Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Tuwazoeze Wengine Ili Watimize Sifa Zinazoombwa

Tuwazoeze Wengine Ili Watimize Sifa Zinazoombwa

Tuwazoeze Wengine Ili Watimize Sifa Zinazoombwa

‘Kila mutu aliyefundishwa kikamili atakuwa kama mwalimu wake.’—LUKA 6:40.

1. Wakati wa huduma yake duniani, namna gani Yesu alitia musingi wa kutaniko lililopaswa kuendelea na kazi?

 MWISHONI mwa Injili yake, mutume Yohana aliandika: ‘Kwa kweli, kuna mambo mengine mengi pia aliyofanya Yesu, ambayo, kama yangeandikwa kirefu, nazani ulimwengu wenyewe haungeweza kuwa na nafasi ya kuviweka vitabu vya kukunjwa ambavyo vingeandikwa.’ (Yoh. 21:25) Kwa muda mufupi, Yesu alitimiza huduma yake kwa bidii, wakati huohuo alitafuta wanaume ambao angezoeza ili waendelee na kazi yake kisha yeye kuondoka duniani. Yesu aliporudi mbinguni mwaka wa 33, alikuwa ameanzisha kutaniko ambalo liliongezeka kwa haraka na kuwa na washiriki wengi.—Mdo. 2:41, 42; 4:4; 6:7.

2, 3. (a) Kuna uhitaji gani mukubwa katika makutaniko, nao wanaume wenye kubatizwa wanapaswa kufanya nini? (b) Tutazungumuzia nini katika habari hii?

2 Leo, ulimwenguni kuna watangazaji wa Ufalme zaidi ya milioni saba katika makutaniko zaidi ya 100,000, makutaniko hayo yana lazima ya wanaume ili kuongoza mambo. Kwa mufano, kuna uhitaji mukubwa wa wazee. Ndugu wanaojikaza kutimiza sifa ili kuwa wazee wanastahili kupongezwa, kwa kuwa ‘wao wanatamani kazi njema.’—1 Tim. 3:1.

3 Hata hivyo, ili kuwa na madaraka katika kutaniko ni lazima ndugu watimize sifa zinazoombwa na maandiko. Elimu ya mutu, kazi ao mambo ambayo mutu anajua ao kutimiza maishani si hayo tu yanayomufanya mutu awe tayari kupewa madaraka. Mutu anapaswa kutimiza sifa za kiroho zinazoombwa. Namna gani ndugu katika kutaniko wanaweza kusaidiwa ili kutimiza sifa hizo? Yesu alisema: ‘Kila mutu aliyefundishwa kikamili atakuwa kama mwalimu wake.’ (Luka 6:40) Katika habari hii, tutazungumuzia yale ambayo Mwalimu Mukuu Yesu Kristo alifanya ili kuwasaidia wanafunzi wake wastahili kuchukua madaraka makuu, na tutaona yale tunayoweza kujifunza kutokana na hilo.

“Nimewaita Ninyi Rafiki”

4. Namna gani Yesu alionyesha wanafunzi wake kwamba alikuwa rafiki wa kweli?

4 Wanafunzi wa Yesu walikuwa rafiki zake, hakuwaona kuwa watu wasiofaa kitu. Alipitisha wakati pamoja nao, aliwatumainia, na ‘aliwajulisha mambo yote ambayo alisikia kutoka kwa Baba yake.’ (Soma Yohana 15:15.) Alipojibu ulizo lao: ‘Ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mufumo wa mambo?’ bila shaka walifurahi sana. (Mt. 24:3, 4) Pia, aliwafunulia mawazo yake na jinsi alivyojisikia. Kwa mufano, usiku ule alisalitiwa, Yesu alichukua Petro, Yakobo, na Yohana na kwenda nao katika shamba la Gethsemane; huko alisali kwa bidii na moyo wake ulikuwa na uchungu sana. Labda mitume hao watatu hawakusikia mambo ambayo alikuwa akisema katika sala, lakini ni wazi kwamba waliona kwamba alikuwa mwenye kusumbuliwa sana wakati huo. (Marko 14:33-38) Fikiria pia jinsi mitume hao watatu walivyojisikia walipomwona Yesu akigeuka sura siku fulani hapo mbele. (Marko 9:2-8; 2 Pet. 1:16-18) Urafiki wa karibu ambao Yesu alifanya pamoja nao uliwasaidia sana baadaye ilipowaomba kutimiza madaraka mazito.

