Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Walijiacha Waongozwe na Roho ya Mungu: Wakati wa Mitume na Katika Siku Zetu

Walijiacha Waongozwe na Roho ya Mungu: Wakati wa Mitume na Katika Siku Zetu

Walijiacha Waongozwe na Roho ya Mungu: Wakati wa Mitume na Katika Siku Zetu

“Ni roho ileile moja inayofanya utendaji huu wote.”—1 KOR. 12:11.

1. Tutajifunza nini katika habari hii?

 PENTEKOSTE ya mwaka wa 33 inatukumbusha mambo ya ajabu yaliyotokea siku hiyo! (Mdo. 2:1-4) Ni siku hiyo, Mungu alimwanga roho yake takatifu juu ya watumishi wake ili kuonyesha kwamba katika karne hiyo ya kwanza alianza kutumia roho yake ili kuongoza watu wake kwa njia ya pekee. Katika habari iliyotangulia, tulizungumuzia jinsi Mungu alivyotumia roho yake ili kuwasaidia watu wake waaminifu wa zamani watimize mambo ya ajabu na migawo migumu. Lakini, je, namna roho ya Mungu ilivyotenda mbele ya kuja kwa Kristo ni tofauti na namna ilivyotenda wakati wa mitume? Basi, namna gani roho takatifu ya Mungu inawaongoza Wakristo leo? Acheni tuone.

“Tazama! Kijakazi wa Yehova!”

2. Namna gani Maria aliona utendaji wa roho takatifu?

2 Wakati roho takatifu iliyoahidiwa ilipomiminiwa juu ya wanafunzi, Maria pia alikuwa pamoja nao katika kile chumba cha juu huko Yerusalemu. (Mdo. 1:13, 14) Lakini miaka zaidi ya 30 mbele ya tukio hilo, alijionea mwenyewe jinsi roho ya Yehova ilivyotenda kwa njia ya ajabu. Yehova alihamisha uhai wa mwana wake kutoka mbinguni na kuutia katika tumbo la uzazi la Maria, aliyekuwa angali bikira. Mimba ya Maria ‘ilitokana na roho takatifu.’—Mt. 1:20.

3, 4. Maria alionyesha roho ya namna gani, na namna gani tunaweza kumwiga?

3 Kwa nini Maria alipata pendeleo hilo la pekee? Malaika alipomwelezea Maria ni nini iliyokuwa mapenzi ya Yehova kumwelekea, Maria alisema: “Tazama! Kijakazi wa Yehova! Na itendeke kwangu kulingana na tangazo lako.” (Luka 1:38) Aliposema hivyo, alionyesha kwamba alikuwa na moyo muzuri, na Mungu alikuwa ametambua jambo hilo. Jibu lake la bila kusita lilionyesha kwamba alikubali mapenzi ya Mungu yatimizwe. Hakumwuliza malaika kile angepaswa kufanya ikiwa watu wangemwona ana mimba ao ikiwa muchumba wake angemukataa. Kwa kujiita kijakazi wa Yehova, Maria alionyesha kwamba anamutegemea Yehova kwa moyo wote.

4 Je, wakati fulani unajisikia kuwa unalemewa na madaraka yako katika utumishi wa Mungu? Kila mumoja wetu anapaswa kujiuliza: ‘Ninamutegemea Yehova kwa moyo wote kwamba atashugulikia mambo kulingana na mapenzi yake? Kwa kweli, niko tayari kukubali kazi anayonitolea?’ Uwe hakika kwamba Mungu anawapa roho yake wale wanaomutumainia kwa moyo wote na kutambua enzi yake kuu.—Mdo. 5:32.

Roho Takatifu Ilimusaidia Petro

5. Namna gani Petro alijionea utendaji wa roho takatifu mbele ya Pentekoste ya mwaka wa 33?

5 Kama Maria, mutume Petro alijionea namna roho takatifu ya Mungu ilivyotenda kwa nguvu mbele ya Pentekoste ya mwaka wa 33. Yesu alimutolea Petro na pia mitume wengine uwezo wa kufukuza mashetani. (Marko 3:14-16) Hata ikiwa Maandiko hayatoe maelezo mengi kuhusu jambo hilo, inaonekana kwamba Petro alitumia uwezo huo. Utendaji wa roho ya Mungu ulionekana pia wakati Yesu alipomukubalia Petro atembee juu ya maji ili kukutana naye. (Soma Mathayo 14:25-29.) Ni wazi kwamba, Petro alitegemea roho takatifu ili kutimiza mambo ya ajabu. Siku chache baadaye roho hiyo ilimusaidia Petro na wanafunzi wenzake kutimiza mambo mengine ya ajabu.

