake, jambo ambalo hatupaswi kupuuza ni kwamba tunaweza pia kuwafundisha kupitia mufano wetu. Kuwaelezea mambo ambayo tulikutana nayo katika maisha kunaweza kuwasaidia sana wamutegemee Yehova. Tunaweza pia kuwaelezea mambo yenye kutia moyo tuliyosoma katika vichapo vyetu. *

8. (a) Kwa nini ni jambo la maana mwanafunzi wa Biblia “aonje na kuona ya kuwa Yehova ni mwema”? (b) Namna gani tunaweza kumusaidia mutu tunayejifunza naye Biblia ajionee wema wa Yehova?

8 Ili mwanafunzi awe na imani yenye nguvu haitoshi tu asome na kusikiliza namna wengine walivyobarikiwa na Yehova. Anahitaji pia kujionea katika maisha yake wema wa Yehova. Mutunga zaburi aliimba hivi: ‘Onjeni mwone ya kuwa Yehova ni mwema; mwenye furaha ni mwanaume ambaye humukimbilia.’ (Zab. 34:8) Namna gani tunaweza kumusaidia mwanafunzi aone kwamba Yehova ni mwema? Tuseme kwamba mwanafunzi ana shida ya feza lakini pia yeye ni mwenye kujikaza ili kuachana na tabia mbaya, kama vile kuvuta tumbako, kucheza michezo ya feza, ao kulewa. (Met. 23:20, 21; 2 Kor. 7:1; 1 Tim. 6:10) Itakuwa vizuri kumufundisha mwanafunzi huyo amwombe Mungu musaada ili ashinde tabia yake mbaya. Kwa kufanya hivyo atajionea wema wa Yehova, sivyo? Tunaweza pia kumutia moyo atie mambo ya kiroho pa nafasi ya kwanza kwa kufanya programu ya kujifunza Biblia kila juma, kutayarisha mikutano ya Kikristo na kuihuzuria. Hivyo, atajionea jinsi Yehova anavyobariki jitihada zake, na imani yake itaendelea kuwa nguvu!

Kuogopa Yale Ambayo Watu Watasema

9, 10. (a) Kwa nini Nikodemo na Yosefu wa Arimathea waliendelea kupendezwa na mafundisho ya Yesu kwa siri? (b) Kwa nini wanaume fulani leo wanasita kumufuata Kristo?

9 Kwa sababu ya mikazo ya wengine, wanaume fulani wanaweza kusita kumufuata Kristo kwa ukamili. Nikodemo na Yosefu wa Arimathea walipendezwa na mafundisho ya Yesu kwa siri, lakini waliogopa yale ambayo Wayahudi wengine wangesema ao kufanya ikiwa wangejua hilo. (Yoh. 3:1, 2; 19:38) Kwa nini waliogopa? Viongozi wa kidini walimuchukia Yesu sana, kwa hiyo kumwamini kungemufanya mutu afukuzwe katika sinagogi.—Yoh. 9:22.

10 Mahali fulani leo, ikiwa mwanaume anapendezwa sana na Mungu, Biblia, ao dini, anaweza kusumbuliwa na wafanyakazi wenzake, marafiki, ao watu wa jamaa. Mahali pengine, inaweza kuwa hata hatari kuelezea wengine kwamba unataka kubadili dini. Mikazo inaongezeka zaidi sana ikiwa mutu ni askari, ni mutu wa politike, ao anasimamia kikundi fulani cha watu mahali anapoishi. Kwa mufano, mwanaume mumoja huko Ujerumani, alisema hivi: “Yale ninyi Mashahidi munahubiri juu ya Biblia ni kweli. Lakini nikiwa Shahidi leo, watu hawatakawia kujua hilo. Wafanyakazi wenzangu, majirani wangu, watu wanaonijua na watu wa familia yangu watawaza nini juu yangu? Sitaweza kuvumilia jambo hilo.”