5. Ni katika njia gani mbalimbali wazee wanaweza kusaidia wengine?

5 Kama Yesu, leo pia wazee wanapenda kusaidia ndugu na dada na wanapenda kuwa marafiki zao. Wanafanya urafiki wa karibu na wenye shauku kwa kuchukua wakati wa kupendezwa nao. Wazee wanajua umaana wa kuchunga siri, lakini hilo halimaanishi kwamba wao hawawezi kuzungumuza jambo lolote na wengine. Wazee wanatumainia ndugu zao na wanawaambia wengine kweli za Biblia ambazo wamejifunza. Wazee hawapaswi kujiona kuwa wa maana kuliko mutumishi wa huduma anayeonekana kuwa kijana. Lakini, watamwona kuwa mwanaume wa kiroho aliye na uwezo, na kwamba utumishi anaofanya kwa ajili ya kutaniko ni wa maana.

‘Niliwawekea Ninyi Mufano’

6, 7. Eleza mambo ambayo Yesu alifanya ili awe mufano kwa wanafunzi wake, na hilo lilikuwa na matokeo gani kwao?

6 Ijapokuwa wanafunzi wa Yesu walipenda mambo ya kiroho, wakati fulani mawazo yao yaliongozwa na malezi yao na desturi za kwao. (Mt. 19:9, 10; Luka 9:46-48; Yoh. 4:27) Lakini, Yesu hakuwachambua ao kuwaogopesha. Hakuwaomba wafanye mambo yaliyopita uwezo wao wala hakuwaamuru wafanye mambo ambayo yeye mwenyewe hakuwa anafanya. Yesu aliwafundisha kupitia mufano wake.—Soma Yohana 13:15.

7 Ni mufano gani ambao Yesu aliwaachia wanafunzi wake? (1 Pet. 2:21) Aliishi maisha rahisi ili aweze kuwatumikia wengine bila magumu. (Luka 9:58) Sikuzote Yesu alikuwa mwenye kiasi alipokuwa akifundisha; mafundisho yake yalitegemea Maandiko. (Yoh. 5:19; 17:14, 17) Alikuwa mwema na watu walimukaribia kwa urahisi. Kila jambo alilofanya alichochewa na upendo. (Mt. 19:13-15; Yoh. 15:12) Mufano wa Yesu ulikuwa na matokeo mazuri juu ya wanafunzi wake. Kwa mufano, Yakobo hakuogopa kifo lakini alimutumikia Mungu kwa uaminifu mupaka alipouawa. (Mdo. 12:1, 2) Mutume Yohana alifuata hatua za Yesu kwa uaminifu zaidi ya miaka 60.—Ufu. 1:1, 2, 9.

8. Ni katika mambo gani wazee wanakuwa mufano kwa vijana wanaume na wengine katika kutaniko?

8 Wazee walio na roho ya kujinyima, wanyenyekevu, na wenye upendo wanawekea vijana mufano wanaohitaji. (1 Pet. 5:2, 3) Pia, wazee walio mufano muzuri katika imani, namna yao ya kufundisha, maisha yao ya Kikristo, na katika mahubiri wanafurahia kuona kwamba wengine wanaweza kuiga imani yao.—Ebr. 13:7.

