Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Usipoteze Furaha Yako kwa Sababu ya Magonjwa

Usipoteze Furaha Yako kwa Sababu ya Magonjwa

Usipoteze Furaha Yako kwa Sababu ya Magonjwa

WAZIA unaamuka asubuhi, unateseka kiakili na kimwili. Unajisikia kwamba itakuwa vigumu kuvumilia mupaka mwisho wa siku; hiyo ni siku nyingine tu ya taabu inayoanza. Unaweza hata kujisikia kama Ayubu alivyojisikia, aliposema: ‘Kifo ni bora kuliko mateso hayo.’ (Ayu. 7:15, Verbum Bible) Utafanya nini ikiwa hali kama hiyo inaendelea, hata kwa muda wa miaka mingi?

Mefiboshethi, mwana wa Yonathani aliyekuwa rafiki ya Mufalme Daudi, alipambana na hali kama hiyo. Mefiboshethi alipokuwa na miaka mitano, ‘aliangushwa na kulemaa.’ (2 Sam. 4:4) Kwa kuwa alikuwa kilema aliteseka sana kiakili aliposhitakiwa kwa uongo kwamba alimusaliti mufalme, na kunyanganywa vitu vyake vingi kwa sababu ya mashtaka hayo. Hata hivyo, yeye ni mufano muzuri kuhusu jinsi alivyovumilia ulemavu wake, mashitaka ya uongo, na mambo yenye kuvunja moyo. Hakuruhusu mambo hayo yamufanye apoteze furaha yake.—2 Sam. 9:6-10; 16:1-4; 19:24-30.

Mufano mwingine ni wa mutume Paulo. Aliandika kuhusu “mwiba katika mwili” ambao alikuwa akivumilia. (2 Kor. 12:7) Inawezekana mwiba huo ulikuwa ugonjwa wa muda murefu, ao labda watu waliona kwamba yeye hastahili kuwa mutume. Kwa vyovyote, jambo hilo lilidumu, na kwa hiyo alilazimika kuvumilia mambo yaliyotokana na mwiba huo.—2 Kor. 12:9, 10.

Leo pia, watumishi fulani wa Yehova wanasumbuliwa na magonjwa ya muda murefu ao wanateseka kiakili. Alipokuwa na miaka 18, Magdalena alipatwa na ugonjwa unaoitwa lupus (ugonjwa ambao kinga ya mwili inashambulia viungo fulani vya mwili). Anasema hivi: “Niliogopa sana. Polepole hali yangu ilizidi kuwa mbaya kwa sababu ya maumivu tumboni, shingoni, na vidonda kinywani.” Kwa upande mwingine, Izabela, alipambana na hali isiyoonekana wazi. Anaeleza: “Tangu utoto, nilikuwa na ugonjwa wa kuteseka kiakili. Hivyo, leo ninashituka-shituka, nina matatizo ya kupumua, na maumivu tumboni. Najisikia mwenye kuchoka kila wakati.”

Kubali Hali Yako Kama Ilivyo

Magonjwa na ulemavu vinaweza kukufanya usitimize mambo mengine katika maisha. Unapokuwa katika hali hiyo, ni vizuri kukaa na kufikiria hali yako kama ilivyo. Huenda isiwe vyepesi kukubali hali yako. Magdalena anasema: “Ugonjwa wangu unazidi kuwa mubaya kila siku. Mara nyingi ninashindwa kutoka kitandani. Kwa kuwa maumivu ya magonjwa yangu yanashitukia, ni vigumu kwangu kupanga mambo kimbele. Jambo linalonisumbua ni kwamba siwezi tena kufanya mengi kama nilivyokuwa nikifanya katika utumishi wa Yehova.”

Ndugu Zbigniew anaeleza: “Mwaka baada ya mwaka, ugonjwa wa rhumatisme kali unanifanya kuwa zaifu, polepole unaharibu maunganisho ya mifupa. Wakati fulani ikiwa maumivu ni makali, siwezi hata kufanya kazi nyepesi. Ugonjwa huo unanifanya nijisikie kuwa mimi ni mutu wa bure.”

Miaka iliyopita, dada Barbara alikuwa na kansa ya ubongo. Anaeleza hivi: “Mwili wangu umekuwa ukibadilika kwa gafula. Najisikia sina nguvu, kichwa changu kinauma kila wakati, na nina magumu ya kufikiri juu ya jambo fulani kwa muda murefu. Kwa sababu ya ugonjwa huo, nimelazimika kufikiria upya kila jambo nililokuwa nikifanya.”

Watu wote ambao tumezungumuzia hapo juu ni watumishi wa Yehova waliojiweka wakfu kwake. Jambo wanalotia pa nafasi ya kwanza ni kufanya mapenzi yake. Wanamutegemea Mungu kwa moyo wao wote, naye anawasaidia.—Met. 3:5, 6.