11. Namna gani Yesu aliwasaidia wanafunzi ili waweze kushinda tatizo la kuwaogopa wanadamu?

11 Mitume wa Yesu walikuwa wanaume hodari, hata hivyo wao pia walishindana na tatizo la kuwaogopa wanadamu. (Marko 14:50, 66-72) Namna gani Yesu aliwasaidia wafanye maendeleo hata ikiwa watu wangewapinga? Yesu aliwatayarisha wanafunzi ili wajue jinsi ya kupambana na upinzani. Aliwaambia: ‘Wenye furaha ni ninyi wakati wowote ule watu wanapowachukia ninyi, na wakati wowote ule watu wanapowatenga ninyi na kuwashutumu na kulitupa inje jina lenu kuwa ovu kwa ajili ya Mwana wa binadamu.’ (Luka 6:22) Yesu aliwaonya wanafunzi wake kwamba wangelaumiwa. Lakini aliwaonyesha kwamba kulaumiwa kwao ni “kwa ajili ya Mwana wa binadamu.” Yesu aliwahakikishia pia kwamba ikiwa wanamwomba Mungu musaada na nguvu, Mungu angewategemeza. (Luka 12:4-12) Zaidi ya hilo, Yesu aliawaomba wapya wajiunge na wanafunzi wake na kufanya urafiki pamoja nao.—Marko 10:29, 30.

12. Namna gani tunaweza kuwasaidia wapya washinde tatizo la kuwaogopa wanadamu?

12 Ni lazima sisi pia tuwasaidie wale tunaojifunza nao Biblia wasiwaogope wanadamu. Mara nyingi ni rahisi mutu kushinda tatizo ikiwa alijitayarisha mbele ya wakati. (Yoh. 15:19) Kwa mufano, kwa nini usimusaidie mwanafunzi kutayarisha majibu rahisi na yenye kutegemea Biblia ili kujibu maulizo ambayo wafanyakazi wenzake na watu wengine wanaweza kuuliza ao vipingamizi ambavyo wanaweza kutokeza? Zaidi ya kuwa rafiki yetu, tunaweza kumusaidia afahamiane na washiriki wengine wa kutaniko, zaidi sana wale walio katika hali zinazofanana na zake. Pia, tunapaswa kumufundisha kusali kwa ukawaida na kutoka moyoni. Hilo litamusaidia amukaribie Mungu na kumufanya Yehova kuwa kimbilio lake na Mwamba wake.—Soma Zaburi 94:21-23; Yakobo 4:8.

Mutu Kujisikia Kwamba Hastahili

13. Namna gani mutu kujisikia kwamba hastahili kunaweza kumufanya asifurahie mambo ya kiroho?

13 Wanaume fulani hawafurahie mambo ya kiroho kwa kuwa hawasome vizuri ao hawawezi kuzungumuza kwa urahisi ao kwa sababu tu ya haya. Wengine hawajisikie vizuri ao ni wenye haya na hivyo wanakuwa na magumu ya kutoa mawazo yao wanapokuwa na watu wengi. Kwa hiyo inakuwa vigumu sana kwao kujifunza, kutoa maelezo kwenye mikutano, ao kuwahubiria wengine. Ndugu mumoja alieleza kwamba alipokuwa bado kijana, alienda haraka kwenye mulango, akijaribu kupiga kengele ya mulango na kisha aliondoka haraka kwa kujificha, hakupenda mutu yeyote amusikie ao amwone. Wazo la kwenda mulango kwa mulango lilinifanya niwe mugonjwa.

14. Kwa nini wanafunzi wa Yesu hawakumuponya kijana aliyekuwa na roho mwovu?

14 Fikiria jinsi wanafunzi wa Yesu walivyojisikia waliposhindwa kumuponya kijana aliyekuwa na roho mwovu. Baba ya kijana huyo alimufikia Yesu na kumwambia: ‘[Mwanangu] ana kifafa na ni mugonjwa, kwa maana yeye huanguka ndani ya moto na ndani ya maji mara nyingi; nami nilimuleta kwa wanafunzi wako, lakini hawakuweza kumuponya.’ Yesu akamufukuza roho mwovu huyo, na kumuponya kijana yule. Baadaye wanafunzi wakamukaribia Yesu na kumuuliza: ‘Kwa nini sisi hatukuweza kumufukuza?’ Yesu akajibu: “Ni kwa sababu ya imani yenu kidogo. Kwa maana kwa kweli ninawaambia, Mukiwa na imani iliyo kama mbegu ya haradali, mutauambia mulima huu, ‘Ondoka hapa uende pale,’ nao utaondoka, na hakuna jambo litakalowashinda.” (Mt. 17:14-20) Ni lazima mutu amwamini Yehova ili aweze kushinda vizuizi vilivyo kama mulima. Ikiwa hafanye hivyo na anaanza kutegemea uwezo wake mwenyewe, atashindwa, sivyo? Na hilo linaweza kumufanya ajisikie kuwa hastahili.