‘Yesu Aliwapa Wanafunzi Wake Maagizo na Kisha Akawatuma’

9. Namna gani tunajua kwamba Yesu aliwazoeza wanafunzi wake ili watimize kazi ya kuhubiri?

9 Baada ya kuhubiri kwa bidii kwa miaka miwili hivi, Yesu alipanua kazi yake ya kuhubiri kwa kuwatuma mitume wake 12. Lakini aliwapa kwanza maagizo. (Mt. 10:5-14) Mbele ya kulisha kimuujiza kikundi cha watu wengi, Yesu aliwaambia wanafunzi wake namna ya kuwapanga watu hao vikundi-vikundi ili waweze kuwagawia chakula. (Luka 9:12-17) Ni wazi kwamba, Yesu aliwazoeza wanafunzi wake kwa kuwatolea maagizo ili wajue yale wanayopaswa kufanya na namna ya kufanya. Mazoezi hayo pamoja na uongozi wenye nguvu wa roho takatifu viliwasaidia mitume baadaye ili wajue kupanga kazi kubwa ya kuhubiri kuanzia mwaka wa 33 W.K.

10, 11. Namna gani wazee na wengine wanaweza kuendelea kuwatolea wapya mazoezi?

10 Leo, mwanaume anapokubali kujifunza Biblia anaanza kupata mazoezi ya kiroho. Labda tunahitaji kumusaidia ajue kusoma vizuri. Kadiri tunavyojifunza naye tutaendelea kumusaidia katika mambo mengine. Anapoanza kuhuzuria mikutano kwa ukawaida, tutaendelea kumusaidia ili ashiriki katika Shule ya Huduma ya Kiteokrasi, awe muhubiri asiyebatizwa, na kazalika. Kisha kubatizwa, anaweza kuzoezwa ashiriki katika kazi ya kutunza Jumba la Ufalme. Kisha muda fulani, ndugu huyo anaweza kusaidiwa ili ajue yale anayohitaji kufanya ili astahili kuwa mutumishi wa huduma.

11 Anapomutolea ndugu anayebatizwa mugawo fulani, muzee atamufasiria kwa furaha utaratibu wa kufuata ili kufanya kazi hiyo vizuri na pia atamutolea maagizo anayohitaji. Ndugu anayezoezwa anapaswa kuelewa mambo anayotazamiwa kufanya. Ikiwa hafanye kazi hiyo vizuri kama inavyoombwa, muzee mwenye upendo hataamua haraka kwamba yeye hastahili. Lakini, atamwonyesha kwa upendo kabisa ni wapi hafanyi vizuri na kurudilia tena pamoja naye maagizo ya kufuata. Wazee wanafurahi wanapoona jinsi wanavyojikaza kufuata maagizo na jinsi wanaume hao wanavyopata furaha wanapotumikia wengine.—Mdo. 20:35.

“Anayesikiliza Shauri Ni Mwenye Hekima”

12. Ni nini kilichofanya mashauri ya Yesu yawe na matokeo mazuri?

12 Yesu aliwatolea wanafunzi wake mashauri ya pekee kulingana na mahitaji yao. Kwa mufano, aliwakemea Yakobo na Yohana kwa kuwa waliomba moto ushuke kutoka mbinguni na uwaangamize Wasamaria fulani ambao hawakumupokea Yesu. (Luka 9:52-55) Mama ya Yakobo na Yohana alipomukaribia Yesu ili kuwaombea vyeo katika Ufalme wake, Yesu aliwaambia ndugu hao hivi: “Kuketi upande wangu wa kuume na upande wangu wa kushoto sina haki ya kutoa, bali wataketi wale ambao Baba yangu amewatayarishia.” (Mt. 20:20-23) Kila wakati, Yesu alitoa mashauri yaliyokuwa wazi, yenye kumusaidia mutu ajue jinsi ya kufanya jambo fulani, na yenye kutegemea kabisa kanuni za Mungu. Aliwafundisha wanafunzi wake kufikiria kwanza kanuni za Mungu mbele ya kufanya jambo lolote. (Mt. 17:24-27) Pia, Yesu alijua uwezo wa wanafunzi wake na hakutazamia wafanye mambo kwa ukamilifu. Aliwatolea mashauri kwa upendo.—Yoh. 13:1.

13, 14. (a) Ni nani anayehitaji mashauri? (b) Ni mashauri gani muzee anaweza kumutolea mutu asiyefanya maendeleo ya kiroho?