6. Kwa musaada wa roho ya Mungu, Petro alikuwa na uwezo wa kufanya nini siku ya Pentekoste ya mwaka wa 33 na kisha hapo?

6 Kwenye Sikukuu ya Pentekoste ya mwaka wa 33, Petro na wengine walipewa kwa njia ya muujiza uwezo wa kuzungumuza katika luga za watu waliokuja Yerusalemu. Petro akasimama na kutolea umati wa watu hotuba. (Mdo. 2:14-36) Ndiyo, wakati fulani, Petro alikuwa mwoga na alifanya mambo bila kufikiri. Lakini kisha kupokea roho takatifu, hakuwa tena na woga wa kuhubiri ijapokuwa vitisho na mateso. (Mdo. 4:18-20, 31) Pia, roho takatifu ilimupatia ujuzi wa kujua mambo yaliyofichwa. (Mdo. 5:8, 9) Alipewa hata uwezo wa kumufufua mufu.—Mdo. 9:40.

7. Ni mafundisho gani ya Yesu ambayo Petro alielewa vizuri kisha kutiwa mafuta kwa roho takatifu?

7 Hata mbele ya Pentekoste, Petro alielewa mambo mengi ambayo Yesu alifundisha. (Mt. 16:16, 17; Yoh. 6:68) Lakini kuna mambo mengine ambayo alielewa vizuri kisha tu Pentekoste. Kwa mufano, Petro hakuelewa kwamba Kristo atakapofufuliwa siku ya tatu, atafufuliwa na mwili wa kiroho, wala hakuelewa kwamba Ufalme wa Kristo ungetawala mbinguni. (Yoh. 20:6-10; Mdo. 1:6) Wazo la kwamba wanadamu wanaweza kuwa viumbe wa kiroho na kutawala katika Ufalme mbinguni lilikuwa jambo geni kwake. Wakati alipobatizwa kwa roho takatifu na kupata tumaini la mbinguni, ndipo alipoelewa mafundisho ya Yesu kuhusu mambo hayo.

8. Je, Wakristo watiwa-mafuta na “kondoo wengine” wanajifunza mambo tofauti?

8 Wanafunzi wa Yesu walipomiminiwa roho takatifu, ndipo walipoelewa mafundisho ambayo hawakuelewa hapo mbele. Waandikaji wa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo waliandika kwa uongozi wa roho ya Mungu, mambo ya ajabu kuhusiana na kusudi la Yehova, kwa faida yetu. (Efe. 3:8-11, 18) Leo, Wakristo watiwa-mafuta walio duniani na “kondoo wengine” wanalishwa kwenye meza moja ya kiroho, na kupata ujuzi uleule wa mambo hayo. (Yoh. 10:16) Je, unafurahia sana ujuzi na uelewevu huo wa Neno la Mungu ambao roho takatifu inatutolea?

Paulo “Alijazwa Roho Takatifu”

9. Roho takatifu ilimusaidia Paulo atimize mambo gani?

9 Mwaka mumoja hivi kisha Pentekoste ya mwaka wa 33, Saulo aliyeitwa baadaye Paulo alipokea zawadi ya Mungu ya roho takatifu. Roho takatifu ilimusaidia afanye mambo yanayotufaidi leo, ilimuongoza kuandika vitabu 14 vya Biblia. Kama vile roho ya Mungu ilivyomusaidia Petro, ilimusaidia pia Paulo aelewe na kuandika mambo waziwazi kuhusu tumaini la kuishi mbinguni katika hali ya kutokufa na kutoharibika. Roho hiyo takatifu ilimusaidia Paulo kuponya wagonjwa, kufukuza mashetani, na hata kumufufua mufu! Hata hivyo, nguvu aliyopata kupitia roho takatifu ilimusaidia afanye kazi fulani ya maana sana. Leo, watumishi wa Mungu wanatimiza kazi hiyohiyo hata ikiwa hawapokee nguvu hiyo kwa njia ya muujiza.

10. Namna gani roho takatifu ilimutolea Paulo uwezo wa kusema?

10 Paulo, ambaye “alijazwa roho takatifu,” alimukemea muchawi mumoja bila woga. Jambo hilo lilikuwa na matokeo mazuri kabisa kwa kuwa lilimusaidia liwali wa Kipro asikilize mazungumuzo yote! Yeye alikubali ukweli, “kwa kuwa alistaajabishwa na fundisho la Yehova.” (Mdo. 13:8-12) Ni wazi kwamba, Paulo alijua vizuri kuwa ni roho takatifu ya Mungu tu ndiyo ingeweza kumusaidia ili aseme ukweli bila woga. (Mt. 10:20) Baadaye aliomba Wakristo wa kutaniko la Efeso waendelee kusali kwa ajili yake ili apate “uwezo wa kusema.”—Efe. 6:18-20.

