Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Yehu Aliitegemeza Ibada Safi Kwa Bidii

Yehu Aliitegemeza Ibada Safi Kwa Bidii

Yehu Aliitegemeza Ibada Safi Kwa Bidii

YEHU aliitegemeza ibada safi kwa bidii. Alifanya hivyo bila kuchoka, bila kuchelewa, kwa kuazimia, kwa bidii, na kwa uhodari. Yehu alionyesha sifa ambazo ni vizuri tuige.

Yehu alipewa mugawo fulani wakati taifa la Israeli lilikuwa katika hali mbaya. Inchi ilikuwa katika uvutano mwovu wa Yezebeli. Mume wa Yezebeli Ahabu, alikuwa tayari amekufa, kwa hiyo alikuwa mujane na pia mama wa mufalme Yehoramu aliyekuwa akitawala. Yezebeli aliwatia watu moyo wamwabudu Baali kuliko kumwabudu Yehova; aliwauwa manabii wa Mungu, na kupotosha watu kupitia “uasherati” na “ulozi” wake. (2 Fal. 9:22; 1 Fal. 18:4, 13) Yehova aliamuru nyumba yote ya Ahabu iharibiwe, kutia ndani mufalme Yehoramu na Yezebeli. Ni Yehu aliyepewa mugawo huo.

Maandiko yanamutaja Yehu kwa mara ya kwanza alipokuwa na viongozi wa jeshi huko Ramothi-gileadi, Waisraeli walipokuwa wakipigana vita na Siria. Yehu alikuwa mutu mwenye cheo cha juu, ao labda kiongozi wa jeshi la Israeli. Nabii Elisha alimutuma mumoja wa wana wa manabii amutie Yehu mafuta ili awe mufalme na akamuagiza auwe kila mwanamume wa nyumba ya Ahabu.—2 Fal. 8:28; 9:1-10.

Wakati wakuu wenzake walipomuuliza kwa nini alikuja, Yehu hakupenda kuwafunulia jambo hilo. Lakini walipomukaza, aliwafunulia mambo yote; yeye pamoja na wenzake wakafanya mipango ili kumuua Yehoramu. (2 Fal. 9:11-14) Labda jeshi lilikuwa tayari limeanza kupinga Ahabu na Yezebeli. Kwa vyovyote, Yehu alifikiri kwa uangalifu ili kujua namna nzuri zaidi ya kufanya ili kutimiza mugawo wake.

Mufalme Yehoramu aliumizwa katika vita na akakimbilia katika muji wa Yezreeli akitumaini kwamba atapona. Yehu alijua kwamba ili mupango wake utimie haingefaa watu huko Yezreeli wapate habari yoyote. Ndiyo sababu, Yehu alisema: ‘Musiache yeyote akimbie kutoka jijini na kupeleka habari Yezreeli.’ (2 Fal. 9:14, 15) Labda alifikiri kwamba wanajeshi waliokuwa waaminifu kwa Yehoramu wangepambana naye. Kwa hiyo Yehu hakutaka wapate habari yoyote ili wajitayarishe kufanya vita.

ALIKUWA AKITEMBEZA GARI KIWAZIMU!

Jambo la kushangaza ni kwamba Yehu alitembeza gari lake kutoka Ramothi-gileadi mupaka Yezreeli, umbali wa kilometa 72. Alipoelekea haraka Yezreeli, mulinzi aliyekuwa juu ya munara ‘aliona umati wa watu wa Yehu.’ (2 Fal. 9:17) Huenda Yehu alikuwa na kikundi chenye watu wengi ili atimize kusudi lake.

Mulinzi alimwona Yehu mwenye ujasiri akiendesha gari la vita, akapaaza sauti: “Yeye huendesha kiwazimu.” (2 Fal. 9:20) Ikiwa Yehu alijulikana kuwa mutu mwenye kutembeza gari la vita kiwazimu, basi kipindi hicho alitembeza zaidi kupita ili atimize haraka mugawo wake.

Yehu alikataa kuwaambia lolote wale wajumbe wawili waliotumwa kukutana naye. Kisha alikutana na Mufalme Yehoramu na rafiki yake Ahazia, mufalme wa Yuda, kila mumoja akiwa katika gari lake la vita. Yehoramu akamuuliza, “Je, kuna amani, Yehu?” Yehu akamujibu kwa hasira eti: “Kunaweza kuwa na amani gani wakati kungali na uasherati wa Yezebeli mama yako na ulozi wake mwingi?” Yehoramu aliogopeshwa na jibu lake, akageuka ili kukimbia. Lakini Yehu alikuwa mwenye kutembeza mbio kuliko yeye, akachukua mushale, akamupiga Yehoramu, mushale huo ukapita katika moyo wa mufalme Yehoramu, naye akaanguka katika gari lake na akafa. Ijapokuwa Ahazia alikimbia, baadaye, Yehu alimupata na akamuua.—2 Fal. 9:22-24, 27.