13 Kila mwanaume anayetaka kuwa na madaraka anahitaji kupewa mashauri ya Biblia inapohitajiwa. Methali 12:15 inasema: “Anayesikiliza shauri ni mwenye hekima.” Ndugu mumoja kijana alisema: “Nilitambua kwamba tatizo langu kubwa lilikuwa la kufikiri kwamba sitaweza. Shauri ambalo muzee alinitolea lilinisaidia niwe na maoni yanayofaa.”

14 Ikiwa wazee wanatambua kwamba ndugu fulani hafanyi maendeleo ya kiroho kwa sababu mwenendo wake unashakiwa, watachukua hatua ya kumusaidia ndugu huyo katika roho ya upole. (Gal. 6:1) Nyakati nyingine, ndugu anahitaji kushauriwa kwa sababu ya utu wake. Kwa mufano, ikiwa ndugu anaonekana kuwa muzembe, muzee anaweza kumusaidia kwa kumwonyesha kwamba Yesu alikuwa muhubiri wa Ufalme mwenye bidii na aliwapatia wafuasi wake kazi ya kufanya wanafunzi. (Mt. 28:19, 20; Luka 8:1) Ikiwa ndugu anaonekana kuwa mwenye kujitakia makuu, muzee anaweza kumwonyesha jinsi Yesu alivyowasaidia wanafunzi wake waone hatari inayotokana na kutafuta makuu. (Luka 22:24-27) Namna gani ikiwa ndugu ana mwelekeo wa kutosamehe wengine? Mufano wa mutumwa aliyekataa kumusamehe mutu aliyekuwa na deni yake ndogo, ijapokuwa yeye alisamehewa deni kubwa, unaweza kumusaidia sana. (Mt. 18:21-35) Wakati mutu anahitaji mashauri, ni vizuri wazee wamusaidie haraka.—Soma Methali 27:9.

‘Ujizoeze Mwenyewe’

15. Namna gani familia ya ndugu inaweza kumusaidia awatumikie wengine katika kutaniko?

15 Wazee ndio walio na daraka la kuwazoeza wanaume ili wachukue madaraka katika kutaniko, lakini wengine wanaweza pia kuwasaidia. Kwa mufano, muke na watoto wa ndugu wanaweza kumusaidia awe na madaraka katika kutaniko. Ikiwa yeye tayari ni muzee wa kutaniko, muke wake mwenye upendo anaweza kumutegemeza na pia watoto wake wanaweza kufanya hivyo kwa roho yao ya kujinyima. Ni lazima watu wa familia yake wakubali kwamba wakati mwingine ambao angepitisha pamoja nao anapaswa kuutumia ili kushugulikia madaraka yake katika kutaniko. Roho yao ya kujinyima itamufurahisha na itafurahisha pia wengine.—Met. 15:20; 31:10, 23.

16. (a) Ni daraka la nani kwanza kuonyesha kwamba anataka kuwa na madaraka katika kutaniko? (b) Namna gani ndugu anaweza kuonyesha kwamba anataka kuwa muzee ao mutumishi wa huduma?

16 Ijapokuwa wengine wanaweza kumusaidia na kumutegemeza, kwanza ni daraka la ndugu mwenyewe kuonyesha kwamba anataka kuwa na madakara katika kutaniko. (Soma Wagalatia 6:5.) Ili kuwasaidia wengine katika kutaniko na kuhubiri kwa ukamili, si lazima ndugu awe kwanza mutumishi wa huduma ao muzee. Ikiwa ndugu anataka kuwa muzee ao mutumishi wa huduma ni lazima ajikaze kutimiza sifa zilizo katika Biblia. (1 Tim. 3:1-13; Tito 1:5-9; 1 Pet. 5:1-3) Kwa hiyo, ikiwa mwanaume anataka kuwa mutumishi wa huduma ao muzee lakini hajakubaliwa, anapaswa kufikiria sehemu ambazo anahitaji kufanyia maendeleo. Hilo linaomba kusoma Biblia kwa ukawaida, kuwa na funzo la pekee, kutafakari kwa uzito, kusali, na kuhubiri kwa bidii. Kwa kufanya hivyo anafuata shauri la Paulo kwa Timotheo: “Uwe ukijizoeza ujitoaji-kimungu ukiwa ni shabaha yako.”—1 Tim. 4:7.