11. Namna gani Paulo aliongozwa na roho ya Mungu?

11 Roho takatifu haikumutolea Paulo uwezo wa kusema tu, lakini pia kuna wakati, ilimukataza kusema mahali fulani. Katika safari zake za misionari, Paulo aliongozwa na roho ya Mungu. (Mdo. 13:2; soma Matendo 16:6-10.) Yehova anaendelea bado kuongoza kazi ya kuhubiri kupitia roho yake. Kama Paulo, watumishi wote waaminifu wa Yehova wanajikaza kutangaza ukweli kwa bidii na bila woga. Hata ikiwa leo roho ya Mungu inatuongoza tofauti na namna ilivyomwongoza Paulo, tunaweza kuwa hakika kwamba Yehova anatumia roho yake ili watu wenye kustahili wasikilize ukweli.—Yoh. 6:44.

“Utendaji wa Namna Mbalimbali”

12-14. Je, roho ya Mungu inatenda kwa namna moja juu ya watumishi wake? Eleza.

12 Habari zinazozungumuzia jinsi Yehova alivyobariki kutaniko la watiwa-mafuta wakati wa mitume zinawatia moyo watumishi wa Yehova leo, sivyo? Tufikirie maneno ambayo Paulo aliandikia kutaniko la Korintho kuhusu zawadi ya miujiza ya roho katika siku zake: “Basi kuna zawadi za namna mbalimbali, lakini kuna roho ileile; na kuna huduma za namna mbalimbali, na bado kuna Bwana yuleyule; na kuna utendaji wa namna mbalimbali, na bado ni Mungu yuleyule anayefanya utendaji wote katika watu wote.” (1 Kor. 12:4-6, 11) Ndiyo, roho takatifu inaweza kutenda kwa njia tofauti juu ya watumishi tofauti wa Mungu kwa kusudi fulani. Kwa kweli, iwe Wakristo wa “kundi dogo” ao pia wale wa “kondoo wengine,” wote wanaongozwa na roho takatifu. (Luka 12:32; Yoh. 10:16) Hata hivyo, roho hiyo haitendi kila siku namna moja juu ya kila mushiriki wa kutaniko.

13 Kwa mufano, ndugu wanatiwa kuwa wazee kwa uongozi wa roho takatifu. (Mdo. 20:28) Lakini si kila mutiwa-mafuta aliye muzee katika kutaniko. Hilo linatusaidia kuelewa kwamba roho ya Mungu inatenda kwa njia tofauti juu ya washiriki wa kutaniko.

14 Roho inayowafanya watiwa-mafuta wajue kwamba Mungu ‘amewafanya kuwa wana,’ ni roho ileile ambayo Yehova alitumia ili kumufufua Yesu na kumupa mwili usiokufa mbinguni. (Soma Waroma 8:11, 15.) Ni roho hiyohiyo ambayo Yehova alitumia ili kuumba ulimwengu wote muzima. (Mwa. 1:1-3) Kupitia roho hiyo, Yehova alimusaidia Bezaleli ili kutimiza kazi ya pekee kuhusu maskani. Kupitia roho hiyo, alimutolea Samsoni nguvu ya kufanya mambo ya ajabu, na kupitia roho hiyo alimusaidia Petro kutembea juu ya maji. Lakini, tujue kwamba kuna tofauti kati ya kuwa na roho ya Mungu na kutiwa mafuta na roho ya Mungu. Kutiwa mafuta ni namna nyingine inayoonyesha utendaji wa pekee wa roho takatifu. Kumutia mutu mafuta kwa roho ni jambo linalomuangulia Mungu peke yake.

15. Je, mupango wa kubatiza watu kwa roho takatifu utaendelea milele? Eleza.

15 Nguvu ya utendaji ya Mungu imekuwa ikitenda juu ya watumishi wake waaminifu kwa njia mbalimbali. Imekuwa ikitenda juu yao kwa muda wa miaka mingi mbele Mungu aanze mupango wa kuwatia watu mafuta kwa roho. Siku ya Pentekoste 33, Mungu alianza kuwatia mafuta watumishi wake kwa roho. Lakini mupango huo hautaendelea milele. Siku fulani ubatizo kwa roho takatifu utakwisha, lakini roho takatifu itaendelea kutenda juu ya watu wa Mungu ili wafanye mapenzi yake milele na milele.