Mutu mwingine wa nyumba ya Ahabu aliyeuawa ni Malkia Yezebeli. Yehu alimwita Yezebeli kuwa “mutu aliyelaaniwa.” Yehu alipofika Yezreeli, alimwona Yezebeli akitazama chini kupitia dirisha la jumba la kifalme. Akaamuru waziwazi wakuu wa makao ya mufalme wamutupe Yezebeli chini kupitia dirisha. Kisha akaamuru punda zake zimukanyage-kanyage mwanamuke huyo aliyepotosha Israeli. Baadaye, Yehu aliwauwa watu wengine wengi wa nyumba ya Ahabu.—2 Fal. 9:30-34; 10:1-14.

Ijapokuwa jeuri ni tendo lenye kuchukiza, tunapaswa kujua kwamba katika siku hizo, Yehova alitumia watumishi wake ili kutimiza hukumu zake. Maandiko yanasema: ‘Kuanguka kwa Ahazia kulitokana na Mungu, alipomujia Yehoramu; naye alipokuja, alienda pamoja na Yehoramu kwa Yehu mujukuu wa Nimshi, ambaye Yehova alikuwa amemutia mafuta ili aikatilie mbali nyumba ya Ahabu.’ (2 Nya. 22:7) Yehu aliutupa mwili wa Yehoramu kutoka gari lake la vita; Yehu alitambua kwamba tendo hilo lilitimiza ahadi ya Yehova ya kutekeleza hukumu juu ya Ahabu aliyemuua Naboti. Zaidi ya hilo, Mungu alimwamuru Yehu ‘alipize kisasi damu ya watumishi wake’ ambayo Yezebeli alimwanga.—2 Fal. 9:7, 25, 26; 1 Fal. 21:17-19.

Leo watumishi wa Yehova hawapigane na maadui wa ibada safi kwa kutumia nguvu ya kimwili. “Kisasi ni changu,” anasema Mungu. (Ebr. 10:30) Lakini ili kulinda kutaniko na uvutano mbaya, wazee Wakristo wanaweza kutenda kwa ujasiri kwa kufuata mufano wa Yehu. (1 Kor. 5:9-13) Na washiriki wote wa kutaniko wanapaswa kukusudia kuepuka kushirikiana na watengwa.—2 Yoh. 9-11.

YEHU HAKUVUMILIA USHINDANI WOWOTE KUMWELEKEA YEHOVA

Nia ya Yehu ya kutimiza mugawo wake inaonekana wazi katika maneno aliyomwambia Yehonadabu: “Enda pamoja nami, utazame jinsi ambavyo sivumilii ushindani wowote kumwelekea Yehova.” Yehonadabu alikubali mwaliko huo, akapanda katika gari la Yehu la vita, na kwenda naye Samaria. Huko, Yehu “alitenda kwa ujanja, kusudi awaharibu waabudu wa Baali.”—2 Fal. 10:15-17, 19.

Yehu akatangaza kwamba anataka kufanya ‘zabihu kubwa’ kwa ajili ya Baali. (2 Fal. 10:18, 19) Mutu mumoja mwenye elimu alisema kwamba: ‘Huo ni usemi wa kucheza na maneno ambao Yehu alitumia kwa akili sana.’ Neno linalotumiwa hapa “kwa kawaida linamaanisha ‘zabihu,’ lakini pia linatumiwa kuhusiana na ‘kuwaua’ waasi-imani.” Kwa kuwa Yehu hakutaka mwabudu yeyote wa Baali akose tukio hilo, aliwakusanya wote katika nyumba ya Baali na kuwaomba wavae mavazi ya pekee. “Na ikawa kwamba mara tu alipomaliza kutoa lile toleo la kuteketezwa,” Yehu aliamuru wanaume 80 wenye silaha wawaue waabudu wa Baali. Kisha akabomoa nyumba ya Baali na mahali hapo pakafanywa kuwa choo; hapakustahili tena kuwa mahali pa ibada.—2 Fal. 10:20-27.

Ni kweli kwamba Yehu alimwanga damu nyingi. Lakini, Maandiko yanamutaja kuwa mwanaume mwenye ujasiri ambaye alikomboa Israeli na utawala wenye kukandamiza wa Yezebeli na familia yake. Mufalme yeyote wa Israeli ambaye angependa kupata matokeo hayo, angepaswa kuwa mwanaume mwenye ujasiri, mwenye kuazimia, na mwenye bidii. Kamusi moja ya Biblia ilieleza: “Ilikuwa kazi ngumu na ilitimizwa kwa ukamili. Kutenda bila bidii hakungeweza kumaliza ibada ya Baali katika Israeli.”