17, 18. Ndugu mwenye kubatizwa anaweza kufanya nini ikiwa mahangaiko ya maisha, hali ya kujisikia hana uwezo, ao kutokuwa na nia ya kutumika vinamuzuia kutumikia kutaniko?

17 Lakini tuseme nini ikiwa ndugu hajikaze kwa sababu ya mahangaiko ya maisha ao kwa sababu anajikisia kuwa hana uwezo? Itakuwa vizuri afikirie mambo ambayo Yehova na Yesu wanatufanyia. Kwa kweli, Yehova, ‘anatubebea muzigo wetu kila siku.’ (Zab. 68:19) Kwa hiyo, Baba yetu wa mbinguni anaweza kumusaidia ndugu achukue madaraka katika kutaniko. Ni lazima afikirie pia kwamba kuna uhitaji mukubwa wa wanaume wenye kukomaa wanaopaswa kuchukua madaraka katika tengenezo la Mungu. Kufikiria jambo hilo kunaweza kumuchochea ndugu ashinde maoni yasiyofaa. Anaweza kuomba roho takatifu, akijua kwamba tunda la roho linatia ndani amani na kujizuia—sifa ambazo zinasaidia kushinda mahangaiko ao kujisikia kwamba hauna uwezo. (Luka 11:13; Gal. 5:22, 23) Na mutu anaweza kuwa hakika kabisa kwamba Yehova anawabariki wote wanaotamani kuwa na madaraka katika kutaniko wakiwa na nia nzuri.

18 Ikiwa mwanaume mwenye kubatizwa hana nia ya kuwa na madaraka, ni nini kinachoweza kumusaidia awe na nia hiyo? Mutume Paulo aliandika: “[Mungu] ndiye ambaye, kwa ajili ya mapenzi yake mema, anatenda ndani yenu ili ninyi muwe na nia na kutenda pia.” (Flp. 2:13) Ni Mungu anayetupatia nia ya kutumikia, na roho yake inaweza kutupatia nguvu ili tutimize utumishi mutakatifu. (Flp. 4:13) Pia, Mukristo anaweza kumwomba Mungu amusaidie ili afanye yaliyo sawa.—Zab. 25:4, 5.

19. Kusimamishwa kwa “wachungaji saba, ndiyo, watawala wadogo wanane” kunatuhakikishia nini?

19 Yehova anawabariki wanaume wazee wanaowazoeza wengine. Wale wanaojikaza kufikia madaraka katika kutaniko wanajionea wao wenyewe baraka zake. Maandiko yanatuhakikishia kwamba kati ya watu wa Mungu “wachungaji saba, ndiyo, watawala wadogo wanane,” yaani, hesabu inayohitajiwa ya wanaume wenye uwezo, watasimamishwa ili kuongoza katika tengenezo la Yehova. (Mik. 5:5) Ni baraka kabisa kuona kwamba wanaume wengi Wakristo wanazoezwa na kwa unyenyekevu wanatimizwa sifa zinazoombwa kwa utukufu wa Yehova!

Unaweza Kujibu Namna Gani?

• Namna gani Yesu aliwasaidia wanafunzi wake wawe na sifa zinazostahili ili kushugulikia madaraka makubwa?

• Namna gani wazee wanaweza kumuiga Yesu wanaposaidia ndugu wengine ili wachukue madaraka katika kutaniko?

• Namna gani familia ya ndugu fulani inaweza kumusaidia ili awe muzee ao mutumishi wa huduma?

• Ni mambo gani ambayo ndugu anaweza kufanya yeye mwenyewe ili atimize sifa za kuwa muzee ao mutumishi wa huduma?

[Maulizo ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 31]

Ni mazoezi gani unayoweza kumutolea mutu unayejifunza naye Biblia kadiri anavyofanya maendeleo?

[Picha katika ukurasa wa 32]

Namna gani wanaume wanaweza kuonyesha kwamba wanajikaza kufikia madaraka?