16. Leo, watumishi wa Mungu wanatimiza kazi gani kwa musaada wa roho takatifu?

16 Watumishi wa Mungu wanatimiza kazi gani leo kwa musaada wa roho takatifu? Ufunuo 22:17 inajibu: “Roho na bibi-arusi huendelea kusema: ‘Njoo!’ Na yeyote anayesikia na aseme: ‘Njoo!’ Na yeyote anayeona kiu aje; yeyote anayetaka achukue maji ya uzima bure.” Leo, roho ya Mungu inachochea Wakristo kuwatangazia watu kwamba Yehova anaita “yeyote anayetaka” aje kuchukua maji ya uzima. Watiwa-mafuta wanaonyesha mufano katika kazi hiyo. Wale wa kondoo wengine pia wanajiunga nao. Vikundi hivyo viwili vinasaidiwa na roho takatifu ileile ili kutimiza kazi hiyo. Wote wamejiweka wakfu kwa Mungu na kubatizwa “katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu.” (Mt. 28:19) Wote wanajiacha waongozwe na roho ya Mungu katika maisha yao, na wanaonyesha tunda la roho hiyo. (Gal. 5:22, 23) Kama watiwa-mafuta, wale wa kondoo wengine wanakubali musaada wa roho ya Mungu. Kwa musaada wa roho ya Mungu, wanajikaza ili kupatanisha maisha yao na kanuni takatifu za Yehova.—2 Kor. 7:1; Ufu. 7:9, 14.

Tuendelee Kuomba Uongozi wa Roho Takatifu

17. Namna gani tunaweza kuonyesha kwamba tuna roho ya Mungu?

17 Iwe tumaini letu ni la kwenda mbinguni ao kuishi duniani, Yehova anaweza kututolea “nguvu zinazopita zile za kawaida” ili tuendelee kuwa waaminifu kwake na kupata zawadi. (2 Kor. 4:7) watu wanaweza kutuchekelea kwa sababu tunaendelea kuhubiri habari njema. Lakini tukumbuke kwamba ‘ikiwa tunashutumiwa kwa ajili ya jina la Kristo, sisi ni wenye furaha, kwa sababu ile roho ya utukufu, yaani roho ya Mungu, inatulia juu yetu.’—1 Pet. 4:14.

18, 19. Namna gani Yehova atakusaidia kupitia roho yake takatifu, na unapaswa kuendelea kufanya nini?

18 Roho takatifu ni zawadi isiyo na malipo ambayo Mungu anawatolea wale wanaoiomba kwelikweli. Inaweza kukuongezea uwezo na kukufanya uwe na tamaa zaidi ya kutimiza kazi ya Mungu vizuri zaidi. “Mungu ndiye ambaye, kwa ajili ya mapenzi yake mema, anatenda ndani yenu ili ninyi muwe na nia na kutenda pia.” Zawadi nzuri ya roho takatifu, pamoja na jitihada zetu za kuendelea “kulishika sana neno la uzima,” vitatusaidia ‘tuendelee kuufanyia kazi wokovu wetu wenyewe kwa kuogopa na kutetemeka.’—Flp. 2:12, 13, 16.

19 Tegemea kwa moyo wote roho ya Mungu; hivyo jikaze sana kutimiza mugawo wako, ufanye vizuri kazi yoyote unayopewa, na omba Yehova akusaidie. (Yak. 1:5) Atakusaidia ili uelewe Neno lake, ili ushinde matatizo, na ili uweze kutangaza habari njema. ‘Endeleeni kuomba, nanyi mutapewa; endeleeni kutafuta, nanyi mutapata; endeleeni kupiga hodi, nanyi mutafunguliwa,’ na hilo linatia pia ndani kuomba uongozi wa roho takatifu. (Luka 11:9, 13) Basi, twendelee kumwomba Yehova ili tuwe kama watu waaminifu wa zamani na wa wakati wetu, ambao walijiacha waongozwe na roho takatifu.

Unaweza Kueleza?

• Maria alionyesha roho ya namna gani, na jinsi gani tunaweza kumuiga ili tubarikiwe?

• Namna gani Paulo alijiacha aongozwe na roho ya Mungu?

• Namna gani watumishi wa Mungu wanajiacha waongozwe na roho ya Mungu leo?

[Maulizo ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 24]

Mutume Paulo alishinda roho waovu kwa musaada wa roho ya Mungu

[Picha katika ukurasa wa 26]

Leo, roho takatifu inasaidia kila Mukristo, iwe ana tumaini la kwenda mbinguni ao kuishi duniani