Bila shaka unatambua kwamba Wakristo leo wanapatikana katika hali zinazoomba kutumia sifa fulani kama za Yehu. Kwa mufano, tunaweza kutenda namna gani tunaposhawishiwa kufanya mambo ambayo Yehova anakataza? Tunapaswa kuwa tayari kutupilia mbali mambo hayo na kufanya hivyo kwa bidii. Wakati uhusiano wetu na Mungu unahusika, hatuwezi kuvumilia ushindani wowote kumuelekea Yehova.

UWE MWANGALIFU UNAPOTEMBEA KATIKA SHERIA YA YEHOVA

Mwisho wa hadisi hii unatutolea onyo. Yehu ‘hakugeuka asizifuate ndama za zahabu katika Betheli na katika Dani.’ (2 Fal. 10:29) Namna gani mutu aliyekuwa na bidii kwa ajili ya ibada safi aliruhusu ibada ya sanamu?

Labda Yehu alifikiri kwamba ili ufalme wa Israeli usitegemee ule wa Yuda iliomba kuwe utengano wa kidini kati ya falme hizo mbili. Kwa hiyo, Yehu alijaribu kufanya kama wafalme wa Israeli waliotangulia, yaani kutenganisha falme hizo mbili kwa kuruhusu ibada ya ndama iendelee. Hivyo, Yehu alikosa imani kwa Yehova ambaye alimufanya kuwa mufalme.

Yehova alimupongeza Yehu kwa kuwa ‘alitenda vema kwa kufanya yaliyo sawa machoni pake.’ Hata hivyo, Yehu “hakuwa mwangalifu ili atembee katika sheria ya Yehova, Mungu wa Israeli, kwa moyo wake wote.” (2 Fal. 10:30, 31) Tunapofikiria mambo ambayo Yehu alifanya hapo mbele, tunaweza kuona jambo hilo kuwa lenye kushangaza na lenye kuhuzunisha. Lakini, tunajifunza somo fulani. Ni lazima tuchukue kwa uzito uhusiano wetu pamoja na Yehova. Kila siku, ni lazima tuonyeshe uaminifu wetu kwa Mungu kwa kujifunza Neno lake, kutafakari juu ya neno hilo, na kusali kutoka moyoni kwa Baba yetu wa mbinguni. Acheni basi, tuwe waangalifu kabisa ili tuendelee kutembea katika sheria ya Yehova kwa moyo wetu wote.—1 Kor. 10:12.

[Sanduku katika ukurasa wa 4]

Yehu Anazungumuziwa Katika Historia ya Ulimwengu

Watu wanaoichambua Biblia mara nyingi wanashakia ikiwa watu wanaozungumuziwa katika Biblia waliishi kwelikweli kama sisi. Je, zaidi ya Biblia kuna vitabu vingine vinavyozungumuza kuhusu Yehu?

Maandishi matatu hivi ya zamani ya Asuria yanamutaja mufalme huyo wa Israeli kwa jina. Moja ya maandishi hayo yanaonyesha picha ya mutu anayefikiriwa kuwa Yehu ao labda mujumbe wake akiinama mbele ya Shalmanesa III, mufalme wa Asuria, akimulipa kodi. Kwenye maandishi hayo, kulikuwa maelezo yafuatayo: ‘Nilipokea kwa Yehu (Ia-ú-a), mwana wa Omri (Hu-um-ri); feza, zahabu, bakuli ya zahabu inayoitwa saplu, chombo cha zahabu chenye kuchongwa chini, vikombe vya zahabu, mbegeti za zahabu, majiwe meupe yenye bei, fimbo ya mufalme, (na) vitu vya mbao kama malipo ya kodi.’ Ni kweli kwamba Yehu hakuwa moja kwa moja “mwana wa Omri,” lakini maneno hayo yalitumiwa ili kuonyesha mufuatano wa wafalme wa Israeli. Labda jina Omri lilitajwa kwa kuwa alijulikana sana na kwa kuwa alijenga muji mukuu wa Israeli, Samaria.

Madai ya mufalme wa Asuria kwamba Yehu alilipa kodi, hayawezi kuelezwa kwa uhakika. Hata hivyo, alimutaja Yehu mara tatu—katika maandishi yaliyo kwenye jiwe, kwenye sanamu ya Shalmanesa, na katika vitabu vinavyozungumuzia historia ya wafalme wa Asuria. Yote hayo yanatuhakikishia kwamba maelezo ya Biblia kuhusu Yehu ni historia ya kweli.