15, 16. Namna gani tunaweza kumusaidia mwanafunzi wa Biblia apambane na hali ya kujisikia kwamba hastahili?

15 Njia nzuri ya kumusaidia mutu ashinde mawazo ya kujisikia kwamba hastahili ni kumutia moyo amutumainie Yehova kuliko kujitumainia. Mutume Petro aliandika hivi: ‘Jinyenyekezeni chini ya mukono wenye nguvu wa Mungu, ili awainue ninyi katika wakati unaofaa; huku mukitupa mahangaiko yenu yote juu yake, kwa sababu yeye [anawahangaikia] ninyi.’ (1 Pet. 5:6, 7) Hilo linaomba tuwasaidie watu tunaojifunza nao Biblia wakomalishe uhusiano wao pamoja na Mungu. Mutu anayependezwa na mambo ya kiroho anaona mambo ya kiroho kuwa ya maana sana. Anapenda Neno la Mungu na anaonyesha ‘tunda la roho’ katika maisha yake. (Gal. 5:22, 23) Anasali kwa ukawaida. (Flp 4:6, 7) Pia, anamutegemea Mungu ili amupe nguvu na roho ya kutoogopa ili aweze kupambana na hali yoyote ao kutimiza vizuri mugawo wowote anaopewa.—Soma 2 Timotheo 1:7, 8.

16 Wanafunzi fulani wa Biblia wanaweza pia kusaidiwa ili wajue kusoma vizuri ao kuzungumuza na watu. Wengine wanaweza kujisikia kwamba hawastahili kumutumikia Mungu kwa sababu ya matendo mabaya waliyofanya mbele ya kumujua Yehova. Tunaweza kuwasaidia kwa kuwaonyesha upendo na uvumilivu, huenda hayo ndio mambo wanayohitaji tu. Yesu alisema hivi: ‘Watu wenye afya hawahitaji tabibu [muganga], bali wenye kuugua ndio wanaomuhitaji.’—Mt. 9:12.

Tuwahubirie Wanaume Wengi Zaidi

17, 18. (a) Tunaweza kufanya nini ili tuwahubirie wanaume wengi zaidi? (b) Tutazungumuzia nini katika habari inayofuata?

17 Tunatumaini kwamba wanaume wengi zaidi watakubali ujumbe unaofanya watu wawe na furaha ya kweli unaopatikana tu katika Biblia. (2 Tim. 3:16, 17) Basi, tunaweza kufanya nini ili tuwahubirie wanaume wengi zaidi? Kwa kupitisha wakati mwingi katika mahubiri wakati wa mangaribi, mwishoni mwa juma kisha midi, ao wakati wa mapumuziko, wakati huo wanaume wengi wanapatikana nyumbani. Inapowezekana, tunaweza kuomba kuzungumuza na mwanaume katika familia. Acheni tuwahubirie inapofaa wafanyakazi wenzetu wanaume hata ikiwa hatukupanga kufanya hivyo, tuwahubirie pia waume wa dada zetu wasio Mashahidi.

18 Tunapohubiria kila mutu tunayekutana naye, tunaweza kuwa hakika kwamba wale walio na moyo unaotafuta kweli watakubali ujumbe wetu. Basi, tuwasaidie kwa uvumilivu wale wanaopendezwa kabisa na kweli. Namna gani basi tunaweza kuwasaidia wanaume waliobatizwa katika kutaniko ili wafikie mapendeleo katika tengenezo la Yehova? Habari inayofuata itazungumuzia jambo hilo.

[Maelezo ya chini]

^ Ona Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova na pia masimulizi ya maisha ya watu katika Munara wa Mulinzi na Amkeni!

Unaweza Kujibu Namna Gani?

• Namna gani tunaweza kuwasaidia wanaume ili watie mambo ya kiroho pa nafasi ya kwanza?

• Namna gani tunaweza kuwasaidia wapya washinde mikazo wanayopata?

• Ni nini kinachoweza kuwasaidia wengine washinde hali ya kujisikia kwamba hawastahili?

[Maulizo ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 25]

Je, unatafuta nafasi za kuwahubiria wanaume habari njema?

[Picha katika ukurasa wa 26]

Namna gani tunaweza kuwatayarisha wale tunaojifunza nao Biblia wajue jinsi ya kupambana na majaribu?