Yehova Anasaidia Namna Gani?

Tunapaswa kutupulia mbali wazo la kwamba magonjwa yanayotupata ni alama ya kwamba hatukubaliwe na Mungu. (Omb. 3:33) Tufikirie mambo yaliyomupata Ayubu ijapokuwa yeye alikuwa ‘mutu asiye na lawama na munyoofu.’ (Ayu. 1:8) Mungu hamujaribu yeyote na mambo maovu. (Yak. 1:13) Magonjwa yote, iwe ya muda murefu ao ya kuteseka kiakili, ni matokeo ya zambi tuliyoriti kutoka kwa Adamu na Hawa.—Rom. 5:12.

Hata hivyo, Yehova na Yesu hawatakosa kuwasaidia wenye haki. (Zab. 34:15) Tunapopambana na hali ngumu maishani, ndipo hasa tunafikia kuelewa kwamba Mungu ni ‘kimbilio letu na ngome yetu.’ (Zab. 91:2) Kwa hiyo, tunapopambana na hali ambazo ni ngumu kwetu, ni nini kinachoweza kutusaidia tusipoteze furaha yetu?

Sala: Kwa kufuata mufano wa watumishi wa Mungu wa wakati wa zamani, tunaweza kumutupia Baba yetu wa mbinguni muzigo wetu katika sala. (Zab. 55:22) Kufanya hivyo kunaweza kutuletea “amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote.” Na amani hiyo ya ndani ‘itailinda mioyo yetu na nguvu zetu za akili.’ (Flp. 4:6, 7) Kwa kumutegemea Yehova katika sala, Magdalena alivumilia ugonjwa wake. Anasema hivi: “Kumufunulia Yehova yaliyo moyoni mwangu kunanifariji na kunaniletea furaha. Sasa ninaelewa kabisa kinachomaanisha kumutegemea Yehova siku baada ya siku.”—2 Kor. 1:3, 4.

Yehova anaweza kujibu sala zako kwa kukutolea nguvu kupitia roho yake takatifu, Neno lake, na ndugu na dada. Hautamutazamia Mungu akuponye kimuujiza. Lakini, unaweza kumutegemea ili akupe hekima na nguvu unayohitaji ili kuvumilia magumu yako. (Met. 2:7) Anaweza kukusaidia kwa kukutolea “nguvu zinazopita zile za kawaida.”—2 Kor. 4:7.

Familia: Hali ya upendo na ya kuhangaikiana katika familia inaweza kukusaidia uvumilie ugonjwa unaokusumbua. Lakini usisahau kwamba washiriki wa familia yako wanateseka pia. Wanaweza kujisikia kwamba hawana uwezo wa kukusaidia. Hata hivyo, wanakuhangaikia, hata katika nyakati za magumu. Kusali pamoja nao kutakusaidia uendelee kutulia moyoni.—Met. 14:30.

Dada Barbara anasema hivi kuhusu binti yake na dada wengine vijana katika kutaniko: “Wananisaidia kushiriki katika mahubiri. Bidii yao inanitia moyo na kuniletea furaha.” Ndugu Zbigniew kwa upande wake anapendezwa sana na jinsi muke wake anavyomutegemeza. Anasema hivi: “Muke wangu anashugulikia kazi nyingi za nyumba. Ananisaidia kuvaa mavazi na mara nyingi anabeba sakoshe yangu tunapokwenda kwenye mikutano ao katika mahubiri.”

Mashahidi wenzetu: Kuwa pamoja na ndugu na dada kunatutia moyo na kunatufariji. Lakini namna gani ikiwa afya yako haikuruhusu kuhuzuria mikutano? Dada Magdalena anaeleza: “Kutaniko linafanya mipango ili nifaidike na mikutano kupitia kaseti zilizorekodiwa. Mara nyingi ndugu wanakuja kuniona ili kujua ni jambo gani lingine wanaweza kufanya ili kunisaidia. Pia, wananiandikia barua zenye kutia moyo. Kujua kwamba wananifikiria na kunihangaikia kunanisaidia kuvumilia.”

Dada Izabela, aliye na ugonjwa wa kuteseka akilini, anaeleza: “Katika kutaniko, nina ndugu na dada wengi ninaowaona kama “baba” ao “mama;” wananisikiliza na kunielewa. Kutaniko ni familia yangu—mahali ambapo ninapata amani na furaha.”

Wale wanaopatwa na magonjwa mbalimbali ni vizuri wasijitenge na wengine. Kwa hiyo, wanapaswa kuendelea kushirikiana na kutaniko. (Met. 18:1) Kwa kufanya hivyo, wanawatia wengine pia moyo. Mwanzoni, huenda ukasita kuwajulisha ndugu na dada mahitaji yako. Hata hivyo, jua kwamba ndugu watafurahi ikiwa unawaelezea waziwazi mahitaji yako. Hilo litawatolea nafasi ya kuonyesha “upendo wa kindugu usio na unafiki.” (1 Pet. 1:22) Kwa mufano, unaweza kuwajulisha kwamba unahitaji musaada ili ufike kwenye mikutano, ao kwamba ungetaka kuhubiri nao, ao ungetaka kuwa na mazungumuzo pamoja nao nyumbani kwako. Kwa kweli, si vizuri kupitisha kiasi, hata hivyo, furahia musaada wanaokutolea.

Linda furaha yako: Kulinda furaha yako unapopambana na ugonjwa wa muda murefu, mara nyingi inakutegemea wewe. Kuwa mwenye huzuni-huzuni na kuvunjika moyo kunaweza kukuletea mawazo mabaya. Biblia inasema: “Roho ya mwanadamu inaweza kuvumilia ugonjwa wake; lakini ni nani anayeweza kuvumilia roho iliyopondeka?”—Met. 18:14.

Dada Magdalena anaeleza: “Nafanya nguvu ili nisikazie akili matatizo yangu. Najaribu kuwa mwenye furaha siku ambazo ninajisikia vizuri. Ninaposoma habari za watu waliobaki waaminifu ijapokuwa magonjwa yao ya muda murefu, hilo linanitia moyo.” Dada Izabela anatiwa nguvu anapokumbuka kwamba Yehova anamupenda na anamwona kuwa mutu wa maana. Anasema hivi: “Najisikia kuwa mutu wa maana, na nina yule ninayeishi kwa ajili yake. Pia, nina tumaini nzuri kuhusu wakati ujao.”

Ndugu Zbigniew anasema: “Ugonjwa wangu unanifundisha unyenyekevu na utii. Unanifundisha kuonyesha utambuzi na akili nzuri, na pia unanisaidia kusamehe kutoka moyoni. Nimejifunza kumutumikia Yehova kwa furaha kuliko kujisikitikia. Kwa kweli, nimechochewa kuendelea kufanya maendeleo ya kiroho.”

Kumbuka kwamba Yehova anaona uvumilivu wako. Anajitia pa nafasi yako unapoteseka na anakuhangaikia. ‘Hatasahau kazi yako na upendo ulioonyesha kwa ajili ya jina lake.’ (Ebr. 6:10) Chunga moyoni ahadi anayowatolea wote wanaomwogopa: “Sitakuacha wala kukutupa hata kidogo.”—Ebr. 13:5.

Wakati fulani unapovunjika moyo, fikiria tumaini nzuri la kuishi katika dunia mupya. Wakati huo unakaribia sana, wakati ambapo macho yako yataona baraka za Ufalme wa Mungu hapa duniani!

[Sanduku/​Picha katika ukurasa wa 28, 29]

Wanaendelea Kuhubiri Ijapokuwa Wanasumbuliwa na Magonjwa ya Muda Murefu

“Siwezi tena kutembea, kwa hiyo muke wangu ao ndugu na dada fulani wananisindikiza katika mahubiri. Ninachunga mambo nitakayosema na maandiko ya Biblia akilini.”—Jerzy, ana matatizo ya kuona.

“Zaidi ya kuhubiria watu kupitia telefone, ninafanya hivyo kupitia barua na ninaandikiana kwa ukawaida na watu wachache wanaoonyesha kupendezwa. Ninapolazwa katika hospitali, mara nyingi ninaweka Biblia na vichapo vyetu karibu ya kitanda changu. Hilo limenisaidia kuanzisha mazungumuzo na watu wengi.”—Magdalena, ana ugonjwa wa lupus.

“Ninapenda kuhubiri nyumba kwa nyumba, lakini wakati afya yangu hainiruhusu kufanya hivyo, ninahubiri kwa njia ya telefone.”—Izabela, ana ugonjwa wa kuteseka kiakili.

“Nafurahia kurudilia watu na kuwasaidia wajifunze Biblia. Siku ambayo ninaamuka vizuri, ninahubiri nyumba kwa nyumba.”—Barbara, ana kansa ya ubongo.

“Ninachukua tu sakoshe ndogo ya magazeti. Ninabaki katika mahubiri kadiri ugonjwa wangu wa kuumizwa sana kwa viungo vya mwili unavyoniruhusu.”—Zbigniew, ana ugonjwa wa rhumatisme kali.

[Picha katika ukurasa wa 30]

Vijana na wazee wanaweza kukutia moyo